Uchambuzi Wa Habari: JK , Rungu Na Kichwa!

maggid

JF-Expert Member
Dec 3, 2006
1,084
1,246
Ndugu zangu,

Kuna vumbi linatimka kule Arumeru Mashariki. Gazeti Mwananchi leo Jumatatu limebeba kichwa hiki cha habari; " Rungu la Kikwete lilimwokoa Siyoi".


Mwananchi linaandika;


"Juzi katika kikao hicho cha CC, ushindi huo wa mara ya pili wa Siyoi uliipasua tena kamati hiyo kuu yenye mamlaka ya juu ya uamuzi ndani ya chama hicho, baada ya baadhi ya wajumbe kudaiwa kutaka atoswe na apitishwe Sarakikya kutokana na tuhuma za matumizi makubwa ya fedha wakati wa kampeni.

Vyanzo vya habari vya kuaminika kutoka katika kikao hicho cha CC, vilifafanua kwamba waliosimama kidete kutaka Siyoi atoswe ni Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wassira.

Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, Nape alipinga Siyoi kurejeshwa akizingatia matukio mbalimbali ya tuhuma za matumizi makubwa ya fedha yaliyokuwa yakifanywa na baadhi ya watu ili wamchague mgombea huyo, kitu ambacho hakikupaswa kuvumiliwa.

Hoja hiyo ya Nape iliungwa mkono na Wassira ambaye naye alitaka Siyoi atoswe kutokana na tuhuma hizo za matumizi makubwa ya fedha kutoka kwa baadhi ya wapambe wake waliotaka mgombea huyo achaguliwe."
( Mwananchi, Jumatatu Machi 5, 2012)


Yumkini mhariri aliongeza ' mbwembwe' za kiuandishi, vinginevyo, maelezo ya hapo juu yanatoa tafsiri kuwa ni akina Nape na Wassira waliobeba marungu tayari kumtwanga Siyoi . Ni Mwenyekiti wa Chama hicho, Jakaya Kikwete ndiye anayeonekana kutumia zaidi kichwa kwa maana ya kutanguliza busara na hekima na hivyo kumnusuru Siyoi na marungu ya akina Nape na Wasira.


JK anaripotiwa na Mwananchi kutamka; "Basi na wewe ( Siyoi)usiende kutamba huko mitaani kwamba umeangusha watu, fanya kampeni, ushinde jimbo tuangalie mambo mengine mbele."


Hapa JK anaonekana kuwatuliza akina Nape na Wassira kwenye ugomvi wao na watu wa ' kambi ya Siyoi'. Kwamba Siyoi ataondoka kimya kimya na wala huko mitaani hatatoa kauli za kuwakera akina Nape. Naam, JK anaongoza chama kilichogawanyika kwenye makundi na hata vijiwe.


Na kiongozi hupimwa kwenye matatizo. Tofauti na miaka ya nyuma, CCM ya sasa, na kutokana na mabadiliko ya wakati, inaonekana kupigwa zaidi na mawimbi, tena mengine makubwa. Na mawimbi mengine yanatishia kabisa kukipasua chama na hivyo kuhatarisha chombo kuzama. Hadi sasa, JK ameonyesha umahiri mkubwa wa kuyakabili mawimbi hayo.


Je, mawimbi yamekwisha?



Hapana, kuna makubwa zaidi yanakuja. Katibu Mkuu, Wilson Mukama anaweka wazi, kwamba hakuna aliyemo kwenye chombo ( CCM) bila kuwa na kambi yake. Mukama anasema; kila mjumbe ana kambi na zinajulikana. Na akawataka wajumbe kufanya uamuzi ambao utakuwa na maslahi kwa chama na si ya kambi.


Na kambi hapa ndio mawimbi yenyewe. Kambi za sasa huenda bado ni ndogo ndogo na nyingi. Ilivyo CCM kuna kambi zitakazoungana na kufanya kambi kubwa zaidi. Hivyo basi, mawimbi makubwa zaidi yanakuja kuelekea 2015. Bila shaka, Katika hali ya sasa haiwezekani kukawepo na wanachama wengi wa CCM wanaokitamani cheo cha Uenyekiti wa chama hicho kabla haijatimu 2015.


Na hivi Siyoi ameshinda mara ngapi?



CCM wana mizengwe yao. Hili alipata hata kulisema Baba wa Taifa. Wanaokosea ni wenye kusema Siyoi ameshinda mara mbili. Ukweli Siyoi Sumari alishinda mara moja tu, ni kwenye ile raundi ya kwanza. Ya juzi ni marudio ya ushindi ule ule. Ila sasa inasemwa ameshinda zaidi. Hivyo basi, amejihakikishia ushindi. Kwenye chama chake.


William Lukuvi anaripotiwa na Mwananchi akimuunga mkono Mwenyekiti wake akisema haoni sababu ya kumwondoa Siyoi katika kinyang'anyiro hicho kwani ushindi wake ulikuwa mkubwa.


Naam, katika CCM hakuna ushindi tu. Kuna ushindi mkubwa na mdogo. Haitoshi kushinda tu, unatakiwa ushinde sana ili uepukane na hatari ya kupigwa marungu kama walio upande mwingine wataamua kukuvalia njuga!


Na mambo ya Ngoswe?



Alipoulizwa na Mwananchi Stephen Wassira alikataa kuzungumzia suala hilo akisema: "Hili linahusu chama na mambo ya chama mwulize Nape." Naam, mambo ya Ngoswe mwulize Ngoswe mwenyewe!


Maggid Mjengwa,

Dar es Salaam
Machi 5, 2012
Mjengwa Blog::Habari,Picha,Matangazo
 
Wimbi la madaktari linaweza kumuondowa na maji, this time hatuwezi kukubali ndugu zetu wafe alafu atokee mtu na utetezi wa kizembe eti Kikwete anaangushwa na wasaidizi wake! je ni nani alimteulia? hivi ukishindwa kumfuta kazi mteule wako unaweza ukafanya maamuzi yepi tena yenye afya kwa Taifa zima. kamwe hatutokubali tena ndugu zetu wafe kwa ajili ya uroho wa madaraka w watu wawili.
 
Back
Top Bottom