Taarifa kwa umma kuhusu kufukuzwa wanafunzi 43 chuo kikuu cha Dar Es Salaam

MWAMBAPA

New Member
Jan 3, 2012
1
0
KIINI CHA TATIZO LA MIGOGORO VYUONI:

Tangu kuanza kwa utekelezaji wa sera ya kuchangia elimu ya juu kumekuwepo migogoro mingi inayohusiana na mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu . Ingawa vyanzo vya migogoro hii vimekuwa tofauti tofauti, wanafunzi ndio wamekuwa wahanga wakubwa wa matokeo ya migogoro hiyo. Tunaomba migogoro itatuliwe kwa kuelekeza nguvu kwenye kuondoa vyanzo vya migogoro.

Tuna imani kuwa moja ya chanzo cha migogoro Vyuoni kwa siku za karibuni ni serikali kushindwa kutimiza ahadi zake inazotoa kuhusu kupatikana kwa mikopo kwa wakati muafaka. Mfano wa karibuni kabisa ni ahadi ya Rais Kikwete ya tarehe 20/10/2011 aliyoitoa Chuo kikuuu cha Dar es salaam kuwa hakuna mwanafunzi mwenye sifa atakayeshindwa kusoma kwa kukosa mkopo.

Chanzo kingine cha migomo ni kutokuwepo kwa mawasiliano mazuri kiutendaji kati ya Tanzania Commission for Universities(TCU),Higher Education Students' Loans Board(HESLB) na vyuo kuhusu idadi ya wanafunzi waliodahiliwa ( kupata "admission") na kuhitaji mikopo toka HESLB ukilinganisha na uwezo wa HESLB kuwapatia mikopo hiyo na kuchelewa katika kuipata mikopo yenyewe.

HISTORIA FUPI YA MGOGORO ULIOTOKEA UDSM.

Mwishoni mwa mwezi wa nane, bodi ya mikopo ilitoa orodha ya majina ya wanafunzi waliofanikiwa kupata mikopo, ambapo walikuwa takribani wanafunzi elfu ishirini na nne (24000). Wanafunzi takribani elfu kumi na tatu (13000) walikosa mikopo nchi nzima ilihali wengi wao walipata udahili kwenye vyuo na pia walikuwa na sifa zote za kupata mkopo.

Umoja wa vyuo vikuu nchini (TAHLISO) ulitoa tamko kuwa wanafunzi wote walikosa mikopo waripoti vyuoni na matatizo yao ya mikopo yangeshughulikiwa wakiwa vyuoni. Wakiwa vyuoni wanafunzi hao ambao wengi ni kutoka familia duni, walikuwa wakikabiliwa na maisha magumu yaliyotokana na ukosefu wa mikopo maarufu kama "NO LOAN".



Kwa upande wa Chuo kikuu cha Dar es salaam, takribani wanafunzi 1673 walikosa mikopo. Tulipofungua chuo, mnamo tarehe 10/10/2011 tuliwakuta wanafunzi wa mwaka wa kwanza waliokosa mikopo wakiishi maisha ya kusikitisha chuoni. Baadhi yao walikuwa wakishinda kwa kula mlo mmoja ambao ni mkate mkavu na maji asubuhi, wengine walikuwa wakishinda njaa mpaka siku mbili hali iliyopelekea kuzimia ovyo mabwenini. Sisi tuliokuwa na mikopo tulilazimika kukatiana chapati moja na baadhi ya wanafunzi hao ili tu siku ziende.

Baadhi ya wanafunzi waliokosa mikopo walikuwa wamekwisha kufungasha vitu vyao na kurudi makwao baada ya kushindwa kulipa ada na gharama nyingine za maisha chuoni. Hivyo basi, tuliyokuwa tunayaona UDSM yalitoa taswira ya hali ya mambo ilivyokuwa katika vyuo vingine nchini.
Baada ya kutoridhishwa na maisha waliyokuwa wakiishi wanafunzi hao, wanafunzi wengine walianza kufuatilia suala hilo kwa karibu ili kupata suluhisho.

Waliwasiliana na serikali ya wanafunzi DARUSO, ili kujua walikofikia katika kutatua tatizo hilo. Jibu walilotoa ni kwamba waliwasiliana na Waziri wa Elimu Mh Kawambwa na kuwajibu kuwa Serikali haina fedha na bajeti imefika kikomo. Wanafunzi walijiuliza maswali mengi juu ya serikali kuweza kupata fedha za dharura kwa masuala mengine kama vile kuridhia malipo ya DOWANS kwa wakati huo lakini si kwa suala la mikopo kwa wanafunzi. Wanafunzi wa UDSM walikusanyika mara kadhaa katika eneo lao maarufu kama "REVOLUTION SQUARE" na kujadili suala hilo kwa kina.

Mnamo tarehe 18/10/2011 katika eneo hilo hilo wanafunzi waliridhia kuwa uandikwe waraka kwenda kwa Waziri wa Elimu Mh. Kawambwa kupitia serikali ya wanafunzi DARUSO, ofisi ya mshauri wa wanafunzi na Uongozi wa chuo. Waraka huo ulikuwa ukieleza sababu za msingi juu ya ustahili wa wanafunzi hao waliokosa mikopo, ulipelekwa DARUSO tarehe 21/10/2011 lakini ulirudishwa wakidai ulihitaji marekebisho kadhaa. Marekebisho hayo yalifanyika na waraka huo ulipelekwa tena DARUSO tarehe 25/10/2011 ambapo wanafunzi walimwomba Waziri awe ameujibu ndani ya siku kumi kutokana na ukweli kwamba tatizo lenyewe lilikuwa limekwisha sababisha athari kubwa kwa wenzao wale.

Tarehe 4/11/2011 ndiyo ilikuwa tarehe ya mwisho ya kusubiri majibu kutoka kwa waziri kwani waraka ule uliambatanishwa na barua. Waraka ule haukumfikia Waziri kwani ulikomea katika Ofisi ya Mshauri wa Wanafunzi.
Mnamo tarehe 7/11/2011 wanafunzi walimwandikia barua Waziri Mkuu wa Serikali ya wanafunzi (DARUSO) kumuomba amwalike Waziri Mkuu wa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Kayanza Peter Pinda afike chuoni akiwa ameambatana na Waziri wa Elimu pamoja na Mkurugenzi wa wa Bodi ya Mikopo ili kujadili na wanafunzi juu ya tatizo la "NO LOAN" na kulipatia ufumbuzi kwa njia hiyo ya majadiliano.

Lakini pamoja na juhudi zote hizo hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa na DARUSO katika kutekeleza hilo.
Mnamo tarehe 9/11/2011 siku ya Jumatano, wanafunzi walikusanyika tena eneo lao la kawaida "REVOLUTION SQUARE" na kukubaliana kwamba endapo Waziri Mkuu hatofika chuoni kufikia tarehe 10/11/2011 siku ya Alhamisi basi tarehe 11/11/2011 wangefanya maandamano ya amani ili kuishikiniza Serikali kuwapatia mikopo wanafunzi wote nchini waliokosa mikopo.

Hii ni kwa sababu ndiyo njia pekee iliyokuwa imebakia kuwanusuru wanafunzi wenzetu kwa kuzingatia ukweli kwamba baadhi yao hasa wasichana wangeweza kujiingiza katika vitendo vya ukahaba na vingine ambavyo ni kinyume na sheria ikiwemo wizi ili kukabiliana na hali ngumu ya maisha waliyokuwa nayo. Ni ukweli kwamba vitendo vya ukahaba vimekuwa ni sababu kubwa ya kuongezeka kwa maambukizi ya gonjwa hatari la UKIMWI hapa nchini na kupelekea Taifa kupoteza hazina kubwa ya wasomi.


Kweli Waziri Mkuu hakufika chuoni kama wanafunzi walivyoomba na hivyo maandamano yakafanyika kwa amani kama ilivyopangwa. Wanafunzi walianza kutawanyika kufuatia amri ya polisi wa kutuliza ghasia lakini jambo la kusikitisha polisi hao walitumia nguvu kubwa ikiwa ni pamoja na kutumia mabomu ya machozi ambapo wanafunzi takribani 47 walikamatwa katika eneo la tukio.

Idadi hiyo iliongezeka na kufikia 51 baada ya wanafunzi 4 kukamatwa katika kituo cha polisi Oysterbay walipokwenda kuwawekea dhamana wenzao.
Wanafunzi waliokamatwa waliwekwa mahabusu kituoni hapo kwa siku tatu ambapo wanafunzi 5 walitumiwa barua za kusimamishwa masomo wakiwa mahabusu.

Mnamo tarehe 14/11/2011 wanafunzi waliokamatwa walipandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na kusomewa mashtaka mawili ambayo ni kufanya mkusanyiko usio halali na kukaidi amri ya polisi ya kutawanyika. Masharti ya dhamana yalisomwa ambapo mdhamini alitakiwa kusaini bondi ya shilingi 1,000,000/= ambapo wanafunzi 9 pekee ndio walioweza kukidhi masharti hayo na wengine 41 walishindwa masharti ya dhamana na kupelekwa katika gereza la segerea hadi tarehe 16/11/2011 walipowekewa dhamana na DARUSO kupitia Chuo Kikuu cha Dar es salaam baada ya shinikizo kubwa kutoka kwa wanafunzi waliobaki chuoni waliokuwa wakiandamana muda wote wakishinikiza kuachiliwawa huru kwa wenzao.


Tuliporudi kutoka gerezani tarehe 16/11/2011 tuliwakuta wanafunzi wenzetu wakiendelea kushinikiza na tuliwasihi kutulia na kuendea na masomo wakati uongozi wa chuo ukishughulikia tatizo na hatimaye amani ya chuo ilirejea na masomo kuendelea kama kawaida. Kamati mbili za nidhamu ziliundwa ambapo tarehe 27/12/2011 tulianza kuhojiwa hadi tarehe 29/11/2011 zoezi hilo lilipokamilika.


Maamuzi juu ya hatma yetu baada ya kuhojiwa yalikawia kutolewa tofauti na matarajio ya wanafunzi wengi hali iliyosababisha wanafunzi kuanza tena kuandamana kushinikiza Utawala wa Chuo kuyatoa mapema kwani ni kweli kwamba kuchelewa kutoka kwa majibu hayo kuliwaathiri kitaaluma wanafunzi waliokuwa wamesimamishwa masomo kwa muda usiojulikana wakisubiri uamuzi wa Chuo.


Mnamo tarehe 8/12/2011 majibu hayo yalitoka ambapo wanafunzi 8 walisimamishwa masomo kwa miezi 9, wengine 35 kusimamishwa masomo mpaka hapo mahakama itakapotoa hukumu ya kesi yao kulingana na sheria ndogondogo za wanafunzi (Student's by-law) na wengine 15 kupewa onyo kali. Majadiliano yalifanyika kati ya Serikali ya wanafunzi (DARUSO) na Uongozi wa Chuo na kuamuliwa kuwa wanafunzi 35 waliokuwa wamesimamishwa masomo kusubiri maamuzi ya Mahakama juu ya kesi yao warudi chuoni kuendelea na masomo na wale wengine 8 waliosimamishwa kwa miezi 9 waendelee kutumikia adhabu yao.


Mnamo tarehe 12/12/2011 baadhi ya wale wanafunzi 8 waliokuwa wamesimamishwa masomo kwa miezi 9 walifika auxiliary police Chuoni ili kuchukua barua zao za kusimamishwa masomo. Kundi la wanafunzi takribani 20 waliokuwa miongoni mwa umati mkubwa wa wanafunzi uliokuwa umekusanyika mbele ya majengo ya utawala wa chuo walifika katika eneo la auxiliary police wakidai kuwa wanafunzi wanataka waje watusindikize kuchukua barua.

Tuliwasihi wawaambie wasifanye hivyo kwani jambo hilo lingetafsiriwa kama kuvamia kituo cha polisi. Wanafunzi wale waliokuwa wameshatuzunguka, walikubali kwa sharti la kututaka tukutane nao. Nasi kwa kuangalia usalama wetu na hali ya amani ya chuo ilivyokuwa tete, tulikubali kwani walidai pamoja na kudai fedha zao za kujikimu vilevile walikuwa wakidai wale wenzao 8 waliosimamishwa masomo kwa miezi 9 kurudishwa chuoni na wasingekubali kutulia kwani walikuwa tayari kukesha pale bila kula wala kunywa mpaka madai hayo yatimizwe na Utawala wa Chuo.

Walitueleza pia kuna wawakilishi wao waliokwenda kuongea na Utawala wa chuo, hivyo tusiondoke mpaka watakapoleta majibu.
Wanafunzi wale wawakilishi waliporudi waliwaeleza wenzao kuwa ni kweli uongozi wa chuo ulikuwa umekubali kuwarudisha masomoni wanafunzi 35 waliosimamishwa masomo wakisuburi hukumu ya kesi yao mahakamani kama walivyokuwa wameelezwa na raisi pamoja na waziri mkuu wa DARUSO siku kadhaa nyuma. Pia waliwaeleza kuwa uongozi wa chuo unahitaji kuonana na wale wanafunzi 8 walosimamishwa masomo kwa miezi 9 ili kujadili namna ya kurudi kwao chuoni.

Tulionana na uongozi wa chuo siku hiyo ya tarehe 12/12/2011 kwa kuitikia wito wa wanafunzi wenzetu, na Utawala wa Chuo ulitushauri tukate rufaa kupinga adhabu iliyokuwa imetolewa huku tukiendelea na masomo kama kawaida na pia tuhubiri amani chuoni na tumsihi kila mwanafunzi awe balozi wa amani chuoni.
Tulipotoka ndani ya jengo la utawala tuliwaeleza wanafunzi wenzetu makubaliano yaliyofikiwa baina yetu na Utawala lakini tuliwakumbusha kwamba makubaliano hayo yangezaa matunda endapo tu amani itakuwepo chuoni.

Ikumbukwe kuwa wakati tulipokuwa tunazungumza na uongozi ndani ya jengo la Utawala ndipo huko nje vitendo vya magari kupasuliwa vioo, kuharibiwa vitu katika cafeteria na wengine kuchapwa viboko kama ilivyodaiwa na uongozi wa chuo vilikuwa vinafanyika,hivyo sisi hatukuhusika kwa namna yoyote ile. Hii ni kuzingatia kuwa uwepo wetu chuoni ulitegemea masharti ya kuwepo kwa amani chuoni na hatukuwa na dai lolote dhidi ya uongozi wa chuo wakati huo.


Mnamo tarehe 13/12/2011 siku ya Jumanne, wanafunzi wa Kitivo cha Uhandisi (COET) na Shule ya Uandishi wa Habari (SJMC) walikusanyika mbele ya jengo la Utawala wakidai fedha zao za kujikimu kwani hawakupewa fedha hizo kama wenzao siku ya jumatatu tarehe 12/12/2011. Kwa siku hiyo ya tarehe 13/12/2011 amani chuoni iliyumba tena ndipo mmoja wa wale wanafunzi 8 akiwawakilisha wenzake alikwenda kumwona Makamu Mkuu wa chuo,Prof. Mukandala na kumweleza kuwa fujo za tarehe 13/12/2011 hawahusiki kwa namna yoyote ile na makubaliano waliyoafikiana tarehe 12/12/2011 waliyatekeleza kikamilifu. Makamu Mkuu wa Chuo alikubali baada ya kufanya uchunguzi.


ADHABU ZILIZOTOLEWA AWALI DHIDI YETU SISI TULIODAIWA KUWA VINARA WA MIGOGORO:

Baada ya mgogoro wa tarehe 11/11/2011 wanafunzi takribani 58 walipewa hati za mashitaka(charge sheet) kwa mujibu wa sheria ndogondogo za wanafunzi(students by-laws) na kuhojiwa na Kamati za Nidhamu za Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Wanafunzi 8 walisimamishwa masomo kwa miezi 9, wengine 35 kusimamishwa masomo mpaka kesi zao zitakapoamuliwa mahakamani Kisutu na wengine 15 kupewa onyo.

ADHABU YA KUFUKUZWA CHUO:


Tunaotoa taarifa hii kwa umma ni wanafunzi 35 na pia wale 8 waliotajwa hapo juu tuliopewa adhabu ya kufukuzwa Chuo kabisa tarehe 14/12/2011. Pia, sisi ndiyo wale wanafunzi ambao TCU na HESLB wameshauriwa na Chuo kuwa tusidahiliwe katika vyuo vyote vya umma wala kupewa mikopo. Tunadhani uamuzi wa kutufukuza kabisa ulifanyika kwa hasira kutokana na kuibuka kwa mgogoro mwingine, uliosababishwa na wanafunzi wengine ambao kwa siku husika walikuwa wakidai fedha zao za kujikimu zilizokuwa zimecheleweshwa.

Pia kulikuwepo siku ile madai ya wanafunzi kwa ujumla waliokuwa wanadai Chuo kitufutie adhabu zilizokuwa zimetolewa kwetu hapo awali
Adhabu ya sisi kufukuzwa kabisa ilitolewa pasipo kupewa hati ya mashitaka, kuhojiwa wala kusikilizwa kwetu kama watuhumiwa. Hatua hii dhidi yetu ilikuwa ni kinyume na sheria ndogondogo za wanafunzi (students' by laws) kifungu cha 13.1(ii,iii,v,vi,vii,viii,ix na xii) na 13.2(i,na ii ). Pia hatua hii ni kinyume cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ibara ya 13.6(a), pamoja na kuwa kinyume cha kanuni ya Natural Justice. Kupewa adhabu hii ya kufukuzwa kabisa bila kusikilizwa mmoja mmoja inatufanya tujihisi kupewa adhabu ya jumla (collective punishment) na tunajiona tumefanywa kafara kama njia ya kuwanyamazisha wanafunzi wengine . Hakuna ushahidi uliotolewa kudhibitisha kuwa sisi sote ndiyo haswa vinara wa vurugu Chuoni kwani hata tulipokuwa gerezani migogoro iliendelea kuwepo chuoni.

HITIMISHO:


Ukweli ni kwamba amani iliyopo Chuoni kwa sasa ni kwa uwepo wa ulinzi mkali wa polisi ilihali tatizo likibakia bila utatuzi. Pamoja na sisi kufukuzwa chuo bila hata kusikilizwa,Utawala wa chuo kikuu cha Dar es Salaam pia umekataa kuwahoji na kuwasikiliza wanafunzi wengine wanne{4} ambao wamesimamishwa masomo.

Kwa sasa wanafunzi hao hawajui hatma na mustakabali wa maisha yao kielimu kwani Utawala kukataa kuwasikiliza wanafunzi waliowasimamisha masomo ni sawa na kuwafukuza kinyemela.

Kwa unyenyekevu kabisa tunaomba yafuatayo yafuatiliwe na wahusika ili Chuo kiweze kuwa na amani na utulivu endelevu na wa hiari kwa upande wa Wanafunzi
:


1. Mawasiliano ya kiutendaji kati ya TCU,HESLB na VYUO yaboreshwe ili kuepuka kudahiliwa wanafunzi wanaopewa matumaini hewa ya kukopeshwa na serikali ilihali uwezo huo haupo.

2. Wanafunzi wanaojitokeza kutoa maoni yao na kujaribu kutetea maslahi na haki za msingi za wenzao wasichukuliwe kama wahalifu.


3. Uongozi wa Chuo utoe adhabu kulingana na taratibu na sheria za Chuo na siyo kwa shinikizo toka nje ya Chuo au hasira kwa nia ya kuwatisha na kuwanyamazisha wanafunzi kwani matatizo ya wanafunzi yasipotatuilwa yataendelea kuibua migogoro isiyokwisha. Kutolewa kwa adhabu za ujumla(collective punishment) kuepukwe.Kila mmoja mwenye kutuhumiwa aadhibiwe kutokana na kudhibitika kwa hatia yake mwenyewe.


4. Tunaomba kila mmoja wetu aitwe, asikilizwe na kujitetea mbele ya Kamati za Nidhamu Chuoni ili tuhukumiwe kwa haki vinginevyo adhabu tuliyopewa ifutwe kwani haikufuata utaratibu wa kisheria.


Pamoja na sisi kufukuzwa chuo bila hata kusikilizwa,Utawala wa chuo kikuu cha Dar es Salaam pia umekataa kuwahoji na kuwasikiliza wanafunzi wengine wanne{4} ambao wamesimamishwa masomo.

Kwa sasa wanafunzi hao hawajui hatma na mustakabali wa maisha yao kielimu kwani Utawala kukataa kuwasikiliza wanafunzi waliowasimamisha masomo ni sawa na kuwafukuza kinyemela
Tunaomba kila anayehusika au kuguswa na suala hili kuhakikisha kwamba anasimama katika nafasi yake kwa uaminifu na kweli, bila kujali itikadi wala tofauti za aina yoyote ile kuhakikisha tunatendewa haki.

MUNGU IBARIKI TANZANIA, MUNGU IBARIKI AFRIKA.
 
Polen madogo,endelea kudai haki yenu,hii bodi inazingua sana,mi nakumbuka tupo mwaka wa kwanza2006(udsm) walisema wote 40%tukakaza(mgomo)ndo wakaleta magroup,kama walikua sahihi kwa nini walibadilisha,huwa wanabip,sema sisi tuligoma kalibia wote,ila nasikia mke wa Riz1(alafa)amepata 100%
 
mbona suala hili wabunge wa dar hawasaidii?mbona wananchi wa dar mmekaa kimya?jamani sikumoja hawa watakuwa mawaziri wa VIVUKO tunatarajia majibu gani kwa watu wanao pigwa mabomu kila siku?Wananchi wa Kigamboni kama mpo humu jamvini jaribuni kuhusianisha hii habari na matamshi ya magufuli.By the way natamani niite alshaababu walipue chuo.
 
CHADEMA MPO WAPI? Huu ndo wakati wenu kutetea haki za watanzania hao wengine ndo walowafukuza.
 
Back
Top Bottom