Josh Michael
JF-Expert Member
- Jun 12, 2009
- 2,523
- 77
- Siasa zaliumiza taifa, Zitto akumbukwa
HATIMAYE Shirika la Ugavi wa Umeme Tanzania (TANESCO) limetangaza mgawo wa umeme nchi nzima kutokana na upungufu wa maji kwenye vituo vya kuzalisha umeme vya Kihansi na Pangani.
Hatua hiyo ya TANESCO imekuja miezi michache tu baada ya Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo, Dk. Idris Rashid, kuonya kuwa taifa litaingia gizani iwapo mitambo ya Kampuni ya Dowans yenye uwezo wa kuzalisha megawati 100 haitanunuliwa.
TANESCO ilikuwa na mpango wa kununua mitambo ya Dowans ambayo ilirithi mkataba kutoka Kampuni ya kuzalisha umeme wa dharura ya Richmond iliyobainika kutokuwa na uwezo wa kuzalisha nishati hiyo.
Dhamira hiyo ya shirika hilo ilikumbana na upinzani mkali kutoka kwa wanasiasa mbalimbali, hususan Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini iliyo chini ya Mbunge wa Bumbuli, William Shellukindo, ambaye alisema kuinunua mitambo hiyo ni kukiuka sheria ya manunuzi ya umma pamoja na kukiuka maagizo ya Bunge.
Kutokana na upinzani huo, TANESCO ililazimika kuondoa mpango wake huo huku Dk. Idris akionya kuwa kuna kila dalili kuanzia Septemba mwaka huu taifa likakabiliwa na mgawo wa umeme kama ule wa mwaka 2006.
Taarifa iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari na Mkurugenzi wa TANESCO, Dk. Idris Rashid, imesema kumekuwapo na upungufu wa uzalishaji wa umeme kwenye gridi ya taifa, ambao kwa kiasi kikubwa umesababishwa na uhaba wa maji katika vituo vya Kihansi na Pangani, kutokana na ukame katika kipindi hiki cha kiangazi.
Sababu nyingine iliyotolewa na shirika hilo ni kuharibika kwa mtambo wa Songas UGT1 (20 MW), kuharibika kwa mtambo wa Kihansi (60 MW) na kuharibika kwa mtambo wa Hale (8 MW).
Dk. Rashid amesema athari za upungufu huo zimelisababishia shirika kufanya mgawo wa 65MW kwa maeneo mbalimbali kuanzia saa tatu asubuhi hadi saa tano usiku.
Aidha, amesema ili kukabiliana na tatizo hilo, TANESCO inajitahidi kukamilisha ujenzi wa mtambo mpya wa Tegeta 45 MW ili ikiwezekana uanze kazi mwezi ujao na kuharakisha matengenezo ya mtambo wa Songas unit 1 (20 MW) kabla ya mwisho wa mwezi huu.
Jitihada nyingine zinazofanywa na shirika hilo ni kuharakisha matengenezo ya mtambo wa Kihansi unit 1 (60 MW) ili yaweze kukamilika katikati ya mwezi Desemba mwaka huu.
Aidha, Dk. Rashid alisema katika kipindi hicho cha magwo wanatarajia mvua za vuli zitaanza kunyesha mwezi ujao, hali itakayosaidia kuboresha hali ya uzalishaji umeme kwa kutumia maji.
Aliongeza kuwa, pamoja na sababu hizo, TANESCO itaendelea kushirikiana na serikali kuanza maandalizi ya ununuzi wa mitambo mingine ya kuzalisha umeme ili kukidhi mahitaji ya umeme kwa mwaka ujao na siku za baadaye.
Hatua hii ya TANESCO kutangaza mgawo wa saa 12 itaathiri shughuli mbalimbali kwa wananchi pamoja na uchumi, ambao katika siku za hivi karibuni umekuwa katika mdororo.