Taa ya njano yaiwakia CHADEMA

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
6c4630b217df3d5944fab45e2514d3dc

Na Paschally Mayega - Imechapwa 06 July 2011

lema.jpg


RANGI ya njano imetumika mahali pengi kama alama ya tahadhari. Wanaoendesha vyombo vya moto kama vile magari na pikipiki wanajua kwamba taa ya njano ikiwaka inamtahadharisha dereva kujiandaa kuchukua uamuzi; kusimama au kuendelea kuendesha.

Dereva atasimamisha chombo chake taa nyekundu ikiwaka au ataendelea kuendesha taa ya kijani ikiwaka. Alama hizo zinaweza kutumika kueleza safari ya kisiasa ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). Iko kwenye mataa ichukue tahadhari kabla ya hatari.

Nimekuwa nikipigiwa simu nyingi na kutumiwa meseji nyingi kutoka kwa wanachama cha CHADEMA walioko sehemu mbalimbali nchini hasa Kahama, Kanyigo, Mwanza, Musoma na Arusha zikinitaka nitoe ufafanuzi wa masuala kadhaa ndani ya chama chao.

Jibu langu kwao, ufafanuzi rasmi lazima utoke ndani ya CHADEMA yenyewe. Tunafanana kwa mengi hasa kiharakati na wakati mwingine kifikra, lakini ieleweke si mwanachama wa CHADEMA wala wa chama chochote cha siasa.

Sijawahi kujiunga na chama cha siasa tangu kuzaliwa kwangu. Lakini nakiri kama alivyokiri Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere kuwa chama alichokiona kuwa makini zaidi baada ya kuanzishwa mfumo wa vyama vingi ni CHADEMA. Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimechusha.

Kuna watu wengi ndani ya CCM wenye busara, makini na heshima mbele ya wananchi, ndani na nje, lakini wamewekwa kando. Kwa bahati mbaya sana nao wamekubali kukaa kando na hivyo kufanana na wale wachache, ambao kwa uroho na unafiki wao, wameweza kuufanya uongozi wa chama na serikali yao kuonekana babaifu.

Jakaya Kikwete ndiye rais wa nchi hii. Anastahili hadhi kubwa ya kuwa mtumishi mkuu wa wananchi. Ana wajibu wa kuwasikiliza wanaoulalamikia uongozi wake na kujipanga vema badala ya kuwabandika vitambulisho vya upinzani au udini. Kufanya hivyo ni kudhihirisha udhaifu kuwa anawagawa wananchi ili atawale kilaini.

Sijapata neno zuri badala ya neno ‘usaliti' uliofanywa na viongozi wa Chama cha Wananchi (CUF) kwa kukubali kuitumikia serikali ya CCM huku wakipewa vyeo walivyovipigania kwa muda mrefu – kuanzia makamu wa rais, mawaziri na viongozi wengine wote.

Kule Zanzibar CUF wanatii na kutekeleza sera za CCM chini ya Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ).

Imewezekana vipi magumu ya maisha, shida za muda mrefu za Wazanzibari na hasa Wapemba zilizokuwa zikiimbwa na viongozi wa CUF kila siku zote zikaisha siku moja, tena siku viongozi walipokubali kubatizwa na kuwa waumini wa sera za CCM? Hivi dawa ya shetani ni kuungana naye? Kwamba kama huwezi kumshinda ungana naye?
CUF Zanzibar ipo lakini katu si chama tawala hata kama baadhi ya viongozi wake wamepewa vyeo ndani ya CCM. Nani atawapigania Wanzanzibari waliokuwa wanapiganiwa na CUF pindi SMZ ikiwakandamiza?

Tuzikumbuke roho za marehemu waliokufa Pemba wakati wakipigania haki. Wangejua kwamba walikuwa wanapigania maslahi ya watu fulani wangekubali kweli kuzitoa roho zao?

Wanasiasa wetu wengi ni wanafiki, waroho wa vyote, mali na madaraka. Kufanikisha nia zao huishia kuhubiri chuki ili kuwafitinisha watu. Kinachohubiriwa katika sera ya kuvua gamba ni chuki binafsi, majungu na fitina basi. Hii ndiyo kazi anayoifanya shetani na wasaidizi wake.

Wana CHADEMA wanataka waambiwe tofauti kati ya tukio la CUF kule Zanzibar na tukio la madiwani wao kule Arusha. Kama leo ni madiwani kesho watakuwa viongozi gani?

Nina imani kubwa na uongozi wa CHADEMA lakini lazima wafahamu kuwa yanahitajika maelezo thabiti kwa sababu roho za watu zilipotea Arusha kwa jambo hili! Wanachoona ni taa ya njano, watahadhari kabla ya hatari.

CHADEMA ilihitaji karibu kila mtu waliyedhania kwamba angeweza kushinda ili kupata viti vya kutosha Bungeni na katika Baraza la Madiwani. Katika mahitaji hayo ikajikuta imewachukua hata wale waliokataliwa na vyama vyao au walioshindikana na wenye mtazamo tofauti.

Litakuwa jambo la busara kwa watu hawa kukiheshimu chama, kuwa watiifu kwa viongozi wao pamoja na wanachama wenzao. Kwa hiyo, tofauti ya kimtazamo na kimsimamo kati ya watu kama John Shibuda na viongozi wenzake lazima yatolewe maelezo ya kina kwa wanachama.

Jambo jingine ni habari kuwa waliokisaliti chama chao na viongozi wao wakaanzisha Chama cha Jamii (CCJ), walikuwa na mpango wa kugombea uongozi kwa kushirikiana na CHADEMA. Hili nalo linahitaji maelezo.

Ni bahati njema kuwa hiyo bahati mbaya haikutokea. Leo wana CHADEMA wanashuhudia walioasisi CCJ ndani ya CCM wanavyokiyumbisha na kukivuruga chama tawala. CHADEMA waone hiyo kuwa ni taa ya njano wasiwe ‘dampo'.

Halafu kuna hili la matamshi yaliyotolewa hadharani na kiongozi wa CHADEMA kuwa mwaka 2015 atagombea urais. Kugombea urais katika nchi yetu ni haki ya kila Mtanzania lakini, je, huo ndio utaratibu wa chama? Kama mapenzi yaliyoonyeshwa na Watanzania wengi kwa Dk. Willibrod Slaa yataendelea hadi mwaka 2015 itakuwaje mtu mwingine anapotangaza nia sasa? Lengo lake nini?

Ukweli utabaki kuwa ni vigumu kumshinda Dk. Slaa na kukaribisha wengine kutangaza nia sasa itakuwa fujo. Chama kilichopo madarakani – CCM – kwa kuhisi uchovu na uchakavu kinaweza kumuunga mkono mwana-CHADEMA yeyote kwa lengo la kukipasua. Hii ni alama ya njano, CHADEMA lazima ichukue tahadhari mapema.

Watanzania wanahitaji Jukwaa la Umoja yaani mahali pasipokuwa na maslahi ya kisiasa bali nchi kwanza. Mahali pa kauli moja kwa sisi wote bila kujali tofauti za kisiasa au za kidini itakayoheshimika na viongozi wetu.

Juu ya jukwaa hilo kwa pamoja watahakikisha kuwa nchi na raslimali zote zilizomo zinabaki kuwa mali ya wananchi wote kwa ujumla.

Watanzania wautambue ukweli kuwa hakuna wa kuwakomboa. Si dini, si chama, wala si mtu. Lazima wajikomboe wenyewe. Mwalimu Forum ni jukwaa la kuwaunganisha Watanzania wote.

Atakayetoka miongoni mwetu kwenda Bungeni au katika Mahakama au Ikulu kuwa Rais wetu awe na uelewa kuwa yeye si chochote zaidi ya kuwa mwakilishi na mtumishi wa tuliomtuma. Anayekwenda huko kuutafuta uheshimiwa huyo hatufai. Mwenyezi Mungu aitangulie Mwalimu Forum – MWAFO.

Tel: 0713334239, Email
: ngowe2006@yahoo.com
 
mwalimu alisema vile kwa sababu alimjua mzee makani na mzee mtei ila mbowe kaharibu ile kitu jamani msitegemeee kipya hadi akae kando huyu mmachame
 
Ni vema huu ushauri ukafanyiwa kazi na viongozi wa CHADEMA, kwani siasa ni inahitaji muda mwingi kuwa makini.
 
Nashawishika kuamini kuwa mwandishi amesukumwa na uzalendo na mapenzi mema kwa nchi kuandika makala hiyo.
 
mwalimu alisema vile kwa sababu alimjua mzee makani na mzee mtei ila mbowe kaharibu ile kitu jamani msitegemeee kipya hadi akae kando huyu mmachame
Mkuu kwani Mzee Mtei, E alihamia chama gani kiasi kwamba hawezi kutoa ushauri ndani ya CHADEMA,alafu kama hujui CDM chini ya MBOWE ndiyo mafanikio haya unayo yaona, otherwise chama kingekufa kama CCJ cha NAPE wako pia jua CDM ni CHAMA NA SIYO MTU " ameni "
 
mwalimu alisema vile kwa sababu alimjua mzee makani na mzee mtei ila mbowe kaharibu ile kitu jamani msitegemeee kipya hadi akae kando huyu mmachame

Hata kama umetumwa (kama ni kweli umetumwa), anaekutuma ahakikishe anakupa hoja za kujenga na kuwashawishi wasomaji. Kwa bahati mbaya sijawahi kuona mtu akishinda kwa hoja ya kupewa siku zote huishia njiani!

Sina maslahi na Mhe. Mbowe, lakini maelezo yako hayatoshi tukuamini kirahisi hivyo. Hebu fafanua kidogo mkuu!
 
Back
Top Bottom