Wananchi wavamia ofisi ya serikali, waua mtuhumiwa

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,319
33,125
headline_bullet.jpg
Wanne wauawa Dar, Polisi waua wawili
headline_bullet.jpg
Yumo anayedaiwa kuiba mpunga.



Pinda%2824%29.jpg

Waziri Mkuu Mizengo Pinda.



Matukio ya watu kujichukulia sheria mkononi na polisi kuua raia yameendelea kushika kasi ambapo watu watano wameuawa katika matukio matatu.
Katika tukio la kwanza, wakazi wa kijiji cha Saragurwa, kata ya Chigunga wilayani Geita, Mkoa wa Mwanza, wamevamia na kuvunja ofisi ya serikali ya kijiji hicho, kisha kumuua mtuhumiwa wa wizi wa magunia ya mpunga aliyekuwa amekimbilia ofisini humo kujificha.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Simon Sirro, aliithibitishia Nipashe kutokea kwa tukio hilo na kumtaja kwa jina moja mtuhumiwa aliyeuawa na wananchi hao kwa tuhuma za kuvunja ofisi ya kijiji kuwa ni Deus (35), mkazi wa kijiji hicho.
Kamanda Sirro alisema kuwa tukio hilo lilitokea jana majira ya saa moja asubuhi ambapo mtuhumiwa huyo alidaiwa kuiba magunia matatu ya mpunga akishirikiana na mwenzake ambaye alitoroka kabla ya kukamatwa na kwamba magunia ya mpunga yalioibiwa ni mali ya Selestine Raurent, ambaye alikuwa ameyahifadhi katika ghala hilo.
Kamanda Sirro alisema hakuna mtuhumiwa aliyekamatwa kuhusiana na tukio hilo, lakini alitoa onyo kwa wananchi wenye tabia ya kujichukulia sheria mkononi kuacha mara moja tabia hiyo kwa kuwa wanavunja sheria za nchi.
Mwenyekiti wa kijiji hicho, Patrick Cosmas, alisema watuhumiwa hao walidaiwa kuiba magunia matatu kati ya 12 yaliyokuwa yamehifadhiwa na kwamba tayari walikuwa wamekwishachukua matatu na ndipo mmiliki wake alishtuka usingizini majira ya saa 11 alfajiri.
Cosmas alisema mmiliki wa mpunga huo aliposhtuka na kupiga kelele za kutaka msaada, watuhumiwa walikimbia, lakini wananchi waliendelea kufuatilia hadi nyumbani kwa marehemu na kuyakuta magunia matatu huku yeye akikimbia kujificha kwa mke mdogo.
Kwa mujibu wa Cosmas, umati wa wananchi ulimfuata na kumtaka atoke ndani ya nyumba, lakini akagoma.
Alisema baadaye marehemu alitoka na kukimbilia ofisi ya kijiji iliyopo karibu na kuvunja mlango na kujifungia ndani.
Baadaye umati wa wananchi uliizingira ofisi hiyo na kumtaka marehemu atoke huku wengine wakimshambulia kwa mawe na yeye kujibu mapigo hayo kwa kuwarushia mawe, kitendo kilichowaongezea hasira na baadhi walianza kuvunja madirisha na kuanza kumpiga kwa mawe hadi kumuua.
Pamoja na kumuua mtuhumiwa huyo, wananchi hao waliharibu mali kadhaa za ofisi hiyo ziwemo meza, kabati na viti pamoja na baadhi ya nyaraka muhimu za serikali zilizokuwa zimehifadhiwa ofisini humo.
Katika tukio lingine, Jeshi la polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam wameua watu wawili kwa tuhuma za ujambazi na kuwakamata wengine 34 katika operesheni ya wiki moja iliyofanyika maeneo ya pembezoni mwa Jiji.
Kamanda wa Polisi wa kanda hiyo, Suleiman Kova, alisema jana kuwa watuhumiwa hao waliuwawa Jumamosi iliyopita wakati wakirushiana risasi na polisi.
Aliwataja watuhumiwa hao waliouawa kuwa ni Willy Haruna maarufu kama ‘Akon’ ambaye alikuwa kiongozi wao na mwingine aliyefahamika kwa jina moja la Ambrossy.
Alisema tukio hilo lilitokea siku hiyo usiku muda mfupi baada ya polisi kupata taarifa dhidi ya watuhumiwa hao waliofika eneo hilo kwa lengo la kutaka kupora mali kwenye nyumba mbili pamoja na duka.
Alisema baada ya kupata taarifa hiyo, polisi iliweka mtego wake eneo hilo ambapo watuhumiwa wawili wa ujambazi walifika hapo wakiwa na pikipiki.
“Baada ya muda kidogo watuhumiwa wengine watatu waliongezeka na walipowaona polisi walianza kuwafyatulia risasi ambazo zilipelekea nao (polisi) kujibu mashambulizi, katika zoezi la kurushiana risasi watuhumiwa wawili walifariki dunia na wengine watatu kufanikiwa kukimbia na juhudi za kuwasaka zinaendelea,” alisema.
Kova amewaomba wamiliki wa zahanati pindi wanapofika wagonjwa wenye majeraha yasiyoeleweka watoe taarifa polisi badala ya kuwapa huduma.
Alisema katika uchunguzi wao, wamebaini kuwa watuhumiwa hao wamekuwa wakifanya vitendo vya kihalifu Tanzania Bara na Zanzibar.
Alisema silaha iliyokuwa ikitumiwa na watuhumiwa hao wamefanikiwa kuikamata ambayo ni bunduki aina ya SMG iliyokuwa na magazine yake yenye risasi saba.
Pia alisema katika eneo hilo walifanikiwa kuyapata maganda kadhaa ya risasi pamoja na kulipata begi la watuhumiwa hao ambalo ndani yake kulikuwa na bisibisi na panga.
Alisema uchunguzi zaidi juu ya tukio hilo unaendelea ikiwa ni pamoja na kuwasaka watuhumiwa watatu waliokimbia.
Katika tukio lingine, watuhumiwa wengine 34 wanaodaiwa kujihusisha na vitendo vya ujambazi wanashikiliwa na jeshi hilo.
Kova alisema watuhumiwa hao walikamatwa katika operesheni maalum iliyoanza wiki iliyopita maeneo mbalimbali jijini Dar es Salaam.
Alisema maeneo hayo ni Mbezi Makabe, Mbezi Luis, Kimara, Tegeta, Boko, Pugu na Vingunguti.
Alisema watuhumiwa hao wamegawanyika katika makundi matatu tofauti na kwamba upelelezi dhidi yao unaendelea kufanyika.
Hata hivyo, Kamanda Kova alikataa kuyataja majina yao kwa maelezo kuwa upepezi utaharibika.
Alisema watuhumiwa hao tayari wameshawataja wenzao waliokuwa wakishirikiana nao.
Wakati huo huo, watu wawili wameuawa kwa kupigwa na kuchomwa moto na watu wanaodaiwa kuwa waendesha pikipiki eneo la Goba mwisho wilayani Kinondoni Mkoa wa Dar es Salaam.
Tukio hilo lilitokea mwishoni mwa wiki katika eneo hilo nje ya ofisi ya serikali ya mtaa na kushuhudiwa na viongozi wa mtaa huo na wananchi.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Elias Kalinga, watu hao waliuawa na watu wanaodaiwa kuwa waendesha pikipiki.
Kalinga alisema jana kuwa usiku wa kuamkia Jumamosi iliyopita, mmoja wa waendesha pikipiki alitaka kuporwa chombo hicho baada ya kuchomwa kisu shingoni, hatua ambayo iliwapa hasira wafanyabiashara ya pikipiki na kuanza kuwasaka watuhumiwa.
Alisema Jumamosi mchana, waendesha pikipiki walifanikiwa kuwakamata watu ambao hata hivyo hawakuwa na uhakika kama ndiyo waliohusika katika jaribio la uporaji huo kwa kuwa lilitokea usiku ambapo baada ya kuwakamata walianza kuwapa kipigo hadi kuwaua.
Hata hivyo, katika jaribio hilo la uporaji huo, waporaji hawakufanikiwa kuchukua pikipiki baada dereva kupiga kelele na wao wakaamua kutimua mbio.
Watu hao waliuawa baada ya kukamatwa na kupewa kipigo hadi walipofikishwa Goba mwisho kabla ya mmoja kuchomwa moto na mwingine kuuawa kwa kupigwa na mawe, matofali pamoja na vitu vyenye ncha kali kichwani.
Baada ya kutekeleza mauaji hayo wananchi wote wakiwemo waendesha pikipiki walitawanyika na kuwaacha viongozi wa serikali ya mtaa wakilinda maiti kabla ya polisi kufika na kuchukua maiti.
Imeandikwa na Renatus Masuguliko, Mwanza, Richard Makore na Romana Mallya, Dar.



CHANZO: NIPASHE
 
Serikali iache kukoroma tumechoka kusikia habari hizi. Hivi ni kweli mpaka sasa serikali haijashtuka kuwa hali hii inatisha? Polisi wanaua raia wakisema ni majambazi, raia wanavamia ofisi za serikali na vituo vya polisi na kuua watuhumiwa, wananchi wanaua watu wanaowadhania ni wezi, mkuu wa mkoa anamfukuza ofisini mwenyekiti wa baraza la ardhi na nyumba la mkoa, mkuu wa mkoa anafukuza kazi mhandisi wa jiji, madiwani wanampinga mkuu wa mkoa kwa hilo kwa nguvu moja etc . Hii inaashiria kuwa tuendako sio kuzuri kabisa ni kuwa hakuna utawala wa sheria na badala yake kuna anarchy.

Katika jamii yoyote ya kistaarabu utawala wa sheria ni muhimu sana!
 
Back
Top Bottom