Tumbaku yaipuku dhahabu kuingizia mapato ya halmashauri | Send to a friend |
Wednesday, 18 April 2012 19:51 |
0diggsdigg Shija Felician, Kahama KILIMO cha tumbaku ambacho ni maarufu Kanda ya Ziwa, kinaonyesha kuongoza katika kuingizia mapato makubwa Halmashauri ya Wilaya Kahama na kuishinda migodi miwili ya dhahabu ya Bulyanhulu na Buzwagi inayomilikiwa na Kampuni ya African Barrick Gold Mine. Katika makadirio ya bajeti ya mwaka 2012/13, halmashauri hiyo inatarajia kukusanya zaidi ya Sh43 bilioni kutoka vyanzo mbalimbali, likiwa ni ongezeko la asilimia 27.6 ya mwaka 2011/12. Akiwasilisha bajeti hiyo kwa madiwani, Ofisa Mipango wa Halmashauri ya Wilaya ya Kahama, Duncan Thebas alisema Sh4.9 bilioni zinatarajiwa kutoka vyanzo vya ndani vya mapato ikiwamo migodi ya dhahabu ya Bulyanhulu na Buzwagi na kampuni za kununua la tumbaku. Thebas alisema migodi ya Buzwagi na Bulyanhulu itachangia Dola 400,000 za Marekani (Sh6 milioni), huku kampuni za kununua tumbaku zikitarajiwa kulipa ushuru wa Sh720 milioni. Kutokana na bajeti hiyo, tumbaku inaonyesha ndiyo inayoongoza kuchangia mapato kwenye bajeti tofauti na jamii inavyofikiri, kuwa dhahabu ndiyo inayochangia mapato zaidi kwa Halmashauri ya Wilaya ya Kahama. Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kahama, Eliza Bwana alisema miradi mingi ya mwaka jana ilishindwa kukamilika kutokana na ucheleweshaji fedha za ruzuku kutoka Srikali na baadhi ya wadau kushindwa kulipa ushuru. Bwana alisema sababu zingine zilizochangia kukwama kwa miradi hiyo, ni kupanda kwa gharama za uendeshaji ikiwamo mafuta mitambo, dizeli na petroli na uwapo kwa bajeti finyu iliyopangiwa Idara ya Ujenzi kukarabati barabara. Alisema mtandao unaotolewa fedha na Serikali ni kilometa 484 za barabara, hali ambayo ni kidogo ukilinganisha na uharibifu wa barabara unaofanywa na wananchi kwa kuendesha shughuli za kilimo kwenye hifadhi na kupitisha mifugo. Hata hivyo, Bwana alisema tayari mikakati imeshafanyika kwa kushirikiana na mkoa, Tamisemi kuhusu mtandao halisi wa barabara Wilaya ya Kahama ili ziweze kupata bajeti halisi na kilichosalia ni wizara kwenda kuhakiki. Madiwani walipitisha bajeti ya Sh43,760,610,726 ikiwa ni ongezeko la asilimia 1.5 ya bajeti iliyopita ya Sh43,112,652,848. CHANZO: Tumbaku yaipuku dhahabu kuingizia mapato ya halmashauri |