Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,475
- 39,988
Na. M. M. Mwanakijiji
Hatuendi mbele, wala hatutoki tuliko. Kama ni jeshini tunaweza kusema tuko kwenye marktime! Na kama ni lori basi tumekwama kwenye matope na magurumu yanazunguka kwa kasi na ngurumo ya gari inapasua anga huku harufu ya moshi wa matairi ikichafua pua zetu. Hata hivyo, hatuendi kokote. Tumebakia kama tumefungwa kamba karibu na vundo la uchafu, na kama tuliokaribishwa karamu kwenye shimo la uchafu, tumeketi, tunajaribu kuziba pua na huku tunajisikia kichefu chefu, lakini hatutoki.
Ni mfano mbaya ninaotumia, lakini inabidi.
Tumepiga kambi kwenye bonde la kashfa. Tulipoanza kujenga Taifa letu tulitaka tuendelee mbele, tulitaka tulete mabadiliko kwa watu wetu na siyo majengo yetu, tulitaka kuona katika Taifa letu watu wote wanakuwa sawa na wenye kufurahia haki zote za msingi za binadamu na huku wakifurahia pia haki zao kama raia. Na sisi tulitaka kujenga taifa la kisasa ambalo lina mazingira mazuri ya maisha na lenye kutoa nafasi sawa ya mafanikio. Bahati mbaya haya sasa yanaendelea kuwa ndoto inayofikiwa na wachache, huku wengi wetu kama taifa tumeendelea kukaa pembeni na kunung'unika kwenye bonde hili la kashfa.
Taifa letu kwa miaka karibu mitatu sasa limejikuta katika mijadala yake limekwama kwenye ile ya kashfa. Sipendi kuziorodhesha tena lakini wingi wake unajulikana na gharama yake inashtua mioyo. Na kama vile watu wasioona mbele tayari tumeshatengeneza kashfa zijazo kwa kuahirisha kushughulikia yanayowezekana sasa! Hatuwezi kuishi bila kashfa.
Tatizo kubwa nilionalo (na nimewahi kuandika huko nyuma) ni kutokuwa tayari kushughulikia jambo la kitaifa na kulimaliza na kufunga mjadala. Inashangaza mwaka mmoja baadaye suala la Richmond bado lipo, miaka nane baadaye suala la rada ndio hata halijaanza kushughulikiwa, miaka karibu kumi na kitu suala la IPTL bado linatoa harufu yake, na miaka karibu 20 uchafu wa BoT bado tunao! Hatuwezi kuendelea mbele kwa kadiri ya kwamba tunaendelea kuketi kwenye kambi hii ya kashfa za ufisadi.
Hatuwezi kwenda mbele kama katika mawazo na fikra zetu tunahangaika na mambo ambayo yangepaswa kushughulikiwa mara moja na daima. NI tabia hii ya kuvumilia uchafu na uovu ndiyo imetufanya tuuzoee kiasi kwamba usafi na wema vinaonekana kuwa ni tunu za "watakatifu" wachache na sehemu ya "waadilifu wateule".
Hatuwezi kwenda mbele na kujadali masuala ya mabadiliko ya taifa ambayo yatachochea kupiga hatua "ile kuu" ya maendeleo kwa kadiri ya kwamba tumeng'angania utamu wa kashfa mbalimbali tukikwepa kuzishughulikia mara moja. Tunaendelea kuchechema kama kulungu aliyenaswa mtegoni!
Tumefika mahali pa kuelezea na kusifia "hatua za maendeleo" ambayo yamo mawazoni mwetu. Tunapita kati ya watu wetu na kuwataka waimbe nyimbo za maendeleo ya kitu ambacho hawakuwa nacho. Unapojenga kisima mahali ambapo hakuna kisima ulichofanya siyo maendeleo bali kukutana na mahitaji ya watu. Maendeleo yatakuwa ni pale ambapo wakazi wa sehemu hiyo wanaweza kupata maji safi ya bomba kwenye nyumba zao!
Unapojenga kliniki mahali ambapo hapana kliniki ya msingi siyo umeendelea bali umekutana na mahitaji ya watu. Maendeleo hapo yatakuwa ni huduma ya kisasa, wataalamu wa kutosha na mchakato bora wa kupata tiba.
Unapojenga barabara ya lami unaweza kuona ni maendeleo. Hata hivyo hilo ni jambo la lazima katika ulimwengu wa leo. Maendeleo basi hapo yatakuwa ni kutengeneza mitaro ya maji machafu, taa zinazofanya kazi za kuongezea magari na zile za kumulika njia, alama nzuri za usalama wa barabarani n.k
Ndiyo maana wengine tulitakaa pale kina Lowassa walipotaka tuimbe wimbo wa kupaa ati kwa sababu tumejenga shule nyingi za msingi kupitia MMEM na miradi mingine. Tulikataa kwa sababu walikuwa wanatuonesha ongezeko la vitu. Walitaka tuone idadi ya wanaffunzi wanajiunga na sekondari na shule ya msingi. Lakini walikwepa kabisa kuangalia kufaulu kwa watoto hao.
Leo hii tulichokisema karibu miaka minne iliyopita kinaendelea kuwa kweli. Tumeongeza mashule, tumeongeza idadi ya wanafunzi wanaoingia shule lakini tumepunguza kiwango cha kufaulu, na kwenye masomo ya sayansi na kiingereza bado tuko nyuma sana. Siyo kwenye shule za awali bali hata kwenye vyuo! Tumepiga kambi kwenye kashfa nasi tumezizoa.
Naamini wakati upo, na haja ipo ya kubadili fikra zetu na kukataa kucheza mdumange wa kashfa huku tukipiga filimbi za ufisadi. Ni lazima tukatae kulazimishwa kucheza mganda wa sifa za uongo huku tukiruka ruka kamba za kudanganyana.
Kama taifa ni lazima tutoke kwenye kambi hii ya kashfa na kuingia katika uwanja wa ujenzi mpya wa taifa la kisasa. Tuweze kukusanya nguvu zetu za kifikra kujadiliana jinsi ya kuboresha vilivyopo na vipya. Tuweze kutoka katika kashfa za BoT, Bunge, n.k na kuanza kujadiliana jinsi ya kuiboresha BoT, Bunge, Mahakama n.k Tuweze na sisi kutumia uwezo wetu na vipaji vyetu tulivyopewa na Mungu bure kutatua matatizo yetu.
Vinginevyo, tutaendelea kukodoleana macho, kutukanana, kutafutana wachawi, kubezena, kupigana vijembe, huku tukicheka cheka, tukiremburiana macho na kukonyezana, katika bonde hili la kashfa na ufisadi, kiasi kwamba kizazi kijacho kitakapoamka kitatulaani kwa kupoteza muda katika shimo la takataka!
Tuamue kutoka, na wale ambao hawataki tuwafukie na takataka zao!
Mwenzenu,
Ndugu yenu,
Rafiki yenu,
Na kwa wengine....
Adui yenu
Na isimame kama ushahidi na mashtaka dhidi yetu!
M.M. Mwanakijiji
Feb 13, 2009
Hatuendi mbele, wala hatutoki tuliko. Kama ni jeshini tunaweza kusema tuko kwenye marktime! Na kama ni lori basi tumekwama kwenye matope na magurumu yanazunguka kwa kasi na ngurumo ya gari inapasua anga huku harufu ya moshi wa matairi ikichafua pua zetu. Hata hivyo, hatuendi kokote. Tumebakia kama tumefungwa kamba karibu na vundo la uchafu, na kama tuliokaribishwa karamu kwenye shimo la uchafu, tumeketi, tunajaribu kuziba pua na huku tunajisikia kichefu chefu, lakini hatutoki.
Ni mfano mbaya ninaotumia, lakini inabidi.
Tumepiga kambi kwenye bonde la kashfa. Tulipoanza kujenga Taifa letu tulitaka tuendelee mbele, tulitaka tulete mabadiliko kwa watu wetu na siyo majengo yetu, tulitaka kuona katika Taifa letu watu wote wanakuwa sawa na wenye kufurahia haki zote za msingi za binadamu na huku wakifurahia pia haki zao kama raia. Na sisi tulitaka kujenga taifa la kisasa ambalo lina mazingira mazuri ya maisha na lenye kutoa nafasi sawa ya mafanikio. Bahati mbaya haya sasa yanaendelea kuwa ndoto inayofikiwa na wachache, huku wengi wetu kama taifa tumeendelea kukaa pembeni na kunung'unika kwenye bonde hili la kashfa.
Taifa letu kwa miaka karibu mitatu sasa limejikuta katika mijadala yake limekwama kwenye ile ya kashfa. Sipendi kuziorodhesha tena lakini wingi wake unajulikana na gharama yake inashtua mioyo. Na kama vile watu wasioona mbele tayari tumeshatengeneza kashfa zijazo kwa kuahirisha kushughulikia yanayowezekana sasa! Hatuwezi kuishi bila kashfa.
Tatizo kubwa nilionalo (na nimewahi kuandika huko nyuma) ni kutokuwa tayari kushughulikia jambo la kitaifa na kulimaliza na kufunga mjadala. Inashangaza mwaka mmoja baadaye suala la Richmond bado lipo, miaka nane baadaye suala la rada ndio hata halijaanza kushughulikiwa, miaka karibu kumi na kitu suala la IPTL bado linatoa harufu yake, na miaka karibu 20 uchafu wa BoT bado tunao! Hatuwezi kuendelea mbele kwa kadiri ya kwamba tunaendelea kuketi kwenye kambi hii ya kashfa za ufisadi.
Hatuwezi kwenda mbele kama katika mawazo na fikra zetu tunahangaika na mambo ambayo yangepaswa kushughulikiwa mara moja na daima. NI tabia hii ya kuvumilia uchafu na uovu ndiyo imetufanya tuuzoee kiasi kwamba usafi na wema vinaonekana kuwa ni tunu za "watakatifu" wachache na sehemu ya "waadilifu wateule".
Hatuwezi kwenda mbele na kujadali masuala ya mabadiliko ya taifa ambayo yatachochea kupiga hatua "ile kuu" ya maendeleo kwa kadiri ya kwamba tumeng'angania utamu wa kashfa mbalimbali tukikwepa kuzishughulikia mara moja. Tunaendelea kuchechema kama kulungu aliyenaswa mtegoni!
Tumefika mahali pa kuelezea na kusifia "hatua za maendeleo" ambayo yamo mawazoni mwetu. Tunapita kati ya watu wetu na kuwataka waimbe nyimbo za maendeleo ya kitu ambacho hawakuwa nacho. Unapojenga kisima mahali ambapo hakuna kisima ulichofanya siyo maendeleo bali kukutana na mahitaji ya watu. Maendeleo yatakuwa ni pale ambapo wakazi wa sehemu hiyo wanaweza kupata maji safi ya bomba kwenye nyumba zao!
Unapojenga kliniki mahali ambapo hapana kliniki ya msingi siyo umeendelea bali umekutana na mahitaji ya watu. Maendeleo hapo yatakuwa ni huduma ya kisasa, wataalamu wa kutosha na mchakato bora wa kupata tiba.
Unapojenga barabara ya lami unaweza kuona ni maendeleo. Hata hivyo hilo ni jambo la lazima katika ulimwengu wa leo. Maendeleo basi hapo yatakuwa ni kutengeneza mitaro ya maji machafu, taa zinazofanya kazi za kuongezea magari na zile za kumulika njia, alama nzuri za usalama wa barabarani n.k
Ndiyo maana wengine tulitakaa pale kina Lowassa walipotaka tuimbe wimbo wa kupaa ati kwa sababu tumejenga shule nyingi za msingi kupitia MMEM na miradi mingine. Tulikataa kwa sababu walikuwa wanatuonesha ongezeko la vitu. Walitaka tuone idadi ya wanaffunzi wanajiunga na sekondari na shule ya msingi. Lakini walikwepa kabisa kuangalia kufaulu kwa watoto hao.
Leo hii tulichokisema karibu miaka minne iliyopita kinaendelea kuwa kweli. Tumeongeza mashule, tumeongeza idadi ya wanafunzi wanaoingia shule lakini tumepunguza kiwango cha kufaulu, na kwenye masomo ya sayansi na kiingereza bado tuko nyuma sana. Siyo kwenye shule za awali bali hata kwenye vyuo! Tumepiga kambi kwenye kashfa nasi tumezizoa.
Naamini wakati upo, na haja ipo ya kubadili fikra zetu na kukataa kucheza mdumange wa kashfa huku tukipiga filimbi za ufisadi. Ni lazima tukatae kulazimishwa kucheza mganda wa sifa za uongo huku tukiruka ruka kamba za kudanganyana.
Kama taifa ni lazima tutoke kwenye kambi hii ya kashfa na kuingia katika uwanja wa ujenzi mpya wa taifa la kisasa. Tuweze kukusanya nguvu zetu za kifikra kujadiliana jinsi ya kuboresha vilivyopo na vipya. Tuweze kutoka katika kashfa za BoT, Bunge, n.k na kuanza kujadiliana jinsi ya kuiboresha BoT, Bunge, Mahakama n.k Tuweze na sisi kutumia uwezo wetu na vipaji vyetu tulivyopewa na Mungu bure kutatua matatizo yetu.
Vinginevyo, tutaendelea kukodoleana macho, kutukanana, kutafutana wachawi, kubezena, kupigana vijembe, huku tukicheka cheka, tukiremburiana macho na kukonyezana, katika bonde hili la kashfa na ufisadi, kiasi kwamba kizazi kijacho kitakapoamka kitatulaani kwa kupoteza muda katika shimo la takataka!
Tuamue kutoka, na wale ambao hawataki tuwafukie na takataka zao!
Mwenzenu,
Ndugu yenu,
Rafiki yenu,
Na kwa wengine....
Adui yenu
Na isimame kama ushahidi na mashtaka dhidi yetu!
M.M. Mwanakijiji
Feb 13, 2009
Last edited: