sulphadoxine
JF-Expert Member
- Nov 1, 2010
- 2,257
- 644
KAMA takwimu zinaweza kudanganya, kwa mujibu wa Profesa Yule, basi inawezekana kwa asilimia kubwa zimetumika kuwadanganya wananchi wa Tanzania juu ya kukua kwa uchumi ilhali hali ya kipato binafsi ni ya kutia mashaka!
Hata kama takwimu halisi zinazotolewa na serikali juu ya maendeleo ya kukua kwa uchumi kuna kila sababu ya kudhani kwamba, takwimu za kiuchumi zinazotolewa hazikuzingatia hali halisi ya upimaji wa kina juu ya maendeleo ya vitu kwa manufaa ya watu.
Kama dhana, uchumi ni kuchuma! Ni chumo la watu pale wanapotumia mali ya asili na au rasilimali adimu kwenye mchakato wa kuzalisha ili kwa chumo (kipato cha kiuchumi) waweze kukidhi haja zao za kiuchumi, kijamii na kisiasa kwa uwiano unaozingatia ugavi na utashi.
Binadamu, kama kiumbe, ana mahitaji yake muhimu ambayo hukidhiwa kwa shughuli na au harakati za kiuchumi zinazowezesha upatikanaji wa mahitaji ya binadamu kama vile chakula, mavazi, nyumba, huduma za kijamii, ulinzi na usalama sawia.
Uchumi ni sayansi ya matumizi makini na endelevu ya rasilimali. Kama nchi, Tanzania yenye mali ya asili na rasilimali zinazotosha kwa maendeleo ya watu, ni masikini japokuwa takwimu zinaonyesha uchumi unakua!
Cha kustaajabisha ni hali ya viongozi wa kisiasa wa chama tawala na serikali yake kupigia mistari ukuaji wa uchumi unaokua pasipo kuweka mizania ya uhuru, haki na usawa baina ya hali hali ya kiuchumi inayowakabili wananchi wengi wa Tanzania.
Ka ujumla, hali ya wananchi wengi wa Tanzania ni tete na yenye kutia simanzi kwa jinsi yake. Uchumi wa wananchi unaozaa kipato binafsi kwa sehemu kubwa ya wananchi unategemea harakati za kubangaiza kwenye sekta isiyo rasmi na inayotambuliwa kama uti wa mgongo, yaani, kilimo!
Ni kweli kwamba kilimo, kama harakati muhimu ya uchumi katika Tanzania, inachukua takriban asilimia 75 ya wananchi hususan vijijini na maeneo yanayozunguka miji. Sehemu ndogo sana ya wananchi ndiyo wamebahatika kuwa kwenye sekta rasmi ya uchumi, kama vile ajira rasmi kwenye sekta ya umma au sekta binafsi.
Ukweli wa kiuchunguzi (kisayansi) pamoja na mantiki yake unaifanya Tanzania kuwa nchi ya kilimo (agrarian). Na kwa jinsi yoyote ile, kilimo kitaendelea kuwa uti wa mgongo wa uchumi wa wananchi kwa kuwa ndiyo njia pekee inayowawezesha wananchi wengi kumiliki rasimali yao, yaani nguvu kazi.
Kwa jinsi yoyote iwayo, na hii ni kweli na hakika tangu tulipopata uhuru miaka hamsini iliyopita, kwamba kilimo kilitangazwa kuwa, ndiyo baba; ndiyo mama kilimo ni kufa na kupona! Pamoja na ukweli wote huu kilimo na wakulima (ambayo ndiyo sekta nyeti inayochukuwa sehemu kubwa ya nguvukazi ya Tanzania) imetelekezwa na kusahaulika kabisa!
Serikali, pamoja na jitihada na au juhudi za hapa na pale katika kuboresha mazingira ya kilimo, bado inasuasua kwenye kuunda sera zisizokuwa na mikakati sahihi na makini ya kuleta tija na ufanisi kwenye maendeleo ya sekta ya kilimo, hususan kuongeza uzalishaji na thamani ya mazao.
Serikali imekosa uoni sahihi na wenye ubunifu angavu katika kuifanya sekta ya kilimo kuleta tija kwa wananchi na hatimaye kuinua uchumi jumla wa jamii na taifa sawiya. Kilimo kimekuwa sehemu ya uwekezaji usiyozingatia hali halisi, mazingira na wananchi.
Kama kilimo hakina tija kwa wananchi waliyo wengi waishio vijijini ambako ndiko kwenye sehemu kubwa ya nguvukazi; matokeo yake ni kwa nguvukazi hiyo kutokutumika vema; na hata ile nguvukazi inayotumika inakosa muelekeo wa tija na maslahi ya kiuchumi na hatimaye uzalishaji hushuka na kusababisha kupungua kwa kipato binafsi na cha taifa (pato la taifa kwenye kilimo). Hakuna asiyefahamu kwamba wananchi wengi wa Tanzania hawana umiliki wa rasilimali isipokuwa nguvukazi yao isiyotumika. Kwa kuwa rasilimali watu (nguvukazi) ya wananchi wengi wa vijijini haitumiki kwenye kilimo; na kwa kuwa wengi wao wamekata tamaa ya kushiriki kwenye kilimo kilichotelekezwa cha jembe la mkono; na kwa kuwa kilimo cha jembe la mkono ni kazi ya harubu (ngumu na inayotumia nguvu nyingi); wananchi wengi wa vijijini wameacha kulima!