Tusikimbilie kujiunga na mashirika/makubaliano ya kimataifa

Sijali

JF-Expert Member
Sep 30, 2010
2,586
1,678
Nimechunguza sana na kuona mara nyingi nchi za Afrika hukurupuka na kujiunga na shirika/mikataba/makubaliano yeyote yaitwayo ya Kimataifa bila kwanza kufikiria kwa kina faida na athari zake. Jambo hili lina matatizo makubwa sana huko tuendako.

Kuna minong'ono mingi, na mimi naanza kuiamini, kuwa vyombo hivi viitwavyo vya Kimataifa kwa kweli ni mfumo wa kikundi kidogo tu ambacho lengo lake la mwisho ni kutaka kuitawala dunia. Kuitawala dunia nzima kutawezekana tu kwa kupitia mashirika haya ambayo ukishatia mkataba huwezi kamwe kujinasua.

Yeyote anayechunguza uendeshaji wa mashirika haya na jinsi yalivyogeuka kuwa ya kidikteta ataona wazi mustakbali tunakoelekea. Hapo zamani, mashirika haya yalikuwa yanaendeshwa kwa ridhaa na ijimai ya wote (consensus). Waama hivi sasa, kidogo kidogo mengi yanaonekana wazi kuendeshwa kwa nguvu, mikeke, rushwa na hata vitisho. Mwenye kufuatia sakata la shirika la Umoja wa Mataifa la nguvu za nuklia duniani IAEA (International Atomic Energy Agency) baina yake na Iran, ataona dhahiri udhalimu na ukandamizaji wa shirika hilo. Linalotisha zaidi ni kuwa Iran kamwe 'haina haki' ya kuthubutu hata kujitoa katika shirika hilo, na kwamba ikijitoa hii leo itashambuliwa kwa visingizio mbali mbali.

Hapa ndipo mashirika haya yanayoitwa ya Kimataifa yalipofikia katika kuburuzwa na nchi chache, ambazo zenyewe kwa kweli zinatawaliwa na kikundi cha watu wachache wajanja.

Hali ya mashirika mengine ya Kimataifa si nzuri pia. Angalia kama ICC, na hata UN yenyewe, kweli zinakidhi maslahi ya nani?

Nilifurahi sana wakati UN iliposhindwa hivi karibuni kuzilazimisha nchi ziweke mkataba wa kuzuia mauzo ya silaha ndogo ndogo duniani. Si kwa sababu napinga hatua hiyo, la hasha. Silaha ndogo ndogo kwa kweli zimesababisha mauaji mengi zaidi duniani hata kuliko nuklia. Lakini furaha yangu ni kwa kujua mkataba kama huo siku moja ungekuja kutumiwa na kikundi hicho kwa kuzizuia nchi zilizovamiwa na rafiki zao, wasinunue silaha za kujikinga. Angalia hali ya Syria hii leo iliyowekewa vikwazo kama hivyo, ama Iran ambayo wanaitishia kuipiga kila siku, lakini nchi hiyo haina ruhusa kununua silaha. Hata silaha za kujilinda tu, kama vile radari ya S-300 ambayo Iran ilikwishailipa Urusi....imezuiwa! Walifanya hivyo kwa Iraq pia.

Namalizia kwa kusema, Tanzania ina Uranium. Hawa jamaa kwa vile watataka kununua madini haya kwa bei ya kutupa, na pia kuzuia nchi kama Iran na Korea ya Kaskazini au Pakistan zisiweze kununua, kuna juhudi za kuandika 'mkataba wa Kimataifa' wa namna ya ununuzi wa madini haya.

Kwa kweli kikundi hicho nilichokielezea ni wajanja sana. Wana uwezo wa kulifanya jambo lionekane kama jambo la maana na la msingi, lakini kumbe watalipotoa ili liwatumikie wao, kama ilivyotoeka katika ICC ambayo sasa inatumiwa dhidi ya Waafrika zaidi ingawaje akina Bush na Blair wameamuru vita vilivyoangamiza zaidi ya watu milioni mbili, tena kwa sababu za uongo, lakini hutasikia hata siku moja hawa wakiburuzwa mbele ya mahakama hiyo. Au IAEA, ambayo miaka hiyo ya 50 ilipobuniwa ilionekana ni fikra nzuri kuzuia kutawanya silaha za nuklia.... lakini angalia hii leo wanaitumia dhidi ya Iran ingawaje wao wenyewe wana silaha hizo na wanazidi kuziboresha kila siku, kinyume cha vipengee vya IAEA.

Kama ningekuwa kiongozi wa Tanzania, au nchi yote nyingine ya Afrika, kwa kweli ningekuwa mwangalifu sana wa kuingia mikataba yeyote ya Kimataifa. Kumbuka, hawa jamaa wanapanga kwa kutazama miaka 50-100-150 ijayo, kwa hiyo ni vigumu kwetu sisi twenye maono ya leo na kesho, kufichua makusudiao hasa ya mambo wanayoyafanya hii leo.

Nina shaka hata hii mikataba ya mazingira, ina siri fulani ya kuwanufaisha wao hapo baadaye.
 
Back
Top Bottom