Thomas Hamilton na mauaji ya kutisha ya watoto wasio na hatia…!

Mtambuzi

Platinum Member
Oct 29, 2008
8,810
15,398
hamilton_001.jpg


006.jpg


008.jpg

Thomas Hamilton

015.jpg

Nyumba aliyokuwa akiishi Thomas hamilton

dunblane_class_photo.jpg

watoto walioshambuliwa na baadhi yao kuuawa

012.jpg


101.jpg


022.jpg


Ilikuwa ni majira ya saa 3:00 asubuhi siku ya Jumatano ya Machi 13, 1996, Thomas Hamilton aliyekuwa na umri wa miaka 43 wakati huo, alionekana na akitoka katika nyumba chakavu aliyokuwa akiishi katika mji wa Stirling nchini Scotland.

Wakati anaingia katika gari lake alimpungia mkono jirani yake Kathleen Kerr aliyekuwa na miaka 77. Hamilton alionekana ni mwenye furaha na uso wake ulipambwa na tabasamu wakati wote alipokuwa akielekea katika gari lake. Lakini kumbe jirani yake huyo hakujua kwamba Hamilton alikuwa ameficha bastola mbili aina ya Magnum Revolvers katika koti lake refu alilokuwa amelivaa.Nusu saa baadae Hamilton alisimamisha gari lake katika shule moja ya msingi iliyoko katika eneo la Dunblane lililopo takriban kilomita 24 kutoka katika mji wa Stirling.

Alishuka kutoka katika gari lake na kutembea kuelekea katika mlango mkuu wa kuingilia katika shule hiyo huku akiwa ameichomoa bastola moja kutoka katika koti lake na kuishika mkononi barabara tayari kwa kushambulia. Hamilton alianza kuwashambulia watoto waliokuwa wakicheza katika eneo hilo la shule kwa kuwafyatulia risasi. Baadae alianza kushambulia madarasa yaliyokuwa na wanafunzi kwa kufyatua risasi kupitia katika madirisha.

Baada ya shambulio hilo, Hamilton alipitia katika mlango wa mbele na kuipita ofisi ya waalimu huku akiendelea kufyatua risasi hovyo akielekea katika chumba cha kufanyia mazoezi cha shule hiyo.

Wakati akielekea katika chumba hicho cha mazoezi njiani alikutana na mwalimu Mary Blake ambapo alimfyatulia risasi. Ni bahati nzuri madaktari walifanikiwa kuokoa maisha yake, kwani risasi ilikwama nyuma ya sikio. Shambulio hilo liliwatisha sana wanafunzi na wote walikuwa katika hali ya taharuki.

Laura Bryce mwanafunzi aliyekuwa na miaka 12 baadae aliwaeleza Polisi jinsi yeye na mwanafunzi wenzie walivyolala sakafuni nyuma ya madawati yao kwa ajili ya kujikinga dhidi ya risasi za moto kutoka kwa muuaji huyo. "Risasi zilifyatuliwa kupitia dirishani na mlangoni na miongoni mwa risasi hizo, moja ilielekea walipo marafiki zangu ambao nao walikuwa wamejikinga nyuma ya madawati yao. Nilijua wote tutakufa na hatuhaonana tena." Alisema Laura.

Muda mfupi baadae Hamilton aliibukia katika chumba cha mazoezi ambapo kulikuwa na wanafunzi 29 wanaosoma darala la kwanza waliokuwa na umri kati ya miaka mitano na sita ambao walikuwa wakifundishwa namna ya kufanya mazoezi ya viungo na mwalimu wao Eileen Harrild na Gwenne Mayor.

Eileen Harrild ndiye aliyekuwa mhanga wa kwanza kushambuliwa na muuaji huyo ambapo alishambuliwa kwa risasi ya kifuani, lakini madakatari walifanikiwa kuokoa maisha yake.

Baadae Hamilton alisimama katika kona ya chumba hicho cha mazoezi na kuendelea kufyatua risasi, ambapo mwalimu wa darasa hilo Gwenne Mayor alipojaribu kuwakinga watoto wasidhuriwe na risasi hizo ziliishia mwilini mwake na kumuua pale pale.

Hamilton aliendelea kuzunguka katika chumba hicho cha mazoezi huku akiwafyatulia risasi wanafunzi waliokuwa wakipiga kelele kuomba msaada ambapo alikuwa akifatua risasi mara tatu kwa kila mwanafunzi aliyekuwa akipiga kelele kuomba msaada.

Baadae alikaa kwenye kona ya chumba hicho na kujifyatulia risasi kichwani na kufa hapo hapo. Na huo ukawa ndio mwisho wa muuaji huyo.

Kwa muda usiozidi dakika tano Thomas Hamilton alikuwa ameua wanafunzi 16 na mwalimu mmoja. Pia alikuwa amejeruhi wanafunzi 12, wengi wao wakiwa wamejeruhiwa vibaya. Ni mwanafunzi mmoja tu katika chumba cha mazoezi ndiye aliyekutwa bila jeraha. Polisi walimkuta akiwa amefunikwa na miili ya wanafunzi wenzie waliouawa, alikuwa amelowa damu mwili mzima. Alikuwa akitweta na alionekana kutaharuki.

Waalimu na wafanyakazi wa shule hiyo walifika katika eneo la tukio katika chumba hicho cha mazoezi muda mfupi baada ya Hamilton kujipiga risasi. Hali waliyokutana nayo ilikuwa haielezeki na ya kutisha. Mwalimu mkuu wa shule hiyo Ron Taylor alikuwa ndiye wa kwanza kufika katika chumba hicho.

"Hali tuliyokutana nayo, kwa kweli haielezeki." Alisema. "Picha niliyokutana nayo kamwe haitotoka katika akili yangu. Tulifanya kila linalowezekana kuzuia mauaji haya. Wote walionusurika katika mauaji haya, wako katika hali ya taharuki isiyo kifani."

Muda mfupi baadae mhuduma wa kitabibu wa dharura (paramedic) John McEwan alifika katika chumba hicho cha mazoezi. Hali aliyokutana nayo katika chumba hicho ilimtisha sana kwani tangu aanze kazi hiyo hakuwahi kukutana na hali kama hiyo. "Miili ya watoto wale ilikuwa imetapakaa sakafuni ikiwa imelowa damu." Alinukuliwa aisema. "Mtoto mmoja alikuwa amekaa sakafuni huku akiwa ameegemea ukuta na alionekana kushikwa na taharuki huku akinionyesha jeraha la risasi mkononi mwake. Aliniliangalia kwa jicho la udadisi kama vile alikuwa anataka ufafanuzi kutoka kwangu kuhusiana na mauaji yale. Watoto wengine walikuwa wamekaa sakafuni bado wakiwa katika taharuki, miili yao ilikuwa ikivuja damu, walishindwa hata kuongea wala kulia. Ninaweza kuelezea kile nilichokiona kama jehanam."

Dunblane ni mji mdogo na taarifa za mauaji hayo zilisambaa kama moto wa mwituni. Kulikuwa hakuna familia hata moja ambayo haikuwa na mtoto, mtoto wa ndugu wa karibu au mtoto wa familia rafiki aliyekuwa akisoma katika shule hiyo. Nyumba na ofisi zilitelekezwa na watu wote walikimbilia katika shule hiyo huku wakiwa na kihoro kuangalia kama watoto au jamaa zao wamesalimika katika mauaji yale ya kutisha. Mpaka wanafika katika eneo hilo, waliwakuta tayari Polisi wamefunga geti la shule hiyo huku eneo lote likiwa limezingirwa na Polisi hao wakilinda usalama. Magari ya kubebea wagonjwa ndiyo yaliruhusiwa kuingia katika shule hiyo.

Hata hivyo baadae waliruhusiwa kuingia lakini walielekezwa kusimama katika eneo maalum lakini si ndani ya shule hiyo. Hali katika eneo hilo la shule ilikuwa ni ya kutisha na watu wote waliofika shuleni hapo walikuwa wametaharuki. Wazazi wa wanafunzi wa darasa la pili mpaka la sita waliruhusiwa kuondoka na watoto wao. Mpaka kufikia muda huo, ilikuwa imejulikana wazi kwamba watoto walioathirika na shambulio hilo ni wa darasa la kwanza ambalo lilikuwa na wanafunzi wapatao 100 waliokuwa na umri wa miaka mitano na sita na walikuwa wamegawanywa katika madarasa matatu tofauti.

Polisi na washauri kutoka katika kitengo cha ushauri wa kijamii katika mji huo wa Stirling walikuwa na kazi kubwa ya kuwatuliza wazazi waliokuwa katika hali ya taharuki na hofu kubwa.

"Muda ni kama vile ulikuwa hauendi." Alisema mama mmoja ambaye alimsindikiza jirani yake aliyekuwa na mwafunzi wa darasa la kwanza katika shule hiyo. "Tulisimama huku tukipigwa na baridi kali kwa masaa mawili. Hatimaye aliitwa na kujulishwa kwamba mwanaye amenusurika katika shambulio hilo na hakuwa amejeruhiwa. Polisi walichukua nafasi hiyo kuomba radhi kwa kuchelewa kwao kutoa taarifa kwa wazazi wa watoto walionusurika katika shambulio hilo. Walifafanua kwamba sababu ya kuchelewa huko ni kutokana na kuwajulisha wazazi wa watoto waliojeruhiwa na wale waliopoteza maisha, ndio sababu ilibidi tusubiri."

Mama mwingine aliyetajwa kwa jina la Beverly Birnie bintiye aliyekuwa na umri wa miaka mitano alinusurika katika shambulio hilo, lakini alijeruhiwa na hivyo kulazimika kukimbizwa katika hosptali ya Stirling Royal Infirmary kwa upasuaji wa haraka ili kunusuru maisha yake. "Niliposikia kwamba ni watoto wa darasa alilokuwa akisoma mwanangu kuwa ndio walioshambuliwa mwili wote ulikufa ganzi, lakini sasa nawafikiria wazazi ambao hawakuwa na bahati kama sisi." Alisema mama huyo.

Kitengo cha huduma ya dharura cha Hospitali ya Stirling Royal Infirmary kilikuwa katika wakati mgumu kukabiliana na hali hiyo ya kutibu majeruhi. Mmoja wa madaktari wa hospitali hiyo aliyekuwa zamu Kathryn Morton aliyekuwa akimhudumia binti mmoja majeruhi wa shambulio hilo, aliitwa na mmoja wa wafanyakazi katika hospitali hiyo na kufahamishwa kwamba binti yake aitwaye Emily ameuawa katika shambulio hilo na alikuwa amehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha hospitali hiyo hivyo kumlazimu kuungana na wazazi wengine waliokusanyika nje ya chumba hicho cha maiti ili kutambua miili ya watoto wao. Jim Benson mhudumu wa kiroho katika hospitali hiyo alikuwa mstari wa mbele kuwafariji wazazi waliopoteza watoto wao. "Wazazi hawakupata taabu kutambua miili ya watoto wao. Wote nyuso zao zilionekana zikiwa kama vile wamelala kwa amani."

Taarifa za mauaji hayo zilisambaa nchi nzima. Salaamu za rambirambi zilianza kumiminika kutokea kila kona zikiwemo zilezilizotoka ikulu.

Siku mbili baada ya tukio hilo la mauaji aliyekuwa waziri mkuu wa Uingereza wa wakati huo John Major aliitembelea shule hiyo. Alisimama katika chumba cha mazoezi ambacho ndipo walipouawa wanafunzi wengi ambapo alitokwa na machozi.

Swali lililokuwa likiwaumiza vichwa wadadisi wa mambo ni kutaka kujua, huyu Thomas Hamilton ni nani hasa, na kitu gani kilimsukuma hadi kufikia kufanya mauaji yale ya kutisha. Kidogo kidogo picha halisi ya muuaji ilianza kufahamika.Hamilton alitokea katika familia iliyovunjika na alilelewa na kukuzwa na bibi yake. Mpaka alipofikia umri wa ubarubaru alikuwa anaamini kwamba mama yake aliyemzaa aitwaye Agnes alikuwa ni dada yake mkubwa.

Baba yake aitwae Thomas Watt ambaye wakati huo alikuwa amaestaafu, alikuwa ni dereva wa mabasi na hakuwahi kumuona mwanaye huyo tangu alipomuona kwa mara ya mwisho akiwa na umri wa miezi 18 na hakuonekana kutaka kuwa karibu na mwanaye hadi alipokuja kusikia taarifa za mauaji yaliyofanywa na mwanaye huyo. "siamini kabisa kama ni mimi niliyemleta huyu muuaji hapa duniani" alisema mzee Thomas Watt baada ya kupata taarifa za mauaji hayo yaliyofanywa na mwanaye Hamilton.

Historia yake inaonyesha kwamba baada ya kuacha shule kutokana na kuonekana kuwa dhaifu katika masomo, Thomas Hamilton alijiunga katika kituo cha skauti cha vijana kama kiongozi. Wengi waliomjua walimuona kama mtu asiyemudu kazi hiyo, lakini kibaya zaidi alikuwa na tabia zinazoashiria kunajisi watoto (Pedophile).

Hata hivyo alifukuzwa katika nafasi hiyo kama kiongozi wa kituo cha skauti cha Dunblane hapo mnamo mwaka 1974 kwa kile kilicholezwa kwamba alikuwa na tabia zisizofaa.

Hatua hiyo haikumkatisha tamaa kwani aliendelea kutafuta kazi katika vituo vingine vya vijana lakini mara nyingi aliishia kufukuzwa kutokana na wazazi wa watoto waliokuwa katika vituo hivyo kulalamika kwamba alikuwa akiwafanyia watoto wao vitendo visivyo vya kistaarabu. Jambo la kushangaza ni kwamba, pamoja na tuhuma hizo lakini hakuwahi kushitakiwa kwa makosa ya kujaribu kunajisi watoto, ingawa dalili zote za kuwa na tabia za kuwafanyia watoto vitendo vya mapenzi zilikuwa zinajulikana dhahiri.

Gerry Fitzpatrick, ambaye wakati huo alikuwa na miaka 27 alidai kushuhudia vitendo visivyofaa walivyokuwa wakifanyiwa na Thomas Hamilton wakati fulani wakati alipokuwa akihudhuria katika moja ya vituo vya vijana miaka ya nyuma. "Alikuwa ni mtu wa ajabu kwa kweli…." Alisema kijana huyo. "Alikuwa anatutaka tuvue mashati yetu muda wote na na alikuwa anapenda sana kuangalia miili yetu….. Inaonyesha alikuwa na matatizo yasiyo ya kawaida kichwani mwake." Alimalizia kusema kijana huyo…….

Mmoja wa majirani zake aliyekuwa akiishi naye katika eneo hilo la Stirling aitwae Grace Ogivie alikumbuka siku moja Thomas Hamilton alimwalika katika nyumba aliyokuwa anaishi hapo mnamo mwaka 1994, ambapo alimkuta akiangalia mikanda ya video ya vijana wa kiume wa umri wa kati ya miaka 20 hadi 30 ambao walikuwa wamejipanga mfano wa gwaride kando ya bwawa la kuogelea huku wakiwa wamevaa c.h.u.p.i za kuogelea. "jambo hilo lilinishangaza sana kwani nilijua wazi kwamba hivyo siyo vitendo vinavyoweza kufanywa na mtu mstaarabu." Alisema binti huyo.

Watu wa mamlaka zinazohusika na upelelezi wa tukio hilo walikuwa na wakati mgumu kujua sababu hasa ya Hamilton kutekeleza mauaji hayo. Anne Dixon, aliyekuwa akifanya kazi katika kitengo cha ushauri katika mji huo wa Dunblane alieleza jinsi wakati fulani Hamilton alivyopewa kibali cha kuandaa matamasha ya burudani katika shule moja, lakini kibali hicho kilifutwa kwa sababu alam ya shule hiyo iliwashwa na mtu asiyejulikana. "Tulijua kulikuwa na tatizo, lakini hata tulipoenda hakuna aliyejitokeza kueleza sababu ya kuwashwa kwa alam hiyo."

Kila alipojaribu kuomba kibali cha kufanya tamasha katika vituo vya vijana maombi yake aidha yalikataliwa au alikuwa anapewa kibali lakini kikafutwa katika hatua za mwisho.

Hamilton alionekana kukerwa na hali hiyo na kuanzia hapo akajenga hisia kwamba kuna njama zinafanywa kitaifa dhidi yake katika shughuli zake. Kutokana na hisia hizo, Hamilton aliandika barua kadhaa kwa wabunge wa bunge la nchi hiyo, wajumbe wa baraza la ushauri wakiwemo wakuu wa taasisi za kijamii akilalamika kwamba amekuwa ni mhanga wa vitendo vya kutengwa na kunyanyaswa na jamii.

Siku tano kabla ya kutekeleza mauaji hayo Hamilton alikwenda mbali zaidi kwa kuandika barua kwa Malkia wa Uingereza (Scotland iko chini ya Malkia wa Uingereza).

Katika barua yake alimlalamikia Malkia kwamba, kuna kampeni ambayo imenzishwa dhidi yake ambayo imemfikisha mahali ambapo amejikuta akiwa ameathirika kisaikolojia. "Vitendo ninavyofanyiwa na jamii vimenifanya niwe na msongo wa mawazo, na kushindwa kusimama mwenyewe na nimepoteza biashara nyingi na hivyo nimeshindwa kuendesha maisha yangu." Aliandika katika barua hiyo…..

"Siwezi hata kutembea mtaani kwa kuhofia mizaha na kunyanyapaliwa na jamii iliyonizunguka." Aliongeza.

Ni kweli kwamba, Hamilton alikuwa na tabia ya vitendo vinavyoashiria kunajisi watoto, lakini tabia hiyo, haitoshi kutoa jibu la sababu ya yeye kuuwa watoto 16 ambao hata hawakuwa na uwezo wa kujitetea.

Hata hivyo kulikuwa na dalili za kuujua ukweli. Hamilton kama ilivyo kwa wauaji wengi, alikuwa ametengwa na jamii. Kushindwa kwake kuchagua taaluma na kutomudu kujenga urafiki kulimfanya kuwa mpweke. Hakuna aliyemjua, wala kujali uwepo wake. Hakuna aliyeonekana kumjali kama binadamu anayestahili kutambuliwa.
 
Haya ni Ijumaa nyingine tena kama kawaida nimewaletea tukio hili la kusikitisha lililowahi kutokea huko Uskotish.
Naamini kuna kitu mtajifunza katika mkasa huu.
 
HALAFU MTAMBUZI MIMI KWAKWELI SIELEWI,KWANINI HAWA WENZETU WADHUNGU KILA ANAYEKUWA NA HIZI KESI ZA KUUA AU MASERIAL KILLERS WOTE ukitrace back wana tatizo kwenye makuzi yao?ina maana Afrika hakuna watu wenye kukua katika mazingira hayo?nielewesheni wadau!
 
HALAFU MTAMBUZI MIMI KWAKWELI SIELEWI,KWANINI HAWA WENZETU WADHUNGU KILA ANAYEKUWA NA HIZI KESI ZA KUUA AU MASERIAL KILLERS WOTE ukitrace back wana tatizo kwenye makuzi yao?ina maana Afrika hakuna watu wenye kukua katika mazingira hayo?nielewesheni wadau!
snowhite watuhumiwa wa mauaji walioathiriwa na malezi wapo wengi sana tatizo mfumo wetu wa sheria hauangalii back ground ya mtuhumiwa ili ku-justfy makosa ya mtuhumiwa.......... Lakini pia coverage ya matukio ya mauaji katika vyombo vyetu vya habari iko chini sana na pia hakuna uchambuzi wa kitaalamu ambao uko makini utakaoiwezesha jamii kujifunza kupitia tukio la mauaji lililotokea hususan kwa upande wa malezi.

Magazeti mengi huzungumzia habari za mauaji katika mfumo wa kupasha habari tu na ni mara chache sana kukuta uchambuzi yakinifu ulioandikwa kitaalamu kuzungumzia sababu zilizopelekea mtuhumiwa kufika hapo.....
TV zetu nazo zimeshindwa kuandaa vipindi vinavyokutanisha wataalamu wenye weledi wa masuala ya saikolojia kujadili matukio ya kutisha yanayojitokeza katika jamii yetu. Mnyororo ni mrefu sana kwa sababu hata tukilaumu mwishowe utaambiwa serikali ndiyo haijaweka kipaumbele.

Labda kupitia JF, tunaweza kuanzisha vuguvugu hilo la kuielimisha jamii kupitia matukio mbalimbali zikiwemo kesi za mauaji na matukio mengine ya ubakaji......... Naamini Great Thinkers wa humu JF wataliona hilo na kulifanyia kazi....
 
Last edited by a moderator:
PSYCHOLOGY,naamini ni katika masomo magumu kabisa kuwahi kuwepo duniani...huwezi kilinganisha na physics,neurology na mengineyo....

Yaan,sooo saaad!!!!

Thanks Mtambuzi
 
Yaani nimesisimka mwili, hv ndo upo hom unapigiwa cm kuna mauaji shuleni kwa mwanao, c utatoka bila kuvaa, na mwanangu anaposoma geti halifungwi, mlinzi yupo nje, we ukisema ni mzazi wa mtoto unapita tu, sasa c hata muuaji anapita, mpaka naogopa kumpeleka dogo shule, thanx mtambuzi
 
Leo sina comments za ziada Mtambuzi kuhusiana na hizi kesi, zaidi ya kukandamiza kitufe cha LIKE! Uchambuzi na uwakilishaji wako wa hizi kesi ni wa kiwango cha juu sana .....
 
Last edited by a moderator:
malezi ni kia kitu kwa mtu yeyote...mara nyingi madhara ya malezi mabovu huwa yanakuja kuonekana ukubwani..hii ni changamoto kwa wazazi/walezi wote....pamoja sana mkuu Mtambuzi
 
Last edited by a moderator:
So sad, kwa kweli imesikitisha sana
Si angeenda huko bungeni akawashambulie risasi.
Masikini malaika wa mungu!

Thanks Gustavo.
 
Huwa inaogopesha sana binadamu akifikia state ya kusema 'sasa basi, liwalo na liwe'. Really huwa anakuwa insane kabisa na anaweza akafanya jambo ambalo jamii lazima ijutie kuwa naye duniani na kwamba kama wangejua atakuwa nane, wangeitoa mimba yake tumboni mwa mama yake.
Huyu bwana alichoka na maisha kiasi kwamba akaishia kusema kabla sijaondoka lazima niache somo hapa.
 
Mkuu ahsante sana makala haya. Lakini tunajifunza kitu hapa ya kwamba malezi mabaya ndiyo yanayoleta uhasama ktk jamii nyingi. pia wazungu hawa hawajifunzi kitu matokeo yake kila kukicha hutunga sheria mpya kwa ajili yakutetea watoto na matokeo yake watoto wanakuwa watundu na pia ndoa huvunjika kutokana na sheria zinazoanzishwa kila kukicha matokeo yake watoto hulelewa na upande moja wa mzazi hasa wamama
 
Ahsante sana mkuu. Shida kubwa ni kwamba binadamu ni wagumu wa kujifunza lakini wepesi wa kusahau.
 
Back
Top Bottom