Waliofuja fedha Jiji Arusha wahamishwa

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Paul Sarwatt

Arusha

halmashauri.jpg



Jengo la Halmashauri ya Arusha


Ni watumishi 19 wa Hazina, Fedha, Ardhi na Biashara

Lyatonga Mrema asema dawa ni kuwashitaki, si kuwahamisha
Madiwani wajipanga kujadili ufisadi huo

SERIKALI imewahamisha kwa mpigo watumishi 19 wa Halmashauri ya Jiji la Arusha kwa madai ya kuhusika na tuhuma za upotevu na ufisadi wa fedha za miradi mbalimbali ya maendeleo katika kipindi cha miaka mwili iliyopita.

Taarifa zilizofikia Raia Mwema kutoka vyanzo mbalimbali ndani ya Halmashauri hiyo kwa wiki moja sasa zilieleza kuwa watumishi hao kutoka idara mbalimbali wamehamishwa kwenda katika Halmashauri nyingine za wilaya za mikoa ya Kanda ya Kaskazini katika kipindi cha kati ya Septemba na Oktoba mwaka huu.

Inaelezwa kuwa upotevu wa fedha hizo ambazo kiasi chake hakijajulikana rasmi uligunduliwa na maafisa wa Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Fedha za Serikali (CAG) pamoja na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa inayoongozwa na Mbunge wa Vunjo, Augustine Lyatonga Mrema.


Baadhi ya watumishi hao ambao Raia Mwema ilifanikiwa kupata majina yao ni pamoja na mmoja aliyeelezwa ya mkuwa alikuwa mweka hazina lakini kutokana na wizi huo ameshushwa kuwa mhasibu wa kawaida na wegine ambao kwa sasa majina yao gazeti hili halitayataja wanaotoka katika Idara za Fedha, Ardhi, Biashara na Hazina na tayari watumishi wapya wa kuziba nafasi zao wamekwishakuanza kuripoti ndani ya Halmashauri hiyo.


Habari zaidi zinanaleleza kuwa Serikali ilichukua uamuzi wa kuwahamisha watumishi hao baada ya kuchoshwa na kushamiri kwa vitendo vya ufisadi na matumizi mabaya ya fedha za umma zilizotengwa kwa miradi kadhaa ya maendeleo hasa katika kipindi cha Mwaka wa Fedha wa kuanzia 2008/9 na 2010/11.


"Katika kipindi cha miaka mitatu hivi Halmashauri ya Jiji la Arusha imepoteza fedha nyingi kutokana na watumishi kujihusisha na vitendo vya ufisadi kuanzia wakati wa kuaandaa bajeti, kusimamia miradi na utekelezaji wa miradi yenyewe," alisema moja wa maafisa wa Serikali mkoani Arusha.


"Katika kipindi hicho mabilioni ya fedha yamepotea kutokana watumishi waliohusika kujihusisha na vitendo vya ukwapuaji wa fedha zilizotengwa kwa miradi ya maendeleo hivyo kuathiri kwa kiasi kikubwa mipango ya Serikali katika kuwaletea wananchi wa Arusha maendeleo," aliongeza Afisa huyo.


Afisa huyo alieleza pia ya kuwa baadhi ya watumishi wanadaiwa kugeuza idara zao kama makampuni binafsi kwa kuongeza fedha katika miradi hewa pamoja na kuongeza kiasi kikubwa cha fedha katika mahesabu ya miradi husika na fedha zilizoongezwa kuingia katika mifuko yao.


Baadhi ya miradi ambayo inadaiwa kuwa utekelezaji wake uligubikwa na ufisadi ni pamoja na ukarabati wa Soko la Sanawari ambalo linadaiwa kugharimu kiasi cha shilingi milioni 400 huku kazi iliyofanyika ikionekana wazi kutofikia thamani ya fedha zinazoelezwa kutumika.


Mradi mwingine ambao unadaiwa kugubikwa na ufisadi ni ujenzi wa vizimba sita na paa moja katika Soko la Kilombero ambao umetumia kiasi cha shilingi milioni 400 ambacho kinatajwa kuwa ni kikubwa sana na hakiendani na thamani ya mradi wenyewe.


Aidha, taarifa zaidi zinaeleza kuwa wakaguzi pia wamegundua utata katika malipo ya shilingi 475,701,760.00 zilizotumika kutengeneza na kukarabati barabara na vivuko tisa kwa kiwango cha changarawe katika maeneo kadhaa ya Halmashauri ya jiji la Arusha.


Fedha za mradi mwingine unaolalamikiwa kwa ufisadi ni uendelezaji wa shughuli za utalii katika Mlima Suye uliopo Kata ya Kimandolu ambako inadaiwa kuwa mradi huo tayari umetumia zaidi ya shilingi milioni 60 huku wasimamizi wakiomba kuongezewa milioni 35 zaidi katika bajeti ya mwaka huu.


Taarifa zaidi zinaeleza kuwa kuna watumishi hasa wa idara ya fedha walifikia kuwa na vitabu vyao wenyewe vya kukusanya mapato kutoka vyanzo mbalimbali kama masoko, vyoo vya kulipia pamoja ushuru wa maegesho ya magari na fedha walizokusanya waliingiza katika mifuko yao binafsi badala ya kuingiza hazina ya Halmashauri.


"Kuna miradi mingi fedha zake zimetumika vibaya mpaka kufikia hatua ya viongozi wa juu wa Serikali kufikia uamuzi wa kuwahamisha kwa mpigo watumishi hao 19, kiasi cha fedha zilizopotea katika kipindi cha miaka mitatu kinakadiriwa kufikia bilioni zaidi ya tatu,"alieleza moja wa watumishi wa Halmashauri aliyeomba jina lake lihifadhiwe.


Mtumishi huyo aliongeza kuwa fedha nyingi zilitumika vibaya pia katika kipindi cha mwaka wa fedha 2010/11 kutoka na mgogoro wa kisiasa ulioikumba Halmashauri hiyo baada ya madiwani wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kususuia kuhudhuria vikao vya Halmashauri wakipinga uchaguzi wa nfasi ya Meya wa Arusha.


"Kutokana na madiwani wa CHADEMA kukosekana maamuzi mengi yalifanywa bila majadiliano ya kina hivyo kutoa mwanya kwa watumishi wasio waaminifu kutumia vibaya fedha za miradi kadhaa bila kuhojiwa na madiwani wa CCM ambao walikuwa wanahudhuria vikao,"alieleza mtumishi huyo.


Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Arusha Estomih Chang'a hakupatikana juzi kupitia simu yake ya mkononi kuelezea hatua ya kuwahamisha watumishi hao, na Afisa Utumishi Gerald Tesha, alipoulizwa kwa njia simu alikataa kuelesea chochote kwa maelezo kuwa yeye si msemaji wa Halmashauri.


"Siwezi kuzungumzia suala hilo kwanza kwa sababu sikufahamu, na pia si utaratibu wa taasisi za Serikali kwani mimi si msemaji wa hilo," alisema Tesha na kukata simu.


Akizungumzia uhamisho wa watumishi hao Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), Mrema alithibitisha kuwa ni kweli Kamati yake ilikagua hesabu za Halmashauri ya Jiji la Arusha na kugundua "madudu" mengi na halmashauri hiyo ilipata hati chafu ya ukaguzi.


Mrema hata hivyo, alipinga hatua ya Serikali ya kuwahamisha watumishi hao kwa kuiita kuwa ni mwendelezo wa kulea vitendo vya kifisadi ndani ya taasisi za umma badala ya kuwachukulia hatua za kisheria wahusika.


"Ni jambo linaloshangaza kuona kuwa Serikali imeendelea kufumbia macho ufisadi huo kwa zaidi ya muongo mmoja tangu ianze kupeleka ruzuku katika halmashauri na manispaa nyingi pamoja na kuundwa kwa wizara inayosimamia taasisi hizo, huku ukaguzi wa mahesabu ukioonyesha madudu kila wakati,"alisema Mrema.


Alisema kwa tafsiri iliyo rahisi watumishi hao walijihusisha na uwizi wa fedha za umma na hatua sahihi kama kweli Serikali ilikuwa na nia njema ni kuwafikisha katika mkondo wa sheria kwani ushahidi wa tuhuma za ufisadi huo ziko wazi.


Alisema kushamiri kwa vitendo hivyo ni ishara kuwa Serikali haina utashi wa kuvikomesha, kwani inaonekana wazi kuwa kuna mtandao mkubwa uliojengwa miongoni mwa watendaji wa Serikali Kuu na Serikali za Mitaa ambao unajishughulisha na ufisadi wa kupindukia wa fedha za wananchi.


"Kamati yangu ilikutana na Waziri wa Wizara hiyo George Mkuchika wiki iliyopita na tulimbana Waziri kuhusu vitendo vinavyofanywa na watumishi katika Halmashauri na Manispaa kadhaa nchini vitendo ambavyo vinahatarisha hata ustawi wa Taifa letu na Waziri aliahidi kuwa atalishughulikia lakini hili la uhamisho si njia sahihi," alieleza.


Mwenyekiti huyo wa LAAC pia aliyataka Mabaraza ya Madiwani katika Halmashauri zote nchini kukataa kuwapokea watumishi wanaodaiwa kuhamishwa kwao kwa sababu za kujihusisha na vitendo vya wizi wa fedha za miradi ya wananchi.


"Serikali inapochukua uamuzi wa kuwahamisha watumishi wanaojihusisha na ufisadi, je, ndiyo njia sahihi ya kuwarekeisha? Hapana hiyo si dawa, kwani hata huko wanakohamishiwa wanakwenda kufanya kazi zilezile zinazohusiana na kusimamia fedha za miradi ya maendeleo ya wananchi," alisema.


"Narudia tena kuwasihi Madiwani katika Halmashauri zao wasimame kidete kuwakataa watumishi wezi na hii itasadia Serikali kuzinduka badala ya kuwahamisha iwachukulie hatua za kisheria kwa kuwapeleka mahakamani,"aliongeza Mrema.


Naye Mjumbe wa Kamati ya Fedha katika Halmashauri ya Jiji la Arusha ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Sokon 1, Michael Kivuyo, alieleza kushitushwa kwake na madai yanayotolewa kuhusu upotevu wa fedha za miradi hiyo.


Alihoji Kivuyo: "Inasikitisha sana. Hii maana yake ni kwamba kuna baadhi ya maeneo wananchi watakosa huduma muhimu walizoahidiwa na Serikali kwa kuwa fedha zimepotea. Napenda kuweka wazi suala hilo tutalijadili katika kikao kijacho cha kamati yetu kwa kumhoji mkaguzi wa ndani imekuwaje ameshindwa kugundua ufisadi huo mpaka umekuja kufahamika kwa wakaguzi wa nje"?


Kwa muda mrefu Halmashauri ya Jiji la Arusha imekuwa ikilalamikiwa kuhusu matumizi mabaya ya fedha na kwa muda wote pamoja na Serikali kuwahamisha baadhi ya watendaji katika kutafuta dawa ya tatizo hilo, hatua hiyo haijaweza kusadia sana kwani ufisadi umekuwa kama "jadi" ya utendaji kazi katika Halmashauri hiyo.










 
hakutakuwa na mabadiliko yeyote kama system yote haijabadilishwa, nani asiyejua wizi imeshakuwa kawaida nchi hii?
 
wewe iba kuku uone??
Wao fresh tu wanahamishiwa kuiba kwengine
 
Kwanini usitutajie majina yao?Tunataka kuwajua ni akina nani na wamehamishiwa katika halmashauri zipi
 
Back
Top Bottom