Wachimbaji watoboa siri ya namna madini yanavyoibiwa

Mallaba

JF-Expert Member
Jan 30, 2008
2,554
47
Wachimbaji wadogo wa madini ya almasi katika mikoa ya Shinyanga na Mwanza wamefichua siri ya jinsi wanunuzi wanaoingia nchini kutoka nje wanavyoshiriki kuliibia taifa mabilioni ya fedha kwa kukwepa kulipa mrabaha na kodi ya madini hayo wanayonunua kutoka kwa wachimbaji hao.

Aidha, wachimbaji hao wamedai kuwa wanunuzi hao wamekuwa wakitoa bei "kiduchu" kwao ambapo wanunuzi hao hujipatia faida kubwa huku serikali ikikosa mapato yake halali, wameishauri serikali kuwajengea uwezo mkubwa wanunuzi wazalendo kwa kuwapatia mikopo ili waweze kununua madini hayo kwa manufaa ya nchi na siyo hao wanaoyapora na serikali kukosa kodi na mrabaha.

Hayo yameelezwa na wachimbaji hao kwa nyakati tofauti wakati walipokuwa wakieleezea hali halisi ya ugumu wa maisha ya wachimbaji licha ya kujikita katika sekta ya kuchimba madini hayo katika maeneo ya Mwanangwa Wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza na Maganzo wilayani Kishapu mkoani Shinyanga na kuelezea baadhi ya siri za wanunuzi hao wanaoingia nchini kwa vibali vya kuishi kwa muda kama wawekezaji na kupewa leseni za kati lakini wamekuwa wakitumia njia za panya kutorosha madini na kukwepa kulipa kodi na mrabaha bila serikali kujua.

Wakizungumza na NIPASHE kwa niaba ya wachimbaji wenzao mapema wiki hii wachimbaji hao majina yamehifadhiwa walitoboa siri hiyo kufuatia almasi kubwa ambayo wao huita (ng'hana) kupatikana katika eneo la Mwanangwa likiwa na kareti 166 na wachimbaji kulipwa sh milioni 50 tu kwa mmoja wa wanunuzi hao wa kati kutoka mjini Shinyanga jina na nchi anayotoka vimehifadhiwa ambaye haijafahamika ni wapi alipopewa kibali cha kuuza na nchi gani ilikouzwa almasi hiyo yenye thamani kubwa.

Habari kutoka moja ya ofisi ya madini imedai kuwa almasi hiyo inakadiriwa kuwa na thamani ya shilingi bilioni tatu ambapo kabla ya kupewa kibali na nyaraka muhimu kutoka ofisi ya madini alikopewa leseni, mnunuzi hupaswa kulipa asilimia tano ya (mrabaha) thamani ya mauzo ya almasi na kodi ya asilimia 35 kwa faida iliyopatikana baada ya mauzo halali ya almasi inayouzwa.

Baadhi ya wanunuzi wa kati wenye leseni za kununua madini hayo hapa nchini wanaojishughulisha na ununuzi wa madini hayo katika mikoa hiyo wamedai kuwa mbali ya kuwapunja wachimbaji hao pia kuna dalili za uwezekano mkubwa kuwa almasi hiyo imetoroshwa na kupitia njia za panya huku ofisi za madini ziwa na magharibi zikiwa zimelala "usingizi wa pono' kwa kutojua nini kinachoendelea juu ya upatikanaji wa almasi hiyo ambayo ingekuwa ni hazina ya nchi ndani ya benki kuu. Alisema mnunuzi mmoja mzalendo.

Juhudi za kumpata mnunuzi huyo mwenye asili ya Kiasia anayedaiwa kuwa na ofisi yake Mjini Shinyanga ziligonga mwamba licha ya NIPASHE kwenda mara tano kwa siku tofauti ofisini kwake bila mafanikio huku wasaidizi wa ofisi yake akiwemo mdogo wake akijikanganya kwa majibu kuwa Mkurugenzi huyo ambaye ndiye msemaji wa kampuni akiwa safarini nje ya nchi.

CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

HII NDIO NCHI YETU, WACHACHE SANA NDIO WANAOFAIDIKA HUKU WANANCHI WAKIFA NA UMASIKINI.
 
wachimbaji hao wamedai kuwa wanunuzi hao wamekuwa wakitoa bei "kiduchu" kwao ambapo wanunuzi hao hujipatia faida kubwa huku serikali ikikosa mapato yake halali, wameishauri serikali kuwajengea uwezo mkubwa wanunuzi wazalendo kwa kuwapatia mikopo ili waweze kununua madini hayo kwa manufaa ya nchi na siyo hao wanaoyapora na serikali kukosa kodi na mrabaha.
 
Back
Top Bottom