Wasomi wakacha madeni yao Bodi ya Mikopo.......................

Rutashubanyuma

JF-Expert Member
Sep 24, 2010
219,470
911,173
Wasomi wakacha madeni yao Bodi ya Mikopo

Imeandikwa na Mwandishi Wetu; Tarehe: 8th December 2010 @ 23:30

WANAFUNZI wa elimu ya juu waliokopeshwa fedha za masomo na Serikali, wameendelea kukacha kurejesha mikopo hiyo katika kipindi cha miaka 16 tangu kuanza kutolewa mikopo hiyo.

Mbali na hilo, Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HELSB), imetangaza kusitisha mikopo kuanzia mwakani kwa wanafunzi watakaokataa au kuchelewa kusaini fomu za kuonesha walipokea fedha za ada, chakula na malazi.

Tangu mwaka wa masomo wa 1994/95 hadi 2010/11 Sh bilioni 630.6 zimetolewa kama mikopo kwa wanafunzi hao na kati ya hizo, Sh bilioni 51.1 zilitolewa kupitia iliyokuwa Wizara ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia na Sh bilioni 579.4 zimetolewa na bodi ya mikopo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi hiyo, George Nyatega alisema hayo wakati akitoa taarifa ya bodi hiyo kwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa aliyetembelea bodi hiyo jana.

Alifafanua kuwa wanafunzi hao wamerejesha Sh bilioni 5.6 kati ya Sh bilioni 19.5 ambazo zinapaswa kuwa zimelipwa.

"Makusanyo haya yanaonesha kiwango cha urejeshwaji ni asilimia 28.8 ikilinganishwa na asilimia 0 mwaka 2007 wakati bodi ilipoanza kutekeleza jukumu hili wakati Kenya urejeshwaji ni asilimia 60 na Afrika Kusini ni asilimia 80," alifafanua.

Alisema wanufaika wa mikopo waliotafutwa na kujulikana walipo ni 25,792 sawa na asilimia 45.5 kati ya wanufaika 56,801 ambao wanastahili kurejesha mikopo.

Kiwango cha fedha za wanufaika waliopatikana wanachopaswa kulipa ni Sh bilioni 39.3.

Akizungumzia wanafunzi kutosaini fomu za kuonesha walipokea fedha za ada, chakula na malazi, alisema "wanafunzi wengi wanakataa au wanachelewa kwa makusudi kusaini returns
(taarifa za marejesho ya matumizi) ya fedha wanazokopeshwa kupitia vyuo vyao, kuanzia mwakani bodi itasitisha mkopo kwa atakayekataa kusaini au kuchelewa kusaini kwa makusudi," alionya.

Kuhusu wanafunzi wanaostahili kupewa mikopo kwa mwaka huu wa fedha, Nyatega alisema ni 86,451 ambao wametengewa Sh bilioni 231.2 na kati yao wanafunzi 34,096 ni wa mwaka wa kwanza na 52,355 ni wanaoendelea na masomo.

Alisema wanafunzi waliopo katika vyuo vikuu kwa mwaka huu ni 135,801 hivyo wanafunzi 50,482 hawajapata mikopo kutokana na kutoomba au kutokuwa na sifa.

Naye Waziri Kawambwa aliagiza bodi hiyo kupitia upya sheria yake namba tisa ya mwaka 2004 ambayo ilirekebishwa mwaka 2007, ili kufanya marekebisho maeneo yanayolalamikiwa katika utoaji wa mikopo na kuondoa upungufu kwenye utaratibu wake wa kutoa mikopo.

"Unakuta mwenye uwezo anapata mkopo na anajulikana mtoto wa fulani labda wa
Kawambwa lakini mwingine asiye na uwezo hapati, hii si sahihi kuangaliwe huu utaratibu licha ya kuanzishwa kwake ni kuzuri," alisema.
 
Back
Top Bottom