Tumejiandaa vipi na El Nino?

Gudboy

JF-Expert Member
Aug 14, 2009
867
77
NI hakika kwamba mwaka huu mvua za el nino zitaikumba nchi yetu kama ambavyo zitakumba pia majirani zetu. Hizi ni mvua zinazonyesha kwa wingi na mfululizo, zikisababisha mafuriko yanayoleta uharibifu mkubwa wa miundombinu.

Kwa mara ya mwisho nchi hii ilikumbwa na mvua hizo mwaka 1998, ambazo zilinyesha kwa wingi sana na kuharibu miundombinu yetu kwa kiwango kikubwa. Zipo barabara, madaraja na hata nyumba za watu ambavyo vilibomolewa na sehemu nyingine hali haijarejea kuwa kama zamani, miaka 11 baada ya uharibifu huo.

Kwa wakazi wa Dar es Salaam watu wenye nyumba karibu na baharini na kwenye mikondo ya maji wanakumbuka jinsi nyumba zao zilivyokumbwa na mafuriko. Zipo zilizofutika kwa kwenda na maji ilhali nyingine zikiharibiwa kwa kiwango kikubwa.

Hakuna anayeweza kubisha ukweli kwamba el nino ni maafa kwa miundumbinu, mali na maisha ya raia na mifugo.
Kwa kuwa Mamlaka ya Hali ya Hewa imetangaza wazi kwamba el nino inakuja, na kwa kuwa hili ni janga la asili, sisi kama taifa kwa kuwa hatuwezi kuzuia janga hili kutokea, walau tunahitajika kujipanga kwa maana ya kuwa tayari kukabili madhara yatakayosababishwa na mvua hizo zinazotarajiwa kuanza mwishoni mwa mwezi huu au mapema mwezi ujayo.
Ni kwa jinsi hii tunauliza mamlaka mbalimbali zenye dhima ya kuandaa taifa kukabiliana na majanga zinafanya nini katika kipindi hiki ili kuhakikisha kwamba tunahimili madhara yote ya mvua hizi.

Mathalan, tunajua kwamba wapo wananchi wanaoishi mabondeni, wapo wanaoshi karibu sana na kingo za mito, kwenye fukwe za bahari, lakini pia wapo ambao wamevamia njia za mito kwa sababu tu kwa muda mrefu mito hiyo imekauka wakidhani ni maeneo salama.

Mbali na wote hao, tunatambua kwamba mvua nyingi kwa nchi za ukanda wa kitropiki maana yake ni ongezeko kubwa zaidi la mazalia ya mbu, na kwa hali hiyo ongezeko kubwa la wagonjwa wa malaria kwa sababu sasa mbu watakuwa wanazaliana kwa kasi zaidi.

Masual haya yote yanajulikana kwamba yatajitokeza mvua za el nino zikianza, kwa hali hii basi tunahoji mamlaka zetu kama Kitengo cha Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Mamlaka ya Hali ya Hewa na wadau wengine wanafanya nini katika kuandaa umma kukabiliana na madhara ya el nino?

Mbali na mamlaka hizo mbili, kuna Wizara ya Miundombinu yenye wajibu wa kusimamia ujenzi wa barabara, njia za reli na madaraja nchini; hawa tunawauliza wamejiandaa vipi kuhakikisha kwamba mitaro ya kuondoa maji barabarani inafanya kazi vizuri ili kupunguza uharibifu wa barabara unaosababishwa na maji kutuama barabarani? Je, madaraja yetu yamekaguliwa na kuhakikishwa kwamba yako imara kukabili el nino ya mwaka huu?

Je, halmashauri za majiji, manispaa, miji na wilaya nazo zimejipanga vipi kukakikisha kwamba mitaro ya maji machafu kwenye maeneo ya mamlaka zao ipo yatari kukabiliana na eli nino kwa maana kwamba imezibuliwa, imekarabatiwa na kuweza kutiririsha maji kwenda baharini bila kusababisha mafuriko kwenye makazi ya watu?

Zipo mamlaka za Afya, kama vile Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii; kuna Bohari Kuu ya Madawa (MSD) hawa wana wajibu wa kuhakikisha kwamba dawa za malaria na nyinginezo ambazo zitahitajika kutokana na madhara ya mvua hizi zinapatikana bila mizengwe, ikiwamo magonjwa ya milipuko yanayoweza kutokea kwa sababu ya kuvurugika kwa ama vyanzo vya maji au miundombinu yake.

Tukitafakari kwa mapana, tunaona kwamba kama taifa tuna muda mfupi sana uliobaki kujiweka tayari kukabiliana na madhara ya el nino, kwa hali hii wiki hizi mbili au tatu zilizobakia kabla ya mvua kuanza ni vema basi mamlaka zinazohusika kama tulivyozitaja hapo juu, zikajipanga kupunguza hasara na makali ya madhara ya el nino kwa wananchi wetu. Tuamke sasa!
CHANZO: NIPASHE
haya wale ndugu zangu wa mabondeni wale tahadhari hiyo. Tafakari na chukua hatua haraka
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom