Waraka kumkataa Sioi wasambazwa - SITTA, KILANGO, SENDEKA, WAHUSISHWA KUUANDAA

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797


• SITTA, KILANGO, SENDEKA, WAHUSISHWA KUUANDAA

na Grace Macha, Arusha

ZIKIWA zimesalia siku tano kabla ya kufanyika kwa uchaguzi mdogo wa jimbo la Arumeru Mashariki, kampeni hizo zimeingia katika hatua mbaya ya mnyukano wa kuchafuana, kutishiana vifo, huku vitendo vya rushwa vikidaiwa kushamiri hasa kwa Chama cha Mapinduzi (CCM).


Mbali ya hilo, mwelekeo wa kampeni hizo umebadilika baada ya jana kuwapo waraka mzito wa kumkataa mgombea wa CCM, Sioi Sumari.
Waraka huo ambao umekuwa gumzo mjini hapa, unadaiwa kuandikwa na wabunge waliopata kujipambanua kama wapambanaji wa ufisadi, wakidai kuwa ni chaguo la mafisadi.

Waraka huo ambao Tanzania Daima Jumatano lina nakala yake, umesambazwa katika maeneo mbalimbali ya jimbo hilo.


Chini ya waraka huo, kuna picha za wabunge wa CCM, akiwemo Anne Kilango (Same Mashariki), Waziri wa Ushirikiano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, (EAC), Samwel Sitta, James Lembeli (Kahama), Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk. Harrison Mwakyembe, na Mchungaji wa Kanisa la Uzima na Wokovu Kawe, Josephat Gwajima.


Waraka huo unadai kuwa kiongozi mmoja aliyejiuzulu kwa tuhuma ya ufisadi ambaye hakutajwa jina lake, ndiye aliyemwaga pesa jimboni humo kuhakikisha Sioi anapitishwa ndani ya vikao vya CCM kugombea ubunge wa jimbo hilo ambalo lilikuwa likiongozwa na marehemu Jeremia Sumari.


“Lengo la kigogo huyo ni kujitambulisha kama mwanasiasa mwenye nguvu zaidi kwa kutumia fedha zake. Alitumia mafedha mengi kumsaidia Sioi kuwabwaga wana CCM wenye maadili ya Kitanzania. Sote tulishuhudia umwagaji wa rushwa uliokithiri na hivyo kuwanyima kina Sarakikya (William) na Kaaya (Elirehema) haki yao,” inasomeka sehemu ya waraka huo.


Waraka huo wa ukurasa mmoja uliendelea kueleza kuwa wamekata tamaa na mafisadi huku wakiwashutumu kwa kumpa sumu iliyotengenezwa nchini Urusi, Dk. Mwakyembe na kumfanya ataabike kwa maumivu makali.


Waraka huo unadai kuwa Dk. Mwakyembe alipata sumu hiyo kutoka kwa kigogo huyo ambaye hakutajwa jina na badala yake ametajwa kwa sifa kuwa ni fisadi papa.


“Nasi wanachama wa CCM tunaochukia ufisadi na ufalme katika siasa za Tanzania tunawaomba enyi watu wa Arumeru mumtendee mwenzetu haki kwa kuhakikisha kuwa mgombea wa mafisadi kijana Sioi hapati kiti hicho cha ubunge. CCM hatutaki ubunge wa kurithishana. Vivyo hivyo hatutaki kuwaona mafisadi wakiendelea kujiimarisha kwa ajili ya urais mwaka 2015,” ulisomeka waraka huo.


Akizungumzia waraka huo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alisema kuwa waraka huo hauna uhusiano wowote na CCM na hakuna mbunge wala mwanachama wa chama hicho tawala anayeweza kufanya hivyo.

“Hizi ni kampeni za kipuuzi kabisa na sijui kwa nini tunafika huko.

Nakuhakikishia waraka huo hauna uhusiano kabisa na CCM, kwanza hatujauona na hauwezi kuandaliwa na mwanachama yeyote wa CCM,” alisema Nape.


Nape aliituhumu CHADEMA kwamba inahusika na waraka huo na kwamba ndio waliouandaa kwa lengo la kumchafua mgombea wao.


“Huo ni waraka wa CHADEMA na najua wamefanya hivi kulipiza kisasi kwani wao waliwahi kufanyiwa hivyo Igunga na Arumeru na watu wao wa CHADEMA, wakafikiri ni CCM, hivyo naona wanalipiza kisasi,” alisema Nape na kuwataka wana CCM waupuuze na watambue kuwa Sioi ndiye chaguo la CCM.


Kwa upande wao CHADEMA, Mkuu wa Operesheni na Uchaguzi wa CHADEMA, John Mrema, alikana chama chake kuhusika na waraka huo akifafanua kuwa hizo ni siasa za kijinga ambazo CHADEMA kama chama makini kinachoheshimika, hakiwezi kuzifanya.


“Hizi ni siasa za kijinga ambazo kamwe CHADEMA kwa heshima iliyonayo, hakiwezi kuzishiriki kwani tumejipanga kunadi sera ili mgombea wetu Joshua Nassari apate ushindi wa kishindo,” alisema Mrema.


Hata hivyo uchunguzi uliofanywa na gazeti hili, umebaini kuwa huenda waraka huo umeandaliwa na makundi yanayokinzana ndani CCM yanayotokana na majeraha ya kura za maoni na harakati za urais mwaka 2015.


Huu ni waraka wa tatu kusambazwa kwenye jimbo hilo tangu kuanza kwa kampeni.


Waraka wa kwanza ulidaiwa kuandaliwa na Naibu Katibu Mkuu na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, ukiwalaumu viongozi wa CHADEMA akiwemo meneja kampeni wa chama hicho, Vicent Nyerere, kwa madai ya kumshambulia Rais mstaafu Benjamini Mkapa kwa kumhusisha na kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.


Waraka mwingine uliandaliwa hivi karibuni na watu wasiojulikana dhidi ya Dk. Slaa ambao unaungana na waraka uliodaiwa kuwa ni wa Zitto kubeza viongozi wa chama hicho wanaomchafua Mkapa.


Katika hatua nyingine, taarifa zinasema kuwa Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa, pamoja na Nape, wanatarajia kupanda jukwaani keshokutwa kumnadi mgombea wao.


Hii itakuwa ni mara ya kwanza kwa viongozi hao wa CCM kukaa na kupanda jukwaa moja tangu mwenyekiti wao, Rais Jakaya Kikwete alipoasisi vita ya kujivua gamba, huku Nape akimtaja hadharani Lowassa kama mmoja wa wanachama wa CCM wanaopaswa kujivua gamba.


Hali hiyo imewafanya wanasiasa hao kuonekana kama mahasimu kisiasa na ni nadra kwao kukutana au kufanya shughuli za chama pamoja.

Lowassa ambaye ni Mbunge wa Monduli, anapanda jukwaani kumnadi Sioi ambaye pia ni mkwewe, huku Nape akilazimika kufanya hivyo kuhakikisha CCM inaibuka mshindi.


Mbowe abeza kampeni za matusi

Katika hatua nyingine, Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, amewataka wanachama wa chama hicho kutojibizana na wanachama wa CCM ambao kwa sasa wanatumia majukwaa ya kampeni kuwatukana viongozi wa CHADEMA na mgombea ubunge wa chama hicho, Joshua Nassari.

Badala yake amewataka wawaombee ili waache matusi na wasichakachue kura siku ya uchaguzi kwa kile alichoeleza kuwa mpaka sasa kwa tathmini waliyofanya mgombea wa chama hicho atashinda huku CCM ikiangalia.


Mbowe aliyasema hayo jana kwa nyakati tofauti kwenye mikutano ya kampeni ya kumnadi mgombea wa chama hicho kwenye mikutano mbalimbali kwenye kata za Leguruki, Nkoaranga, Akheri, Nkoarisambu, Songoro na Mbuguni.


Alisema kuwa ni vema wananchi wa Arumeru Mashariki wakaishi kwa amani lakini si kwa woga wakielewa kuwa uchaguzi utapita lakini wao watabaki.


“CCM wameamua kuendesha siasa za matusi, wanatukana viongozi wakuu wa
CHADEMA, wanatukana wabunge wetu pamoja na mgombea wetu Nassari, nyie msijibizane nao mnachotakiwa kufanya ni kuwaombea kwenye mikutano yao waache matusi, tuwaombee siku ya kupiga kura wasichakachue huku tukiendelea kuwashawishi wampigie kura mgombea wetu ili kuongeza asilimia ya ushindi,” alisema Mbowe.


Kwa upande wake mgombea wa CHADEMA, Nassari alikemea wale wanaofananisha uchaguzi huo na mchezo wa maigizo au mpira wa miguu (soka) kwa kile alichoeleza kuwa uchaguzi huo ni muhimu sana kwani ndiyo unaoenda kuamua mustakabali wa wananchi wa Arumeru Mashariki ambao kwa kipindi kirefu wamekosa mwakilishi makini wa kushughulikia kero zao kwenye vikao mbalimbali vya maamuzi.


Alisema kuwa zaidi ya shilingi milioni 141 za mfuko wa maendeleo ya jimbo (CDF) ambazo zilitolewa kwa ajili ya jimbo hilo kwa kipindi cha miaka mitatu cha kuanzia 2010 mpaka 2012 hazijulikani zimefanya nini wakati kimsingi zilipaswa kutumika kutatua matatizo ya jimbo hilo kwenye sekta za afya, elimu, miundombinu na maji.


“Ndugu zangu nichagueni nikapiganie maendeleo ya jimbo letu, fedha nyingi za jimbo letu zinaliwa hapa, hizi shilingi milioni 141 zingeweza kumaliza tatizo la uhaba wa madawati kwenye shule zetu, zingetengeneza barabara za ndani, zahanati zetu ambazo kinamama wanazalia chini zingeboreshwa hata ziwe na hadhi ya vituo vya afya mama zetu wazalie kwenye eneo salama,” alisema Nassari.



 
Mmmmmhh!!

Ama kweli mafisadi wamekwenda na majiiiiiiiiiii!!!!

Ndipo hili NENO linakamilika!
KUPASUKA KWA PAKACHA "nafuu kwa mchukuzi"

Kwishineeeeee!!
 
Mama Kilango yupo; hivi sasa William Malecela anagombea Ubunge wa E.Africa atampinga pia? au la?

Kweli nyani hajioni nyuma yake!!!
 
Back
Top Bottom