Umeme, barabara jinamizi linalokwaza uchumi

Jul 6, 2012
5
0
Na Joseph Zablon

NI kilometa zaidi ya nane kutoka barabara kuu ya kwenda Kilimanjaro, Arusha na Moshi, lakini jirani na eneo la Msata kuna Kijiji cha Kwadoya ambako lori la mahindi mabichi limekwama kwa siku kadhaa katika tope kutokana na ubovu wa barabara.

Jitihada za wanakijiji na wadau wengine za kusaidia kulinasua hazijazaa matunda na mbaya zaidi mahindi ambayo yalikusudiwa kuuzwa Dar es Salaam-sasa yanakauka na huenda mmiliki akabadili biashara aliyokusudia ili kulinda mtaji wake.

Kulingana na utafiti wa taasisi ya BEST-AC, miundombinu ya barabara, umeme, rushwa na ukosefu wa huduma ya mawasiliano ya simu katika baadhi ya maeneo ni kikwazo cha ukuaji wa biashara na hata uwekezaji.

"Umeme ni tatizo la mara kwa mara na barabara zikishika nafasi ya pili" inasema sehemu ya taarifa hiyo ya utafiti na kubainisha kwamba rushwa ambayo mwaka 2010 ilionekana kupungua imeongezeka sasa.

Utafiti huo unataja pia tatizo la uhaba wa maji ni moja ya matatizo ambayo yanaathiri sekta ya biashara kwa kiasi kikubwa.

Benki ya Dunia (WB) katika utafiti wake inasisitiza umuhimu wa kuboresha mazingira wezeshi ya biashara ili kuongeza kiwango cha uwekezaji kwenye sekta binafsi na itasaidia kuongeza ajira na kupunguza umaskini.

Nikirejea taarifa ya Benki ya Dunia iliyoitwa Doing the Business, inahoji ni vipi Serikali itaboresha mazingira wezeshi katika sekta ya biashara na namna gani itashughulikia vipaumbele vya sekta binafsi katika ukuaji wa uchumi.

Lakini hata hivyo taarifa hiyo inabainisha kuwa kukosekana kwa utashi wa Serikali katika kupata majibu ya maswali ya namna hiyo kumesababisha kutokuwapo kwa mabadiliko yoyote ya maana tangu 2008 mpaka mwaka jana 2011.

Kwa matazamo wangu, jitihada za makusudi zinahitajika kukabili hali hiyo ikiwa ni pamoja na Serikali kuondoa utegemezi katika bajeti yake.

Kiuchumi nchi inatakiwa kujitosheleza katika bajeti yake badala ya kutegemea wahisani.

Kama ni kutegemea wahisani, tuwategemee kwa asilimia 15 mpaka20 tofauti na sasa, tunawategemea kwa asilimia 60.

Uwiano wa kibajeti baina ya fedha za matumizi ya kawaida na zile za maendeleo, hazilengi kuboresha mazingira ya kufanya biashara.

Serikali katika bajeti iliyopita 2010/2011 ilitenga Sh2.7 trilioni kwa ajili ya miundombinu kwa ajili ya reli, barabara, na viwanja vya ndege.

Katika hali isiyo ya kawaida fedha za kutekeleza miradi hiyo mwaka 2012/2013 ilitenga Sh1.5 trilioni.

Kiasi hicho ni pungufu ya bajeti ya 2010/2011 kwa asilimia 49, fedha hizo hazijumuishi miradi ya nishati ya umeme.

Serikali inatakiwa kuwekeza fedha za kutosha katika miundombinu na umeme ili Serikali iweze kufikia malengo yake ya kuwaletea maendeleo wananchi kama ilivyojipanga.

Mfano rahisi Rwanda ambayo bajeti yake ni Sh17 trilioni na imevitaja vipaumbele vitatu tu ambavyo ni elimu, umeme na miundombionu.

Kutokana na hali hiyo nchi inatakiwa kuwa na malengo ya muda mfupi na mrefu badala ya kutekeleza vipaumbele vyote kwa pamoja huku ikwia haijiwezi kifedha.

Kimsingi Serikali inapaswa kutekeleza vipaumbele vichache kwa mfano, inaweza kutatua tatizo la nishati ya umeme na miundombinu tu.

Pia Serikali ina tatizo la utekelezaji wa bajeti yake kwa kuhamisha fungu lililotengwa kutekeleza mradi fulani na kulipeleka kwenye miradi mingine. Sasa tabia hii ndio inayokwamisha utekelezaji wa vipaumbele.

Lakini tukirudi kwenye barabara hakuna shaka kwamba ubovu wa barabara unachangia kupandisha bidhaa sokoni na gharama zingine za uzalishaji.

Tanzania inapaswa kutekeleza mikataba ya kufikiwa kwa malengo mbalimbali kimataifa ambayo ni pamoja na lile la milenia 2015 na mkataba wa Cardiff.

Azimio la Cardiff linataka nchi kukuza uchumi wake angalau kwa asilimia nane mpaka 10, lakini Tanzania hali ni tofauti.

Uchumi wa Tanzania mwaka 2010 ulielezwa kuongezeka kwa asilimia 4.2 na mwaka jana 2011 uchumi ulishuka mpaka asilimia 3.6.

Pamoja na mwenendo wa kiuchumi kutokuwa mzuri, moja kwa moja naunga mkono kauli ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Mgongo kwamba anakusudia kumaliza tatizo la umeme nchini ambao siyo wa uhakika.

Tabia ya kutegemea chanzo kimoja cha umeme wa maji ambacho kinazalisha megawati 561 za umeme sawa na asilimia 41 ni jambo ambalo limepitwa na wakati.

Natambua kwamba hivi sasa kuna megawati 1,375 kutokana na vyanzo vipya-hivyo vimesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza utegemezi wa umeme wa maji, lakini bado juhudi zinahitajika ili kuhakikisha wananchi wanapata umeme wa uhakika.

Natambua kwamba shirika hilo lina malengo ya kuingiza megawati 200 za umeme katika gridi ya Taifa kutokana na makaa ya mawe ifikapo 2015/2016, lakini mipango hiyo inanapaswa kufanyiwa kazi na isiwe ni porojo tu.

Mipango ya Serikali ya kutafuta vyanzo vingine ikiwa ni pamoja na matumizi ya umeme wa upepo kulingana na malengo ya dira ya Taifa 2025, inapaswa kutekeleza malengo hayo kwa vitendo na siyo porojo kama tunavyoshuhudia katika mipango yake mingi.

Lakini pamoja na hayo utafiti unapaswa kufanyika ili kuongeza uzalishaji na kuondoa vikwazo ambavyo vinachangia kudumaa kwa uchumi wa taifa.

Bajeti tegemezi ndio chimbuko la nchi kushindwa kutanzua matatizo yanayokwaza biashara na uwekezaji nchini ambazo ni pamoja na umeme, barabara na miundombinu mingine.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom