BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,790
- 288,007
Date::1/21/2009
Vyuo vikuu kuandamana kote nchini
*Wanapinga udahili mpya
Hussein Issa na Kuruthum Ahmed
Mwananchi
Vyuo vikuu kuandamana kote nchini
*Wanapinga udahili mpya
Hussein Issa na Kuruthum Ahmed
Mwananchi
WAKATI zoezi la kudahili wanafunzi likiwa linaendelea katika vyuo vya umma nchini, hali imebadilika baada ya mtandao wa wanafunzi Tanzania (TSNP) kutangaza maandamano nchi nzima yanayolenga kupinga udahili huo na yaliyopangwa kufanyika Jumamosi.
Mwenyekiti wa TSNP, Mulokozi Elgius aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa maandamano hayo, ambayo yamepangwa kuanzia mkoani Dar es Salaam, yatashirikisha wadau wa elimu nchini wakiwemo wazazi wa wanafunzi hao pamoja na wanafunzi wa wote wa elimu ya juu na wale wa shule za sekondari.
Elgius alisema maandamano hayo yataanzia Ubungo Mataa saa 3:00 asubuhi na kuishia viwanja vya Jangwani.
Alisema wamelitaarifu Jeshi la Polisi ili wapatiwe ulinzi na si kwamba wameomba kibali cha maandamano, hivyo akasema wana imani wanafunzi wote wataunga mkono maandamano hayo.
"Hapa tumeshatoa taarifa kwa Jeshi la polisi ili lituipe ulinzi... sasa ni jukumu lao. Likikataa, tunaendelea na maandamano ili waje watuue kama wanavyotaka," alisema.
Munishi Deogratius, mbunge wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam (Daruso) ambayo imetangazwa kuvunjwa na uongozi wa chuo, alisema maandamano hayo yana lengo la kupinga sera ya uchangiaji wa elimu ya juu, kuhitaji wanafunzi wote warudishwe vyuoni bila masharti yoyote.
"Lengo ni kulinda na kutetea maslahi ya wanafunzi hivyo hatuna nia ya ugomvi na serikali au polisi tunajua watakufa wengi lakini haki itendeke tu," alisema.
Serikali ilifunga vyuo vikuu saba vya umma baada ya wanafunzi kugomea masomo wakipinga sera ya uchangiaji elimu ya juu kwa madai kuwa mfumo unaotumiwa kujua uwezo wa mwanafunzi kiuchumi (means testing) ili apate mkopo unabagua na hivyo kutaka sera ifutwe, au wanafunzi wote wapate mkopo kwa asilimia 100.
Kamanda wa kanda maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema kuwa wameipata barua kutoka kwa wanafunzi hao, lakini akasema jeshi lake litatoa jibu lake kabla ya Januari 24.
"Hatuwezi kujibu leo kwani tunakaa nayo kwa masaa ishirini na nne ndio sheria ya jeshi la polisi linapoletewa maombi kama hayo, hivyo tutawajibu tu hamna tabu,"alisema Kova
Makamu mkuu wa UDSM, Profesa Lweikaza Mukandala alikataa kusungumzia suala hilo na badala yake akaelezea kuwa zoezi la udahili linaendelea vizuri na kwamba ulinzi ni mzuri.
Mukandala alikanusha habari kwamba chuo kinaongozwa kisiasa, akisema kuwa huo ni uzushi mtupu na kwamba chuo hakina dini wala chama.
Wakati huo huo Patricia Kimelemeta na Ellen Manyangu wanaripoti kuwa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimeeleza kusikitishwa na kitendo cha serikali kuwafutia udahili wanafunzi 2,000 wa UDSM na kuwakamata wanafunzi wanne kwa madai ya kuandamana kupinga kufutiwa kwa udahili wenzao.
LHRC imeitaka serikali kuangalia upya mfumo mzima wa uchangiaji elimu nchini na hasa kuipitia sera ya uchangiaji ili kupata mwongozo wa kutatua migogoro hiyo.
Mkurugenzi mtendaji wa LHRC, Francis Kiwango aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa iwapo itapitia upya sera hiyo, serikali itaweza kupata njia mbadala ambayo itasaidia kupunguza migogoro vyuoni.
Alisema migogoro iliyopo sasa inatokana na sera mbovu ya uchangiaji elimu ambayo ndio inayotoa mwongozo kuhusu ulipaji wa ada kwa wanafunzi. Alisema ili kutatua matatizo kama hayo, wajibu wa serikali ni kuhakikisha kuwa inawasaidia wanafunzi wote bila ya kuangalia tofauti na matabaka yao.
Alisema serikali imeshindwa kutafuta njia mbadala ambayo itasaidia kutatua tatizo hilo ndio maana inatumia nguvu za dola kuwatisha wanafunzi badala ya kuzingatia haki zao.
Udahili kwenye lango la Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam (Duce) ulitawaliwa na malalamiko ya wanafunzi, wengi wakiwa wamesimama nje ya geti la chuoni hapo na kudai utaratibu wa kuvaa kitambulisho ili uweze kuingia ndani ni swa na ‘Kipande Yystem'.
Waliiambia Mwananchi kwa nyakati tofauti kuwa masharti yaliyowekwa ili kuweza kurejea chuoni, likiwemo la kumaliza kwanza kulipa ada, ni magumu.
"Mimi ninadaiwa Sh50,000 yamatibabu na jina halijatoka na mimi sijui kama watanifukuza shule kwa ajili ya kiasi hicho cha pesa kwani mfukoni nimesaliwa na Sh20,000 ndiyo zinazoniwezesha kuishi mjini hapa," alisema mmoja wa wanafunzi wa mwaka wa tatu ambaye akutaka jina lake liandikwe na ambaye anatokea Kigoma.
Pia baadhi ya wanafuzi walisema michango iliyoongezwa kama ya kulipia kitambulisho kipya Sh5,000 haina msingi na inawaongezea mzigo.
"kuna michango ambayo wameiongeza ambayo mimi naiona kama vile wanajaribu kutoa adhabu kwani mchango wa wa matibabu mwanzo ulikuwa umechanganjwa kwenye ada lakini sasa unajitegemea lakini pia hii Sh5,000 tunayolipa ya kitambulisho niwizi mtupu kwani kitambulisho akijabadilika kitu ukilinganisha na kile cha awali zaidi ya rangi, lakini namba ni ileile, hadi picha" alisema mwanafunzi aliyejitambulisha kwa jina moja la Bonge.
vitu vingine ambavyo vimelalamikiwa na wanafunzi hao ni kulipia vyumba kwa awamu ya pili wakati walishalipia awali kabla ya mgomo.
"Uongozi wa chuo unasema kiendacho kwa mganga hakirudi, kwa maana hiyo hawazitambui Sh60,000 tulizo lipa kwa ajili ya muhula ambao hatukusoma, sasa kama si wizi wa machomacho, ni nini," alihoji mwanafunzi wa mwaka wa tatu aliyekataa kutaja jina.