nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Tuesday, 17 July 2012 21:39 |
UTEUZI wa Kadhi Mkuu na makadhi wa mikoa 14 uliofanywa na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Mufti Issa Shaaban Simba, umeibua mvutano miongoni mwa Waislamu. Juzi, Mufti Simba alimtangaza Sheikh Abdallah Mnyasi kuwa Kadhi Mkuu na pia aliwateua Manaibu wake wawili, Sheikh Abubakar Zubeir na Sheikh Muhidini Mkoyogole. Wakizungumzia uteuzi huo, baadhi ya viongozi wa taasisi za Kiislamu walisema kilichofanyika ni uteuzi wa kiserikali na si wa Kiislamu. Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda alisema uteuzi huo ni wa kiserikali na siyo wa dini... "Hata mkutano wenyewe ulisimamiwa na Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib Bilal ndiyo maana tunasema uteuzi huu una ladha ya kiserikali." Sheikh Ponda alisema uteuzi huo ni wa Baraza Kuu la Waislamu wa Tanzania (Bakwata) na haujawashirikisha Waislamu kutoka katika taasisi zao nyingine. Alisema moja ya malengo ya uteuzi huo ni kuwaondoa Waislamu katika ajenda yao ya kutaka Mahakama ya Kadhi katika utoaji wa maoni ya Katiba Mpya. Alisema lengo jingine ni kutaka kuwaondoa Waislamu kwenye msimamo wao wa kutoshiriki kwenye Sensa ya Watu na Makazi inayotarajiwa kufanyika mwishoni mwa Agosti, mwaka huu. "Lakini, tunasema msimamo wetu upo palepale. Uteuzi huu hautarudisha nyuma harakati zetu kwa sababu Bakwata ni sehemu tu ya Waislamu nchini," alisema Sheikh Ponda. Katibu wa Baraza la Habari la Kiislamu Tanzania (Bahakita), Said Mwaipopo alisema kwa kuwa hawajashirikishwa, kuna uwezekano wa kila taasisi kuwa na kadhi wake. "Bakwata si wamewateua makadhi wa mikoa bila ya kuzishirikisha taasisi nyingine za dini ya Kiislamu? Basi nazo zikiamua zinaweza kuteua makadhi wake wa mikoa," alisema. Alisema kuna taasisi nyingi za Kiislamu nchini na kwamba, Bakwata ni moja ya taasisi hizo... "Sasa kama linafanyika jambo kubwa kama hilo halafu wadau wanalisikia kwenye vyombo vya habari unategemea nini? Nao wataamua kuteua makadhi wao." Akizungumzia uteuzi huo, Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano kwa Umma wa Bakwata, Shaaban Simba alisema ulifanyika juzi Mjini Dodoma baada ya mkutano wa Tume ya Dini ya Baraza hilo na kwamba makadhi wa mikoa mingine watateuliwa baadaye. "Mufti anaendelea na mchakato wa kuwateua makadhi wa mikoa mingine na watakapokamilika watatangazwa," alisema. Simba alisema baada ya kuteuliwa makadhi wengine wa mikoa uteuzi utakaofuata ni wa makadhi wa wilaya. Kwa upande wake, Kadhi wa Mkoa wa Dodoma, Sheikh Mustafa Rajab alisema uteuzi huo umefanyika katika kipindi muafaka.Alisema Serikali ilitoa tamko la kuwataka Waislamu waanzishe Mahakama ya Kadhi ambayo wataiendesha wao wenyewe. "Badala ya kuendelea kubishana na Serikali, Baraza limeamua kufanya uteuzi kwa ajili ya kuanzisha chombo hiki lakini, bado tunaendelea kuzungumza na Serikali kuangalia namna inavyoweza kukiendesha chombo hiki kwa kushirikiana na Waislamu," alisema. Walioteuliwa Simba aliwataja makadhi wa Mikoa 14 walioteuliwa juzi kuwa ni Sheikh Masoud Himid Jongo (Dar es Salaam), Sheikh Mustafa Rajab Shaaban (Dodoma), Sheikh Zukher Bin Sheikh Bakher (Tanga) na Sheikh Hamis Maalim Abbas Mtupa (Pwani). Wengine ni Sheikh Shaaban Bin Jumaa (Arusha), Sheikh Shaaban Rashid (Kilimanjaro), Sheikh Salum Fereji (Mwanza), Sheikh Ismail Habib Makusanya (Shinyanga), Sheikh Abdallah Ali (Mtwara), Sheikh Muhamad Hamis Mushangani (Lindi) Sheikh Athuman Magee (Mara), Sheikh Idrisa Abdul Muhsin Kitumba (Kigoma), Sheikh Rashid Akilimali (Rukwa) na Sheikh Shaaban Salum (Tabora). |