Candid Scope
JF-Expert Member
- Nov 8, 2010
- 11,883
- 6,884
EU yalaani mauaji ya Mwangosi
Umoja wa Ulaya (EU), jijini Dar es Salaam umelaani mauaji ya mwahabari Daudi Mwangosi, aliyedaiwa kuuawa na polisi na kuzitaka mamlaka zinazoshughulikia mauaji yake kuchunguza kifo hicho kwa uwazi mkubwa na kuwachukulia hatua stahiki watuhumiwa.
EU ilisema imezifuatilia hatua za mwanzo za kisheria zilizochukuliwa kufuatia mauaji hayo ikiwemo kumfikisha kizimbani askari anayeshtakiwa kwa mauaji ya Mwangosi, lakini ikisisitiza juu ya kuwepo uwazi zaidi kwenye mamlaka zote zinazoshughulikia kifo chake.
Mwangosi aliuawa Septemba 2, mwaka huu akiwa kazini kwenye tukio la Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) la uzinduzi wa tawi la chama hicho kwenye mji mdogo wa Nyololo mkoani Iringa.
Mshitakiwa wa mauaji hayo ni polisi Pacificus Simon (23) wa Kikosi cha Kuzuia Ghasia (FFU), aliyefikishwa mahakamani Septemba 12, mwaka huu kujibu mashtaka ya kumuua kwa bomu la machozi mtumishi huyo wa zamani kituo cha televisheni cha Channel Ten mkoani Iringa.
Taarifa ya EU iliyotolewa jijini muda mfupi baada ya ujumbe wake ulioongozwa na Balozi Filberto Ceriani Sebrogondi kuzuru ofisi za vyombo vya habari vya IPP zinazohusisha The Guardian Limited, vituo vya televisheni vya ITV, East Africa , Capital , Radio One na East Africa Radio, kadhalika ilitoa salamu za pole kwa familia yake na tasnia ya habari nchini.
EU ilisisitiza kuwa licha ya kwamba ni jukumu na haki ya serikali kuchukua hatua za kulinda amani na kudumisha utawala za sheria, ni jukumu la serikali pia kutekeleza majukumu hayo katika hali inayokubalika na kuzuia matumizi makubwa ya nguvu dhidi ya raia huku ikilinda haki za wananchi.
Taarifa hiyo ilikumbusha kuwa tasnia ya habari inatekeleza jukumu nyeti la kuwezesha uhuru wa haki ya kujua na kutoa maoni na kujieleza .
Kwa hiyo basi Umoja wa Ulaya, unaitaka Serikali ya Tanzania kufanya kila kinachowezekana kudumisha uhuru wa habari na hivyo kuhakikisha uwepo wa haki ya kutoa maoni, ilisema taarifa hiyo.
Mshitakiwa wa mauaji hayo alifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mfawidhi Wilaya mjini Iringa ambapo alisomewa mashtaka na kurudishwa rumande. Pamoja na kupandishwa kizimbani, pia Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Nchimbi, aliunda kamati ya kuchunguza mauaji hayo ikihusisha polisi, wanahabari na, Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Katika ziara hiyo, ujumbe huo wa EU, ukiwa kwenye vyombo vya habari vya IPP, ulieleza kufurahishwa na kazi zinazofanywa na vyombo hivyo vya habari.
Balozi Sebrogondi, alivisifu vipindi vya televisheni na redio vinavyoelimisha jamii kuhusu mikakati ya kupunguza umaskini na uwezeshaji wa wananchi eneo ambalo umoja huo pia unalifanyia kazi ili kuziwezesha nchi maskini kuondokana na umaskini.
Ujumbe huo ulikuwa wa viongozi na wafanyakazi wa umoja huo kutoka mataifa ya Kusini mwa Afrika Kusini mwa Sahara yakiwemo Ghana, Kenya, Zambia na Uganda.
CHANZO: NIPASHE