Rev. Kishoka
JF-Expert Member
- Mar 7, 2006
- 4,526
- 1,529
Ee Bwana, kumbuka yaliyotupata, utazame na kuiona aibu yetu. Urithi wetu umegeuka kuwa mali ya wageni, na nyumba zetu kuwa mali za makafiri... tumekunywa maji yetu kwa fedha na kuni zetu tunauziwa, furaha za mioyo yetu zimekoma na machezo yetu yamegeuka maombolezo, Taji ya kichwa chetu imeanguka.. ole wetu! kwa sababu mioyo yetu imezimia kwa ajili ya hayo, macho yetu hayaoni vema. Hekima hukaa katika moyo wake mwenye ufahamu, bali yaliyo ndani ya wapumbavu, hudhihirikia. Haki huinua Taifa, bali dhambi ni aibu ya watu wote!
Kwa hiari yetu wenyewe, kwa kutumia nguvu zetu wenyewe, kwa akili zetu na utashi wetu ulioambatana na upofu uliojaa tamaa, uvivu, usengenyaji na uroho, Tumeuza Uhuru wetu na hazina yetu tumeifuja.
Sisi ni koloni lililo na Uhuru wa Bendera, tumejitakia kwa ujuvi wetu kuwa masikini wa kudumu, wanyonge ndani ya nchi yao na kuburuzwa kila siku kama majuha.
Angalieni jinsi neema tulizopewa na Mola tulivyoziharibu kutokana na tamaa, majaribu, ujinga na kiburi kilichojaa uvivu na utegemezi.
Zi wapi zile ndoto za Kujitegemea, Siasa safi, Uongozi Bora kwa kutumia Juhudi na Maarifa kuupiga vita Ujinga, Umasikini na Maradhi?
Kila siku kukicha ni baragumu za ufujaji na uhujumu. Leo ni Benki Kuu, mara ni ATCL, TRL, Tanesco, Misitu, Utalii, ardhi, madini, uvuvi na hata kujiingiza katika kuatakia shari jirani zetu na kuneemesha maangamizi ndani ya ardhi yao.
Siwalaumu viongozi pekee, bali lawama za kwanza ni kwangu mimi (na wewe), niliye mjinga ambaye kwa upumbavu nimekimbia majukumu yangu na wajibu wangu niliopewa na Mola na kulindwa na Katiba ya Nchi yangu, kwa kuuza haki yangu ya kupiga kura kwa kukubali kuburuzwa kwa kulishwa andazi na chai.
Laiti ningekuwa mjasiri na kuitafuta kweli na haki na hata kuamua dira ya Taifa langu kwa kutumia umakini na busara, leo hii nisingekuwa hapa nikiangua kilio na kujitwisha mavumbi nikiwa nimevaa kaniki, nikihangaika kwa tabu na mateso, njaa na magonjwa yakiniwinda kwa urahisi nami nikawa mkimbizi wa ardhi niliyopewa na muumba.
Ni aibu ya kutisha, utajiri wote nimeutapanya kwa manufaa ya wageni na si ya ukoo na jamaa zangu. Nimeendelea kuwa mpumbavu kwa kulewa mvinyo na asusa za bure, nilizovimbiwa huku nikisifiwa kuwa nimejaaliwa neema na ni mpole.
Tumeuza nchi yetu, sasa tuamue tuendelee na maombolezo huku tukinyanyaswa na kusulubiwa na njaa na umasikini au tuamke tupukute vumbi, majivu na kufuta machozi na kuanza upya kwa kujitutumua na kutumia busara katika kutafuta haki.
Haki na hadhi yetu itarudi pale tutakapoamua kwa sauti moja iliyo kubwa na kishindo kuwa tumechoka kunyonywa, kunyanyaswa na kudharauliwa.
Tuikimbilie haki yetu kwa nguvu bila woga, tutumie dhamana yetu kwa ufasihi, ili hazina na rasilimali zetu ziwe kwa manufaa yetu, kama Muumba alivyotupangia.
Jiulize, mpaka lini utaendelea kuamini ahadi hewa, ukiwa umelewa togwa ya ukwaju na kupewa leso kufuta jasho, huku maji na kuku wa karamu ni yule uliyemtoa zaka?
Kuwang'oa mafisadi na kuushinda umasikini utaanzia na nafsi yako, kisha familia yako, ndipo cheche zitakaposambaa katika mtaa, kaya, kijiji, kata, tarafa, wilaya, jimbo, mkoa na Taifa.
Kuushinda Unyonge, Umasikini na Maradhi utaanzia kwako binafsi na kwa nguvu zako na majirani zako utaweza kuushinda utumwa.
Ni hiari yako kuendelea kuwa mtumwa au kuurudisha Uhuru wako na kulinda hazina yetu!