BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,790
- 288,007
Mbatia ataka mafisadi waachwe
2009-01-05 14:24:34
Na Muhibu Said
Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia, amewataka Watanzania kuachana na mtindo wa sasa wa kundi moja kulinyooshea kidole lingine kuhusu kashfa za ufisadi na kutumia madaraka vibaya akisema kwamba kitendo hicho kinaigawa nchi. 2009-01-05 14:24:34
Na Muhibu Said
Sanjari na kuigawa nchi, Mbatia, ambaye muda wa uongozi wake katika chama hicho ulifikia tamati jana, aliuambia Mkutano Mkuu wa uchaguzi wa chama hicho kuwa kitendo hicho pia kinakwamisha uzalishaji kwa vile hakuna aliyemsafi katika kashfa hiyo tangu enzi za utawala wa Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere.
Badala yake, amewataka Watanzania wakae chini na kujadiliana kuhusiana na suala la ubinafsishaji, ambalo alisema ndio chanzo kikubwa cha kuibuka kwa kashfa hiyo.
Mbatia alisema hayo alipokuwa akitoa nasaha katika Mkutano Mkuu wa Uchaguzi wa chama hicho, uliofanyika katika ukumbi wa kituo cha Msimbazi, jijini Dar es Salaam.
Alisema suala la kutumia madaraka vibaya, ni la muda mrefu kwa Watanzania nchini na kwamba hakuna asiyeguswa kwa namna yo yote na kashfa hiyo.
``Kwa mfano, jana (juzi) alikuja mtu ofisini kwangu kutoka Mtwara, akaniambia kuwa usikanyage Mtwara na hoja yako ya kutaka Mkapa aondolewe kinga ili ashtakiwe, akaniambia kama unataka Mkapa aondolewe kinga, basi aondolewe na Mzee Mwinyi pia, kwa kubariki ubadhirifu wa IPTL (mradi wa kuzalisha umeme) wakati wa utawala wake.
Hata leo Nyerere akifufuka ataambiwa alitumia madaraka yake vibaya, hivyo naye ashtakiwe. Kila mtu anamnyooshea mwingine kidole,`` alisema Mbatia.
Alisema nchi hivi sasa imefikia pabaya, ambapo Watanzania wameanza kuitana mafisadi, baada ya kuacha kuitana ndugu na mheshimiwa, kama walivyokuwa wakifanya hivyo huko nyuma.
``Tumetoka kwenye kuitana ndugu, tukaenda kwenye kuitana mheshimiwa sasa tumekwenda kwenye kuitana mafisadi.
Kama hujatoa kibanzi katika jicho lako, ona boriti la jicho lako,`` alisema Mbatia, ambaye kauli zake zilionekana kupingana na juhudi za makundi mbalimbali ya jamii nchini kupinga vitendo vya ufisadi.
Alisema amesikitishwa na gazeti moja nchini, ambalo lilimkariri wakati akiwa masomoni nje ya nchi akishauri Rais Mstaafu Benjamin Mkapa aondolewe kinga ili ashtakiwe mahakamani kwa tuhuma za ufisadi zinazomkabili, wakati hakuwahi kusema kitu kama hicho.
``Naviomba vyombo vya habari vinitendee haki,`` alisema Mbatia akimaanisha kuwa haungi mkono hoja zinazotolewa na baadhi ya watu kuwa Mkapa anapaswa kushitakiwa kutokana na kutumia vibaya madaraka yake katika mchakato wa ubinafsishaji wa mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira, mkoani Mbeya.
Mkapa na wenzake wanadaiwa kujimilikisha hisa asilimia 80 kupitia Kampuni ya Tan Power Resources Limited kwa Sh. milioni 700 badala ya thamani halisi Sh. bilioni nne. Pia wanadaiwa kulipa Sh. milioni 70 tu.
Kutokana na hali hiyo, Mbatia, aliyekuwa akigombea uenyekiti wa chama hicho, aliwataka Watanzania kutoa hoja zenye kujenga ustawi kwao badala ya kuendelea na mjadala unaozua mgogoro miongoni mwao, ambao alidai kuwa unaigawa nchi na kukwamisha uzalishaji.
``Hakuna uzalishaji, ni mjadala tu wa mgogoro, alisema Mbatia.
Naye Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, John Tendwa, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika Mkutano Mkuu huo, alivitaka vyama vya siasa kutekeleza yale wanayosema.
``Ninavitaka vyama vya siasa, wazingatie wanayosema.
Wamekuwa wakisema kuwe na mshikamano na tuwe na utaifa. Watekeleze kwa vitendo. Siyo baada ya hapo kila chama kinafuata yake,`` alisema Tendwa.
Pia, alisisitiza mahitaji ya mabadiliko ya sheria ya ruzuku na kuvitaka vyama vya siasa kuwafikia wananchi na pia serikali ibadilike na kudhibiti rushwa katika vyama vya siasa.
SOURCE: Nipashe