Elections 2010 Viongozi wa dini wanadi kura ya maoni Zanzibar

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,315
33,111
Viongozi wa Kiislamu Zanzibar, wamesema wanaunga mkono Serikali ya Umoja wa Kitaifa na kusisitiza kuwa watabeba jukumu la kuzunguka visiwani na kushawishi wananchi kupiga kura ya ndiyo.
Kauli hiyo ilitolewa na Masheikh, maimamu wa dini hiyo na viongozi wengine wa jumuiya za dini ya Kikristo wakati wakitoa maazimio katika mkutano ulioandaliwa na Kamati ya Kusimamia utekelezaji wa kura ya maoni Zanzibar katika Ukumbi wa Baraza la Wawakilishi.
" Sisi viongozi wa dini tunachukua jukumu la kwenda kuwaelimisha waumini kuhusu umuhimu wa kuwa na Serikali ya Umoja wa Kitaifa na tunawaomba Wazanzibari wote waliojiandikisha wajitokeze kwa wingi kupiga kura ya maoni, ” walisema katika maazimio yao saba.
Viongozi hao, walisema kuna haja ya Rais wa Zanzibar, Amani Abeid Karume na Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad kufanya mkutano wa hadhara wa pamoja kabla ya Julai 31, mwaka huu ambayo ndiyo siku ya kura hiyo ya maoni ili kuwaeleza wananchi faida yake.
Maazimio hayo yaliyosainiwa na viongozi wa madhehebu ya dini ya Kiislamu wakiwemo afisa kutoka Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana Zanzibar, Sheikh Abdala Talib na Katibu wa Jumuiya ya Maimamu Zanzibar, Sheikh Muhidin Zubeir.
Jumuiya nyingine ni ya Wanawake wa Kiislamu Zanzibar, Zainab Thani, Tariqa, Sheikh Khamis Abdalla, Jumuiya ya Khoja, Mohammed Bhallo na Jumuiya ya Alyamin.
Walisema Serikali hiyo ya umoja wa kitaifa Zanzibar, inalenga kujenga mshikamano wa wananchi na kuondoa siasa za chuki na uhasama ambazo zimedumu visiwani hapa kwa muda mrefu na kusababisha baadhi ya watu kupoteza maisha.
Wakati huo huo, Jumuiya za Watu wenye ulemavu Zanzibar, wameibana Kamati ya utekelezaji wa kura ya maoni Zanzibar kwa kuitaka iweke bayana majukumu atakayokuwa nayo Makamu wa Kwanza wa Rais wa SMZ chini ya utaratibu wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wasioona Zanzibar (Zanab), Mohammed Kassim, alisema muundo uliopendekezwa wa Serikali hiyo hauleti sura nzuri kwa vile nafasi ya Makamu wa Kwanza wa Rais itakuwa kama ya heshina na mamlaka yote ya utendaji amepewa Makamu wa Pili wa Rais.
Alisema kimsingi Makamu wa Kwanza wa Rais ndiye alitakiwa awe mtendaji mkuu wa shughuli za SMZ na kupewa mamlaka ya kukaimu nafasi ya Rais anapokuwa hayupo.
“ Chama kilichopata mshindi wa pili kwanini kisipewe nafasi ya Makamu wa Pili wa Rais na uwezo wa kukaimu nafasi ya Rais pale anapokuwa nje ya Zanzibar?”alihoji Mwenyekiti huyo.
Kwa upande wake Katibu Mkuu Zanab , Adil Mohammed, alisema inashangaza kuona suala wanaloulizwa wananchi katika kura ya maoni linatofautiana na hoja ya msingi iliyopitishwa katika Baraza la Wawakilishi.
Alisema suala linaloulizwa wananchi na Tume ya Uchaguzi Zanzibar (Zec) ni iwapo wanakubaliana na mabaliko ya muundo wa Serikali wakati wananchi walitakiwa waulizwe je, unakubaliana na muundo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa.
Wanachama wa jumuiya hiyo waliilaumu Zec kwa kushindwa kutoa vipeperushi vyenye elimu kwa wapiga kura wenye ulemavu wa macho na viziwi ili nao washiriki kikamilifu kupiga kura.
Naye Salma Haji Saadat kutoka Umoja wa Watu Wenye Ulemavu Zanzibar (UWZ), alisema kuna haja jumuiya hizo ziwezeshwe ili zitoe elimu kwa wapiga kura wenye ulemavu.
Alisema wenye ulemavu Zanzibar wamekuwa wakipata shida kubwa kuelewa machapisho ya elimu kwa wapiga kura, jambo ambalo vinawafanya washindwe kuelewa malengo ya kuletwa pendekezo la Serikali ya Umoja wa Kitaifa.
Mohammed Haji Khamis kutoka Chama cha Viziwi Zanzibar, aliitaka kamati hiyo kubainisha iwapo watu wenye ulemavu wataweza kunufaika na nafasi za uongozi katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa.
Hata hivyo, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya kusimamia uundwaji wa serikali hiyo, Abubakar Khamis Bakary, alisema marekebisho ya Katiba ya Zanzibar yatakayofanyika ndiyo yatakayoweka bayana majukumu ya Rais, Makamu wa Kwanza na Makamo wa Pili wa Rais.
Hata hivyo, alisema hatua muhimu kwa watu wenye ulemavu kunufaika katika Baraza la Mawaziri na Serikali ya Umoja wa Kitaifa ni kujitokeza kwa wingi kuwania nafasi za uwakilishi kwenye majimbo.
Alisema Rais anazo nafasi 10 za kuteua Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi hivyo kutokana na busara zake, anaweza kutumia fursa hiyo kuteua watu wenye ulemvu.
Wananchi visiwani hapa wanatarajiwa kupiga kura ya maoni Julai 31, mwaka huu kuunga mkono ama kukataa utaratibu wa Serikali hiyo ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar.



CHANZO: NIPASHE

mimi pia nawaunga Mkono Viongozi wa Kidini wawashawishi wanachi wa Visiwa vya Unguja na Pemba wapige kura ya Maoni, itakuwa vizuri zaidi tuone Maoni yao Wananchi wa hivyo Visiwa 2.
 
Back
Top Bottom