Ukongwe Hausaidii Kubaki Madarakani

X-PASTER

JF-Expert Member
Feb 12, 2007
11,610
1,809
Ukongwe Hausaidii Kubaki Madarakani

Kama ni nia ya chama tawala kubaki madarakani, basi lengo la kila chama cha upinzani ni kuingia Ikulu. Lakini Ikulu hawakai wapangaji wawili. Basi vipi vyama vya upinzani vitaweza navyo, kuingia Ikulu pasina kukiondoa katika madaraka chama tawala?

Kukiondoa madarakani chama tawala, kama CCM, si lelemama! Inahitaji mikakati madhubuti, hekima, busara, na juu ya yote, umoja baina ya wapinzani. CCM ni chama kikongwe na chenye mizizi yake kila pahali nchini. Ndicho chama kilichopigania na kuleta uhuru; na ndicho chenye nguvu za dola. Wakati hakuna chama chochote cha upinzani kilichofikisha umri, angalau, wa miaka ishirini tu, CCM ina umri wa karibu nusu karne.

Hiyo ina maana kwamba CCM,mbali ya nguvu za dola, ina uzoefu mkubwa kuliko vyama vya upinzani. Kwa hali hiyo chama hicho kina nafasi nzuri ya kutumia uwezo, ujuzi na uzoefu wake huo, wa miaka mingi,katika kujichimbia madarakani.

Lakini mara nyingine kubaki madarakani kwa kipindi kirefu, kunaweza kukiponza chama kuliko kikisaidia. Angalia mmoja katika wakongwe wa siasa KATIKA ENEO HILI LA Afrika ya Mashariki na Kati, Dk. Kenneth Kaunda. Chama chake cha UNIP ndicho kilichopigania uhuru wa Zambia na kufaulu kuutia uhuru huo mikononi, Kaunda akiwa ndiye kiongozi wa chama hicho. Lakini ulipokuja uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi, Dk. Kaunda pamoja na chama chake, walishindwa na mtu mfupi wa kimo,na pia, mgeni katika uwanja wa siasa, Rais Chiluba. Hiyo ni kwa sababu Wazambia walikuwa wamekwisha choka na utawala huohuo, siku zote. Watu walikuwa tayari wamechoka, walitaka mabadiliko. Alikadharika jirani zetu wa Kenya nao pia wamefanya mapinduzi ya fikra na kukiondoa chama cha KANU madarakani, japokuwa nao siasa zao ni za kikabila lakini wameonyesha kuwa kuondoa cha kikongwe madarakani kunawezekana.

Kwa mujibu wa hali ya mazingira ilivyo Tanzania, kwa hivi sasa, kuna kila sababu ya kuamini kuwa siku za kutamba kwa chama cha CCM zinakaribia mfundoni. Watanzania wamechoka na chama hicho hicho, miaka nenda miaka rudi. Wanataka mabadiliko.

Inaonekana hata na chama chenyewe kimekwisha elewa hilo. Ndiyo maana nasikia kuwa kuna tetesi za makada wakongwe wa chama hicho kutaka kung'atuka kuwapa nafasi damu mpya (kama kweli), katika safu ya uongozi. Lakini haijulikani, kwa hakika, wangapi katika wakongwe hao walio tayari kwa hilo? Na hata kama wapo watakaong'atuka wataathiri nini katika uchaguzi ujao?

Pili, katika uchaguzi mkuu uliopita, wa mwaka 2005, CCM ilitoa ilani ya uchaguzi, ambayo baadaye, imeonekana kuwa haitekelezeki. Na kweli haijaweza kutekelezwa.
Jambo hilo, la kushindwa kutekeleza ilani yake, ni dhahiri, kwa kiwango fulani, limekipunguzia chama hicho nafasi yake ya kuweza kuchaguliwa tena. Aidha, ukosefu wa ajira kwa vijana, ambao ndio walio wengi katika jamii, ukata uliowakumba walala hoi, na kupanda kwa gharama za maisha uku serikali imekataa kupandisha kima cha chini cha mishahara kunakifanya chama hicho, mbele ya macho ya Watanzania wengi kionekane sera zake haziwezi kamwe kumkwamua mwananchi wa kawaida, katika hali duni aliyo nayo.

Zinaweza kuwapo sababu mia moja na moja za kuwafanya walio wengi kutokipigia kura chama hicho safari hii. Kwa mfano, kuna wale wanaodai mafao yao tokea kuvunjwa kwa jumuiya ya Afrika Mashariki (kama bado wapo hai).

Kuna waliopunguzwa makazini kiholela kwa ajili ya kutekeleza zoezi la ubinafsishaji mashirika ya umma kipindi kile cha Muheshimiwa ndugu Rais mstaafu Che Mkapa. Zoezi hilo limewaongezea ukata wa maisha wale walioachishwa kazi. Wamejikuta wakishindwa kuzitunza familia zao na kuendelea kugharamia elimu ya watoto wao. Jee! Hawa watakuwa tayari kukipa tena kura zao chama tawala mwezi wa kumi ukifika?

Je vipi wafanyakazi ambao Rais kupitia hotuba yake kwa wazee wa Dar ES salaam, alisema kuwa haitaji kura zao, na mishahara ya kima cha chini hapandishi ng’o.
Kuhusu swali hili, haijulikani kama Mheshimiwa Rais amelifanyia tathmini ya kina au anabahatisha bahatisha tu. Ni kweli Wafanyakazi wamekasirishwa sana, tena sana na namna hilo swali la kima cha chini lilivyo chukuliwa na serikali. Na wengi wao wametamka, bila ya kificho, kuwa watakinyima kura zao chama tawala. Inaonekana baadhi ya vyama vya siasa vinataka kutumia mwanya huo ili wajizolee kura za chee.

Mradi sababu za kukikosesha chama cha CCM kura, ni nyingi sana. Na kama tulivyokwisha tangulia kueleza hata CCM yenyewe imekwishalielewa hilo. Yasemekana hata yale mabadiliko ya 13 ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yaliyofanywa wakati ule, yalitokana na wasiwasi huo.


Kabla ya kubadilishwa katiba ilikuwa mgombea wa kiti cha Urais ili ahesabike kuwa ameshinda ilibidi apate zaidi ya asilimia hamsini kwa zote. Lakini kwa vile CCM inachelea kuwa, Kila chaguzi haitafikia asilimia hiyo, ndiyo ikabadilisha kifungu hicho, na kufanya mgombea wa kiti hicho ataweza kuwa mshindi kama atawashinda wagombea wengine kwa wingi wa kura tu, hata kama hajafikia asilimia hamsini...!

Kwa hiyo kwa mujibu wa mabadiliko hayo yaliyofanywa, kwa haraka haraka, uwezekanao wa kuwa na Rais asiyekubalika na wengi ni mkubwa sana. Na kwa waheshimiwa wa vyama vya siasa kambi ya upinzani, kwa kukataa kwao kuungana, kuweka mgombea mmoja tu wa kiti cha urais kwa kambi hiyo,kwa kiwango fulani kutachangia kupatikana kwa Rais huyo asiyekubalika.

Jambo moja halina ubishi… Hakuna chama chochote, safari hii, kiwe ni cha upinzani au chama tawala, chenye uhakika, wa mia kwa mia, kupata ushindi wa chee. CCM ambayo katika uchaguzi uliopita wa mwaka 2005, iliibuka mshindi kwa kupata asilimia zaidi ya 80% ambazo ni sawa na kura 9,123,952 nahisi katika uchaguzi ujao haitafikia hata asilimia hamsini; jee vyama vya upinzani kwa ujumla wao wa kupata asilimia 20% tu wana uhakika gani wa kupata ushindi mwaka huu?
Nakumbuka Jaji Makame alitaja kura walizopata wagombea wengine wa Urais kuwa ni: Profesa Ibrahim Lipumba wa CUF kura 1,327,125, sawa na asilimia 11.68 ya kura zote halali, Bw. Freeman Mbowe wa CHADEMA kura 668,756 sawa na asilimia 5.88 ya kura zote halali. Wengine ni Bw. Augustine Mrema wa TLP kura 84,901, sawa na asilimia 0.75 ya kura zote halali, Dk. Sengondo Mvungi wa NCCR-Mageuzi kura 55,819, sawa na asilimia 0.49 ya kura zote halali na Mchungaji Christopher Mtikila wa DP, kura 31,083 sawa na asilimia 0.27 ya kura zote halali.

Wagombea wengine ni Dk Emmanuel Makaidi wa NLD, aliyepata kura 21,574 ambazo ni sawa asilimia 0.9, Bi. Anna Senkoro wa PPT-Maendeleo kura 18,783, sawa na asilimia 0.7, Profesa Leonard Shayo wa Demokrasia-Makini kura 17,070, sawa na asilimia 0.15 na Bw. Paul Kyara wa SAU kura 16,414, sawa na asilimia 0.4

Vyama vya upinzani visisahau kuwa Waswahili walivyosema. "Mla,mla leo, mla jana, kalani?" Basi bidhaa ya mwaka '47 haina soko leo!

Mbali ya kupendwa na watu, nafasi ya Urais inahitaji na uwezo. Kama kweli vyama vya upinzani vina nia ya kuwatumikia Watanzania wanaweza kufanya hivyo kwa kushirikiana. Aidha wawe tayari kuwatumikia katika nafasi yo yote na si lazima iwe nafasi ya u-Rais. Kwa nini vyama vya upinzani havitaki kukutana ana kwa ana, na kuchaguwa kiongozi mmoja watakae msimamisha ili kukiondoa chama tawala!? Hivi vya vya upinzani vina wasiwasi wa nini… Au vimerogwa na mrogaji kafa!?
 
Wakati ndio huu kwa wakongwe kuachia madaraka na kuwaachia vijana wenye kuweza kuleta mabadiriko ya kiuchumi na kijamii.
 
Mkuu wangu sikuwahi kuisoma hii mada na hakika uligonga msumari lakini kama ilivyo sisi wadanganyika hatukuweza kukusoma wakati muafaka. Leo hii tunayajutia..
 
1 Reactions
Reply
Back
Top Bottom