Utoaji mimba

SN_VijanaFM

Member
Mar 25, 2010
58
0
Siku chache zilizopita nili-post makala moja kwenye tovuti ya Vijana FM | Karibuni kuhusu suala la utoaji mimba. Makala ni kama ifuatavyo: Vijana FM: Utoaji mimba

___________________

Kuna mambo nyeti ambayo hupaswa kuangaliwa na kujadiliwa kwa utulivu wa hali ya juu. Hatuna budi kujaribu kuweka hisia na "uzoefu" wetu pembeni ili tuweze kupata suluhisho ambalo litasaidia mabinti na dada zetu; bila kusahau vizazi vyetu vijavyo kwa ujumla.

Abortion_TZ.bmp


Kutokana na utoto wangu, nimekuja kulielewa na kuanza kulifuatilia suala la utoaji mimba nilipokuwa kidato cha pili. Wakati ule nilikuwa nashangaa: Vipi, Vijana wanaonekana wanashiriki sana kwenye vitendo vya ngono, lakini "matokeo" (ukiacha Ukimwi na magonjwa mengine ya zinaa) mbona siyaoni? Na akili yangu ilikuwa inaniambia hivi vitu vitatu vina tabia ya kwenda sambamba kwenye jamii zenye desturi kama zetu.

Bahati mbaya watu walionipa mwangaza kwenye mambo yanayoendelea mitaani walikuwa ni Vijana wenzangu vijiweni.

Utoaji mimba... Unashtukia binti fulani anatoweka darasani kwa siku kadhaa halafu akirudi unaona kuna mabadiliko fulani. Ingawa bado nilikuwa kinda, lakini kuna ile sauti kichwani kwangu iliyokuwa inaniambia kuwa vitu haviko sawa kama inavyotakiwa.

Wiki mbili zilizopita Serikali imeamua kuvalia njuga hili suala na kuanza kufunga zahanati na vituo vyote ambavyo hushiriki (kwenye) utoaji mimba. Inaonekana Serikali kama inatumia ile tactic ya kijeshi ya kumshtukiza adui wakati hategemei kabisa kushambuliwa. Lakini tukumbuke hapa tunapigana vita na kuuana wenyewe tu.

Mimi sio mtaalamu wa afya na nisingependa kuhusisha imani za dini kwenye huu mjadala. Kwa kifupi -- kwa maoni yangu binafsi -- nadhani wazee wetu wangejaribu kulivalia njuga hili suala kwa upole kiasi. Kwanza, kuangalia nini hasa ni chanzo cha hizi mimba zisizo na mpangilio. Pili, kujaribu kupunguza haya matukio kwa kutumia elimu na sauti ya utulivu. Tatu, kuwaonya na kuwaambia watu wanaohusika na utoaji mimba kuwa 'tunawaona, tunawajua na tunaamuru muanze kusafisha nyumba zenu!'

Bila kusahau kuwaasa wazazi kuongea na watoto wao kwa uwazi - mabinti na wavulana, pia. Kwasababu inaonekana jamii yetu bado ina ile soni ya kuongelea mambo ya ngono na madhara yake.

Nisingependa kuwapotezea muda wenu kwasababu nina uhakika hamtajifunza jipya kutoka kwangu. Kwahiyo, nawaasa wale ambao wanasomea haya mambo, kuyafuatilia au kufuatilia nchi ambazo takwimu zao kwenye mambo kama haya ni nzuri, kutupa ujuzi na maoni.

Natumaini sauti zetu zitawafikia wahusika, kwasababu hili jambo ni nyeti mno na linahitaji kuguswa kwa utulivu kama tunavyotoa uchafu kwenye mboni za macho yetu.

___________________

Ningependa kusikia maoni yenu hapa au kwenye tovuti (Unaweza uka-post hapa na ku-copy maoni yako kwenye tovuti). Nia hasa ni kuwafumbua macho Vijana; sio jambo la busara kusikia haya mambo vijiweni tu.

Natanguliza shukrani za dhati kwa ushirikiano wenu.
 
Back
Top Bottom