Tanzania nakupenda sana

Dotto C. Rangimoto

JF-Expert Member
Nov 22, 2012
1,985
1,282
TANZANIA NAKUPENDA SANA.

Mama Tanzania, nakupenda sana,
Nakupigania, usiku mtana,
Zitaangamia, husuda fitina,
Za walo pania, watu kuchinjana
Nakupenda sana, wangu Tanzania.

Siwati kulia, tunapo zozana,
Huomba Jalia, tupate patana,
Tusiwape ndia, wafanya hiyana,
Wapate kimbia, wasirudi tena.
Nakupenda sana, wangu Tanzania.

Siasa ni njia, ya kuongozana,
Katu si jambia, roho kutoana,
Yataka sikia, kushauriana,
Mambo hutimia, kwa kusikizana.
Nakupenda sana, wangu Tanzania.

Ninajivunia, kuwa wako mwana,
Katika Dunia, hata kwa Rabana,
Mi husimulia, Ulaya na China,
Mola kajalia, vitu vingi sana.
Nakupenda sana, wangu Tanzania.

Dotto Rangimoto Chamchua (Njano5)
0622845394/0784845394 Morogoro.
 

Attachments

  • TANZANIA..jpg
    TANZANIA..jpg
    7.1 KB · Views: 61

Similar Discussions

Back
Top Bottom