Wanafunzi Ardhi watangaza mgomo

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
Bunge la Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Ardhi, limetoa baraka zote kwa wanafunzi wa chuo hicho kuanza mgomo wa kuingia madarasani leo.
Mgomo huo ambao haijulikani utaisha lini, unalenga kuishinikiza serikali kusikiliza kilio cha wanafunzi hao na kuweka sawa mambo matano, likiwamo la kutopata fedha za mkopo kwa mwaka ujao wa masomo.
Azimio la mgomo huo lilipitishwa kwa kauli moja katika mkutano wa Bunge la Wanafunzi hao, uliofanyika jijini Dar es Salaam jana jioni, chini ya Spika wake, Emmanuel Jikora.
Sababu nyingine ya mgomo huo, ilidaiwa na wanafunzi hao kuwa ni uongozi wa chuo, Idara ya Mkurugenzi ya Shahada ya Kwanza kuendelea kukaa kimya kuhusu hatma yao juu ya wapi wanafunzi watalala hasa wa mwaka wa kwanza, ambao tayari wapo chuoni.
Baadhi ya wawakilishi wa wanafunzi hao walifika katika ofisi za gazeti hili jana asubuhi na kusema hatua hiyo ni ya mwisho kwao, hasa baada ya serikali kwa zaidi ya miaka mitano sasa tangu chuo kipate hadhi ya Chuo Kikuu kinachojitegemea, kupuuza maombi yao ya kufanyika marekebisho katika utoaji wa fedha za mikopo kwa wanafunzi.
“Inashangaza sana kuona hadi sasa hakuna mwanafunzi hata mmoja, wakiwamo wa mwaka wa kwanza, ambaye amepata fedha za mkopo kwa ajili ya mwaka ujao. Tukiwasiliana na Bodi ya Mikopo, tunaambiwa majina yetu hayajafika, lakini uongozi wa chuo unadai yametumwa, sasa sijui tushike lipi,” alihoji mmoja wa wawakilishi hao.
Alisema kwa kawaida mkataba wa fedha za mikopo huwa kati ya mwanafunzi na Bodi, lakini hadi fedha zitolewe ni lazima uongozi wa chuo uthibitishe kwa Bodi, jambo ambalo limekuwa sawa na mchezo wa danadana hadi sasa.
Pia walidai kuwa serikali imeendelea kukaa kimya kuhusu hosteli za wanafunzi, hasa kutokana na ukweli kuwa chuo kina wanafunzi zaidi ya 2,800 wakati vyumba vilivyopo sasa vina uwezo wa kupokea wanafunzi 400 tu.
“Hata vyumba vilivyopo sasa miundombinu yake imechakaa, mabomba ya maji yamekufa, mifereji ya maji taka imefurika hali inayohatarisha maisha ya wanafunzi kiafya,” alilalamika.
Upungufu mwingine unaolalamikiwa na wanafunzi hao ni hatua ya uongozi wa chuo kupunguza muda wa mazoezi kwa vitendo nje ya chuo kutoka siku 80 hadi 54 kwa mwaka na kupitisha viwango sawa vya malipo ya fedha za nauli bila kujali umbali wa mkoa, ambako mwanafunzi anakwenda.
Kadhalika, wanafunzi wa chuo hicho wamedai watagoma kwa sababu uongozi wa chuo umeshindwa kutekeleza kwa vitendo uboreshaji wa vitambulisho vya wanachuo kutoka mfumo wa sasa wa karatasi na kadi inayolingana na hadhi ya chuo chenyewe.
“Katika hili unaweza usiamini ukiambiwa hadi sasa wanafunzi wa mwaka wa kwanza hawajapata hata hicho kitambulisho cha karatasi, licha ya Makamu Mkuu wa Chuo, Profesa Idrisa Mshorwa, kuahidi mbele ya wanafunzi mkutanoni kuwa angelifanyia kazi jambo hilo kwa muda mrefu sasa,” alisema.
Wanafunzi hao wamedai kasoro hizo na nyingine nyingi, zinakiweka chuo katika sura inayofanana na chuo kinachowaandaa wanafunzi kupata cheti au kama sekondari za kata za mijini, licha ya kwamba ni moja kati vyuo vikuu vinavyotarajiwa kuzalisha wataalam katika kada muhimu za ufundi.
Wakati huohuo, wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom), wamesitisha mgomo baada ya kukutana na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa.
Mgomo huo ulisitishwa huku serikali ikiutaka uongozi wa Udom kuhakikisha unaorodhesha majina yote ya wanafunzi wa mwaka wa tatu kwa ajili ya kupatiwa mafunzo kwa vitendo.
Agizo hilo lilitolewa baada ya wanafunzi wa Kitivo cha Sayansi ya Jamii chuoni hapo kugoma kushinikiza uongozi wa chuo kuwapatia fedha za mafunzo kwa vitendo.
Makamu Mkuu wa Udom, Profesa Idris Kikula, alisema agizo hilo lilitolewa katika kikao cha viongozi wa serikali pamoja na uongozi wa chuo kilichofanyika usiku wa kuamkia jana chini ya Waziri Dk. Kawambwa.
Katika hatua nyingine, uongozi wa wanafunzi wa Udom umetoa tamko la kusitisha mgomo kutokana na kutimiziwa kwa madai yao.
Akizungumza na waandishi wa habari, Rais wa Serikali ya Shirikisho la Wanafunzi, Saimon Bais, alisema wameamua kusitisha mgomo kutokana na kutimiziwa matakwa yao baada ya kikao kilichofanywa kati yao na Dk. Kawambwa.
Alisema matakwa hayo ni kukubaliwa kupatiwa mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi wa mwaka wa pili na watatu.
“Awali, baada ya Seneti ya Chuo kukaa na mimi nikiwa kama mjumbe katika kikao hicho, ilitoa maamuzi ya mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi wa mwaka wa kwanza tu, hali ambayo hatukukubaliana nayo na kuamua kufanya mgomo juzi,” alisema.
Alisema sababu kubwa ya kufanya mgomo ni kudai kwa muda mrefu mafunzo kwa vitendo ambayo uongozi wa chuo ulikuwa unaahidi bila kutekeleza.
Alisema hata waliohitimu mwaka huu hawajawahi kwenda kufanya mafunzo kwa vitendo kwa kitivo cha sayansi ya jamii ambapo takriban mitaala 16 ilikuwa haina mafunzo hayo.
Aidha, wameitaka serikali kuishauri menejimenti ya chuo kuwa na mahusiano mazuri na wanafunzi wanapokuwa na matatizo na kwamba mgomo umetokana na menejimenti kutokuwa karibu na uongozi wa serikali ya wanafunzi.
Imeandikwa na Muhibu Said na Abdul Mitumba (Dar) na Jaqueline Massano, Augusta Njoji na Paul Mabeja (Dodoma).
CHANZO: NIPASHE
 
Ni MZIMU WA CCM Kuchakachua Uchaguzi na Maoni ya Wasomi Dodoma ndio unaoendelea kupita vyuo Vikuu nchini. Bado kidogo na Vyama vya wafanyakazi waliopewa kebehi katika kudai kwao maslahi bora zaidi.

Uchakachuaji ni gharama kubwa sana kwa taifa eti, si lelemama hili hata kidogo!!!!
 
Back
Top Bottom