Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,474
- 39,987
Hii imeingia sasa hivi kutoka "ndani"... Inadaiwa kuwa ni tamko ambalo Pinda anatarajiwa kutoa kesho au wakati wowote kama sakata hili la kauli yake litaendelea hasa baada ya baadhi ya Wabunge hata wa ndani ya CCM kutoridhika moja kwa moja na maelezo yake katika kipindi cha maswali na majibu leo huko Bungeni.
NB: Sijaweza kuthibitisha ukweli au usahihi wa taarifa hiyo. Muda ndio utasema.
Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wenzangu; maneno yaliyonukuliwa katika vyombo vya habari ni maneno niliyoyasema na yamenukuliwa kwa usahihi (pause).
Ni maneno ambayo nimeyatoa kutoka moyoni mwangu hasa na yamezingatia ukweli wa dhamira yangul. Baada ya kukutana na kuona adha ya mauaji ya kinyama yanayoendelea nchini nilitoa kauli ambayo ilisema kuwa wananchi wakiwakuta watu waliofanya vitendo vya mauaji ya albino basi wawaue watu hao papo hapo na hakuna haja ya mahakama.
Nasimama mbele yenu kwa heshima kubwa na taadhima na kukiri kuwa kauli hiyo niliitoa kimakosa, ni kauli iliyotolewa kwa pupa na ilitolewa kutoka katika hazina ya vionjo na hisia. Nasimama mbele yenu nikijuta kutoa kauli hiyo ambayo madhara yake baada ya tafakari ni kuruhusu uvunjaji wa sheria nchini na kutoa kibali kwa kufanyika kile ambacho tunataka kukomesha nacho ni mauaji ya mtanzania mmoja katika mikono ya mtanzania mwingine nje ya utawala wa sheria. Nafuta kauli yangu na kuiondoa bila 'qualification" yoyote.
Ninaifuta kwa sababu natambua kuwa (niseme nilipaswa kutambua.) kuwa kauli hiyo inaweza kuchukuliwa kama kuhalalisha watu kujichukulia sheria mikononi na kwa hakika ingechukuliwa hivyo kwa haki. Ninaifuta kwa sababu kama Waziri Mkuu wenu niliapa kulinda Katiba yetu ambayo imeweka wazi umuhimu wa mgawanyo wa madaraka, uzito wa utawala wa sheria, na uwezo wa vyombo mahakama tu kuhusika na maamuzi yanayohusiana na utafutwaji wa haki. Ninaifuta kwa sababu nimeapa kulinda Katiba hiyo na siyo hisia zangu binafsi. Ninaifuta pia kwa sababu kama kiongozi wa serikali ni jukumu langu kutumia uwezo wangu wote na elimu yangu yote kuhakikisha taratibu na sheria zetu zinafuatwa na kila mtu, nikiwemo mimi.
Hivyo basi, napenda kutangaza kuwa watuhumiwa wote wa mauaji ya albino au watu wengine wanaojihusisha na vitendo hivyo mahali popote watakapopatikana ni lazima wasalimishwe kwenye vyombo vya sheria bila kudhuriwa au kupewa adhabu ya papo kwa hapo. Ninaelewa hasira na uchungu wa wananchi lakini hasira na uchungu huo tuelekeze kwenye kuzuia mambo hayo kwa kuwafichua wafanyabiashara, waganga wa jadi, na wale wote wanaohusika na ughaidi huu dhidi ya Watanzania wenzetu.
Kwa upande wetu, serikali imetenga Shs bilioni 1.5 kama kianzio cha mfuko wa motisha kwa wale wote ambao watawafichua wale wote wanaohusika na biashara hii. Tunaanzisha kitu ambacho kitaitwa kama "Tajirika na Kuwalinda Maalbino - Tuko Pamoja Juani". Programu hii itamzawadia mtu yeyote ambaye atawezesha kupatikana taarifa za uhakika za njama, mipango, na watu ambao wanahusika na biashara hii haramu. Zawadi ya chini katika mpango huu ni Tsh milioni 20, na zawadi ya juu ni Tsh milioni 100! Mfuko huu na zawadi zinaweza kuongezeka kutoka na michango ya watu na taasisi mbalimbali. Kiasi pia kitatumika kusaidia jumuiya ya Maalbino. Hili tutalipanga pamoja na wawakilishi wao na taasisi nyingine husika.
Naomba niahidi kuwa niko tayari na nimedhamiria kuhakikisha kuwa nchi yetu inaendeshwa kwa kufuata utawala wa sheria kwa gharama yoyote ile. Kama binadamu sisi sote hutekwa na hisia na wakati mwingine vionjo vyetu vinatuzidi nguvu. Ndiyo ilivyokuwa kwangu na ninaomba radhi na msamaha Watanzania wenzangu kwa maneno yangu hayo ambayo kwa kiasi kikubwa yamehoji uwezo wangu wa kusimamia sheria au utawala bora.
Hata hivyo, endapo Bunge lako tukufu litaona kuwa sistahili kuendelea na wadhifa huu linaweza kupiga kura ya kuwa na imani au kutokuwa na imani nami. Naomba nitoe hoja Mhe. Spika Bunge lako lifanye hivyo ili kuondoa kiwingu chochote ambacho nimesababisha kitande. Kama halitafanya hivyo nimemuandikia Mhe. Rais barua ya maelezo yangu na kuomba radhi kwake pia na ninatumaini ataendelea kuniamini katika wadhifa huu mkubwa wa kuitumikia nchi yetu.
Mizengo Kayanza Peter Pinda(MB)
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
NB: Sijaweza kuthibitisha ukweli au usahihi wa taarifa hiyo. Muda ndio utasema.