Umri wa kuishi waongezeka Tanzania

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,267
33,039
SHIRIKA la Idadi ya Watu la Umoja wa Mataifa (UNFPA), limezindua ripoti yake ya mwaka 2010 inayoonyesha pamoja na mambo mengine kuwa umri wa kuishi wa Mtanzania ni kati ya miaka 56 na 57 ambao ni wa juu kuliko nchi nyingine za Afrika Mashariki. Vilevile, idadi ya watu kwa sasa inakadiriwa kuwa 45 milioni

Ripoti hiyo ilizinduliwa jana jijini Dar es Salaam na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Elizabeth Nyambibo, kwa niaba ya Waziri wa wizara hiyo, Lawrence Masha, ikibeba ujumbe usemao 'Kutoka vurugu na machafuko, kuelekea mabadiliko'.

Umri huo wa kuishi kwa Mtanzania umeongezeka kutoka miaka 55 kwa wanaume na miaka 56 kwa wanawake kwa mujibu wa takwimu za shirika hilo za mwaka jana.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo katika ukanda wa Afrika Mashariki, umri wa kuishi katika nchi ya Kenya ni kati ya miaka 55 na 56, Uganda 53 na 54, Rwanda miaka 49 na 52, wakati Burundi ni miaka 49 na 52.

"Umri wa kuishi kwa Mtanzania ni miaka 56.1 kwa wanaume na 57.7 kwa wanawake, Uganda ni 53.4 na 54.8, Kenya ni 55 na 56, Burundi ni 49.8 na 52.9 na Rwanda ni miaka 49.2 kwa wanaume na miaka 52.9 kwa wanawake," ilisema sehemu ya ripoti hiyo.

Ripoti hiyo ya UNFPA inaeleza kuhusu idadi ya watu, maendeleo, mabadiliko na afya ya uzazi pia imebeba ushuhuda wa wanawake mbalimbali walioeleza yaliyowakumba na watoto wakati wa machafuko.

Aidha, UNFPA imebainisha kuwa pato ghafi la Mtanzania kuwa ni Dola za Kimarekani 1,230 kwa mujibu wa takwimu za Benki ya Dunia za mwaka 2008, ambapo misaada kutoka nje inakadiriwa kuwa dola za Kimrekni 306,163 kwa mwaka.

Katika ripoti hiyo kwa mwaka 2010, Tanzania imetajwa kuwa na idadi ya watu 45 milioni wakati Kenya ina watu 40 milioni, Uganda,33.8 milioni, Rwanda 10.3 milioni na Burundi watu 8.5 milioni.

Ripoti hiyo imeonyesha kuwa Tanzania na Kenya zina idadi sawa ya vifo vya watoto waliozaliwa wakiwa hai ambapo watoto 60 waliozaliwa hai hufa kati ya kila 1000.

Nchi zinazofuata ni Uganda yenye vifo 70, Burundi ikiwa na vifo 95 na Rwanda yenye vifo 96 vya watoto kati ya 1000 wanaozaliwa.

Hata hivyo, kuhusu afya ya uzazi ripoti hiyo imebainisha Tanzania kuwa na wanawake 130 wanaojifungua wakiwa na umri mdogo wa kati ya miaka 15 na 19 kati ya kila wanawake 1000.

Nchi ya Kenya ina wanawake hao104, Uganda 150,Rwanda wanawake 37 na Burundi 19.

Imeonyesha kuwa asilimia 6.2 ya wanawake wenye umri wa kati ya miaka 15 na 19 huchukua tahadhari na kupima Ukimwi huku kati ya asilimia 20 na 26 wakitumia njia za uzazi wa mpango nchini Tanzania.

Kwa nchi ya Kenya, ripoti hiyo haionyeshi iwapo wanawake hao wanachukua tahadhari au kupima Ukimwi huku asilimia 49 wakitumia njia za kisasa za uzazi wa mpango.

Rwanda asilimia 2.8 huchukua tahadhari na kupima Ukimwi, Burundi asilimia 2 na Uganda asilimia 5.4 pia huchukua tahadhari na kupima Ukimwi.

Akizindua ripoti hiyo, Nyambibo alisema kuwa ripoti hiyo imetoa angalizo kwa Tanzania kujifunza kutoka kwa waliopitia vurugu na machafuko.

Chanzo: Gazeti la Mwananchi

Hata Umri uongezeke vipi bado sisi WaTanzania tuna Umasikini njaa,Maradhi, na ukosefu wa ajira mijini umri ukiongezeka utasaidia kitu gani?
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom