Upinzani umekufa Z'bar umebakia Uzanzibar.

abdulahsaf

JF-Expert Member
Aug 31, 2010
858
130
maalim-17-564x272.jpg

  • Achezea kusi kwa tanga bovu
  • Mseto waelekea kumsonga
Na: Malik Nabwa
Msanii maarufu, machachari, na mwenye vituko vya wali maji nchini Uingereza Sir. Elton John aliwahi kuimba wimbo siku ya kifo cha Princess Diana. Wimbo huo uliitwa ‘’Candle in the wind’’. Yaani mshumaa katika upepo. Wimbo huu ulikifu sadfa ya shuhuli yenyewe ya maombolezi na pia kwa mtu wenyewe aliyefariki yaani Princess Diana. Kwa watu wanaomfahamu Diana, watakubaliana nami kwa kiasi kikubwa kuwa alikuwa mtu maarufu na aliependwa mno na watu. Alikuwa mtu wa watu ukiachilia mbali uluwa aliokuwa nao.
Hali kama hii tulibahatika kujaaliwa nayo sisi wazanzibari. Kama India na Shah Rukh Khan au Amitabh bachan, Iran na Khomeini, Marekani na Martin Luther King (Jr), basi hapa Zanzibar tumejaaliwa Maalim Seif Shariff Hamad, Makamo wetu wa kwanza wa Rais. Maalim Seif ni katika watu wachache wenye kipawa cha kuzaliwa cha kupendwa (inborn Charismatic power) hapa visiwani. Maalim alianza kupata umaarufu mnamo mwaka 1978 baada ya kupanda hafla kutoka mwalimu wa shule huko alikoakisomesha Castro na baadae Unguja ambapo mara aliteuliwa kuwa Waziri wa Elimu na hatimae Waziri Kiongozi.Lakini kwa sasa nahofia jee amekuwa mshumaa katika upepo? Mbona haonekani?
Katika miaka yake hiyo namfahamu vizuri Maalim Seif kama alikuwa mtu mzuri, mchapa kazi na mtendaji mkuu kabisa aliekuwa na huruma na uzalendo wa nchi huu kupita watu wengi. Kipindi cha Maalim kinakumbukwa kwa kujaa neema ya ghafla.Neema ya mungu akitaka kupa hakutumii barua. Kipindi cha Maalim Seif tulikuwa na Zanzibar yenye neema na utulivu. Maalim huyu baadae alihitilafiana na Upande wa Serikali na kukutwa na masahibu mengi ambayo yalimuondoa katika utendaji wa maendeleo hadi alipoamua kuunda chama cha CUF. Maalim Seif ndani ya chama cha CUF alikuwa mtu madhubuti sana na aliweza kujenga imani na matumaini kwa kila mzanzibari jambo lililompa heshima kubwa nchini.
Cha ajabu, Maalim Seif ambae sasa ni sehemu ya Serikali anaonenekana kufifia mno. Sisi wengi wetu tunashangaa kila tunapofikiria uoni wa Maalim wa kukubali kuingia katika mseto. Tulishawahi kusema kutoka siku ya kwanza kuwa Maalim anawezekana kabisa anaona mbali zaidi kuliko sisi wengi lakini yalitoa indhari zetu kuwa kwa maalim Seif kukubali kuingia ujiko na chama Tawala Zanzibar ni kupoteza mwelekeo na kurudisha nyuma juhudi za Zanzibar za kujikwamua na mashaka mengi yanaoyoikabili sasa.
Tulilaumu sana kitendo cha Maalim kupitia chama chake chenyewe kuleta hoja binafsi ya kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa, huku akigawa mamlaka kwa makamo wa kwanza wa Rais kuwa pale bila kazi maalum ya kiutendaji ni mwanzo wa ugonjwa unaoikabili Zanzibar chini ya maamuzi ya CUF na Maalim Seif. Leo maalim yumo Serikalini lakini hana nguvu yoyote ya kuweza kufanya lolote kabisa na tunaona kuwa amejaribu mambo kadhaa ya kimaendeleo lakini kwa vile hana mamlaka na maamuzi basi hakuna kilichokuwa.
Tumeona juhudi kubwa za Maalim za kuiombea misaada Zanzibar mara kadhaa baada ya kuingia madarakani tu na sasa ni zaidi ya siku mia moja. Maalim akirudi na misaada hiyo Mkuu wake wa Kazi yaani Rais hulirudisha hilo kuwa la Muungano na kuzifanya juhudi za Maalim kuwa kazi ya zeze. Maalim Seif ndani ya Mseto uliopo amaejaribu sana kuwa muwazi na kutaka kufanya mashirikiano ya kweli na wenza wake lakini kadiri anaposafi nia na kuleta mawazo ya kimaendeleo hufanyiwa dhihaka na kebehi ya kuambiwa kuwa kitu hichi kipitiwe Muunganoni huko ndio kije huku.
Maalim huyu hata ikiwa haridhishwi na uteuzi, uendeshwaji, na utendaji mdogo wa Serikali yake sasa basi bado hupuuzwa tu na hakuna kinachofanyika. Kinachojitokeza hapa ni kumtia dosari Maalim Seif kwa kumvalisha suti iliyochanika makalioni na kumtoa ukumbini kuonana na mkwewe.. Zanzibar chini ya Serikali ya maalim Seif na wenzake imeshuhudia kasi ndogo ya maendeleo nchi nzima, huku kukiwa na tishio kubwa la njaa mashambani na mijini. Tumeona Kaskazini Pemba na Unguja mikoa ambayo mara nyingi huwa na neema kuliko mengine ndio haswa iliyokomoka sana.
Tumeshuhudia Serikali ikiwa kubwa kupita kiasi na huku ikrudishwa nyuma kwa kuweka mahafidhina na watu wasio na hatma nzuri ya kiungozi wa nchi hii. Kwa mfano uteuzi wa mkurugenzi wa Ardhi kuwa mtu wa bara na mkristo kumezua masuali mengi kuhuusu hatma ya ardhi ya Zanzibar na kuporwa na kanisa. Hili dogo lakini Ukiachilia mbali mawaziri na manaibu Serikali nzima imejaa ‘’wenyewe’’ mahafidhina kindakindaki (Hardcore conservatives) wa CCM ambao rekodi yao ya kupinga kila la heri na kuitisha la shari haijawahi kutiliwa shaka. Yote haya na mengine kiwera ni moja kati ya taka zinazonuka vundo kali puani kwa maalim Seif ambae nina uhakika haridhishwi na yote haya lakini atafanya nini na yumo katika jahazi la MV. MARIDHIANO?
Imefikia pahala Maalim akiwa katika jahazi la MV Maridhiano lenye manahoza panya buku ambao wanalitoboa jahazi hili wanalosafiria, kwa bahati mbaya kumetokea kusi kali na tanga likachanika. Jahazi halina mashine na kwa hapa lilipo ni mkondoni. Maalim hawezi kutoka na sisi kama watoto wake tunamtazama yeye machoni kuona atafanya nini.Lakini wapi hakuna jibu Kimya? Hana la kutwambia maana chombo kinajaa maji na tunaghariki kwa kweli. Maalim amekwama pahala ambapo alikuwa anahitajika sana na wananchi wa kawaida, akiwa kama mtetezi wa wananchi na sio Serikali ya mapatano kama ilivyo sasa.
Wakati huu Maalim akipumulia mashine, Zanzibar inajikakamua kujikwamua na mashaka kadhaa yakiwemo yale ya Muungano. Tunajua Maalim hayupo kuuvunja Muungano lakini naamini yeye angeweza kusimamia vema hoja ya angalau kupunguza na kutatua kero za Muungano kubwa hasa zile zinazotubana sisi kama nchi huru na kamili. Hivi sasa Zanzibar haihitaji chochote ila ni kujikwamua na Muungano Muflisi na hili ndio kero la kila mwananchi wa Zanzibar kwa sasa. Maalim amejikita katika maridhiano ambayo kimsingi si maridhiano kwa kweli bali ni MAPOZANO tu ili watu wapate kujifanyia yao (Seriakli ya Mapozano ya Kitaifa).
Hebu sasa tutizame. Ingekuwa Maalim ni yule tunayemfahamu ambaye angekuwa bado ni mpinzani na mtetezi wa wanyonge na huku kukiwa na nguvu za nje za kizalendo za kutaka kuumegua muungano na kuikomboa Zanzibar ingekuwaje? Bila shaka tumekuwa mbali. Tukiacha hili, Maalim alidhani kwa kuwemo Serikalini angeweza kuingiza nia yake safi ya kuikomboa nchi hii anagalau kimaisha lakini hivi sivyo. Tumeshaona hapo awali kuwa maalim hana kauli kabisa ndani ya Serikali hiyo. Isitoshe pamoja na kama watu kama Abuubakar kupewa Wizara ya Katiba na Sheria basi hakuna lolote atakaloweza kulifanya pale hata ingekuwa vipi. Ingekuwa kuna maridhiano ya kweli (sio Mapozano) na ikawa Maalim anafanya kazi vizuri na wenzake (CCM) ambao hupenda kuona wananwake Waliovaa fulana za njano za CCM maskanini kuazimisha siku mia au kufungua maskani, basi Zanzibar isingekuwa hapa ilipo siku mia tu baada ya huo mseto wa mapozano. Nionavyo Serikali ya Maalim Seif ni zaidi ya jahazi la Nuhu maana jahazi hili alilopandishwa Maalim Halliwezi kufika ufukweni katu na hata likifika basi Maalim ataapa kuwa hatalipanda tena maisha yake yote.
Hayo na mengine mengi natoa tanbihi tena kuwa Maalim Seif ana wakati mgumu sana katika Serikali hii kiasi ya kusema anahitaji msaada wetu kwa kiasi kikubwa. Wazalendo tumsaidieni Maalim. Tusione kanyamza kimya tukaona hana shida lakini mtu mzima halii kwa yowe watuni. Tuunge nguvu jamani tumsaidie maalim kwa kuayafanya yale ambayo tulitegemea atufanyie. Kubwa katika mambo ambayo tungetegemea atuongoze ni hili la kuifanya Serikali ya Zanzibar iwe madhubuti kiutendaji na hata kuiletea maslahi nchi hii jambo ambalo limeshindikana.
Tumsaidie Maalim kuikomboa Zanzibar kwa kuupunguza kasi Muungano ambao ndio hasa kikwazo kikubwa kwa nchi hii.Tumsaidie Maalim azinduke kuwa huko aliko amepotea na kama hatotanabahi sasa basi atadedeleka kabisa kabisa kama kuku mgeni asie na kijugwe. Tumsaidie maalim arudi katika pumzi yake ya kawaida, aondokane na dharuba ya kusi iliyo kubwa akiwa katika jahazi la maridhiano. Tuapambane tuikomboe nchi yetu, Na kwa kufanya hivi maalim atazinduka na atarudi katika hali yake ya kawaida. Tuunge nguvu, tujikomboe
Wakatabahu
Nabwa
#gallery-1 { margin: auto; }#gallery-1 .gallery-item { float: left; margin-top: 10px; text-align: center; width: 33%; }#gallery-1 img { border: 2px solid rgb(207, 207, 207); }#gallery-1 .gallery-caption { margin-left: 0pt; }

 
Back
Top Bottom