Tuwapuuze madaktari, tuwahurumie wabunge

Mzito Kabwela

JF-Expert Member
Nov 28, 2009
18,857
7,615
TUNA kila sababu ya kuwapuuza madaktari ambao wanafanya mgomo unaosababisha vifo na majeraha kwa wagonjwa wanaohitaji huduma za kitabibu kwa lengo la kuishinikiza serikali iboreshe mazingira ya kazi, posho, makazi na mishahara na madai mengineyo.
Wakati tukiwapuuza madaktari tuna kila sababu ya kuwahurumia wabunge walioamua kujiongezea posho ya kikao kutoka sh 70,000 hadi sh 200,000. Kisa ni upandaji wa gharama za maisha mkoani Dodoma ambao hauwahusu wakazi wa mkoa huo wakiwamo madaktari.

Wabunge ni watu wa maana zaidi ndiyo maana kwa siku wanalipwa sh 330,000 wakiwa mkoani Dodoma, wanakopeshwa magari, fedha, wanajengewa ofisi nzuri kwenye majimbo yao, wameanzishiwa mfuko wa jimbo ambao wao ndio waidhinishaji wa matumizi ya fedha hizo.

Hata kama wabunge wanalala bungeni wakati wa vikao vikiendelea hilo si tatizo kwakuwa wanakuwa na matatizo ya kiafya yanayotokana na madaktari kuwapa dawa zinazowasababishia usingizi.

Hawa ni watu muhimu sana ndiyo maana ili waipitishe bajeti ya wizara fulani ni lazima fedha za ‘kuwalainisha’ zitengwe bila kujali zinatoka wapi na kwa vigezo gani.

Ni watu wa kunyenyekewa sana kwani wakiumwa mafua tu lazima wakimbizwe India kuangaliwa afya zao au kutibiwa, madaktari tulionao hawana uwezo mkubwa wa kuwatibu ‘vigogo’, kazi yao kubwa ni kuwahudumia zaidi walalahoi.

Mishahara ya watu hawa haipungui sh milioni saba kwa mwezi, achana na marupurupu mengineyo lakini madaktari waliogoma mshahara wao hauzidi sh milioni 2.5, licha ya kufanya kazi kwenye mazingira hatarishi na magumu.

Madaktari wanafanya kazi bila kuwapo kwa vifaa muhimu, wanalipwa posho ya sh 10,000 kwa kufanya kazi usiku kucha lakini wabunge wanalipwa sh 70,000 na kuendelea kila wanapokwenda kukagua shirika, idara au taasisi fulani.

Hatuwezi kuwalinganisha wabunge na madaktari kwakuwa wao ndio wenye kuwasaidia wananchi kifedha katika misiba, harusi, ujenzi wa shule na huduma nyinginezo ndiyo maana mishahara yao haitoshi.

Wabunge wetu ni watu wa maana sana ndiyo maana kila anayetaka posho na mishahra yao ipunguzwe anakuwa adui kwao. Sijawasikia wabunge katika sakata hili la mgomo wa madaktari na hata mmoja mmoja aliyejitokeza kuusemea, hajafanya hivyo kwa nguvu kubwa kama inavyoonekana bungeni pindi wanapokerwa na hoja fulani.

Sijawaona wabunge waliotumia muda mrefu kuwashambulia wenzao wa CHADEMA kwa kususia kujadili muswada wa mchakato wa uanzishwaji wa Katiba mpya, sijawaona wale waliokuwa mstari wa mbele kupambana na ufisadi wakijitokeza hadharani kupigania masilahi ya madaktari au kuishauri serikali na hasa waziri mkuu kuzungumza na waliogoma

Madaktari wamegoma, rais wetu yupo Davos nchini Uswisi akishiriki kwenye mkutano wa kiuchumi, waziri mkuu hajakutana na madaktari hao anasema milango iko wazi kwao. Viongozi hawa hawaonyeshi kuguswa na mgomo huu.

Tulimuona Rais Kikwete akikatisha mapumziko yake ya mwishoni mwa mwaka jana kwenda jijini Dar es Salaam kukagua madhara ya mafuriko yaliyotokea kwenye jiji hilo, lakini sijamuona akikatisha ziara yake ili kunusuru mgomo huu ambao nina hakika umesababisha vifo vya watu wengi.

Vifo vilivyotokana na mgomo wa madaktari ni vingi zaidi kuliko vile vya mafuriko ya jijini Dar es Salaam, viongozi hawashtuki kwakuwa wanatibiwa nje ya nchi. Rais atakuja kuingilia kati suala hili hapo baadae na ataonekana ni shujaa.

Katika hili sitakuwa miongoni mwa wale watakaompongeza rais, bali nitakuwa miongoni mwa wale watakaomlaumu kwa kuyafumbia macho matatizo ya watumishi wa sekta ya umma.

Mimi siamini kuwa rais anaweza kuwa msafi na imara ilhali watendaji wake ni dhaifu na wasiowajibika kikamilifu katika kutatua matatizo ya wananchi. Wapo wanaosema kiongozi mkuu wa nchi ni mchakapazi lakini anaangushwa na watendaji wa chini.

Kama rais anaangushwa na waziri mkuu na mawaziri wengine kwanini asivunje baraza la mawaziri na kuunda jingine litakalochapa kazi kulingana na mahitaji ya wananchi?

Serikali imeamua kuchagua njia ya kutatua matatizo yetu kupitia migomo mbalimbali, haioni sababu ya kujiwekea utaratibu wa kutafuta suluhu kabla ya migomo.

Leo hii matatizo ya wanafunzi wa vyuo vikuu hayatatuliwi mpaka wagome, walimu hawasikilizwi mpaka watishie kugoma, hivyo hivyo kwa wafanyakazi wengine wa utumishi wa umma na binafsi, kiufupi tujenga utaratibu wa ‘goma, usikilizwe na utimiziwe.’

Mgomo huu angalau umeitoa kichochoroni serikali, imetangaza kuwa imepata fedha za kujenga nyumba za madaktari kwa wilaya 18 zilizopo pembezoni, imetangaza kuangalia upya utaratibu wa kugawa nyumba kwa madaktari. Najiuliza ilikuwa wapi kipindi cha nyuma?

Madaktari wametangaza hawawataki viongozi wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii bali wanataka kuzungumza na waziri mkuu ambaye mpaka sasa anawapiga chenga. Kwanini hataki kukutana nao kama si serikali kuogopa kujibu maswali yenye tija?

Hospitali zetu hazina vifaa, wauguzi, madaktari hawatoshi lakini wanasiasa wanaishi maisha ya peponi yanayoambatana na kupewa vitendea kazi vyote muhimu kila wanapoviomba.

Nina imani kama viongozi wetu hawa wangeitwa leo asubuhi na Rais wa Marekani Barack Obama, jioni wangekuwa ndani ya ndege kuitikia wito huo, kisa, wanajua watapewa misaada.

Wananchi wanafariki dunia, wanateseka lakini waziri mkuu yupo, makamu wa rais yupo hawashtuki na wanadiriki kuwaagiza wenzao wasiotakiwa kwenda kuzungumza na madaktari.

Hata mahakamani watuhumiwa wana haki ya kumkataa haakimu au jaji anayesikiliza kesi yao, iweje Pinda alazimishe madaktari wasikilizwe na viongozi wasiowataka?


 
Imetulia hiyo.... Nacho sema hawa watu wamejisahau na kulewa madaraka. Hivi Tanzania hakuna Dungadunga wamshughurikie huyu Mama ili aone jinsi masikini wanavyopata shida? Dungadunga mpo wapi?? Au mnataka shillingi ngapi? Naona watu tunapoteza matumaini sasa...!
 
Back
Top Bottom