Waislamu wenzangu tujenge shule sahauni kurudishiwa za serikali-jakaya m kikwete

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,720
21,779
PENGINE HILI LITAWAFUMBUA MACHO KWA KUKUMBUKA ALIOSEMA RAIS ALIEPITA MH MWINYI
SRC HABARI LEO
WAISLAMU wameshauriwa kujenga shule zingine badala ya kutarajia kurudishiwa zilizotaifishwa na Serikali.

Ushauri huo ulitolewa na Rais Jakaya Kikwete wakati akihutubia Baraza la Iddi lililofanyika kitaifa mkoani Dodoma jana na hotuba yake kurushwa moja kwa moja na vituo vya redio na televisheni.

“Tukirudisha shule zote hizi kwa wenyewe, Serikali itakosa shule na itazua malalamiko ndiyo maana tuliamua kuziboresha shule hizo badala ya kuzirejesha.

Ushauri wangu kwenu fikirieni kuwekeza katika shule na vyuo vipya,” alisema na kufafanua kuwa suala la kurejesha shule kwa Bakwata litazua mgogoro mkubwa.

Rais Kikwete aliwaambia Waislamu katika Msikiti wa Gaddafi, kwamba suala hilo haliwezekani kwani malengo ya kutaifisha yalikuwa ni kila mtoto wa Mtanzania bila kujali dini na rangi yake, apate elimu inayotolewa na Serikali yake.

Alisema kwa kuwa Serikali haikuwekeza katika ujenzi wa shule kwa kipindi kirefu, shule zilizotaifishwa ndizo zinaisaidia kuwa na shule kwa ajili ya wananchi wote; hivyo akawashauri Waislamu kujenga shule na vyuo vikuu vipya ambavyo havitataifishwa tena.

Ushauri huo ulitokana na risala ya Waislamu hao kutaka warejeshewe shule zao ili waziendeshe wenyewe na watoto wao wapate kusoma kwa kiwango cha kutosha.

Rais pia alitumia fursa hiyo kukanusha madai ya waumini ya dini hiyo kuwa wametengwa na Serikali katika masuala ya maendeleo na kuwahakikishia kuwa Serikali inapenda kuwa na uhusiano mzuri na dini zote na haipendelei kundi lolote.

Rais Kikwete alisema Serikali inashirikiana na Waislamu kama moja ya makundi ya dini nchini kama inavyofanya kwa mashirika mengine ya kidini.

Alitoa jibu hilo baada ya Waislamu kudai kuwa Serikali imekuwa inawawezesha zaidi Wakristo katika mambo ya kiuchumi na kuwaweka Waislamu katika kundi la pili.

Walionya kuwa suala hilo linaweza kusababisha kuvunjika kwa amani kwani Tanzania ni ya wote.

“Tendeni haki sawa na sisi kwa muda mrefu tunalalamika Waislamu hawatendewi haki,” ilisema risala hiyo iliyokuwa na shutuma kuwa Serikali inawezesha makanisa mabilioni ya fedha za umma na kuwaacha Waislamu kuwa watazamaji.

Katika eneo hilo Waislamu walitoa mfano wa makubaliano ya Serikali yaliyofikiwa na makanisa mwaka 1992 kuwa Serikali iwe inatenga nafasi za masomo katika vyuo vya ualimu na vyuo vikuu, kwa ajili ya walimu ambao watakwenda kufundisha kwenye shule za mashirika ya dini hizo.

Katika hali hiyo Waislamu hao waliomba pia Serikali ifanye makubaliano na Bakwata kama ilivyofanya kwa mashirika ya kidini ya Kikristo ili kuondoa ubaguzi huo.

Akijibu hoja hiyo Rais aliwaambia Waislamu kuwa waache kunung’unika na badala yake nao waombe, kwani wenzao wanaowatuhumu waliomba wakapewa.

“Hakuna kitu ambacho Serikali itafanya kwa dini moja na ikainyima dini nyingine. “Msilaumu, yule aliomba akapewa na kama na ninyi mna sifa, ombeni mtapewa na mkifanyiwa vinginevyo mna haki ya kudai na kutoa mfano mbona yule amefanyiwa,” alisema Rais Kikwete.

Alisema amefarijika kuona Bakwata imeamua kupeleka maombi kama yaliyofanywa na Baraza la Maaskofu na Jumuiya ya Kikristo.

“Mmechelewa tangu mwaka 1992 mnanung’unika tu kwa nini wale wamepewa, leteni hayo maombi yatashughulikiwa kwa taratibu zilizopo.”

Rais Kikwete alisema Tanzania haina dini ya kiserikali ambayo kila mtu lazima aifute, hivyo akawataka Watanzania kuendelea kuheshimu dini za wenzao.

Alisema inasikitisha kusikia viongozi wa dini moja wanakashifu viongozi wa dini zingine, jambo alilodai linajenga uhasama na matokeo yake ni uvunjifu wa amani.

Alihoji: “Hivi hamwezi kuendesha shughuli zenu za kidini bila kukashifu dini za wengine? Liacheni hili kwani ajizi yenu inaweza kuleta maafa katika Taifa.”

Alishauri ili kuondoa msuguano kati ya dini moja na nyingine, madhehebu yaweke utaratibu wa kukutana mara kwa mara na kuzungumza kasoro zao na masuala yanayoisibu nchi.

Alilizungumza hilo baada ya kuelezwa na Waislamu hao, kuwa makovu ya kidini yaliyojitokeza wakati wa uchaguzi mkuu bado hayajapatiwa ufumbuzi na Serikali.

Kuhusu kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi ambako pia jana Waislamu walilalamika kuwa Serikali inalegalega kulishughulikia suala hilo, Rais Kikwete alisema hakuna kulegalega, kwani suala hilo liko kwenye Kamati ya Serikali na Bakwata chini ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.

Ila aliwaambia Waislamu, kuwa Serikali haina kipingamizi cha kuanzishwa kwa Mahakama hiyo, ila haiwezi kugharamiwa wala kuendeshwa na Serikali, kwani hiyo ni sehemu ya ibada ya dini moja.

Alisema msimamo huo wa Serikali umetokana na ushauri wa Tume ya Kurekebisha Sheria iliyoko chini ya Profesa Ibrahim Juma wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

“Suala hapa … haliwezi kuwa mikononi mwa Serikali, kwani ni ibada ya Kiislamu,” alisema Kikwete na kuwaambia kuwa Kamati hiyo iko pale kuona chombo kitakachoundwa hakiendi nje ya misingi ya dini na wala hakishughuliki na kesi za jinai na za madai.

Akizungumzia suala la kupeleka mahujaji kuhiji Makka na Madina, Rais Kikwete alikemea taasisi za kitapeli zinazosafirisha waumini lakini wakakosa huduma muhimu za kula, kulala na hata safari ya kurudi nyumbani.

Alishauri Bakwata na taasisi zinazosafirisha mahujaji, kuandaa vigezo vitakavyofuatwa na taasisi yoyote na kila taasisi ili kuepusha usumbufu unaowapata baadhi ya mahujaji.

Aliwashauri pia kushirikiana kusafirisha mahujaji nje ili kuepuka gharama kubwa inayotozwa kwa mtu mmoja mmoja.

Kuhusu suala la Katiba mpya ambalo Waislamu hao walitaka washirikishwe tangu mwanzo, Rais Kikwete aliwahakikishia kuwa viongozi wa dini na waumini wao watashirikishwa kwa kila hatua, ila akatoa angalizo kwa waumini hao, kuwa wasigeuze mchakato wa Katiba kama mdahalo au malumbano kati ya Waislamu na Wakristo na kuingiza maslahi ya dini zao katika Katiba mpya.

Alisema itakapotokea mvutano wa namna hiyo, itakuwa ni ngumu kupata majibu na kuna hatari ya kuikosa hata hiyo Katiba mpya.

Alionya kuwa ikifikia hatua hiyo, pia kuna hatari ya amani kuvunjika na unaweza kuwa mwanzo wa umoja uliodumu kwa nusu karne kumomonyoka na ikawa vigumu kuurejesha.

Katika hotuba yake ya jana Rais pia alizungumzia suala la dawa za kulevya, baada ya risala ya Waislamu hao kuitaka Serikali iwataje wanaojihusisha na biashara hiyo haramu badala ya kuishutumu na kuwakashfu viongozi wa Bakwata, kuwa wamo kwenye mtandao wa biashara hiyo.

Rais akijibu hoja hiyo, alisema atakuwa mtu wa mwisho kuwakashfu na kuwadharau viongozi wa dini na nia yake ya kusema kuna baadhi vya viongozi wa kidini wanajihusisha kwenye biashara hiyo chafu, ilitokana na kupewa taarifa za uchunguzi zilizofanyiwa kazi na kikosikazi cha kupambana na dawa za kulevya.

Alisema baada ya uchunguzi huo, ilimlazimu yeye kama kiongozi wa nchi, kutoa tahadhari kwa viongozi wa dini ili wawaambie na kuwaonya waumini wao ambao wanajihusisha na biashara hiyo.

Alisema alifanya hivyo kwani viongozi wa dini wana ushawishi mkubwa wa kukutana na kundi kubwa la watu.
 
mkuu unafikiri waislam wana uwezo kama huo?labda tusubiri next generation tuone kama wanaweza kubadilika
 
Back
Top Bottom