Tanzania daima wamfagilia Zitto kabwe

Mkwawa

JF-Expert Member
Jun 8, 2011
1,334
1,464
na Bakari Kimwanga


amka2.gif

SHEREHE za kuzaliwa upya kwa taifa la Sudan Kusini zilizofanyika juzi mjini Juba, ziliibua hisia mpya katika siasa za Tanzania baada ya Rais Jakaya Kikwete na Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Zitto Kabwe, kuandamana kuhudhuria tukio hilo la kihistoria.
Ziara hiyo ilifanyika baada ya Rais Kikwete kumaliza safari ya kikazi mkoani Kigoma wiki iliyopita, ambako alizindua miradi kadhaa, ikiwamo ya Barabara ya Mwandiga – Manyovu inayopita katika Jimbo la Kigoma Kaskazini linalowakilishwa na Zitto.
Wakiwa Sudan, Kikwete na Zitto walipata fursa ya kusalimiana na kuzungumza na viongozi mbalimbali waliohudhuria sherehe hizo, akiwamo Rais wa nchi hiyo, Salva Kiir.
Safari hiyo ya Zitto na Kikwete imezua maswali miongoni mwa wadadisi wa siasa wanaofuatilia mwenendo wa rais anayekaribia kuondoka madarakani na mwanasiasa kijana katika harakati za mageuzi nchini. Ingawa inajulikana kuwa Kikwete na Zitto wamekuwa na uhusiano mzuri kikazi, licha ya kupingana kiitikadi, ziara yao ya juzi iliongeza minong’ono, hasa baada ya Zitto kuvujisha sehemu ya mazungumzo kati ya rais na yeye (Zitto) na Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila, walipokuwa kwenye hafla ya uzinduzi wa barabara mkoani Kigoma.

Kwa mujibu taarifa zilizobandikwa na Zitto katika ukurasa wake wa facebook siku chache zilizopita, Rais Kikwete aliwanong’oneza yeye na Kafulila kwamba asingependa baada ya kustaafu kwake nchi iongozwe na rais ‘mzee’ kama yeye.
Rais Kikwete, ambaye aliingia madarakani kwa kampeni ya “ujana” huku akiwa na umri wa miaka 55 mwaka 2005, aliwaambia kina Zitto:
“Msikubali atakayenirithi awe wa rika langu, sasa kizazi chenu kijiandae.”
Wachambuzi wa masuala ya kisiasa wanasema kauli hiyo, kama ilitolewa na Rais Kikwete kweli, ililenga kuhamisha mjadala wa kisiasa kuhusu mrithi wa Kikwete nje na ndani ya CCM.
Inafahamika kwamba wanasiasa “wakali” ambao Rais Kikwete anawaogopa, na ambao wameonyesha nia ya kuutaka urais baada yake, ni watu wa makamo kama yeye.
Vile vile, wananchi wanapokuwa wanajadili mustakabali wa nchi, suala la umri, dini, jinsia na eneo analotoka mtu, havijawahi kuwa vigezo vinavyotumika kumuunga mkono mgombea.
Lakini kwa taifa lililoshuhudia siasa zenye mrengo wa kijinsia katika kumpata Spika wa Bunge, na kauli za udini kwenye kampeni mara baada ya Uchaguzi Mkuu, haliwezi kupuuza kauli hizi za kigezo cha umri.
Hata hivyo, baadhi ya wachambuzi wamekuwa wakisisitiza kuwa ujana au uzee si hoja. Wapo pia wanaosema kwa msisitizo mkubwa kwamba mgombea yeyote wa CCM atakayebebwa na Rais Kikwete ataanguka. Wanatoa sababu kadhaa.

Kwanza, wanasema nguvu yake ndani ya mfumo inalegalega kiasi cha kumnyima uwezo wa kushinikiza wanachama wakubaliane naye katika chaguo atakalowaletea.
Na kwa msingi wa makundi ndani ya CCM, kuna watu wamejipanga kwamba yeyote atakayeonekana kubebwa na JK lazima “apigwe chini.”
Pili, wachunguzi wanasema historia inaonyesha kuwa hakuna aliyebebwa na rais anayeondoka madarakani, akashinda. Wanatoa mifano ya jinsi Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere mwaka 1985, alivyomtaka Dk. Salim Ahmed Salim, lakini akazidiwa kete na wajumbe waliomtaka mzee Ali Hassan Mwinyi. Hata mwaka 1995 alimtaka Dk. Salim, ikashindikana baada ya Dk. Salim mwenyewe kukataa kwa kutazama upepo wa kisiasa wa wakati huo.

Wanasema hata Rais Mwinyi alipokuwa anaondoka, chaguo lake lilikuwa ama Cleopa Msuya au Kikwete. Alishindwa kupitisha mmoja wao.
Hata Rais Benjamin Mkapa alikuwa na mtu wake, lakini alilazimika kumuunga mkono Kikwete baada ya kushindwa na wimbi la mtandao ndani ya chama.
Ingawa “uhusiano” kati ya Kikwete na Zitto unajulikana kwa siku nyingi, na ingawa Zitto mwenyewe hajatamka kwamba anawania urais, kauli hizi za Kikwete na Zitto zilikuwa na ujumbe kwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kinachomsumbua Rais Kikwete.
Wengine wanadai anataka kumtumia Zitto kugombanisha wanaotaka urais ndani ya chama hicho. Wapo wanaodai kwamba hata Zitto mwenyewe atakuwa hajafikisha umri wa kugombea urais mwaka 2015, kwani atakuwa na miaka 39; na kwamba hata kama katiba itakuwa imebadilishwa, umri wa mgombea urais hautarajiwi kushushwa kuwa chini ya miaka 40 inayoruhusiwa sasa.
Zaidi ya hayo, wengine wanahoji, “Kikwete anataka kurithisha urais kwa chama gani? Au ameridhika sasa kwamba CCM haiwezi kutawala tena?”
Hata hivyo, wengine wamedai uhusiano wa Kikwete na Zitto ni mbinu ya wanasiasa hao kujijenga binafsi, kwani Kikwete anadhani akionekana na Zitto hadharani itamwongezea kukubalika na mashabiki wa Zitto na upinzani, ambao ni wengi anaowakosa.
Wanaotetea hoja hiyo wanatoa mfano wa tukio la juzi akiwa mkoani Kigoma, ambapo rais alinong’onezwa kuwa Zitto alikuwa miongoni mwa wananchi waliokuwa mkutanoni hapo, akamwita kwa sauti aje jukwaani, na baada ya mkutano akawa anatembea na kuteta naye huku umati unawatazama.
Wanasema Zitto naye anatumia nafasi ya Kikwete kujihalalisha kwa wana CCM na wananchi wengine kujinasibu kama mwanasiasa anayeweza kufanya kazi bila kufungwa na tofauti za kiitikadi.
Akiwa Sudan Kusini juzi, Rais Kikwete alimtambulisha Zitto kwa Rais mpya wa nchini hiyo, Salva Kiir Mayardit, hali iliyosisimua ujumbe wa Tanzania.
Hivi karibuni wakiwa mkoani Kigoma wakati wa ziara ya Rais Kikwete, Zitto alitoa hotuba fupi ya kumsifia Rais Kikwete, ambayo ilipokewa kwa hisia tofauti.
Hata hivyo, Zitto ndiye anaonekana kuumizwa na uhusiano huu, maana anawakera baadhi ya wanachama wenzake, na enzi za Rais Kikwete kupendwa na kushangiliwa na watu zimepita; kwani hata wana CCM wenyewe wanadai kwamba Kikwete si kete murua ya kisiasa, kwa sababu umaarufu wake umeshuka sana, hasa baada ya serikali yake kushindwa kutekeleza majukumu ya msingi na kuibua hisia hasi kutoka kwa wananchi.
Gazeti hili lilifanya jitihada za kumpata Zitto ili aeleze jinsi alivyoandaa safari hiyo na Kikwete, na alichozungumza na Rais Kiir wa Sudan. Hakupatikana. Lakini baadhi ya viongozi wa chama chake walikiri kufahamu ziara yake hiyo ya Juba, ingawa hawakutaka kusema iliandaliwaje.
Zitto ni mmoja wa wanasiasa vijana machachari katika CHADEMA. Ni Waziri Kivuli wa Fedha na Uchumi, ambaye kwa kushirikiana na wabunge wenzake wa CHADEMA, ameichachafya na kuishinda serikali katika suala la kufuta posho za vikao kwa watumishi wa serikali, wakiwamo wabunge.
Akiwa nchi Sudan Kusini juzi, Zitto alituma ujumbe kupitia mtandao wa Facebook, akasema kuzaliwa kwa taifa hilo jipya kumeamsha matumaini ya wananchi kwa serikali yao.

Source: Gazeti la Tanzania Daima
 
Naona kama kuna tofauti kati ya Title ya thread na contents, au pengine sijaelewa lengo la mleta thread.
 
yeah kuna tofauti kati nya heading na contents. cjui maana ya mleta thread.ila hakuna mlingano
 
kama taarifa hii ndiyo iliyomfanya zitto aseme hajengwi na mtu anajijenga mwenyewe basi atakuwa na matatizo, au hii ni habari mpya baada ya ile ya mwanzo? sioni tatizo wala makosa ya tz daima
 
kama taarifa hii ndiyo iliyomfanya zitto aseme hajengwi na mtu anajijenga mwenyewe basi atakuwa na matatizo, au hii ni habari mpya baada ya ile ya mwanzo? sioni tatizo wala makosa ya tz daima
Hizi ni habari 2 tofauti Mkuu.
 
kama taarifa hii ndiyo iliyomfanya zitto aseme hajengwi na mtu anajijenga mwenyewe basi atakuwa na matatizo, au hii ni habari mpya baada ya ile ya mwanzo? sioni tatizo wala makosa ya tz daima

Baada ya kusoma hii habari mara kadhaa nikishtuka sana kuwa nini kilimfanya Zitto kuhamaki. Najua wajumbe wanasema kichwa cha habari akilingani na habari. Ila ukipewa habari bila kichwa cha habari unatakiwa kukipa kichwa cha habari unachoona kinafaa. Mimi nimeona Tanzania Daima wamempamba Zitto. Ila kundi la Zitti na wafuasi wake waliona Tanzania Daima imemmaliza Zitto. Ila habari hii imeandikwa vizuri na Zitto alipewa credit za kumwaga. Nilichokugundua Zitto alitishwa na kicha cha habari ambacho kilitumika kuuza habari.
 
Back
Top Bottom