Tuhuma za silaha haramu:Serikali ijisafishe, isitubabaishe

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,789
288,009
Serikali ijisafishe, isitubabaishe

Lula wa Ndali-Mwananzela
Raia Mwema
Disemba 9, 2009

KUSEMA kuwa ripoti ya jopo la wataalamu wa Umoja wa Taifa waliopewa jukumu na Baraza la Usalama kufuatilia utekelezaji wa Azimio la Umoja wa Mataifa namba 1857 (2008) kuwa ni "uongo" haitoshi.

Kudai kwamba Tanzania haihusiki katika usafirishaji wa silaha haramu kwenda eneo la migogoro la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo haitoshi; kusema kwamba ripoti hiyo inachafua jina la Tanzania na hivyo Umoja wa Mataifa uiombe radhi Tanzania, nalo halitoshi. Havitoshi kwa sababu vinaonyesha uzalendo uliopotoka.

Tukikubali majibu ya aina hii kwenye mlolongo wa tuhuma nzito za baadhi ya maafisa wa Serikali na baadhi ya vyombo nyeti kuwa wanashiriki katika kuwezesha usafirishaji wa silaha haramu tutakuwa tumekubali kuwa sisi ni wananchi tusiojali kabisa Serikali yetu inafanya nini kwa niaba ya jina letu.
Tukikubali majibu yaliyotolewa na Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje Bernard Membe na kuyakumbatia tukidhania kuwa tunaonyesha uzalendo basi tunatoa kibali kwa watawala wetu kufanya lolote kwa jina “letu” wakiamini kuwa wakibanwa tutajipanga nyuma yao na kuanza kulia kama kasuku walionyweshwa ulanzi “Tanzania Tanzania”.

Serikali yetu na wasemaji wake hawana rekodi ya kusema ukweli na ukweli wote wanapokabiliwa na shutuma mbalimbali. Ushahidi upo kwa mtu yeyote kuuona juu ya hili.

Walipoambiwa kuwa ujenzi wa minara pacha wa Benki Kuu umegharimu kiasi kikubwa cha fedha kushinda gharama za ujenzi wa jengo lenye nafasi kama hiyo huko New York watawala wetu walikataa kabisa.
Walipoambiwa kuhusu ubadhirifu Benki Kuu walikana kabisa na kudai kuwa huo ni uzushi.

Walipoambiwa kuwa shirika letu la ndege la ATCL lina mpango wa kununua ndege mbovu ya Airbus 320 kwa mabilioni ya shilingi walikanusha huku wakitetea kuwa shirika hilo liko katika hali nzuri na madai hayo hayana msingi. Walipoambiwa juu ya mkataba mbovu wa Rites Consortium kuendesha shirika letu la Reli wakatetea huku wakilimwagia fedha za walipa kodi wa Tanzania kama kumwagilia shamba la nyanya!

Na mifano ipo mingi ya jinsi gani watawala wetu si wakweli moja kwa moja na mara kadhaa wameamua kwa makusudi kulificha Taifa ukweli wote kana kwamba ukweli huo tukiufahamu basi tutaanza kulia kama watoto wadogo.
Jambo moja ni dhahiri, kuwa watawala wanawaona Watanzania kama watoto wadogo na hivyo kuwamegea taarifa kwa vipande vipande wakiamini kuwa wananchi hawastahili na hawana haki ya kujua ukweli wote. Matokeo yake ndiyo haya.
Hadi sasa sijaona hata sehemu moja ambayo Serikali imeweza kujisafisha na tuhuma hizi nzito ambazo japo kwa Watanzania wengi yawezekana hii ndio mara ya kwanza kuzisikia ukweli ni kuwa ni tuhuma ambazo zimedumu kwa karibu miaka 10 sasa.

Kuanzia kama mwaka 1998 wakati wa kuiva kwa mgogoro wa Congo ripoti ya kutumiwa kwa ardhi ya Tanzania kupitisha silaha zilianza kuvuja na hata baadaye ripoti mbalimbali za mashirika makubwa ya haki za binadamu zimekuwa zikiitaja Tanzania kuwa ni njia kuu ya kusafirisha silaha na bandari ya Dar es Salaam na uwanja wa ndege wa Mwanza kuwa ni sehemu ambazo silaha hizo haramu zimekuwa zikipitishwa.

Ripoti ya jopo jingine kama la wataalamu ya mwaka 2001 iliyowasilishwa na Katibu Mkuu wa UM wa wakati huo Koffi Annan inadai wazi kuwa rasilimali za Congo ambazo zilikuwa chini ya waasi wa RCD-Goma zinapitishwa kupitia Dar es Salaam. Rasilimali hizo zinajumuisha mbao, dhahabu na almasi.

Miaka nane baadaye ripoti nyingine imetaja hadi maduka na watu wanaohusika kwa hapa Tanzania! Ripoti hiyo ilidai kuwa almasi ilikuwa inashikiliwa katika Benki Kuu ya Tanzania kabla ya kusafirishwa kwenye Ubelgiji.


Katika ripoti yao ya mwaka 2002 jopo la wataalamu walituma maswali kwa nchi 11 zinazohusika na usafirishaji wa bidhaa mbalimbali kutoka Congo (Tanzania ni mojawapo) na ilitaka kupewa maelezo juu ya usafirishaji wa bidhaa, sheria mbalimbali n.k. Ripoti hiyo ikadai kuwa kati ya nchi hizo 11 nchi nne hazikupeleka majibu yake; Tanzania ikiwa ni mojawapo (nyingine ni Jamhuri ya Congo, Msumbiji na Zimbabwe).

Mwaka jana katika ripoti yao kama hii (ikitekeleza azimio 1807 la 2008) jopo hilo la wataalamu liligusia juu ya shehena ya silaha iliyopakuliwa katika bandari ya Dar es Salaam kutoka meli iliyopakia shehena hiyo kwenye bandari ya Oktyabrsk, Ukraine. Katika ripoti yao ya mwaka 2006 ikitekeleza azimio la 1616 (2005) jopo la wataalamu lilielezea jinsi usafiri wa moja kwa moja wa anga toka Mwanza, Tanzania kwenda Doko huko DRC ulikuwa ni kinyume cha sheria za anga za DRC kwani uwanja wa Doko si wa forodha.

Katika ripoti yao ya nyuma jopo lilionyesha jinsi shirika la ndege la Butembo lilivyokuwa likihusika na waasi kusafirisha silaha na dhahabu yao. Ndege ya shirika hilo hilo iliruka toka uwanja wetu wa Mwanza kwenda Doko!
Naweza kutoa mifano mingine na nje ya ripoti za Umoja wa Mataifa. Ninachosema ni kuwa kusema kuwa ripoti ya sasa ni uongo na kuwa ni kuchafua jina la nchi haitoshi. Serikali ya Tanzani inahitaji kufanya zaidi ya kukanusha na kutaka kuombwa msamaha.

Serikali ni lazima itulidhishe sisi wananchi wake kwa kuwa wazi kuhusu mambo mbalimbali yakiwamo:
Uhusiano wa kampuni ya Meremeta na kikundi cha mamluki wa kivita wa Executive Outcomes kuanzia mwaka 1997 kwani ni mamluki hao hao ndio waliompa ulinzi Laurent Kabila ambaye alikuwa akiishi Tanzania alipoanza harakati za kuanzisha uasi Mashariki ya Congo.

Ni kwa kiasi gani Meremeta ilinunua dhahabu toka kwa wauazaji wa Congo kule Kigoma na kama fedha za Meremeta hazikuenda kufadhili vita ya Wacongo. Je, hili ndilo linamfanya Waziri Mkuu aogope kuigusa Meremeta na wabunge wetu wote kwa woga kushindwa kuionyoshea kidole?

Ni kwanini hadi sasa wahusika wa mtandao wa silaha haramu za DRC bado wanaishi wakiwa watu huru katika ardhi ya yetu; watu ambao wanajulikana kwa muda mrefu na sifa zao zimetangaa? Je, si kwa baraka za Serikali watu hao wanaendesha biashara zao bila woga?

Ni hatua gani zimechukuliwa kuhakikisha kuwa ndege zote zinazoruka toka Mwanza kwenda DRC zimekaguliwa vilivyo na yeyote yenye silaha nje ya silaha za Serikali ya DRC au zisizovunja vikwazo vya kijeshi imezuiliwa?

Na yapo maswali mengine mengi ambayo kwa sasa tunayaweka kiporo tukiamini kuwa Serikali haitakurupuka na kudai na sisi tunataka “kulichafua jina la Tanzania”. Kama wananchi uzalendo wetu uko kwa Taifa si kwa Serikali iliyoko madarakani. Serikali iliyoko madarakani kama zilivyo serikali nyingine inaweza kubadilishwa na wananchi pale ambapo haikidhi mahitaji yao au pale ambapo inafanya mambo kinyume na yale ambayo yana maslahi kwa wananchi hao.

Tunaamini badala ya kututaka tuonyeshe uzalendo wa uongo wa kutetea nchi wakati wabovu wetu wanajulikana ni kutokutendea haki. Kujipanga mstari na kuanza kubeza kazi ya kitaalamu kwa sababu inatusuta ni kutokuwa wa kweli kwa akili zetu. Njia pekee ya kutufanya wananchi tuamini Serikali inasema kweli ni kwa Serikali kuwa wakweli. Kusema “haihusiki” haitoshi. Kudai kuwa “mawasiliano ya simu yanaweza kuwa juu ya mambo mengine si lazima iwe silaha” ni kutufanya sote hamnazo.

Na wananiudhi wananchi ambao wanarembua macho wanaposikia “Serikali imesema” na kama watoto wanakumbatia ukweli kana kwamba Serikali zina historia ya kusema ukweli mbele ya wananchi wake! Kama hawaamini wamuulize George Bush na kina Tony Blair. Kwa wale wanaofikiri kuwa wanasiasa wa Tanzania ni tofauti na wanasiasa wengine duniani waendelee kufikiri hivyo hivyo kwa maangamizi yao wenyewe.
 
Kupitia kwa Balozi wa kudumu kule U.N. Augustine Mahiga au ijisafishe kwa kona ipi?
Naomba wadau itakapotoka ripoti ya Tanzania kujibu ile ya hiyo team, mtuwekee kwenye JF.
Ya ile Team of Experts, tunayo, kama mlivyoiweka.
Sie kina SUMAKU,tunanasa na kutafakari, msisahau kuna kupakana matope katika ngazi ya Kimataifa pia! Tutafutieni jibu ambalo m-yetu Mahiga alisema kupitia TBC One.
 
Kupitia kwa Balozi wa kudumu kule U.N. Augustine Mahiga au ijisafishe kwa kona ipi?
Naomba wadau itakapotoka ripoti ya Tanzania kujibu ile ya hiyo team, mtuwekee kwenye JF.
Ya ile Team of Experts, tunayo, kama mlivyoiweka.
Sie kina SUMAKU,tunanasa na kutafakari, msisahau kuna kupakana matope katika ngazi ya Kimataifa pia! Tutafutieni jibu ambalo m-yetu Mahiga alisema kupitia TBC One.

ripoti ya Tanzania ni ripoti ya malalamiko na maelezo jinsi gani hawakuhusishwa bla bla bla..
 
Back
Top Bottom