Taifa likitaka, biashara dawa za kulevya itaisha

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,319
33,125
KATUNI(676).jpg

Maoni ya katuni


Kuzidi kuongezeka kwa biashara ya dawa za kulevya na ongezeko kubwa la vijana wanaozitumia ni mambo ambayo kadri siku zinavyokwenda inakuwa ni janga la taifa kiasi cha kuhitajika kwa nguvu za ziada kukabiliana na hali hii.

Ni kawaida kabisa sasa kupita katika miji mikubwa nchini kama vile Dar es Salaam, Mwanza, Arusha, Mbeya, Moshi, Morogoro kutaja kwa uchache tu, kukuta makundi ya vijana ambao ni waathirika wakubwa wa dawa hizi. Vijana hawa wamekuwa ni mzigo mkubwa kwa familia zao na taifa kwa ujumla.

Wakati nguvukazi ya taifa ikiathirika kutokana na dawa za kulevya, wapo wafanyabiasha wachache wananufaika kutokana na uuzwaji wa dawa hizo ambazo kimsingi ni janga kwa taifa hili.

Tunasema haya hasa tukipiga picha nyuma na kukumbusha wasomaji wetu hasa wa safu ya ya tahariri kuwa Oktoba 13, mwaka jana tuliandika tahariri ikibeba kichwa cha habari “Tuungane kupambana na janga la dawa za kulevya.” Tulitoa wito huo baada ya kumsikia Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi, akielezea athari za dawa za kulevya na kutaja kuwa Tanzania kwa sasa inanuka huko nje kutokana na tuhuma za usafirishaji wa dawa hizo na alieleza kwamba kuporomoka kwa sifa nzuri ya nchi ilipata kumuathiri binafsi akiwa ughaibuni.


Mwaka jana huo huo, Septemba 9, tuliandika tahariri nyingine tukisema “Tatizo la dawa za kulevya nchini ni kubwa mno.” Tulisema hayo kwa kutambua kwamba mwaka baada ya mwaka janga la dawa za kulevya nchini lilikuwa linaongezeka kwa kasi kubwa.

Tulisema kuwa kwa miaka kadhaa sasa biashara ya dawa za kulevya imekuwa ikikukua na kuota mizizi nchini huku watu wachache laghai wakigeuka mabilionea wakati wakiteketeza kizazi cha vijana na kuacha taifa katika ukiwa mbaya.

Tulisema hayo tukikumbuka kuwa Septemba 7, mwaka jana Kikosi cha Kudhibiti Dawa za Kulevya nchini kilikuwa kimetangaza kukamatwa kwa watu watano wakiwa na shehena ya kilo 97 za heroin zenye thamani ya Sh. bilioni 4.36 jijini Dar es Salaam, shehena hiyo ilikamatwa ikiwa imepita miezi michache tu tangu kukamatwa kwa kilo 179 za heroin Februari mwaka jana.

Tulisema kuwa kuanzia Januari mwaka jana hadi Septemba pekee kiasi cha kilo 294 za heroin zilikuwa zimekamatwa nchini, mwaka juzi pekee kilo 190.780 za heroin zilikamatwa wakati huo cocaine yenye uzito wa kilo 64.966 nayo ikiwa imekamatwa kwa mwaka huo pekee.

Wakati hali hii ikiendelea kusumbua taifa, juzi baadhi ya wabunge walicharuka bungeni wakitaka vigogo wa dawa za kulevya wakamatwe na kufikishwa mahakamani kwani tatizo la dawa za kulevya limezidi kuwa kubwa sambamba na kuongezeka kwa vijana wanaotumia dawa hizo maarufu kama mateja.

Wabunge walisema hayo wakati wanachangia muswada wa Sheria ya marekebisho ya Sheria mbalimbali wa mwaka 2011, uliowasilishwa bungeni na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Miongoni mwa hoja zilizojengwa na wabunge ni pamoja na kueleza mshangao wao kuwa wakati kiwango cha dawa za kulevya kinachoingia nchini kikizidi kuongezeka, idadi ya watuhumiwa inapungua. Hali hiyo ilielezwa kuwa hivyo wakati sheria kali zipo lakini tatizo kubwa linaonekana kuwa ni usimamizi duni wa utekelezaji wa sheria hizo. Huo ulitajwa kuwa ni udhaifu mkubwa.

Ni kutokana na hali hiyo, maoni ya wabunge wengi yalilenga kuweka bayana kuwa tatizo la dawa za kulevya si ukosefu wa sheria kali, ila ni usimamizi mbovu wa sheria husika. Tunaungana na msimamo huu na kwa kweli tungefarijika kama tungeona hali ya mambo ikigeuka ili sasa wahusika wa dawa za kulevya washughulikiwe vilivyo.

Hali hii ingeleta matumaini zaidi kama pia vigogo wa dawa za kulevya, yaani wale wanaojikuta ni mabilionea tu kwa sababu ya kuharibu taifa, wangekamatwa, wafikishwe mahakamani ili kukomesha janga hili linalotafuna taifa hasa vijana ambao ni uhai wa taifa.

Kwa muda sasa kumekuwa na madai kutoka kwa watu mbalimbali, hasa wale wanaopambana dhidi ya biashara hii kuwa serikali inawajua vigogo wa biashara hii. Ni kwa jinsi hiyo baadhi ya wabunge waliitaka serikali kuacha kigugumizi na kuchukua hatua za kukomesha biashara ya dawa za kulevya.

Kwa kuwa sasa kilio juu ya kuzidi kushamiri kwa dawa za kulevya kimekuwa kikubwa zaidi nchini kuliko wakati wowote, ni rai yetu kuwa sasa ni jukumu la vyombo vya dola kuongeza usimamizi wa sheria, kuacha kuogopa watuhumiwa na kuchukua hatua stahili za kuponya taifa hili dhidi ya dawa za kulevya.





CHANZO: NIPASHE

 
Haya madawa yanaingizwa hapa nchini chini ya usimamizi wa vigogo wa pale magogoni, kwa kushirikiana kwa karibu na mtoto wa mwenye nchi.
Bila shaka, wakiamua wanaweza kwani wao ndio wahusika namba 1.
 
Back
Top Bottom