Vincent na hukumu ya kunyongwa-ni kweli aliuwa familia yake?

Mtambuzi

Platinum Member
Oct 29, 2008
8,810
15,395

brothers_01.jpg
vincent-brothers-6.jpg
Vincent Brothers
front_yard_1.jpg
Nyumba waliyokuwa wakiishi familia yake
graphic_harperhouse_highlight_prod_affiliate_25.jpg
Ramani ya Nyumba
rentalcarradiatorlarge.jpg
Ushahidi wa kumtia hatiani ulipatikana katika kifaa hiki
judge_01.jpg
Jaji Michael Bush
leegree.jpg
Mwendesha mashitaka Bi, Lisa Green
14220357_240X180.jpg
margaretkern.jpg
Mwanaye pekee aliyesalimika na mauaji hayo Margaret Kern

Ilikuwa ni siku ya Jumapili ya Julai 6, 2003, katika mji wa Bakersfield uliopo katika wilaya Kern jimbo la California, Joanie Harper aliyekuwa na umri wa miaka 39, watoto wake watatu na mama yake aitwae Earnestine Harper aliyekuwa na umri wa miaka 70, walikuwa kanisani kuhudhuria ibada ya Jumapili. Ilikuwa ndio ibada ya kwanza kuhudhuria akiwa na mwanae aliyejifungua wiki sita zilizopita aitwae Marshall Harper. Baada ya ibada walipitia kwenye mghahawa maarufu wa Black Angus kupata chakula cha mchana kabla ya kurudi nyumbani. Baada ya kupata chakula walirudi nyumbani ambapo walijipumzisha kidogo kwa usingizi wa mchana kabla ya kurudi tena kanisani kwa ibada ya jioni.

Mume wake Joanie Harper, aitwae Vincent Brothers aliyekuwa na umri wa miaka 41 wakati huo alikuwa amesafiri hapo mnamo Julai 2, 2003 kwenda katika mji wa Elizabeth ulioko North Caroline kumtembelea mama yake.

Joanie na watoto wake walijipumzisha chumbani wakati mama yake naye alikuwa amejipumzisha chumba kingine. Ni katika muda huo, mvamizi asiyefahamika aliingia katika nyumba hiyo kwa kupitia mlango mwa nyuma kwa kunyata akiwa na bastola aina ya 22-Caliber.

Mnamo siku ya Jumanne ya Julai 8, 2003, majira ya asubuhi, jirani na rafiki wa familia hiyo aitwae Kelsey Spann, aliamua kumtembelea Joanie Harper na familia yake. Ni siku kadhaa zimepita bila kusikia lolote kutoka kwa rafiki yake huyo, kitu ambacho hakikuwa ni kawaida yao, kukaa siku zote hizo bila kuwasiliana. Pamoja na Juhudi zake za kupiga simu mara kadhaa kwa Joanie, lakini simu zake zote hazikupokelewa. Aliamua kumtembelea rafiki yake huyo ili kujua kulikoni. Alifika katika nyumba hiyo na kukuta mlango umefungwa, alifungua mlango huo kwa kutumia funguo ambazo alipewa na Joanie siku za nyuma. Alifungua mlango huo lakini kulikuwa na kitu kinazuia mlango kufunguka zaidi, ilikuwa kama kuna kizuizi kimewekwa mlangoni. Aliamua kuzunguka nyuma ya nyumba hiyo ili kutumia mlango wa nyuma. Alipofika alijaribu kufungua mlango wa kioo, haukuwa umefungwa………halikuwa ni jambo la kawaida kwa mlango huo kutofungwa. Aliingia ndani ya nyumba hiyo na kuelekea moja kwa moja hadi chumbani kwa Joanie.
Humo alikutana na hali ya kutisha na bila kupoteza muda alipiga simu ya dharura Polisi ambapo walifika muda mfupi baadae, ilikuwa ni saa moja za asubuhi.

Polisi walipofika katika eneo hilo walikutana na hali ya kutisha ambayo ndiyo iliyopelekea Kelsey Spann kupiga simu hiyo ya dharura.


joanie_harper_full.jpg
Joanie Harper alikutwa akiwa amelala kitandani kifudifudi. Alikuwa amekufa kwa kupigwa risasi mara tatu kichwani na mara mbili katika mkono, pia alikuwa amechomwa kwa kisu mara saba.Mwanae mchanga aliyekuwa na umri wa wiki sita aitwae Marshall Harper ambaye awali hakuonekana kwenye eneo la tukio na kuripotiwa kama amepotea, alikutwa akiwa amelala pembeni ya mama yake akiwa amefunikwa na mto alikutwaamekufa, pia alikuwa ameuawa kwa kupigwa risasi mgongoni.


marques_harper_full.jpg
Mtoto mwingine aitwae Marques Harper aliyekuwa na umri wa miaka minne na yeye alikutwa akiwa hapo kitandani pamoja na mama yake akiwa amekufa. Alikuwa na jeraha la risasi upande wa kulia wa kichwa chake, lakini hakuwa amefunga macho. Vidole vyake vya mkono wake mmoja vilikuwa vimeng'atwa mpaka kwenye mfupa. Ilielezwa kwamba huenda alimuona muuaji na katika hali ya taharuki, alitia vidole vyake mdomoni mwake na wakati anakata roho aliving'ata.

lyndsey_harper_full.jpg
Mtoto mwingine, Lyndsey Harper aliyekuwa na umri wa miaka miwili alikutwa akiwa amelala upande wa miguuni mwa mama yake, alikuwa ameuawa kwa kupigwa risasi mgongoni, pia TV kubwa flat screen iliyokuwa
imefungwa ukutani, ilikutwa ikiwa imefunguliwa na kuachwa chini, haikuchukuliwa.

earnestine_harper_full.jpg
Mama mzazi wa Joanie aitwae Ernestine Harper alikuwa akiwa amelala kwenye korido, alikuwa ameuawa kwa kupigwa risasi mara mbili usoni. Bastola aliyokuwa ameishika ili kukabiliana na muuaji ilikutwa ikiwa pembeni yake. Polisi waliyaelezea mauaji hayo kama ya kutisha na ya kihistoria kutokea katika mji huo wa Bakersfield.
Wakati huo huo mume wa Marehemu Joanie, Vincent Brothers aliwasili katika uwanja wa ndege wa LAX akitokea Atlanta ambapo alikuwa amekamatwa kwa muda katika jimbo la North Carolina na kuhojiwa kuhusiana na mauaji hayo. Polisi walikuwa wanamshuku kuhusika na mauaji hayo. Wakati anachukuwa mizigo yake alikuta kundi kubwa la waandishi wa habari likimsubiri ili wasikie kauli yake kuhusiana na mauaji hayo.

Lakini mwanasheria wake aitwae Curtis Floyd hakuwapa nafasi hiyo…. "Samahani, hataweza kuzungumza kwa sasa, anayo majonzi ya kumpoteza mkewe na watoto wake"

Tukio la mauaji ya familia hiyo yalitikisa mji huo wa Bakersfield. Misa ya kuwaombea marehemu hao iliyohudhuriwa na waumini wapatao 200 ilifanyika katika kanisa liitwalo Compassion Christian Centre, kanisa ambalo lipo hatua kadhaa kutoka katika nyumba waliyokuwa wakiishi familia ya Joanie Harper ambapo ndipo pia familia hiyo ilipokuwa ikisali. Wasemaji wengi katika misa hiyo waliomba haki itendeke, huku wengine wakiwakumbusha waumini waliohudhuria misa hiyo kwamba, Biblia inasisitiza kutolipiza visasi.
Akizungumza mara baada ya misa hiyo dada wa Joanie aitwae Linda Piggee 51, alisema, "Wameuwa mwili wake, lakini hawajauwa roho yake." Kisha akaendelea "Tusingependa kumhukumu mtu yeyote, kwani Mungu pekee ndiye anayejua."

Linda aliendelea kusema, "Ninachojua ni kwamba haya ni mauaji ya kikatili. Mungu pekee ndiye anayemjua aliyefanya hivi, kamwe sitataja jina la mtu yeyote kuhusiana na mauaji haya."

Kaka wa Joanie Harper ambaye ni Mchungaji huko Florida aitwae Eddie Herper 46, ambaye alihudhuria misa hiyo, akizungumza katika misa hiyo alisema, "Huu ni muda wa uponyaji. Huu sio muda wa kujenga chuki na hasira. Inawezekana Mwanadamu akawa na mamlaka, lakini Mungu ndiye mwenye mamlaka, na ni yeye mwenye kuhukumu."

Baadae Vincent Brothers alikamatwa na kuhojiwa na Polisi katika kituo kikuu cha Polisi cha mji huo wa Bakersfield. Lakini hata hivyo aliachiwa. Polisi walisema kwamba, hawana ushahidi madhubuti wa kumfungulia mashtaka Vincent ya kuhusika na mauaji hayo.

Jambo ambalo lilikuwa likiwaumiza vichwa wapelelezi wa Polisi ni kujua mahali alipokuwa Vincent kati ya siku hiyo ya Jumapili, siku ambayo wahanga hao walionekana hai, na siku ya Jumanne asubuhi, miili ya wahanga hao ilipopatikana. Huu ulikuwa ni mtihani mkubwa sana kwa wapelelezi hao wa Polisi.

Akizungumza mara baada ya Vincent kuachiwa baada ya kuhojiwa na Polisi mwanasheria wake aitwae Curtis Floyd alisema, "Kama mauaji hayo yalitekelezwa siku ya Jumapili, ni wakati gani Polisi wanaamini Vincent aliondoka katika mji huu wa Bakersfield?"

"……… Hakuwepo, wakati walipouwawa." Alimalizia kusema mwanasheria huyo.

Lakini hata hivyo mwanasheria huyo alikataa kusema Vincent alikuwa wapi kati ya Julai 2, na jioni ya tarehe 8, Julai, 2003. Polisi wa upelelezi wa kituo kikuu cha Polisi cha Bakersfield walisafiri mpaka Columbus, katika jimbo la Ohio siku ya Ijumaa na walifuatana na Polisi wenyeji wa mji huo katika maeneo mbalimbali, lakini hata hivyo waliporudi, hawakuzungumza lolote kuhusiana na matokeo ya uchunguzi wao.

Vincent aliendelea kukaa uraiani lakini machoni mwa Polisi alibaki kuwa mtuhumiwa namba moja kuhusishwa na mauaji hayo ya familia yake mwenyewe. Polisi walidai kwamba Vincent hakuwa tayari kuwaeleza kuhusu mahali alipokuwa siku hiyo ya mauaji, na hiyo ndiyo sababu ya wao kumtilia mashaka kuhusika na mauaji hayo.

Je huyu Vincent ni nani? Kwa nini Polisi walikuwa wanamtilia mashaka kuhusiki na mauaji ya familia yake mwenyewe?

Vincent Brothers alizaliwa hapo mnamo Mei 1, 1962, katika familia masikini huko New York. Alianza safari yake kimaisha kwa kusoma katika shule mbalimbali na baadae chuoni. Alikuwa ni mhitimu wa shahada ya kwanza ya elimu aliyoipata katika chuo kikuu cha Califonia – Bakersfield. Alianza kazi kama mwalimu mwaka 1987 katika shule ya Fremont Elementary na hatimaye aliteuliwa kuwa makamu mkuu wa shule hapo mnamo mwaka 1995.

Alikuwa ni mtu aliyefahamika katika mji huo wa Bakersfield uliopo katika jimbo la Califonia. Alikuwa akiheshimika katika jamii na yeye na familia yake walikuwani ni waumini wazuri wa dini ya Kikristo. Vincent alioana na Joanie Harper mnamo Januari 2000, lakini ndoa yao ilivunjika mwaka mmoja baadae, ilikuwa ni Septemba 2001, sababu za kuvunjika kwa ndoa hiyo kulisababishwa na Vincent kutokuwa mkweli kwa mkewe. Joanie alidai kwamba Vincent hakumweleza kuhusu ndoa zake mbili zilizovunjika huko nyuma. Hata hivyo walioana tena mwaka 2003, lakini Vincent alihama katika nyumba waliyokuwa wakiishi na mkewe hapo mnamo April 2003.

Maisha ya ndoa ya wanandoa hao hayakuwa ni mazuri, hata wale waliokuwa wakiwafahamu walidai kwamba maisha yao ya ndoa hayakuwa na amani, ni mara chache Vincent alitumia muda wake na familia na hawakuwa na ukaribu kama wa mke na mume. Pamoja na misukosuko ya ndoa yao, lakini waliowafahamu walidai kwamba Joanie Harper alikuwa akimpenda sana Vincent na alitamani siku moja ndoa yao iwe imara.
Katika mji huo wa Bakersfield ambapo ndipo familia ya Vincent na Joanie walipokuwa wakiishi, jamii ya Wamarekani wenye asili mya Africa waligawanyika katika makundi mawili kuhusiana na tuhuma hizo za mauaji zilizokuwa zikimkabili Vincent. Wakati upande mmoja ukimuona kama mtu muhuni na asiyewajibika katika familia, upande mwingine Vincent alionekana kama mtu alieyeheshimika sana na muelimishaji mahiri ambaye kutokana na utendaji wake mzuri wa kazi aliweza kupandishwa cheo na kuwa makamu mkuu wa shule aliyokuwa akifundishia.

Rafiki zake walimuelezea kama mtu mwenye mapenzi makubwa kwa wanafunzi wake. Janea Davis 38, alisema kwamba alimjua Vincent katikati ya miaka ya 80, wakati alipokuja California akitokea Pwani ya Mashariki. Janea pia aliwahi kufanya kazi katika shule moja hapo Bakersfield na Joanie Harper ambaye alikuwa msimamizi mkuu wa campus ya shule hiyo.

Akizungumzia mahusiano ya Vincent na Joanie, Janea alisema kwamba katika kipindi ambacho Joanie alipokuwa na ujauzito wa huyu mtoto wao wa tatu Vincent alikuwa akimletea mkewe chakula maalum hapo shuleni.

"Wote tulifurahi kuona wanandoa hawa vijana jinsi walivyokuwa wanapendana" alisema Janea Davis.
Kwa mara ya mwisho Junea alionana na wanandoa hao wiki mbili kabla ya tarehe 4, Julai, wakiwa nyumbani kwao. "Walionekana kuwa na furaha na walikuwa wanazungumzia mpango wao wa kujenga nyumba kubwa zaidi." Alisema Janea.

Janea alidhani Vincent alikuwa anaishi na mkewe katika nyumba hiyo muda wote na hata marafiki wengine wa Joanie waliohudhuria sharehe yao ya harusi huko Las Vegas hawakujua kama wanandoa hao walikuwa wameachana mwaka mmoja ulipita na hiyo ilikuwa ni ndoa yao ya pili.

Kitendawili cha tega nikutege chaonekana kuwa kigumu………………..

Kitendawili ambacho wapelelezi wa kesi hiyo walitakiwa kukitegua kilikuwa ni kuthibitisha kama Vincent alikuwa Bakersfield California wakati mauaji ya familia yake yakitokea au alikuwa Ohio kama alivyodai.
Polisi walikuwa na uhakika kabisa kwamba Vincent ndiye aliyehusika na mauaji ya familia yake mwenyewe, na hiyo ilitokana na taarifa waliyoipata kutoka kwa jirani yake mmoja aliyedai kwamba alimuona Vincent akiwa nje ya nyumba inapoishi familia yake hapo Bakersfield muda yalipotokea mauaji.

Kwa kuanzia Askari wa upelelezi walianza kufuatilia safari ya Vincent kutokea Barksfield hadi Columbus Ohio. Askari hao waliamini kwamba Vincent alipanga safari hiyo makusudi ili kutengeneza mazingira kwamba wakati mauaji hayo yanatokea alikuwa hayupo katika mji huo (Alibi). Waligundua kwamba Vincent alisafiri kwa ndege hadi Ohio mnamo tarehe 2, Julai 2003 ambapo alikodi gari aina ya Dodge Neon katika kampuni moja iitwayo Doller Rent –A-Car. Polisi walipofuatilia kampuni hiyo waligundua kwamba wakati gari hilo likiwa mikononi mwa Vincent liliendeshwa umbali wa maili 5,400, umbali ambao unatosha kabisa kwa Vincent kwenda Bakersfield na kurudi Ohio na ziada. Pia Polisi hao walibaini kwamba Vincent aliendesha gari hilo kwa umbali wa maili 4,500 kwa siku tatu. Lakini Vincent alizidi kusisitiza kwamba hakuwahi kutoka nje ya Ohio.

Mwakilishi wa kampuni ya kukodi magari ambayo ndipo Vincent alipokodi gari waliwaeleza Polisi kwamba wakati mwingine wafanyakazi wa kampuni hiyo wanacheza mchezo mchafu wa kuchezea kifaa kinachorekodi umbali wa gari lilipotembea hususan kipindi cha mwishoni mwa juma. Kwa mfano, kwa mujibu wa rekodi zilizochukuliwa katika gari hilo lililotumiwa na Vincent ilionyesha kwamba mtu aliyekodi gari hilo aina ya Dodge Neon kabla ya Vincent aliendesha umbali wa maili 20 tu, wakati kwenye gari ilionyesha aliendesha umbali wa maili 1,800. Hata hivyo rekodi za watu wengine waliokodi gari hilo za umbali ambao gari hilo lilitembea zilichunguzwa na Polisi.

Mtu mwingine aliyekodi gari hilo baada ya Vincent alidai aliendesha gari hilo kwa masaa kadhaa katika viunga vya Virginia. Askari hao walilichukua gari hilo kwa uchunguzi zaidi. Hata hivyo kifaa cha kuchunguzia umbali wa gari lilipotembea (Odometer) kilionyesha kwamba gari hilo lilitembea umbali wa maili 8,552, na mita ya gari hilo haikuonyesha kuchezewa. Kwa mujibu wa rekodi za kampuni hiyo ya kukodisha magari zilionyesha kwamba Vincent aliendesha umbali wa zaidi ya maili 5000 akiwa na gari hilo.

Lakini Vincent alidai kwamba mnamo tarehe 2, Julai 2003, aliondoka Bakersfield kwa basi hadi Los Angeles ambapo alipanda ndege hadi Ohio kumtembelea kaka yake aitwae Melvin, hata hivyo alidai kwamba alipokuwa hapo Ohio alikuwa amegawa muda wake mara mbili ambapo kuna wakati alikuwa akitumia muda wake kuwa kwa kaka yake Melvin na muda mwingine kwa kaka yake mwingine aitwae Troy.

Vincent alidai kwamba wakati mauaji yanatokea alikuwa umbali wa zaidi ya maili 2, 300, ingewezekana vipi awepo katika mji wa Bakersfield mchana wa tarehe 6, Julai, 2003 aiuwe familia yake na kisha arudi Ohio jioni ya tarehe 7, Julai, wakati hata kaka yake anakiri kwamba siku hiyo ya mauaji alikuwa Ohio?

Iliwachukua Polisi takriban miaka mitatu kukusanya ushahidi wa kumtia hatiani Vincent. Askari wawili wa FBI walikuwa na uhakika kabisa wanaye mtu sahihi aliyehusika na mauaji hayo na hakuwa mwingine bali ni Vincent, lakini ugumu ilikuwa ni namna gani watathibitisha kwamba Vincent alikuwa Bakersfield Califonia siku yalipotokea mauaji na si Ohio.

Profesa wa wadudu ahusishwa na upelelezi…………

Askari wa upelelezi wa FBI walipata wazo la kupeleka rejeta na air filter ya kuchujia hewa ya gari alilokuwa amekodi Vincent alipokuwa Ohio kwenye kituo cha uchunguzi wa wadudu cha Bohart Museum Entomology ambapo Profesa Lynn Kimsey aliongoza kazi hiyo ya uchunguzi ambao ndio uliotegua kitendawili hicho.
Wapelelezi hao wa FBI waliamini kwamba Profesa Kimsey angeweza kuwambia aina ya wadudu waliokuwa wamenasa kwenye rejeta na air filter na wanapatikana wapi hapo nchini Marekani. Kwa kawaida wadudu hutambuliwa na wataalamu kutokana na chimbuko lao (Species) na eneo wanaloishi kijiografia.

Katika ripoti yake Profesa Kimsey alibaini kwamba baadhi ya wadudu waliokutwa kwenye vifaa hivyo wanapatikana eneo la Magharibi, na wengine waliokutwa katika vifaa hivyo hupatikana kwa wingi katika eneo la California. Kuonekana kwa wadudu hao kulibainisha kwamba gari hilo lilikuwa liliendeshwa usiku kuelekea California na si majira ya mchana. Kwa ujumla Profesa huyo alikamilisha repoti yake kwa kusema kwamba hakuna wadudu wanaoruka mchana waliokutwa kwenye vifaa hivyo. Huo ulikuwa ni ushahidi wa kitaalamu uliopelekea Vincent kufikishwa mahakamini na kushitakiwa kwa kosa la kuiuwa familia yake mwenyewe. Na kama usingefanyika uchunguzi huo wa kisayansi labda hadi leo Vincent asingekuwa amefikishwa mahakamani.

Labda kwa faida yako wewe msomaji ni kwamba sayansi ya viumbe imetumika sana kufanikisha upelelezi wa kesi nyingi zilizojaa utata nchini Marekani. Wanasayansi ya wadudu wanaweza kubaini kwa usahihi kabisa mwili uliotelekezwa mahali ulikaa hapo kwa muda gani na wakati gani wa mwaka huo mtu huyo alipokufa. Kwa kesi ya Vincent uchunguzi wa wadudu waliokutwa kwenye vifaa vya gari (Rejeta na air filter) alilotumia ndivyo vilivyofanikisha upelelezi wa kesi yake. Lakini kuna kesi nyingi ambazo miili ya watu waliouawa na kutelekezwa mahali, wadudu wanaokutwa kwenye miili hiyo hutumiwa na wanasayansi wa wadudu kubaini kwa usahihi ni muda gani mtu ule aliuawa au kufa na kutelekezwa mahali hapo. (Huko baadae nitaandika makala kuhusiana na utafiti huu wa Kisayansi)

Mtuhumiwa Kizimbani………………

Mnamo Februari 22, 2007, Vincent Brotheres alifikishwa mahakamani rasmi na kushitakiwa kwa kosa la kuuwa familia yake mwenyewe ambapo alimuua mkewe Joanie Harper 39, watoto wake watatu waliotajwa kwa majina ya Marques 4, Lyndsey 2, Marshall aliyekuwa na umri wa wiki sita na mama mkwe wake Ernerstine 70, kati ya tarehe 6, Julai na 8, Julai 2003. Kwa mujibu wa sheria ya jimbo hilo, Iwapo Vincent Brothers akipatikana na hatia ya makosa hayo atahukumiwa kunyongwa kwa kuchomwa sindano ya sumu. Vincent Brothers Alikanusha mashitaka hayo, na alidai kwamba wakati mauaji hayo yanatokea, yeye alikuwa Ohio kumtembelea kaka yake ambaye alipoteana naye kwa takriban mwaka mmoja. Vincent alikuwa akitetewa na wanasheria wawili waliojulikana kwa majina la Michael Gardina na Anthony Bryan.

Makamu mwanasheria wa wilaya Bi, Lisa Green ndiye aliyepewa jukumu la kuwa mwendesha mashitaka katika kesi hii iliyojaa utata mwingi. Mama huyu alikuwa ni mmoja wa wanasheria wanaoheshimika katika ofisi ya mwanasheria wa wilaya ya Kern akiwa amefanya kazi katika ofisi hiyo kwa zaidi ya miaka 20.

Jaji aliyesikiliza kesi hiyo alijulikana kwa jina la Michael Bush. Hata hivyo katika kusikiliza kesi hiyo, alianza na changamoto, baada ya wanasheria wanaomtetea Vincent kumtaka ajiondoe kusikiliza kesi hiyo kwa sababu mwendesha mashitaka Lisa Green aliwahi kumsaidia katika uchaguzi wa nafasi aliyo nayo hapo mnamo mwaka 1996. Muheshimiwa Jaji Bush alipinga hoja hiyo na kudai kwamba hana urafiki na mwendesha mashitaka Lisa Green na akaahidi kutokuwa na upendelea katika kesi hiyo.

Wakati wa kuanza kusikilizwa kwa kesi hiyo Mwendesha mashitaka Lisa Green alianza kwa kuliuliza swali baraza la wanasheria lililokuwa likisikiliza kesi hiyo…..

"Ni nani alikuwa na nia (Motive) ya kuuwa watoto? Hili ni swali ambalo ninataka wote hapa mjiulize tena na tena na tena"

Kisha Lisa Green akalijibu swali hilo mwenyewe……..
"Jibu lake ni kwamba, mtu huyo ni Vincent Brothers."

Kesi hii iliegemea zaidi ushahidi wa kimazingira, kwani silaha iliyotumika haikupatikana, alama za vidole vya mtuhumiwa havikupatikana na hata damu ya mtuhumiwa katika eneo la tukio kwa ajili ya vipimo vya DNA haikupatikana. Lakini pia hapakuwa na mtu mwingine aliyepatikana kuhusishwa na mauaji hayo.
Upande wa mashitaka waliamini kwamba Vincent alikodisha gari na aliendesha kwa siri kutoka Ohio mpaka California kwa nia ya kutekeleza mauaji ya familia yake mwenyewe.

Mwendesha mashitaka huyo alibainisha kwamba Vincent hakuwa baba mwema aliyeipenda familia yake na alikuwa na mahusiano na wanawake wengine nje ya ndoa yake, na nia ya kuuwa familia yake ilikuwa ni kutaka kuondokana na mzigo wa kulea familia hiyo ambayo ilikuwa imeongezeka. Upande huo wa mashitaka uliendelea kubainisha kwamba mnamo Julai 2, 2003 Vincent alisafiri kwenda Ohio kumtembelea kaka yake ili kujenga mazingira kwamba hakuwepo wakati mauaji yakifanyika (Alibi).

Mojawapo ya mazingira aliyoyatengeneza ya kuonesha kwamba alikuwa Ohio wakati mauaji yakifanyika zilikuwa ni risiti alizokuwa nazo ambazo zilionyesha kwamba alifanya manunuzi katika maduka kadhaa katika jimbo hilo la Caroline Kaskazini. Hata hivyo uchunguzi uliofanywa katika maduka hayo ulibainisha kwamba kaka yake aitwae Merlvin ndiye aliyetumia Credit Card ya Vincent baada ya kughushi sahihi yake. Mwanzoni Melvin alidanganya kwamba ni Vincent ndiye aliyefanya manunuzi hayo, lakini baada ya kutishwa kwamba atashitakiwa kwa kuidanganya mahakama kama ikigundulika ni yeye aliyefanya manunuzi hayo, Melvin alikiri kwamba ni yeye alifanya manunuzi hayo kwa maelekezo ya Vincent, na pia hajui mahali Vincent alipokuwa kati ya Julai 4 mpaka Julai 7, 2003.

Upande wa utetezi ulikanusha madai hayo na kusema kwamba mtu kuwa na mahusiano nje ya ndoa yake haimaanishi kuwa mtu huyo kuwa muuaji na haibadili tabia ya upendo kwa familia aliyo nayo. Upande huo wa utetezi uliendelea kudai kwamba hata rekodi ya simu yake ya mkononi ilionyesha kwamba alikuwa Ohio wakati wa mauaji hayo na pia Vincent alihusika na ajali ndogo akiwa Ohio siku hiyo ya mauaji wakati mtoto mmoja wa kiume aliyekuwa akiendesha baiskeli alipoingia barabarani na kulivaa gari la Vincent. Pia upande wa mashitaka umeshindwa kuleta ushahidi wa Video inayomuonyesha Vincent akijaza mafuta katika mojawapo ya vituo vya mafuta vipatavyo 100 vilivyopo kati ya Ohio na California au hata kutumia maduka yaliyopo kwenye vituo hivyo vya mafuta, na hata silaha iliyotumika kutekeleza mauaji hayo haikuwahi kupatikana.
Katika mojawapo ya utetezi wake Vincent alidai kwamba, akiwa Ohio, kuna siku alikuwa na mizunguko na kaka yake mwingine aitwae Troy na ndio sababu Melvin hakujua mahali alipo kati ya Julai 4, mpaka Julai 7. Troy Brothers alipoitwa kutoa ushahidi wake ili kuthibitisha madai hayo ya Vincent, alitoweka katika mazingira ya kutatanisha. Hata hivyo mahakama ilitoa hati ya kukamatwa kwake.

Polisi wa Columbus walifanikiwa kumpata mtu ambaye alipata ajali siku hiyo ya mauaji, ajali ambayo ilimuhusisha kijana mwendesha baiskeli kulivaa gari, ambapo Vincent alidai ni yeye aliyehusika na ajali hiyo. Mtu huyo alijulikana kwa jina la Tamba Libbie, muuzaji wa magari yaliyotumika hapo Ohio. Akitoa ushahidi wake pale mahakamani alidai kwamba alihusika na ajali siku moja mwishoni mwa juma hapo mnamo mwaka 2003. Maelezo yake kuhusiana na ajali hiyo alifanana kwa usahihi kabisa na yale aliyoyatoa Vincent Brothers. Wakati akitoa utetezi wake Vincent alidai kwamba, mnamo Julai 6, 2003 akiendesha gari alilokodi aina ya Dodge Neon ya blue katika viunga vya mji wa Columbus, alifika kwenye njia panda inayotenganisha kati ya eneo Hague na Steele, ambapo kijana moja akiendesha baiskeli kutokea mtaani alilivaa gari lake. Maelezo hayo yalifanana na ya Libbie, isipokuwa tofauti ilikuwa ni kwamba Libbie alidai kijana huyo alilivaa gari lake upande wa dereva. Kwa mujibu wa maelezo yake pale mahakamani Libbie alidai kwamba hakumweleza mtu yeyote kuhusu ajali hiyo kwa sababu aliposimamisha gari lake, Yule kijana na mtu mwingine aliyekuwa naye walishaondoka eneo la tukio.

Ripoti ya gari la wagonjwa siku hiyo Julai 6, 2003 ilionyesha kwamba gari lililohusika na ajali hiyo ni aina ya Mercury Sable ya rangi ya Kijani iliyopauka, gari ambalo ndilo Libbie alilokuwa akiendesha siku hiyo ya ajali na sio Dodge Neon ya blue kama ile iliyokodishwa na Vincent. Hata hivyo Libbie alisema kwamba kwa kumbukumbu zake anaamini ajali hiyo ilitokea mwishoni mwa juma siku ambayo ilikuwa ni sikukuu ya wafanyakazi na si mwishoni mwa juma ya tarehe 4, Julai, kama alivyodai Vincent. Pia ripoti ya gari la wagonjwa lilirekodi namba ya gari la Libbie na ni wiki iliyopita kabla ya kutoa ushahidi wake ndio alikuwa amekamatwa kwa kuhusika na ajali hiyo.

Mtu mwingine aliyetoa ushahidi dhidi ya Vincent alikuwa ni mwanamke aitwae Shann Kern ambaye alikuwa na uhusiano na Vincent ambapo walizaa mtoto wa kike ambaye ndiye pekee aliyebaki aitwae Margeret, 14. Vincent hakuwahi kuoana na mwanamke huyu. Akitoa ushahidi wake Shann alimuelezea Vincent kama mtu katili na mwenye vitendo vya unyanyasaji kwa wanawake. Akielezea juu ya vitendo hivyo Shann alisimulia tukio moja lililotokea mnamo Mei 1988, wakati huo akiwa na ujauzito wa mtoto wao. Ilitokea Vincent hakurudi nyumbani kwa siku tatu. Aliporudi alimuomba ampeleke Lancaster kwa ndugu zake yeye Shann, lakini Vincent alikataa na kuanza kumtukana na kama hiyo haitoshi alimpiga na kumuacha na uvimbe usoni. Shann alipiga simu ya dharura ambapo gari la wagonjwa lilifika na alikimbizwa hospitali.

Vincent alishitakiwa ka kosa hilo, alihukumiwa kwa kuwekwa chini ya uangalizi kwa miaka mitatu. Baadae amri hiyo iliondolewa baada ya kuonyesha mwenendo mzuri.
Shann alitengena na Vincent baada ya tukio hilo hata hivyo alikiri kuendelea na kuwasiliana na Vincent kwa sababu ya kumuweka karibu na mtoto wao Margaret Kern Brothers.

Hata hivyo upande wa utetezi walilielezea tukio hilo kama dogo na lisilo na mashiko.

Maisha ya uasherati ya mtuhumiwa yawekwa peupe...........................

Kesi hiyo iliibua maisha halisi ya mahusiano na wanawake aliyokuwa nayo mtuhumiwa Vincent Brothers.
Ilielezwa pale mahakamani kwamba Vincent aliwahi kumuoa Angela Richardson aliyekuwa na umri wa miaka 26, hapo mnamo Octoba 1988. Waliachana mwaka 1990. Wakiwa kwenye mchakato wa kuachana na Angela, Vincent alianza uhusiano na Shann Kenn, na aliahidi kumuoa. Shann alidai kwamba mwaka mmoja baadae Vincent alitaka kumfarkanisha na familia yake. Alipopata ujauzito na kushuhudia vitendo vya kikatili vya Vincent aliachana naye.

Akiendelea na mduara wake wa kuoa na kuacha, mnamo mwaka 1992, Vincent alimuoa mwanamke mwingine aliyejulikana kwa jina la Sharon Glover. Miezi mitatu baadae waliachana. Sharon alidai kwamba, Vincent alikuwa na tabia unyanyasaji na pia aliwahi kumtishia kumuua. Walirudiana tena, lakini walitengana muda mfupi baadae. Mnamo mwaka 1996 Sharon alifungua kesi ya kudai talaka, kwa madai kwamba Vincent ana vitendo vya unyanyasaji kijinsia na alikuwa na wasiwasi kwamba hali hiyo inaweza kubadilika kuwa ya vurugu zaidi. Pia alikuwa anahofia usalama wa binti yake ambaye hakuwa amemzaa na Vincent. Mwendelezo wa kugombana kwa wanandoa hao kulikoma mwaka 1998, baada ya kuachana rasmi. Kwa upande wake Vincent alidai kwamba, Sharon na bintiye walikuwa hawamuheshimu hata kidogo, na walikuwa hawaheshimu mamlaka yake kama mume na baba wa familia. Walifikia hata hatua ya kumvunjia heshima mbele ya jamii iliyokuwa ikimuheshimu na kumthamini…………. "Mimi ni mtu ninayeheshimika sana, na kamwe sitakuwa tayari kuhatarisha nafasi yangu niliyo nayo ya makamu mkuu wa shule (ya Junior High School)." Alisema Vincent wakati fulani.

Mnamo mwaka 1997, alianza uhusiano na mwanamke mwingine aliyejulikana kwa jina la Carla Tafoya, mwalimu katika shule moja katika mji huo wa Bakersfield, huyu naye alitoa ushahidi pale mahakamani dhidi ya Vincent kuhusiana na tabia zake za uasherati. Yeye alidai kwamba baada ya Vincent kuachana na mke wake wa pili alikuwa na nyumba katika eneo la Southwest ambapo alikuwa na kawaida ya kukutana naye katika nyumba hiyo na kupitisha usiku huko wakifanya mapenzi. Alivalishwa pete ya uchumba yenye kito cha alimas mwaka 1998. Baadae mapenzi yalianza kupungua na hata mawasiliano yao ya simu yakawa sio kama zamani.

Mwaka 1999 Carla Tafoya aligundua kwamba Vincent alikuwa na mtoto wa kiume aitwae Marques ambaye alimzaa na Joanie Harper mwaka 1998. Awali Vincent alikanusha jambo hilo. Mwaka 2000, Carla alipata taarifa kwamba Vincent na Joanie wamepata mtoto wa pili ambaye aliitwa Lyndsay. Vincent alidai kwamba watoto hao sio wake……….lakini baadae alikiri kwamba watoto hao wawili ni wakwake.

Carla alielezea kuhusu namba ya simu aliyoikuta hapo nyumbani kwa Vincent. Alijaribu kuipiga namba hiyo akiigiza sauti kama ya mwanaume, lakini mwanamke aliyepokea simu hiyo aliikata. Baada ya muda kidogo Joanie Harper aliwasili katika nyumba hiyo na wakakutana uso kwa uso baada ya kuwa wamekuwa wakituhumiana kwa muda mrefu. kwa makusudi kabisa Joanie alilikwangua gari la Carla. Joanie aliomba radhi baadae kwa kitendo hicho. Carla alimtaka Vincent amthibitishie kama hajaoa, jambo ambalo lilimuwia gumu kufanya hivyo na ilipofika mwaka 2002, waliachana Vincent alikubaliana na uamuzi wa Carla kwa maelezo kwamba mambo hayakuwa kama alivyotarajia.

Wakati uhusiano wake na mkewe Joanie Harper ukiwa ni kusuasua, Vincent alikuwa na uhusiano na mwanamke mwingine aliyetajwa kwa jina la Esther Quiroz, huyu naye alikuwa ni mwalimu waliyekutana katika shule ya Emerson Middle School. Kwa mujibu wa Esther akitoa ushahidi wake pale mahakamni alisema kwamba hakuwahi kuwa na mtoko (date) na Vincent na hawakuzungumzia sana kuhusu maisha ya kila mmoja wao. Walikutana na kisha kufanya mapenzi tu. Hata hivyo Esther alidai kwamba kuna siku aliwahi kumuuliza Vincent kuhusu watoto wake wawili aliowazaa na Joanie, lakini Vincent alidai kwamba hadhani kama ni watoto wake.

Wakati alipomuoa Joanie kwa mara ya pili, hapo mnamo Januari alihamia nyumbani kwa akina Joanie na kuishi na mama mkwe wake. Ndoa yao ilianza kukumbwa na misukosuko na Vincent aliwaambia baadhi ya marafiki zake kwamba amechoshwa na mama mkwe wake kwa sababu alikuwa na tabia ya kuingilia mahusiano yake na mkewe. Kwa mujibu wa mama mkwe wake alidai kwamba Vincent alikuwa anatoa vitu vyake kwa siri hapo nyumbani. Kumbe hakujua kwamba Vincent alikuwa amepangisha nyumba katika eneo la Real Road kusini mwa mji huo wa Bakersfield, na alikuwa ameanza uhusiano na mwanamke mwingine aliyekuwa na umri wa miaka 48 aliyejulikana kwa jina la Lipe Hernandez. Huyu alikuwa ni karani katika shule ya Fremont Elementary School ambayo ndipo Vincent alipokuwa kifanya kazi kama Makamu mkuu wa shule.

Lipe alidai kwamba, kwa kuwa nyumba hiyo aliyopanga Vincent haikuwa na samani (ferniture) za ndani, walikuwa wakifanya mapenzi sakafuni. Lipe alidai pale mahakamani kwamba hakuwa anajua kuwa Vincent ameoa. Lakini mwanasheria Michael Gardina alimkumbusha kwamba Vincent ameweka picha kadhaa za watoto wake ofisini kwake.

Mwaka huo huo wa 2003, Mwanamke mwingine mhamiaji kutoka Italia ambaye alikuwa ni Dereva wa basi la shule aitwae Maria Cristafulli aliyekuwa na umri wa miaka 39, naye aliingia kwenye mduara wa Vincent. Yeye alidai kwamba aliwahi kufanya mapenzi na Vincent mara nne tu kati ya Mei na Juni 2003.
Mnamo Mei 15, 2007, kesi hiyo iliisha kusikilizwa na jopo la wanasheria waliokuwa wakisikiliza shauri hilo lilimkuta Vincent na hatia kwa kosa hilo. Na mnamo Septemba 27, 2007, Vincent alihukumiwa kunyongwa kwa kuchomwa sindano ya sumu. Hata hivyo mpaka sasa hukumu hiyo haijatekelezwa.

Akizungumza baada ya hukumu hiyo mwanae pekee kwa mama mwingine aliyebaki aitwae Margret Kern Brothers alisema kwamba, anajitoa katika ukoo wa Brothers, na atakapotoka pale mahakamni anataka atambulike kama Margeret Kern. Binti huyo aliendelea kusema, "namuacha na jina lake, mimi sina baba sasa, hatakaa anaione tena mpaka siku ya kifo chake."






 

Attachments

  • judge_02.jpg
    judge_02.jpg
    60.6 KB · Views: 310
Last edited by a moderator:
Ni Ijumaa nyingine tena, kama kawaida nimekuja na kesi hii iliyotokea nchini Marekani. Ni kesi ambayo kwa kweli inasikitisha sana na ninaamini wengi watajifunza kutokana na kesi hii. Mengi yamejieleza na sina sababu ya kuongeza chochote. Kikubwa ni kuwausia wanaume wenzangu waliooa kwamba tuwapende wake zetu na familia zetu, kama tukiendeshwa na mihemko ya kupenda ngono matokeo yake yaweza kuwa kama haya. Zamani tulikuwa tunasema kwamba matukio ya namna hii yanatokea kwa wenzetu, lakini kwa jinsi siku zinavyozidi kwenda tumeanza kushuhudia matukio ya kutisha yanayofanana na haya.

Unaweza ukawa mahiri katika kupanga mikakati ya kutekeleza kile ulichokusudia, iwe ni kudhuru au kuuwa, lakini sayansi na teknolojia imeleta mapinduzi makubwa katika kufanikisha upelelezi wa kesi ambazo zimeonekana kuwashinda magwiji. Mfano mzuri ni kesi hii ya Vincent Brothers.
 
um so...:sad::sad::sad: Mtambuzi....unyama kama huu hutegemei afanye mwanadamu...ama kweli mwanadamu ni mnyama hatari kuliko wanyama wengine wote.

kisa kizuri DAWG!
 
Last edited by a moderator:
Ni Ijumaa nyingine tena, kama kawaida nimekuja na kesi hii iliyotokea nchini Marekani. Ni kesi ambayo kwa kweli inasikitisha sana na ninaamini wengi watajifunza kutokana na kesi hii. Mengi yamejieleza na sina sababu ya kuongeza chochote. Kikubwa ni kuwausia wanaume wenzangu waliooa kwamba tuwapende wake zetu na familia zetu, kama tukiendeshwa na mihemko ya kupenda ngono matokeo yake yaweza kuwa kama haya. Zamani tulikuwa tunasema kwamba matukio ya namna hii yanatokea kwa wenzetu, lakini kwa jinsi siku zinavyozidi kwenda tumeanza kushuhudia matukio ya kutisha yanayofanana na haya.

Unaweza ukawa mahiri katika kupanga mikakati ya kutekeleza kile ulichokusudia, iwe ni kudhuru au kuuwa, lakini sayansi na teknolojia imeleta mapinduzi makubwa katika kufanikisha upelelezi wa kesi ambazo zimeonekana kuwashinda magwiji. Mfano mzuri ni kesi hii ya Vincent Brothers.

Asante sana Mtambuzi yani mpaka machozi yamenitoka.......kuna binadamu walitakiwa kuwa wanyama tu ili mtu ujue moja kwa moja umekutana na mnyama na sio binadamu mwenzio!
 
dah hii kitu Adamu na hawa ndio waanzilishi af hawajui kama wametuashia matatizo makubwa sana kwenye hii TASNIA ya mMAHABA tutayaenzi vip mazuri yao?
 
inabidi kila binadamu afungiwe king'amuzi cha anayoyawaza ili waweze kutusaidia kutatua msongo wa mawazo ambayo hayana kichwa wala miguu,aisee hongera sana.MUNGU ATUREHEMU
 
Hizi ndio shida za idadi kubwa ya sisi wanaume, watu wanazipenda sanaaa faida za mahusiano lakini majukumu yake hawayawezi! Mtu ana wanawake kibao, kuwalea na watoto hawezi na wanawake wa marekani wanavyojua kukaba kwenye maswala ya baba kusupport familia! Jamaa akaona bila kuua hachomoki kimaisha!
Where is the life he's been fighting for now?
Kwa kweli tunakushukuru Mtambuzi kwa kuzidi kutufungua macho, mwenye macho na asome- mwenye ufahamu na aelewe kwamba hizi tabia matokeo yake ni nini...
 
Last edited by a moderator:
Mtambuzi Hakika hii inasikisha sana, hivi niwaulize ninyi wanaume kama unajiona huwezi kumudu gharama za maisha ukiwa na familia mlango wa nyota ya kijani upo kwanini usiingie humo? ili uishi kwa kutegemewa na kichwa chako tu.

Nawapongeza sana wapelelezi wa huko wanajua kujituma ktk kazi yao, lakini vijana wa Mwema lol...ni wao na vibaka tu.
 
Last edited by a moderator:
@Mtambuzi hii Kesi inasikitisha sana na pia sisi kama watanzania na jeshi letu la polisi linatakiwa kujifunza kitu, sina uhakika kama huwa wanasoma kesi kama hizi na kujifunza kitu ila ukweli ni kwamba kesi za mapenzi zimesababisha mauaji mengi sana na twatakiwa kuwa makini sana tunapochagua mtu wa kuishi nae kama mume/mke.
 
Mkuu Mtambuzi pamoja na ugumu wa ushahidi wa kumtia hatiani Vincent brothers lakini hapa unaona namna utaalamu wa kisayansi unavyofanya kazi.
Changamoto kubwa kwa wapelelezi wetu wa jeshi la Mwema ni upatikanaji na matumizi ya sayansi katika kutafuta na kupata ushahidi.
Nina uhakika hapa kwetu kuna kesi za namna hii nyingi sana lakini wahusika wako nje wanadunda bila wasiwasi, kwakuwa pamoja na kutokuwa na uwezo wa kisayansi wa kufanya utambuzi, hata rushwa nayo imewafanya wapelelezi watindikiwe weledi katika kazi zao.
 
Last edited by a moderator:
Back
Top Bottom