nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Burhani Yakub, Tanga
WAKAZI wa Kijiji cha Kwedikwabu, Kata ya Kwamsisi, wilayani Handeni, wamemuomba Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Chiku Gallawa kuingilia kati sakata la mwekezaji mmoja kutoka Dar es Salaam kuvamia eneo lao lenye ukubwa wa ekari 2,000.
Akizungumza kwa niaba ya ujumbe wa wanakijiji hao waliofika ofisi za gazeti hili mjini hapa, Ramadhani Bakari alisema walishtuka baada ya kuona watu wakifyeka eneo kutayarisha shamba hatua iliyowalazimisha kuwafukuza.
Tulishtuka baada ya kuona kuna watu porini wakifanya kazi ya kufyeka, tulipowakamata walimleta mwekezaji huyo ambaye alijitetea kuwa, ameuziwa na mzee mmoja wa kijijini tukamwambia umetapeliwa kwa sababu hukufuata taratibu, alisema Bakari.
Alisema walipomfukuza alirejea Dar es Salaam, lakini baadaye alirudi tena kijijini na kuanza kufyeka huku akisisitiza kuuziwa eneo hilo.
Bakari alisema baada ya kurejea tena kijijini, wananchi waliomba uongozi wa kijiji kuitisha mkutano mkuu ambao uliamua kumkataa mwekezaji huyo, huku akipewa amri ya kuondoka mara moja.
Akizungumzia suala hilo kwa simu, Mtendaji wa kijiji hicho, Juma Shaaban alikiri wanakijiji kumkataa mwekezaji huyo katika mkutano huo kwa kupiga kura nyingi za kutaka aondoke.Shaaban alisema baada ya uamuzi wa mkutano mkuu wa kijiji aliwasiliana na Polisi Kituo cha Mkata, walipelekwa askari na kumuamuru aondoke kwani wanakijiji hawamtaki.
Mkutano mkuu wa kijiji ulifanyika Julai 8, mwaka huu wananchi walipiga kura nyingi za kumkataa, nikapeleka taarifa hadi kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Handeni,alisema.
Chanzo: Mwananchi