Utafiti:Chanjo ya ukimwi yagundulika

HP1

JF-Expert Member
Feb 4, 2012
3,362
874
UTAFITI wa hivi karibuni uliofanywa katika Chuo Kikuu cha Tiba cha Johns Hopkins nchini Marekani, umegundua kuwa matumizi ya dawa za kurefusha maisha (ARV) yanaweza kuwafanya waathirika wa Virusi vya Ukimwi (VVU) kukutana kimwili na wapenzi wao bila kondomu, pasi kuwapa maambukizi.

Wakati wataalamu hao wakifikia hatua hiyo muhimu katika kupata jibu la janga hilo lililoitesa dunia kwa miongo kadhaa sasa, kuna taarifa njema pia za kugunduliwa kwa chanjo mpya ya Ukimwi.

Kwa upande wa utafiti wa ARV walioufanyiwa majaribio kwenye sehemu mbalimbali za dunia, umebaini kuwa mtu ambaye anatumia dawa za kurefusha maisha, anaweza kufanya tendo la ndoa bila ya kutumia kondomu na mtu ambaye hana Ukimwi na asimwambukize kwa asilimia 95.Mkuu wa Mtandao wa Maabara za Kuchunguza VVU katika chuo hicho, Profesa Susan Eshleman, alisema kwenye ripoti ya ugunduzi huo, wamebaini dawa za kurefusha maisha kwa waathirika wa HIV, sasa zinaweza kutumika kama sehemu ya kuzuia maambukizi.

Profesa Eshleman alisema kwamba muathirika wa VVU anayetumia ARV kikamilifu anaweza kujamiiana na mtu ambaye hana virusi bila kondomu na asimwambukize.

“Huu ni ugunduzi wa kustajabisha,” alisema Profesa Eshleman akifafanua: “Matokea haya yameleta mapambazuko mapya katika sayansi ya kuzuia maambukizi na inawaweka watafiti kwenye mazingira mazuri zaidi ya kupata suluhisho la kukabiliana na maradhi haya.”

Walivyogundua njia
Profesa Eshleman anasema utafiti huo walioupa jina la HPTN 052 walifanya kupitia maeneo mbalimbali ya dunia hasa yenye kasi kubwa ya maambukizi kama vile Afrika, Brazili, India na Thailand.

Kwenye ripoti hiyo ambayo pia ilichapishwa kwenye jarida maarufu la kisayansi linaloitwa Science, watafiti hao wanasema kwamba mtu anapotumia ARV, hufikia wakati fulani wingi wa virusi mwilini hupotea kiasi kwamba anakuwa karibu sawa na yule ambaye hajaambukizwa.

“Jambo la msingi katika utafiti huu ni kwamba dawa hizi za kurefusha maisha zinapotumiwa kikamilifu, hupunguza mzigo wa virusi mwilini kwa zaidi ya mara 200. Ni sawa na kusema inapunguza hadi kufikia karibu na sifuri,” inaeleza ripoti hiyo.
Ni katika mazingira hayo, ripoti hiyo inasema kuwa damu ya muathirika inakuwa haina virusi na hivyo uwezekano wa kumuambukiza mpenzi wake unakuwa haupo.

Ripoti hiyo inaeleza kuwa ARV inafanya kazi mbili, kwanza kurefusha maisha ya muathirika kwa kupunguza virusi mwilini na pili ni kumkinga asiambukize wengine.

Sifa nyingine ya ARV, anasema ni kwamba inapunguza uwezekano wa waathirika kupata ugonjwa wa Kifua Kikuu (TB) kutokana na kiwango cha kinga za mwili kupanda.


Onyo la utafiti

Pamoja na kwamba njia hii imeonekana kuwa ni nzuri kwa ajili ya kuzuia maambukizi, wataalamu hao wanasema ni hatari pale itakapotumika vibaya.

Hatari wanayoizungumzia ni kwa muathirika iwapo atatembea na mpenzi ambaye ni muathirika, lakini akawa hajatumia ARV au ametumia, lakini siyo kwa kiwango ambacho VVU vimepunguzwa hadi kufikia karibu na sifuri.

Watalaamu hao wanasema iwapo muathirika atapata maambukizo mapya, atajiweka katika hatari ya kupata usugu kwa aina ya ARV anayotumia.

Ili kuwaweka katika mazingira salama, wataalamu hao wamewashauri waathirika wanaotumia ARV kutobweteka na badala yake kuendelea kutegemea kondomu kama moja ya njia za kuzuia maambukizo mapya na kuimarika kiafya.

Wataalamu wazungumzia utafiti huo

Wataalamu na watafiti mbalimbali wameelezea utafiti huo kuwa ni mafanikio mazuri katika kurahisisha njia ya chanjo katika kutoa kinga kwa waathirika na wale ambao hawajaambukizwa.

Kwa sasa zipo aina nane za chanjo za Ukimwi duniani ambazo wataalamu wapo kwenye hatua mbalimbali za majaribio na wamekuwa wakizielezea kuwa zina matumaini.

Mkuu wa Mambo ya Afya wa Serikali ya Marekani, Profesa Anthony Fauci ambaye pia ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Kuambukiza na Mzio (NIAID), aliuelezea ugunduzi huo kuwa ni wakushangaza.

Wataalamu wengine pia wakauelezea kuwa mtu anaweza kuuchukulia kama ni utani, lakini ni jambo ambalo litaleta mapinduzi makubwa ya kukabiliana na VVU.

Profesa Eshleman alisema utafiti wao utafungua urahisi wa njia ya wanasayansi wanaoendelea na tafiti nyingine kuwa katika mazingira mazuri ya kutatua tatizo hilo.
Profesa Eshleman anasema mkakati walio nao kwa sasa ni kufanya uchunguzi zaidi wa njia hiyo katika ngazi ya kijamii na kimataifa.

Alisema anaamini kwamba njia hiyo itakuwa na matokeo mazuri katika ngazi hiyo kabla haijathibitishwa rasmi kutumika kimataifa.

A.Kusini waiwekea mkakati

Serikali ya Afrika Kusini tayari imeweka mkakati wa kutumia njia hiyo kuliokoa taifa hilo lenye kasi kubwa ya maambukizo kuliko mengine duniani.
Mmoja wa wataalamu wa afya wa nchi hiyo, Dk Brian Williams, anasema tayari wamefanya tathmini na kuona baada ya miaka mitano watakuwa wamefanikiwa kuyakabili maradhi hayo.Dk Willams, anasema Afrika Kusini ina waathirika milioni sita na kwamba ni asilimia 30 tu wanaopatiwa tiba ya ARV.

“Ili kuwagharimia waathirika hao itabidi tutumia Dola za Marekani kati ya milioni mbili hadi tatu (Sh 3.2 trilioni hadi 4.8 trilioni) kununua dawa za ARV kwa mwaka,” alisema Dk Williams.

Kutokana na uzoefu wake, Williams alisema utafiti huo utasaidia waathirika kuwa katika mazingira mazuri ya kupatiwa chanjo ambayo ipo mbioni kupatikana.

Tanzania ipo pazuri

Tanzania ni moja ya nchi ambazo matumizi ya ARV kwa waathirika ni makubwa kutokana na mpango wa Serikali wa kuwapatia dawa hizo bure kote nchini.

Tangu Rais Jakaya Kikwete atangaze mpango wa kupima kwa hiari miaka michache baada ya kuingia madarakani, aliwahakikishia wale wote watakaojikuta wameambukizwa, watapatiwa dawa za kurefusha maisha bure.

Mwananchi Jumapili lilipowasiliana kwa njia ya simu na Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Hadji Mponda, alisema asingeweza kulizungumzia suala hilo kwa kuwa hakuwa ofisini na asingependa kuzungumza kwa njia ya simu.

Mkuu wa Utawala wa Taasisi ya Utafiti wa Tiba ya Binadamu Hospitali ya KCMC (KCRI), Lucy Shara alilimbia gazeti hili kwamba suala la matumizi ya ARV nchini imekuwa ikifanyika ipasavyo kwa wale wanaojitokeza kwa hiari.

Shara alikiri kuwa wataalamu nchini wamekuwa kwenye tafiti mbalimbali za VVU na kwamba hata suala la ufanisi wa dawa za ARV wamekuwa wakiujadili mara kwa mara kupitia vikao na semina mbalimbali.

Lakini akasema suala la utafiti huo wa Marekani lilijadiliwa kwenye mkutano uliofanyika Jijini Dar es Salaam karibuni.

“Juzi tulikuwa kwenye semina hapo Dar es Salaam. Wasiliana na wataalamu wetu wa pale Muhimbili (Hospitali ya Taifa) wanaweza wakakueleza jambo hili kwa uzuri zaidi,” alisema Shara.

Juhudi za kuwapata wataalamu wa Utafiti wa Chuo Kikuu cha Tiba na Sayansi Muhimbili (MUHAS) kulieleza suala hili hazikufanikiwa kutokana na tatizo la kimawasiliano.

Chanjo mpya yagundulika
Utafiti wa chanjo Ukimwi uliosimamiwa na Chuo Kikuu cha Tiba cha Harvard nchini Marekani na kusimamiwa na Profesa Dan Barouch wa chuo unaelezewa kuwa na mafanikio makubwa katika kukabiliana na ugonjwa wa Ukimwi ambao mpaka sasa hauna chanjo wala tiba ambayo imetambuliwa rasmi kimataifa.

Taarifa iliyotolewa NIAID kwa gazeti hili wiki iliyopita, inaeleza kuwa utafiti huo uliofanywa Profesa Nelson Michael wa Jeshi la Marekani, akishirikiana na Profesa Jaap Goudsmit, Dk Vanessa Hirsch na Ilnour Ourmanov, una sema mafanikio ya utafiti huo yanawapa matumaini ya kupata chanjo madhubuti.

Walisema kwenye ripoti hiyo kuwa katika majaribio kadhaa waliyofanya, chanjo hiyo iliweza kumsaidia Nyani kuwa na chembechembe kinga ambazo zina uwezo wa kumkinga asiweze kuambukizwa VVU.

Utafiti huo uliotangazwa Januri 4, mwaka huu unaeleza kuwa kinachofanyika kwa sasa ni kuendelea na utafiti huo katika hatua ya majaribio kwa binadamu.Kwa sasa chanjo hiyo walisema ipo kwenye hatua ya awali ya majaribio ya usalama wa dawa kabla ya kuingia kwenye majaribio ya uwezo wa dawa kwenye mwili wa bianadamu.

Utafiti ulivyofanyika

Walisema walimpa nyani chanjo hiyo na baada ya muda alitengeneza chembechembe kinga za aina ya protini na walipojaribu kumuambukiza VVU, virusi walidhibitiwa na kushindwa kushambulia seli nyeupe za binadamu ama kwa jina la kitaalamu CD4, ambazo ni kinga muhimu dhidi ya maradhi mengine.

Kwa kawaida VVU hushambulia seli hizi nyeupe na kuzifanya makoloni ya kuwawezesha kuzaliana na kuongezeka mara dufu mwilini hivyo kujenga mazingira ya mtu kuugua Ukimwi.

Matokeo ya utafiti huo yanafikisha idadi ya aina nane za chanjo dhidi ya VVU ambazo zimo kwenye majaribio katika hatua mbalimbali duniani.

Mojawapo ya chanjo hizo amabazo zipo kwenye hatua mbalimbali za majaribio, ipo ile ambayo mafanikio makubwa yalichangiwa na wanasayansi wa hapa nchini waliokuwa wanafanya kazi katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC, mkoani Kilimanjaro.

Wanasayansi wa Tanzania waligundua kwamba baadhi ya watu walioathirika na Virusi vya Ukimwi (VVU), kwa muda fulani wanajijengea wenyewe kinga inayoweza kudhibiti virusi hivyo na kuwa na afya njema bila kuwa na haja ya kutumia dawa za ARV.
 


Wataalamu hao wa KCMC mjini Moshi walifanikisha utafiti huo wa mwaka 2006 na 2010 na mwishoni mwa mwaka jana wakaliambia Mwananchi Jumapili kuhusu ugunduzi huo.

Kiongozi wa Ushirikiano wa kiutafiti kati ya KCMC na Chuo Kikuu cha Afya cha Duke cha nchini Marekani, Dk Elizabeth Reddy aliliambia gazeti hili kuwa matokeo hayo yatawezesha kutengeneza chanjo itakayowezesha watu wote kuwa na kinga hizo, hivyo kutoathirika na VVU.



Alisema jambo la msingi katika utafiti huo ni kugundulika kwa VVU kuwa wana gamba lenye protini iliyochanganyika na sukari, ambayo huvifanya kushindwa kutambuliwa na kinga za kawaida za mwili wa binadamu.
 


Lakini, Dk Reddy alisema kuwa katika ugunduzi wao, wamebaini aina ya kinga za mwili ambazo hutambua virusi kupitia aina hiyo ya sukari kwenye gamba la nje la VVU na kuvishambulia hadi kuviua.
 


Alisema kuwa utafiti huo ulifanyika katika maabara ya KCMC kwa ushirikiano wa timu ya wataalamu wa afya wa Tanzania pamoja na wa Marekani.

Alibainisha kuwa utafiti huo ulihusisha Watanzania kadhaa walioambukizwa VVU hapa nchini, lakini wamekuwa wakiishi bila kuathirika. Dk Reddy alisema kuwa utafiti huo umefanyika maeneo mengi duniani, lakini kituo cha KCMC ndicho kilichotoa mwanga mkubwa zaidi ambao hatua zake za mwisho zilithibitishwa na wataalamu waliobobea nchini Marekani.
 


Kiongozi huyo wa utafiti, alisema kuwa Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa inayosimamiwa na Mfuko wa Good Samaritani (GSF) ambao ndio pia unaosimamia taasisi nyingine kama vile Chuo Kikuu cha Afya cha Tumaini na Hospitali ya KCMC, ndiyo inayopaswa kupewa shukurani kwa matokeo hayo.

Dk Reddy anaamini kwamba ndani ya kipindi cha miaka mitano ijayo, chanjo kadhaa zitakuwa zimethibitishwa.
 
Back
Top Bottom