Viongozi wa dini: Tumechoka wageni kunufaika na rasilmali za Watanzania

Zimmermann

JF-Expert Member
Sep 28, 2010
2,790
1,232
VIONGOZI wa dini mbalimbali nchini wamesema wamechoshwa kuona wageni wakinufaika zaidi na rasilmali za taifa kama madini ambazo ni mali ya Watanzania huku wakiwaacha wananchi wakibakia kwenye umaskini wa kutisha.

Katika tamko lao la pamoja lilitolewa jana na kuhusisha viongozi wa madhehebu ya Kikristo na Kiislamu; Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) na Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata), viongozi hao waliitaka serikali ibadili hali hiyo.

Waliishauri Serikali iwe makini katika kubadilisha hali hiyo vinginevyo itaipeleka nchi katika mazingira mabaya ya uvunjifu wa amani huku wakiwataka wananchi wawe macho na rasilmali zao.

Katika maelezo yao walizirejea mara kadhaa ibara ya 8 na 9 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zinazozungumzia haki na misingi ya demokrasia ambayo inampa mwananchi haki na mamlaka yote na kusisitiza manufaa ya kiuchumi kuwa lazime iwe ni kwa wananchi wote na siyo kwa wachache. Wakaelekeza kuwa kwa kuwa haki hiyo ya kikatiba haikuzingatiwa kwenye mikataba hiyo ya madini, katiba haina budi kuandikwa upya ili maslahi ya pande zote yazingatiwe. Waliongeza kuwa kama mtu anaweza kuungama dhambi zake na akasamehewa, hakuna kizuizi cha kubadilishwa kwa mikataba ya madini wakisema kunawezekana.

Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi na Kaskazini Mashariki, Stephen Munga alisema Serikali ikishindwa kudhibiti usawa katika uwekezaji inajiwekea mazingira ambayo sio ya amani.

ìWatanzania wanaona mashimo yanaongezeka nchini mwao, ila wao wanachokipata ni punje ndogo tu, tena punje hiyo ndogo inawanufaisha wenye nguvu,î alilalamika na kuongeza: ìKama inawezekana nchi kuwa na katiba mpya, pia inawezekana kuwa na mikataba mipya itakayoinufaisha nchi, mwananchi na mwekezaji.î

Alisema ni wajibu wa Serikali kusimamia rasilmali za taifa na kwamba watu wana haki ya kuona raslimali zao zikitumika kwa manufaa ya Watanzania wote kama katiba ya nchi inavyozungumza.ìTulikuwa Toronto (Canada) na kukuta nyumba imejengwa kwa dhahabu, watu wanachimba dhahabu mpaka wanaweza kuijengea nyumba, lakini sisi wenye dhahabu inachukuliwa tunabaki maskini wakati tuna rasilmali zenye thamani,î alisema Askofu Munga.

Alisema kama viongozi wa dini, wakati umefika kwa Serikali kuangalia ukusanyaji wa mapato kutoka katika sekta ya madini ili kunufaisha na kuhudumia jamii kwa ajili ya maendeleo ya kizazi cha sasa na kijacho.

ìTupo katika mchakato wa kubadili katiba ya nchi lakini katika suala la kubadili mikataba wasaidizi wa Rais Jakaya Kikwete ndio wanakuwa wa kwanza kulikingia kifua suala hili, wanasema haibadiliki.î

Aliongeza, ìSisi tunasema mikataba iangaliwe upya, utozaji wa kodi ubadilishwe, watu wanachimba madini mwaka wa 10 huu, hivi tukiwambia tunabadili mkataba ili kuwa na uwiano wa maslahi kwa pande zote wangekataa?... Lazima tuwe macho, haya madini hayabaki yanakwenda tu.î

Alisema kama waliopewa dhamana ya kusimamia sekta ya madini wameshindwa kuisimamia viongozi wa dini wataisimamia na kuwa kitu kimoja.
Haki za Binadamu
Wakizungumzia suala la mauaji ya watu watano iliyotokea katika mgodi wa Nyamongo, Tarime Mkoani Mara hivi karibuni, walisema hali hiyo inaashiria amani ya nchi kuhatarishwa kwa lengo la kutetea maslahi ya watu wachache wanaohujumu nchi.

Askofu Munga alisema haki za binadamu katika maeneo ya migodi si za kuchezea na kusisitiza kuwa inatia shaka vinapoibuka vyombo vya kisheria na kuanza kuhatarisha amani kwa raia.

ìHaki za binadamu siyo suala la kisiasa, hata kama kulikuwa na raia wenye makosa wanatakiwa kuchukuliwa hatua stahiki si uvunjifu wa haki za binadamu,î alisema askofu huyo.

Alisema kuwa sekta ya madini inahitaji mabadiliko makubwa na wao kama viongozi wa dini wataendelea kupigania haki za binadamu ikiwa ni pamoja na kuwatetea walioathirika kutokana na kuishi karibu na maeneo ya migodi.

Aliongeza kuwa kamati yao inafuatilia matukio yote ya uvunjwaji wa haki za binadamu nchini na kwamba hivi karibuni watatoa taarifa ya kilichotokea katika mgodi huo wa Nyamongo.
ìHaiwezekani watu wanauawa halafu majibu yanakuwa rahisi rahisi tu. Unaweza kudhani ni jambo la kawaida, lakini kamwe usicheze na maisha ya watu, yana thamani kubwa,î alieleleza Askofu Munga.

Alisema suala la haki za binadamu linatakiwa kutochukuliwa kisiasa na kwamba hata kama wananchi ndio wenye makosa, haki inatakiwa kufuatwa.
Ukusanyaji wa kodi
Mshauri wa Kamati hiyo, Silas Olaníg alisema mfumo wa kusamehe kodi kwa kampuni za madini ni gharama kwa serikali na ruzuku kwa kampuni inayopata msamaha kwa kodi.

ìSerikali maskini inaomba msaada ili kukidhi mahitaji ya wananchi wake. Inaisamehe kodi kampuni tajiri... Halafu nchi hiyo hiyo maskini inakwenda katika nchi hiyo tajiri na kuomba msaada.
"Mantiki na usawa wa mgawanyo wa rasilimali uko wapi,î alieleleza Olaníg. Aliongeza: ìSerikali maskini kama Tanzania ina ubavu upi wa kutoa ruzuku kwa kampuni tajiri ambazo zina bajeti kubwa kuliko bajeti ya serikali? Hapa usawa wa kiuchumi haupo,î.

Alisema serikali inatakiwa kuweka mfumo na mkakati wa kitaifa ambao unaongeza ushiriki wa sekta nyingine za uchumi katika sekta ya madini.

Alisema mkakati huo uangalie kwa mapana sekta ya madini inatoa fursa zipi ambazo wananchi na sekta nyingine zitapata.
ìLazima utizame sekta hii inahitaji nini na Tanzania ina uwezo gani wa kutoa hizo huduma na bidhaa katika sekta hiyo. Sekta hizo zinahitaji wataalam, je, tumeshafanya utafiti kuona ni watalaam gani wanahitajika? Lazima nchi izalishe wataalam wa sekta ya madini na kuacha kutegema wageni. Hii itaongeza ushiriki wa wazawa katika ajira.î

Mikataba
Akizungumzia kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Bakwata, Sheikh Abdallah Matumla, ambaye kitaaluma ni mwanasheria, alisema kuna umuhimu kwa serikali kupitia upya mikataba ya madini kwa kuwa jambo hilo linawezekana na linazungumzika.

ìMikataba inatakiwa kutizamwa upya ili penye udhaifu paweze kurekebishwa, mkataba uwekwa maslahi ya wote si wawekezaji tu. Hili jambo linazunguzika na serikali inatakiwa kuwa sikivu,î alisema Sheikh Matumla.

Naye Katibu wa Tume ya Mahusianmo baina ya dini mbalimbali ya Baraza la Maaksofu Katoliki Tanzania (TEC), Padri Gallus Marandu alisema mikataba ikirekebishwa na kuwa na usawa hakutakuwa na malalamiko wala uvunjwaji wa haki za binadamu kama inavyoonekana sasa.

Kwa upande wake, Profesa Camillus Kassala ambaye ni Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) na Mjumbe wa Chama cha Wanataaluma Wakatoliki Tanzania (TCP), alisema athari zilizopo sekta ya madini zisipotatuliwa mapema ni hatari kwa umoja wa Taifa.


 
Back
Top Bottom