Wabunge wajiandaa kumkimbia Kikwete

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,792
287,994
Wabunge wajiandaa kumkimbia Kikwete

Mwandishi Wetu Julai 9, 2008
Raia Mwema~Muungwana ni Vitendo

Wachoshwa na chama kulinda mafisadi

Wasisitiza kung’oka kwa Makamba

BAADHI ya Wabunge wa Chama cha Mapinduzi (CCM) sasa wanaelezwa kuanza kukichoka chama chao kinachoongozwa na Mwenyekiti wao, Rais Jakaya Kikwete, kutokana na chama hicho kuendelea kuimarisha mtandao wa kifisadi, Raia Mwema limefahamishwa.

Baadhi ya wabunge waliozungumza na Raia Mwema kwa siku kadhaa sasa wameelezea hali hiyo na wengine sasa wanataka kuwapo kwa wagombea binafsi katika uchaguzi mkuu ujao wa 2010 ili “hali ikiwa mbaya zaidi” wanaowataka wajiondoe na kugombea kama wagombea binafsi.

Katika hali inayoashiria kwamba hali inaendelea kuwa mbaya ndani ya chama hicho chenye mtandao mkubwa nchi nzima, baadhi ya wabunge hao wanadiriki kusema kwamba hawana uhakika wa kurejea tena bungeni baada ya 2010 kutokana na kufanyiwa mizengwe na kuandaliwa kwa watu na fedha nyingi katika majimbo yao.

“Kwa kweli sasa tumechoka na CCM, haiwezekani kuwa na chama ambacho kinashindwa kuwadhibiti mafisadi kuanzia ngazi ya chini kabisa ya utawala hadi ngazi ya juu. Tulijua sasa watu wenye rekodi mbaya ya maadili hawawezi kupata nafasi katika chama, lakini sasa ni kinyume,” anasema mmoja wa wabunge hao.

Mbunge huyo anasema watu ambao wamewahi hata kuhukumiwa vifungo na baadhi wanaotuhumiwa makosa ya kijinai na kesi zao ziko katika upelelezi wanapata nafasi katika chama kwa vigezo vya fedha na uhusiano wao na baadhi ya wakubwa wenye malengo makubwa ya kisiasa.

Katika kudhihirisha kuwa hali bado si shwari, mbunge mwingine ameliambia Raia Mwema, kwamba Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete, alipoingia madarakani alitamka wazi kwamba atahakikisha anaweka misingi ya kuepusha kuwa na viongozi wachafu katika chama, lakini sasa anaangushwa na wasaidizi wake katika ngazi zote.

Mbunge mwingine ameliambia Raia Mwema kwamba uongozi wa chama hicho kuanzia shina hadi taifa umekua ukijenga mazingira ya kuhalalisha rushwa kwa wanaotaka uongozi, hali ambayo inazidi kuimarisha mizizi ya kifisadi katika ngazi zote za CCM na serikali yake.

“Kama tunaanza kupokea mafisadi sasa katika ngazi zote za chama, huo ndio mwanzo wa kusimika mafisadi katika ngazi zote za utawala kwa kuwa watakaoingia kwa fedha katika ngazi ya chini, watahakikisha wanarudisha fedha zao kwa njia ya rushwa na watapokea kutoka kwa watu wachafu wanaotaka madaraka, hatutashinda hii vita ya ufisadi bila kuangalia ngazi ya chini,” anasema.

Mbunge huyo alisema kwa sasa ubunge imekua ni sawa na biashara ambayo ina gharama kubwa kuiendesha kwa maelezo kwamba kwa sasa viongozi wa chama ngazi ya shina, kata, wilaya, mkoa na hata taifa wamekua wakiwategemea kwa mapato hata kwa mambo binafsi, kinyume chake utajengewa chuki.

Tayari baadhi ya wabunge wamekua wakitaka kufanyika kwa marekebisho makubwa katika uongozi wa juu wa chama hicho ikiwa ni pamoja na kumuondoa katika nafasi yake, Katibu Mkuu wake, Yusuf Makamba, ambaye pia ni mbunge mwenzao aliyeingia kwa tiketi ya kuteuliwa na Rais.

Hata hivyo, habari zinaeleza kwamba baadhi ya watu walio karibu na Makamba, walipinga kuondolewa kwake kwa madai kwamba itaibua makundi ndani ya chama hicho na badala yake baadhi walipendekeza kiongozi huyo atangaze kujiuzulu nafasi yake kutokana na umri na maradhi. Makamba alilazimika kwenda kutibiwa nchini India hivi karibuni baada ya afya yake kuzorota.

Hatua ya hivi karibuni ya ‘ukigeugeu’ wa uongozi wa juu wa CCM kuhusu mapokezi yaliyofanywa kwa wabunge waliopoteza nafasi zao kutokana na kashfa za ufisadi kwa kusema kwamba wana haki ya kupokewa katika majimbo yao lakini chama hicho kilishindwa kutoa maelezo ya kuhusika kwa viongozi wake wa juu wa mikoa ya Arusha, Mwanza na Shinyanga.

Walioandaliwa mapokezi ni pamoja na Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa na aliyekua Waziri wa Miundombinu, Andrew Chenge, ambao wote walihusishwa na kashfa za ufisadi na kulazimika kujiuzulu nafasi zao lakini waliandaliwa mapokezi makubwa na uongozi wa CCM majimboni mwao.

Hata hivyo, chama hicho mkoani Mbeya, kilipinga na kujiengua katika mapokezi ya Mbunge wa Kyela (CCM), Dk. Harrison Mwakyembe, ambaye yeye alikua Mwenyekiti wa Kamati Teule ya Bunge, iliyosababisha kuanguka kwa mawaziri watatu akiwamo Lowassa. Mwakyembe alipata wakati mgumu kutokana na CCM na serikali mkoani Mbeya kupinga mapokezi yake mkoani mwake pamoja na wananchi wengi kujitokeza na kumshangilia.

Mbali ya matatizo ndani ya mifumo ya uongozi ya chama hicho, wabunge waliozungumza na Raia Mwema kwa nyakati tofauti kuanzia mwezi uliopita, wameelezea wasiwasi wao pia katika chaguzi zinazoendelea sasa ndani ya jumuiya za chama hicho.

“Hivi sasa makatibu wa jumuiya za chama wamekua wakiandaa wagombea wao bila kujali mapungufu yao na sifa walizo nazo, kwa sababu tu wana fedha na zaidi kuna baadhi wamewahi kufungwa kwa kesi za jinai na wengine wanachunguzwa hadi sasa,” anasema mbunge mwingine aliyezungumzia chaguzi za jumuiya za chama hicho zinazoendelea sasa.

Imeelezwa kwamba baadhi ya wanasiasa wanaogombea nafasi katika jumuiya za chama hicho sasa wamewekeza mamilioni ya fedha wakilenga kuzitumia katika kuhakikisha wanashinda nafasi wanazoziomba, fedha ambazo bila shaka zitatumika katika utoaji wa rushwa.

Uchunguzi uliofanywa na Raia Mwema kwa muda mrefu sasa umebaini kwamba wana CCM wengi wanaowania nafasi mbalimbali katika jumuiya za chama hicho wana malengo ya kuchukua nafasi za uongozi katika vyombo vya dola ama kuwasaidia ‘wanaowafadhili’ kufanikisha malengo kama hayo.

Viongozi wa ngazi zote za jumuiya za chama hicho wanaingia katika vikao mbalimbali vya maamuzi vya chama hicho, vikao ambavyo ni muhimu katika mchakato wa chaguzi zote za uongozi serikalini, ikiwamo udiwani, ubunge na hata urais, jambo ambalo linawasukuma wanasiasa wote kuwekeza kwanza katika chaguzi za ngazi zote.

Mbali ya hayo, wenyeviti wa taifa wa jumuiya zote za CCM wanaingia moja kwa moja katika Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, kikao cha juu kabisa cha maamuzi cha chama hicho na hivyo wahusika wanasema “kuwa na mtu katika nafasi hiyo ni suala nyeti.’

“Kama wanasiasa wetu wangekua wanawekeza kwa kumwaga sera na kusaidia jamii, ingekua sahihi lakini kwa sasa wanachofanya ni kutumia fedha nyingi kutoa rushwa na kufanya kampeni chafu kusimika uongozi katika ngazi za chini na baadaye ngazi zote ikiwa ni kuimarisha mtandao ambao ni dhahiri utakua ni mtandao wa kifisadi,” anasema kiongozi mmoja mwandamizi wa CCM, Dar es Salaam, ambaye yuko karibu na chaguzi hizo.

Mfano dhahiri ni uamuzi wa uongozi wa Jumuiya ya Wazazi wilayani Kinondoni, uliopangwa kufanyika hivi karibuni kulazimika kuomba msaada wa Maafisa wa Taasisi ya Kumpambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU), kusaidia kudhibiti vitendo vya rushwa katika uchaguzi huo ambao hata hivyo uliahirishwa kwa “maagizo kutoka ngazi ya juu”.

Jumuiya nyingine za CCM ni Umoja wa Vijana (UVCCM) na Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), ambazo chaguzi zake zitaanza mara baada ya jumiya ya wazazi kumaliza ngazi kwa ngazi.

Habari zaidi zinaeleza kwamba baadhi ya wabunge wameandaliwa mikakati ya kuwang’oa katika nafasi zao na kuwasimika wale ambao watatimiza matakwa ya wale watakaowasimika baada ya wabunge hao kuonekana ‘kutokua na faida’ kwa baadhi ya wanasiasa wenye malengo makubwa ya kisiasa.

Kwa hali ilivyo wabunge wamegawanyika katika makundi yakielemea kwa watuhumiwa wa ufisadi na wengine kuonekana kupambana na watuhumiwa hao kwa gharama zote na hivyo kuzidisha ufa uliopo ndani ya Bunge hilo.

Katika vikao vya CCM hivi karibuni, kulikuwa na taarifa za mmoja wa wakongwe ndani ya CCM kutaka kuwasilisha hoja ya kuwafukuza chamani wabunge kadhaa waliojitokeza “kushupalia” tuhuma za ufisadi, hoja ambayo ingeweza kusababisha kuharakishwa kuanikwa hadharani kwa mpasuko unaoendelea sasa ndani ya chama hicho.

Hatua ya kuachiwa huru kwa wabunge wawili na kiongozi mmoja wa Umoja wa Vijana wa CCM mkoani Arusha, kumeelezwa kuwasha moto mwingine wa kutaka watuhumiwa wengine nao wafikishwe mahakamani ili kama hawana hatia wasafishwe na mahakama huku wengine wakidai kwamba “malengo ya tuhuma hizo yalikwishatimia.”

Wabunge hao na Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Arusha, na wanachama tisa wa CCM walifutiwa kesi ya rushwa iliyokuwa ikiwakabili baada ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) kueleza kwamba hana nia ya kuendelea na kesi hiyo kwa sababu za kisheria.

Wabunge hao ni Elisa Mollel wa Arumeru Magharibi na Lekule Laizer wa Longido, Mkoa wa Arusha, pamoja na Mwenyekiti wa UVCCM, Mkoa wa Arusha, Daniel ole Porokwa na wanachama wengine tisa wa chama hicho mkoani Arusha, ambao CCM iliwazuia kuendelea kuwa wagombea.

Wabunge hao wamewahi kusikika wakisema kwamba kama wao walivyonyimwa haki yao ya kugombea kwa “tuhuma za kutungwa” basi watuhumiwa wengine ambao baadhi Bunge limethibitisha tuhuma dhidi yao wavuliwe nyadhifa zao, hoja ambayo imewahi kufikishwa katika NEC.
 
hawana jipya hao wabunge wameshauza utu wao kwa sababu ya ubinafsi wao sasa wajichanganya tuu. tumewagundua vema 2010 ole wao... ama zetu au .....
jamani tusiendekeze ubwege, MWAKYEMBE katushutua MAPEMAAAAAA
Wabunge more than 80% wa sasa ni wa KUMWAGA 2010.
 
hawana jipya hao wabunge wameshauza utu wao kwa sababu ya ubinafsi wao sasa wajichanganya tuu. tumewagundua vema 2010 ole wao... ama zetu au .....
jamani tusiendekeze ubwege, MWAKYEMBE katushutua MAPEMAAAAAA
Wabunge more than 80% wa sasa ni wa KUMWAGA 2010.

Wanaona 2010 inazidi kusogea na nyota njema huonekana asubuhi, lakini huko CCM haijaonekana na wala hakuna dalili kama itaonekana. Hivyo wameanza kujibaraguza baraguza maana wnajua hasira za wananchi zitawafanya vibaya wengi wao.
 
As money hungry as they are, I don't think so... wengine huo ubunge au uwaziri ndio carreer waliyonayo tangu wakue, waking'atuka hawana pa kwenda watakufa njaa manake CV zao ziko tupuuuuuuuuuuuuuuuuuuuuuuuu, zaidi ya kada wa CCM. Kwa minajili hiyo basi, they are there to stay... hasa wakiongozwa na hii methali " Mtumikie kafiri upate mradi wako".
Its a painful truth, Puhhhhhhhhhhhh its a shame.
 
Tutawahukumu kwa matendo yenu.. hapa tupo kaika hukumu ya upelelzi ya matendo yenu, Na hakika mtavuna mlichopanda!
 
Wakulaumiwa hapa siyo wao(wabunge & mawaziri bwanyenye), wakulaumiwa hapa ni sisi, kwa kuogopa mabadiliko na hii ni kasumba ya mtanzania, tunaogopa kuchangua fulani mpya na mwenye sifa tuzitakazo kwa kuwa tunaogopa kupoteza fisadi na asiye na sifa tuliyemzoea, tuaogopa kumchangua fulani mwenye sifa na vigezo kwa kuwa bendera ya chama chake haina rangi tulizo zizoea, au labda ni zile kanga, na tshirt tunazopewa, moja kila baada ya miaka mitano.
 
Kama kweli wana nia ya kuitosa CCM, wajitokeze hadharani waziwazi sasa hivi. Haya mambo ya kusemea chinichini hatuwezi kuwa na uhakika nayo. Aidha wajitokeze tuwafahamu na malengo yao tuyajue, au wanyamaze kimya
 
Kama kweli wana nia ya kuitosa CCM, wajitokeze hadharani waziwazi sasa hivi. Haya mambo ya kusemea chinichini hatuwezi kuwa na uhakika nayo. Aidha wajitokeze tuwafahamu na malengo yao tuyajue, au wanyamaze kimya

MN, hakuna mwenye ubavu wa kutokea haddharani na hii ni kwa sababu ya unafiki wao. Wangekuwa wa kweli wa nafsi zao basi haya yote wangeyasema hadharani bila kificho.
 
lakini wahenga wanasema "kwenye msafara wa mamba kenge pia wamo" so may be kenge sasa wameamua kuanzisha msafara wao...tungoje coz hata roma haikujengwa kwa siku moja
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom