Uchunguzi wamnasa Mkurugenzi TANESCO; Bodi ya Jenerali Mbona yatishia kujiuzulu

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Waandishi Wetu Toleo la 262 10 Oct 2012




  • Bodi ya Jenerali Mbona yatishia kujiuzulu
  • Bandari nako si shwari, mengine yafichuka


WAKATI Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), Lawrence Mafuru, akisafishwa kutokana na uchunguzi uliofanyika katika benki hiyo kwa ridhaa ya Bodi ya Wakurugenzi, aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania, William Mhando, ambaye naye alisimamishwa kazi ili kupisha uchunguzi, mambo yanazidi kumuelemea, Raia Mwema, limebaini.

Mhando na wenzake walisimamishwa kazi TANESCO ili kupisha uchunguzi wa tuhuma mbalimbali zikiwamo za matumizi mabaya ya madaraka na hususan kuwapo kwa mgongano wa kimaslahi, uchunguzi ulioendeshwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ambao umebaini mgongano wa maslahi kwa kiongozi huyo.


Kwa mujibu wa taarifa za uchunguzi huo uliodumu kwa miezi kadhaa sasa, Mhando amebainika kuwa na mgongano wa kimaslahi na Kampuni ya MC Donald Live Line Technology Ltd.


Kwa mujibu wa nyaraka zilizopo, Mhando ameingia mkataba na MC Donald Live Line Technology Ltd, akipewa majukumu maalumu ndani ya kampuni hiyo. Mhando alipewa jukumu la kuitafutia miradi kampuni hiyo ndani ya shirika alilokuwa akiliongoza, TANESCO.


Tayari ripoti hiyo ya uchunguzi kutoka kwa CAG imekabidhiwa katika mamlaka serikalini, ikiwa ni pamoja na Bodi ya Wakurugenzi wa TANESCO, chini ya Mwenyekiti wake, Jenerali (mstaafu) Robert Mbona na Makamu Mwenyekiti wa Bodi, Mbunge wa Lupa, Victor Mwambalaswa.


Kwa mujibu wa vyanzo vyetu vya habari kutoka serikalini, taarifa ya uchunguzi huo inamuweka katika mazingira magumu zaidi Mhando ambaye, pamoja na baadhi ya wasaidizi wake, aliyekuwa Naibu Mkurugenzi Mtendaji Huduma za Shirika, Robert Shemhilu, Ofisa Mkuu wa Fedha, Lusekelo Kassanga na Meneja Mwandamizi katika Ununuzi, Harun Mattambo, wote walisimamishwa kazi kupisha uchunguzi huo.


Baada ya Mhando na wenzake kusimamishwa kazi aliyekuwa Mkurugenzi wa Masoko na Usambazaji, Felschami Mramba, alikaimu nafasi ya Mkurugenzi Mkuu Mtendaji wa TANESCO.


Pamoja na kashfa hiyo ya MC Donald Live Line Technology Ltd uchunguzi wa Raia Mwema umebaini kuwapo pia kwa kashfa nyingine ambayo pia inaonyesha matumizi mabaya ya madaraka, ikiwa nayo inathibitishwa na nyaraka, ikihusu kujipa kazi za shirika analoliongoza hivyo kujiingiza katika mgongano wa kimaslahi.


Kashfa hiyo ni ile iliyowahi kuandikwa na gazeti hili iliyohusu kuipa zabuni kampuni iliyohusishwa na mkewe.


Kwa mujibu wa nyaraka ambazo Raia Mwema imeziona kuhusiana na kashfa hizo, Mhando aliingia mkataba na Kampuni ya MC Donald Live Line Technology Ltd akiwa na jukumu la ndani ya kampuni hiyo la utafutaji miradi ikiwamo ile ya TANESCO.


Kutokana na kuwapo kwa taarifa hizo zinazothibitishwa na nyaraka mbalimbali, mwandishi wetu aliwasiliana na Mhando ili kwanza kujua kama anaitambua kampuni ya MC Donald Live Line Technology Ltd na kama anahusika nayo kwa kukabidhiwa jukumu la kuitafutia miradi kampuni hiyo binafsi.


Mhando alimjibu mwandishi wetu akisema; "Haya masuala yote ambayo unaniuliza yapo chini ya uchunguzi, kwa hiyo mimi siwezi kuyazungumzia kwa sababu yanachunguzwa."


Bodi ya TANESCO njia panda

Hata hivyo, huku ikiwa na taarifa hiyo tayari kwa kuipitia, Bodi ya TANESCO imejikuta ikiwa njia panda kwa baadhi ya wajumbe wake kuamua kutishia kujiuzulu; licha ya kutakiwa kukamilisha jukumu la kuhitimisha kazi ya kupitia taarifa hiyo ya uchunguzi dhidi ya menejimenti ya TANESCO iliyosimamishwa.

Vyanzo vyetu vya habari kutoka ndani ya bodi hiyo vinabainisha kuwa, mtafaruku huo umejitokeza kutokana na kauli iliyotolewa na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Steven Maselle ambaye alinukuliwa na gazeti moja la kila siku akitangaza kusudio la uongozi wa wizara hiyo kuivunja Bodi ya TANESCO kutokana na kile alichokieleza dhamira ya uongozi wao, pale wizarani, kuhakikisha kwamba mgawo wa umeme hautokei tena.


Pamoja na kumaliza mgawo wa umeme, Maselle alinukuliwa akisema kwamba kukamilika kwa bomba la gesi hapo Machi mwakani na kuanza kutumika kwa gesi hiyo viwandani na majumbani kunahitaji bodi imara yenye weledi na uzalendo kwa nchi.


Kauli hiyo imechukuliwa kwa uzito na wajumbe wa bodi ya sasa kwamba uongozi wa wizara umewahukumu wao kuwa hawana weledi na si wazalendo kwa nchi yao, hivyo wakiamini lengo la kauli hiyo ni kuwadhalilisha.


"Yupi ni mzalendo kati ya Maselle aliyepewa unaibu waziri hivi karibuni na Mkuu wa Majeshi Mstaafu, Jenerali Mboma aliyepigania nchi hii?" anahoji mmoja wa wajumbe wa bodi hiyo na kuongeza:


"Hawa vijana wasilewe madaraka, huwezi kijana umepata unaibu waziri juzi tu unamwambia Jenerali Mboma eti hana uzalendo, hana weledi, hii si sawa. Ni kukosa adabu, huu si utamaduni wetu Waafrika."


Taarifa za ndani za bodi hiyo zinabainisha kuwa Jenerali Mboma, ambaye ni mwenyekiti wa bodi hiyo, pamoja na wajumbe wake wamekasirishwa na kauli ya Naibu Waziri huyo, na waliamua kujiuzulu siku ile ile taarifa za kauli ya Maselle zilipochapishwa gazetini.


Hata hivyo, kuwasilishwa kwa taarifa ya CAG ya uchunguzi kuhusu ufisadi ndani ya menejimenti ya shirika hilo uliiweka bodi hiyo njia panda baada ya kushauriwa kutochukua uamuzi wa kujiuzulu, na badala yake wamalizie kazi iliyopo mbele yao wakiwa kama mamlaka ya ajira ya menejimenti hiyo, na wao wakiwa ndiyo waliotoa maelekezo ya uchunguzi huo.


Raia Mwema ina taarifa za uhakika kuhusu kuwapo kwa uhusiano usioridhisha kati ya uongozi mpya wa wizara hiyo chini ya Waziri Prof. Muhongo na bodi iliyopo ya shirika hilo. Baadhi ya wajumbe wa bodi hiyo wanadai kutopewa ushirikiano na waziri huyo.


"Mara baada ya uteuzi wake, Mwenyekiti alienda wizarani kwa ajili ya kumpongeza, lakini waziri alipiga chenga, wakaenda na Katibu Mkuu wake pale TANESCO na kuzungumza na wafanyakazi, wakakusanya madai yao zikiwamo tuhuma dhidi ya Mkurugenzi Mhando, ndipo akatuita Dodoma na kutukabidhi tuzifanyie kazi," anasema mmoja wa wajumbe wa bodi hiyo.


Hadi tunaenda mitamboni, bodi hiyo ilikuwa bado kutoa taarifa hiyo ya uchunguzi, na juhudi za kumpata Waziri Profesa Sospeter Muhongo na Naibu wake, Steven Masele hazikuzaa matunda.



 
Kuwa Mkuu wa Majeshi kwa miaka mingi si kipimo cha Uzalendo wala Weledi. Wapo Wastaafu wengi wa Serikali hii ya CCM wanabadilika na kuanza kusaka fedha baada ya kugundua Maisha baada ya kustaafu ni Magumu. Mimi bado naamini kauli ya Masele kama kweli aliitoa ni sahihi. Bodi gani haikuwahi kujua kinachoendelea Tanesco mpaka alipokuja Prof Mhongo na Masele kwenye hizo nafasi?
 
anapima uzalendo kw kuwa mkuu wa majeshi, mbona tuna wasisisi hata na uzalendo wa uncle Ben, ana alikuwa President wa nchiiii
 
Nchi hii iko ICU, wahuni wahuni wanafanya mambo ya kihuni bado wanapeta, your days are numbered!
 
mpeni taarifa mboma kuwa yeye si mzalendo wa kweli hata kama alikuwa mkuu wa majeshi ila saizi siyo tena na yeye anatafuta pesa ndo maana wanatu hujumu kila kukicha
 
Masele alishinda kwa kura moja hapo shinyanga, namaanisha kuramoja siyo asilimia moja... kubebwabebwa kapata u naibu waziri kichwa kimevimba, huwa nasema vijana wasipewe madaraka makubwa, sasa on anamtukana Mboma?
kazi kweli kweli vijana wa magamba...?
 
Uzalendo na weledi ni vitu viwili tofauti, Mboma kuwa Jenerali wa jeshi hakumfanyi kuwa mzalendo sana kuliko mtu mwingine yeyote!! na swala la mapungufu ya weledi yako wazi kwa bodi hiyo kushindwa kuisimamia tanesco mpaka ikawa kampuni ya mgao wa umeme (rationing) badala ya kusambaza (supply) umeme! alikuwa wapi Jenerali Mboma!

Waziri Massele udogo wa umri na upya katika cheo hakukupunguzii sifa za weledi na uzalendo hata kidogo; chapa kazi usitishiwe na jazba za kifisadi; hawa wanataka uogope unyamaze, kaza buti nchi hii ni yetu wote sio wakurugenzi hewa wasio na uwezo wa kusimamaia jambo bali kuchumia matumbo yao tu.
 
Wengi wa vijana wa siku hizi ni Kama wavuta bangi tu, mnajadili Mada za kudhalilisha wazee wenu, hivi Masele ni wa kumtusi mboma? Na Bado watu Humu JF mnashangilia, kweli utamaduni na heshima ya Mtanzania imepotea.
 
Wengi wa vijana wa siku hizi ni Kama wavuta bangi tu, mnajadili Mada za kudhalilisha wazee wenu, hivi Masele ni wa kumtusi mboma? Na Bado watu Humu JF mnashangilia, kweli utamaduni na heshima ya Mtanzania imepotea.

PhD,
Unakusudia kusema wazee wetu hawafanyi makosa?
Wanapofanya makosa tuwafanye nini? Elewa Tanzania tumejenga utamaduni mbovu sana wa kutowajibika. Ufujaji/ udokozi wa mali za umma (ufisadi) inaonekana ni ujanja wa kuwa na "maisha bora".

Heshima apewe mtu yeyote anayejiheshimu tu, sio kwa wazee tu.

Anaefanya madudu pale anapokabidhiwa dhamana/majukumu basi ni kujiwajibisha au kuwajibishwa tu. Heshima bila ufanisi katika dhamana aliyopewa mtu ni kuendelea kugawiana umaskini tu.

Utamaduni wa kulindana ukome ili tupate kuleta ufanisi na maendeleo.
 
Wengi wa vijana wa siku hizi ni Kama wavuta bangi tu, mnajadili Mada za kudhalilisha wazee wenu, hivi Masele ni wa kumtusi mboma? Na Bado watu Humu JF mnashangilia, kweli utamaduni na heshima ya Mtanzania imepotea.

We get some of the things in life by our own sweat. If Mbona wants respect, he should also make sure his conducts are ethical and abide the laws governing the country. hata hivyo, once a soldier, you will always be a soldier....I salute the generals!!!!
 
hiyo si kweli.Jen.Mboma ana historia si nzuri saaana jeshini.ukitaka kuelewa zaidi kaongee na wanajeshi waliokuwepo wakati wa utawala wake hasa katika tenda za maduka ya jeshi.Aliweza kuchakachua sana maduka yale na askari wakawa hawana pa kupeleka malalamiko yao.Tafakari
 
Wengi wa vijana wa siku hizi ni Kama wavuta bangi tu, mnajadili Mada za kudhalilisha wazee wenu, hivi Masele ni wa kumtusi mboma? Na Bado watu Humu JF mnashangilia, kweli utamaduni na heshima ya Mtanzania imepotea.
Huyu Mzee ndiye anayetudhalilisha sisi vijana! Kwanza, umri wake wa kutumikia nchi umeshapita, jeshini (ambako ndiko kwenye taaluma yake) wameona apumzike, sasa kwenye masuala ya kitaalamu kama mambo ya umeme anajidai anafaa kuongoza. Hivi wazee wa siku hizi hamuoni haya? Mbona mwenzenu Nyerere aliona apumzike apishe wengine? Kwani huyo Mboma akikaa zake nyumbani tukawa tunamfuata kwenda kupata ushauri wake haoni kuwa ni faraja? Pili, ni kweli kuwa Mboma hana taaluma wala weledi (professionalism) katika masuala ya jeshi. Bunduki na Electric circuits wapi na wapi? Si ni mbingu na nchi? Sasa kama siyo mchumia tumbo, iweje akubali uteuzi wa kuongoza shirika lisilohitaji nguvu (bunduki) wala siasa kama TANESCO? Kama ni mzalendo halisi, si angekataa uteuzi huo wakapewa wataalam na vijana wenye nguvu za kutuletea ufanisi katika shirika letu? Mpuuuzi tu huyo, hana lolote njaa iliwaka hadi akaona uenyekiti dili. Nani wa kujiuzulu hapo? Wameng'ang'ania na watafia hapo kama nzi kwenye kidonda!
 
Wengi wa vijana wa siku hizi ni Kama wavuta bangi tu, mnajadili Mada za kudhalilisha wazee wenu, hivi Masele ni wa kumtusi mboma? Na Bado watu Humu JF mnashangilia, kweli utamaduni na heshima ya Mtanzania imepotea.

Utamaduni wa kijinga haukubaliki hata kidogo, tunachotaka uzalendo na weledi, hata uzee hauna maana kama huna uzalendo na weledi hivyo mambo ya ku-take advantage sababu ya umri uzee na kushika nyadhifa kubwa hayakubaliki hata kidogo, maendeleo kwa wanananchi hayaangalii yote hayo, kama wamekosa weledi na wananuka ufisadi basi kinga ya heshima yote inakwisha, Mboma hajatukanwa hata kidogo acha kuzusha ila ni ukweli uliosemwa na masele, hivi huyu ni yuleyule mboma aliyehusika na kampuni ya wawekezaji ya kuchimba tanzanite kule arusha? kama ni yeye basi maneno ya masele ni 100%
 
Cheo anachotumikia mtu hakimfanyi awe mzalendo Masele aliyaona madudu ya bodi ya Mboma mkuu wa majeshi mfanyabiashara na muwekezaji wa migodi, Wazee hawa ndo wametumaliza hawana maana kabisa
 
Kipimo kipi atatumia kuwapata hao anaowahitaji?. Achapekazi wa chini yake watabadirika aache kelele!.
 
Wengi wa vijana wa siku hizi ni Kama wavuta bangi tu, mnajadili Mada za kudhalilisha wazee wenu, hivi Masele ni wa kumtusi mboma? Na Bado watu Humu JF mnashangilia, kweli utamaduni na heshima ya Mtanzania imepotea.

Kwanini wazee hampendi kuambiwa ukweli????? Mtu kama hana weledi na uzalendo itabaki kuwa hivyo siku zote, na tutaendelea kuwaambia kweli!!! Jifunzeni uzalendo wa kweli na huo ndio utamaduni wa mtanzania na sio kuishi kwa mazoea!!!! :focus:
 
Back
Top Bottom