UDHAMINI WA ELIMU UGHAIBUNI: AMERIKA vs ULAYA - MAKULILO, JR.

MAKULILO

Member
May 30, 2010
84
94
UDHAMINI WA ELIMU UGHAIBUNI: AMERIKA vs ULAYA

Na: ERNEST BONIFACE MAKULILO (MAKULILO, JR.)

View attachment 46467

Watu wengi wamekuwa na ndoto za kupata elimu ya juu ughaibuni siku moja ili kubadilisha hali ya maisha yao binafsi na jamii zao. Ni vizuri kuwa na ndoto za maisha yako, ila ni vyema kuhakikisha unakuwa na mbinu thabiti za kutimiza ndoto hizo. Maana ndoto bila mbinu za utimizaji ni sawa na kutwanga maji kwenye kinu.

Sasabasi katika sehemu ya leo ya Udhamini wa Elimu Ughaibuni nitazungumzia kitu cha msingi na cha kuanzia ili mtu uweze kutimiza ndoto yako ya kupata elimu ughaibuni. Kitu hicho si kingine bali ni Uchaguzi wa bara la kwenda kusoma kati ya Ulaya na Amerika. Uchaguzi huu ni wa msingi wa kukuwezesha kupata ratiba yako vizuri ya uombe vyuo vingapi, masomo gani uombe, maandalizi yapi mengine uyafanye ili kuibuka kidedea.

Uchaguzi wa wapi pa kusoma ni wa msingi sana. Uchaguzi huu utakusaidia mambo mengi sana hususani kujipanga na gharama, muda, nyenzo zipi zitumike nk. Sehemu kubwa mbili ambazo zinatoa sana udhamini wa elimu ya juu ughaibuni ni Ulaya na Amerika (Marekani na Kanada). Hii ndio maana imepelekea katika kitabu changu cha udhamini wa masomo kiitwacho SCHOLARSHIP OPPORTUNITIES IN AMERICA AND EUROPE: The Secret From Makulilo kitakachotoka 2012 kina sura maalumu ielezeayo kwa kina Udhamini wa Elimu – Amerika VS Ulaya.

Katika kufanya uchaguzi huu ni lazima tutumie nyenzo za uchambuzi. Nyenzo hizo ni (i) Gharama za maombi – Application fee (ii) Ufanyaji wa Mitihani ya maombi – Admissions Tests (iii) Uwezo/ujuaji wa lugha ya Kiingereza – English proficiency (iv) Lugha ya kufundishia – Language of instruction

Ngoja tuanze na suala la gharama za maombi. Unapotaka kuomba chuo chochote kile kuna taratibu za kufuatwa. Gharama za maombi kwa vyuo vingi huwa ni kati ya dola za kimarekani 50 hadi 100. Hii inatedgemea chuo na chuo. Habari njema ni kwamba kwa upande wa Ulaya vyuo vingi havina sharti hili, wewe unatakiwa kuomba udahili na udhamini bure bila gharama yoyote ile. Ila inapokuja kwa upande wa Amerika, wote kwa vyuo vya Marekani na Kanada ni LAZIMA ulipe gharama za maombi yako. Na ninajua kuwa wengi hawana uwezo wa kulipa fedha hizo, na pia njia ya ulipaji nayo inaleta kikwazo kwani wengi hawana kadi maalumu za kuweza kulipia kwa njia ya mtandao kama ujuavyo manunuzi kwa njia ya mtandao bado ni mapya kwa jamii ya wengi Tanzania.

Ushauri wangu wa kitaalamu katika suala hili ni kwamba: Kutokana na ukweli kwamba si wewe pekee ambaye ni muombaji wa udahili na udhamini ughaibuni, basi ushindani ni mkubwa sana. Na ili kuweza kujiongezea uwezekano wa kuwa mshindi na kupata udhamini, ni vyema kuweza kuomba vyuo vingi sana kwa kima cha chini vyuo 15. Na ukisema kuwa uombe vyuo hivyo vyote Marekani au Kanada na kutokana na uwepo wa malipo ya maombo, basi itakulazima mtu uwe na kima cha chini cha dola za kimarekani 800 hadi 2000 ambacho ni kiasi kikubwa sana cha fedha. Hivyo ni vyema mtu kuomba vyuo vingi Ulaya ambapo huingii gharama hii ya ulipaji kwenye utumaji maombi yako.

Ufanyaji wa mitihani ya maombi ni kigezo cha msingi sana. Kuna mitihani miwili maarufu sana, Graduate Record Examination (GRE) na Graduate Management Admissions Test (GMAT) ambayo hutumiwa kama kipimo cha kudahili na ufadhili kwa wanafunzi. Mitihani hii inafanyika kwenye mtandao (online) na kwa Tanzania inafanyikia katika University Computing Center –UDSM Mlimani. Ada ya mitihani hiyo kwa kila mmoja ni dola za kimarekani 190. Unatakiwa kufanya mtihani mmoja kati ya hiyo. Mitihani hii hutumika katika nchi za Marekani na Kanada, na kwa nchi za Ulaya hawana kigezo cha GRE au GMAT ili aweze kupata udahili na udhamini.
Ushauri wangu wa kitaalamu ni kwamba kama una mpango wa kusoma Marekani au Kanada na unategemea udhamini, usisubirie njia ya mkato kwa kutofanya mtihani husika. Na kama huna fedha za kutosha kulipia mitihani hiyo ni vyema uombe vyuo vya Ulaya ambavyo hawana mitihani hiyo ili kupunguza gharama.

Uwezo/ujuaji wa lugha ya Kiingereza ni kigezo cha msingi. Katika nchi nyingi ziwe zinazotumia Kiingereza kama lugha mama au la, inapokuja kwenye elimu ya juu hususani shahada ya uzamili na uzamivu, Kiingereza hutumika kama lugha ya kufundishia. Na kwakua nchi ya Tanzania lugha ya Taifa ni Kiswahili (si Kiingereza) basi mwombaji lazima atoe vielelezo kuonesha kuwa mtu huyo anajua na ana uwezo wa kutumia Kiingereza kwenye masomo yake bila matatizo. Njia ya kutambua uwezo wa mtu kama anajua Kiingereza ipasavyo au la inabidi afanye mtihani wa kutathmini. Hapa kuna mitihani miwili, na unatakiwa ufanye mmoja kati ya hiyo. Kuna mtihani wa Test of English as Foreign Language (TOEFL) ambao unafanyikia University Computing Center – UDSM Mlimani kwa ada ya zaidi ya dola 160, na mtihani mwingine ni International English Language Testing System (IELTS) unafanywa pale British Council kwa ada isiyopungua Shilingi 250,000/=. Hii haingalii uwe unaomba Ulaya au Amerika, vyuo vingi vinataka cheti cha mmoja kati ya mitihani hiyo. Lakini kuna baadhi ya vyuo havihitaji mitihani hiyo kwakuwa nchini Tanzania Kiingereza kinatumika kufundishia kuanzia Sekondari hadi Chuo Kikuu, hivyo ni kigezo tosha, japo vyuo vingine havijali hilo ni lazima ufanye mtihani wa lugha.

Lugha ya kufundishia itumikayo katika chuo husika ni kigezo kikubwa sana. Katika nchi ambazo Kiingereza si lugha mama au lugha ya taifa, elimu yao nchi hizo huwa inatumia lugha zao kuanzia chekechea hadi shahada ya kwanza. Mfano, Kinorwei kinatumika huko Norway kuanzia chekechea hadi shahada ya kwanza. Lakini nchi hizo japo Kiingereza sio lugha yao, inapokuja kwenye shahada ya uzamili na uzamivu wanafundisha kwa Kiingereza hivyo kuwawezesha wanafunzi wa kimataifa kusoma katika nchi hizo. Ila ukienda katika nchi ambazo lugha ya taifa ni Kiingereza wao hakuna shida maana kuanzia chekechea hadi shahada ya uzamivu wanatumia Kiingereza hivyo kuweka urahisi kwa mtu wa mataifa mengine kusoma. Hii inafanya mchakato wa watu wapendao kusoma shahada ya kwanza wawe na nchi chache za kuweza kuomba hivyo kufanya mchakato wa uombaji kuwa wa ushindani sana.

Ushauri wangu kwa ujumla kusuhu sehemu ipi nzuri ya mtu kuomba: Kutokana na gharama kuwa kubwa za uombaji, ufanyaji wa mitihani ya GRE au GMAT, TOEFL au IELTS, na ukafanya tathimini ya Ulaya na Amerika, ni bora mtu kuomba vyuo vingi Ulaya na kuwa na uwezekano wa kupata kwa urahisi. Kuomba vyuo Marekani na Kanada ni gharama kubwa. Na ili mtu uweze kupambana na ushindani, ni vizuri kuomba vyuo vingi si chini ya 15, hivyo ukisema uombe Ulaya utatumia kiasi kidogo cha fedha chini ya dola 100 ambazo ni za gharama za utumaji nyaraka zako kwa njia ya posta kwenye vyuo vyote. Ila ukisema uombe vyuo 15 Marekani au Kanada itakulazimu uwe na zaidi ya dola 2000 kwa ajili ya mitihani na hela ya uombaji.

Zifuatazo ni tovuti za msaada wa mitihani husika unapotaka kujiandaa.
1 GRE GRE
2 GMAT The GMAT®
3 TEOFL TOEFL: Home
4 IELTS http://www.ielts.org/

Kwa maswali au maoni, niandikie
makulilo@makulilofoundation.org
MAKULILO, JR.
CALIFORNIA, USA
 
Thanx kaka nashukuru kwa mchango wako ntawasiana na wewe zaid
 
Back
Top Bottom