Wanasiasa wasipotoshe Muswada wa Katiba mpya

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,293
33,078
Rais Jakaya Kikwete ametoa tahadhari kwa viongozi ambao wanawapotosha wananchi kuhusu mchakato wa maandalizi ya kuandika Katiba mpya ambapo amesisitiza kuwa Katiba mpya ya Tanzania itaandikwa na Watanzania wenyewe kwa kupitia maoni watakayotoa wenyewe kwa Tume itakayoundwa kwa mujibu wa sheria ya mwaka huu.

Kauli hiyo ilitolewa juzi na Rais Kikwete wakati akizungumza na Taifa kupitia wazee wa mkoa wa Dar es Salaam, ambapo alisema kuwa kila Mtanzania atapewa fursa ya kutoa maoni yake kwa Tume ambayo ataiunda kwa kushirikiana na Rais wa Zanzibar mara muswada wa marekebisho uliopitishwa juzi na Bunge la Jamhuri utakapokuwa umesainiwa.

Kuhusu malalamiko yanayotolewa na baadhi ya wanaharakati pamoja na wanasiasa, hususan wa upinzani kwamba yeye Rais hastahili kuunda Tume ya kusimamia mchakato wa kuandika Katiba, alishangaa na kusema hii si mara ya kwanza kwa Rais kuunda Tume kama hiyo.

Hata marais waliomtangulia walipata kufanya hivyo, akitoa mfano kwa Rais wa Kwanza, Mwalimu Julius Nyerere ambaye aliihuisha Katiba ya nchi, ikiwemo kuunda tume ya kushughulikia mchakato huo mwaka mara tatu, mwaka 1963, 1967 na 1984.
Rais Kikwete alilikumbusha Taifa kuwa Rais wa awamu ya pili, Ali Hassan Mwinyi aliwahi kuunda Tume mara moja mwaka 1991 chini ya

Jaji Francis Nyalali, na Rais mstaafu awamu ya tatu Benjamin Mkapa naye mwaka 1998 aliunda Tume mara moja ya Jaji Robert Kisanga. Tume hizi zilileta mabadiliko makubwa ya katiba ya nchi.
Kwa mantiki hiyo, Katiba iliyopo inampa mamlaka Rais Kikwete ya kuunda Tume hiyo ambayo itajumuisha watu wa kada mbalimbali na baadaye kufuatiwa na Bunge maalumu la Katiba.

Sasa swali ni je, kwanini baadhi ya watu wanataka kupotosha muswada huo kila ulipopitia mchakato na kujadiliwa? Rais anasema sote tumeshuhudia mchango mkubwa wa majukwaa yaliyoundwa kwa nyakati mbalimbali kuujadili katika mikutano kadhaa ya hadhara ambapo simu zilitumika pamoja na mitandao, akashangaa kwa kuuliza kama kilichokosewa sasa ni kipi?

Hata hivyo anasema kwa kuwa Bunge linataka Tume iundwe na kuanza kazi Desemba mosi mwaka huu, ambapo zimebaki takribani siku 11 tu, yeye na Rais wa Zanzibar wataufanyia kazi na kuunda Tume ili mwakani kazi iwe moja tu ya wananchi kutoa maoni ili ifikapo mwaka 2014 wakati wa sherehe za miaka 50 ya Muungano wa Tanzania zifanyike chini ya Katiba mpya.

Ufafanuzi huo wa Rais Kikwete umekuja baada ya baadhi ya vyama kukataa kuchangia muswada huo Bungeni, ambapo aliwataka wanasiasa pamoja na wanaharakati kuacha kuwapotosha wananchi kwa kutumia vibaya dhana ya nguvu ya umma, huku jambo jema la Katiba mpya likiwa linasubiriwa na wengi.

Tunaunga mkono juhudi zinazofanywa na wabunge wenye nia njema na taifa letu pamoja na wananchi wote katika kuujadili muswada huu katika makongamano ya hadhara na katika njia mbalimbali za mawasiliano. Pia tunampongeza Rais Kikwete kwa kuchukua muda wake muhimu kulifafanulia Taifa hatma ya mchakato huu ambao umekuwa gumzo katika maeneo mengi ya nchi hii.

Suala hili la Katiba ni muhimu kwetu sote na kinachotakiwa ni kuweka maoni yetu pamoja tuyachambue tufikie muafaka kwa wakati tuliopanga. Bunge letu linawakilisha umma wa Watanzania na hivyo hakuna sababu kususia majadiliano yanayoendelea kwa mustakabali wa taifa letu.

Tuwatendee haki wananchi kwa uwakilishi wenye maslahi ya wengi na siyo maslahi ya wachache ambao malengo yao hayajengi taifa imara na endelevu. Tunajenga nyumba moja, ugomvi wa fito wa nini?
Mjadala huu wa muswada wa Katiba ni muhimu kwa uhai wa Taifa letu, na kila mwananchi mzalendo wa nchi hii anayo haki ya kushiriki katika mchakato mzima wa kuundwa kwa katiba mpya.

Tume iliyo mbioni kuundwa itakusanya maoni ya wadau wote ili kupata katiba nzuri itakayolipeleka taifa letu mahali salama. Tunaamini kuwa Wabunge wote watashirikiana kikamilifu kuitengeneza Katiba mpya kwa maslahi ya watu wote na Taifa letu kwa jumla. Mungu libariki taifa letu Tanzania.

CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

 
Tusipokubali mabadilko kwa njia ya hiari na amani, basi mabadiliko yatakuja kwa nguvu. Huwezi ukataka mabadilko afu ukang'ang'ania kufanya yale ya kale kwa madai eti hata wakati huo ndivyo yalivyofanyika. sasa hapa umaana wa mabadilko uko wapi? Kwani suala la madaraka makubwa limetoka wapi? kama tunatengenaza katiba mpya kwa nini madaraka hayo yakapunguzwa kama kweli ni makubwa? kwa nini malalamiko yawepo? halafu mh. anasema et yeye sio dikteta anasahau kuwa kwa jinsi katiba ilivyo anaweza kuwa dikteta (hata kama yeye sio), akitokea mwingine akaamua kuwa dikteta wa ukweli itakuwaje? Kwani mrekebisho yasifanyike kuondoa hilo kwa sasa?Hebu ifike mahli tufikirie kupiga hatua kwenda mbele na sio kubaki pale tulipo au kurudi nyuma.
 
Back
Top Bottom