Ufisadi: Ni mshike mshike tu

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,005
Ufisadi: Ni mshike mshike tu

2007-10-08 17:28:09
Na Mwandishi wetu, Jijini


Lile sakata la kuibuliwa kwa tuhuma za ufisadi kwa baadhi ya vigogo nchini limeendelea kuzua mshike mshike wa aina yake baada ya wananchi wenye hasira kumtoa baru jukwaani Naibu Waziri mmoja.

Taarifa zinamtaja Naibu Waziri aliyekumbwa na balaa hilo la kushushwa jukwaani kutokana na kelele za jazba toka kwa wananchi kuwa ni Dk. Deodatus Kamala wa Wizara ya Afrika Mashariki na Kati.

Taarifa zinasema Dk. Kamala amekumbwa na kisanga hicho wakati akijaribu kutoa ufafanuzi kwa wananchi kuhusiana na swali lililoulizwa na mwananchi mmoja kuhusu tuhuma za ufisadi ambazo wapinzani wamekuwa wakizishikia bango kwa siku kadhaa sasa.

Mashuhuda wa tukio hilo wanasema lenyewe lilijiri pale katika stendi ndogo ya mabasi ya Nyasho mjini Musoma.

Inaelezwa kuwa Dk. Kamala alilazimika kutimka jukwaani kutokana na zomea zomea iliyoibuka kwa kasi baada ya kutoa majibu yaliyoonekana kutowaridhisha wananchi.

Inaelezwa kuwa balaa lilianza wakati mwananchi mmoja aliposimama na kuuliza kuhusu sababu za msafara wa mawaziri hao kuongozwa na Waziri wa Miundombinu.

Bw. Andrew Chenge, ambaye ni miongoni mwa wanatuhumiwa na wapinzani juu ya ushiriki wake katika ufisadi
Inaelezwa kuwa baada ya hapo, ndipo akainuka Dk. Kamala kutaka kujibu swali hilo.

``Tuhuma za ufisadi zilizotolewa na wapinzani dhidi ya viongozi hazina msingi kwa kuwa hao waliozitoa hawana ushahidi wowote,`` alisema Dk. Kamala.

Hata hivyo badala ya wananchi kumsikiliza, walianza kumzomea.
Inaelezwa zaidi kuwa licha ya kuzomewa, Dk. Kamala aliendelea kusema kuwa Serikali ya CCM itaendelea kutawala tu hata kama wapinzani watazidi kuwashambulia viongozi wa Serikali.

Akasema wakiona wapinzani wanawasifu wajue kuwa CCM inaelekea kubaya na wakiona wanawapaka matope ni dalili ya kwamba kazi yao kwa wananchi ni nzuri.

Kauli hiyo iliwafanya wananchi wazidi kupiga mayowe na kuzomea kwa nguvu, hali iliyomfanya Dk. Kamala ashuke jukwaani haraka haraka na kumpisha Mbunge wa Musoma Mjini Bw. Vedasus Mathayo aliyekuja kuwatuliza wananchi hao.

Aidha, mshike mshike mwingine umedaiwa kutokea mkoani Manyara baada ya Waziri wa Mipango, Uchumi na Uwekezaji, Dk. Juma Ngasongwa, kujikuta kwenye wakati mgumu wakati alipotupiwa swali mwananchi mmoja kuhusu sababu za kusimamishwa kwa Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Bw. Zitto Kabwe.

Inaelezwa kuwa wakati Dk. Ngasongwa akijaribu kutoa ufafanuzi kuhusu suala hilo, wananchi wakamchenjia na kuanza kumsomea vikali.

SOURCE: Alasiri
 
Back
Top Bottom