Sitta amvutia pumzi Mrema

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,299
33,080
pix.gif

• Ajiandaa kujibu makombora dhidi yake
SPIKA wa Bunge, Samuel Sitta, amesema anamvutia pumzi Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania Labour (TLP), Augustine Mrema, aliyetaka kulipwa sh bilioni moja ama kumpeleka mahakamani...
Kauli ya spika huyo ambaye ni Mbunge wa Urambo Mashariki kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), imekuja siku moja baada ya Mrema kumwandikia barua ya kumtaka amwombe radhi kwa kumdhalilisha, kumlipa kiasi hicho cha fedha ama kumshitaki.

Huku akionyesha kutokujali muda wa siku saba aliopewa na mwenyekiti huyo, Sitta alisema kwa sasa yupo jimboni akishughulikia kero za wapiga kura wake, hivyo si muda muafaka wa kujadili jambo hilo.

Akizungumza kwa njia ya simu na Tanzania Daima kutoka Urambo Mashariki, Spika Sitta alimtaka mwandishi wa habari hizi kumsubiri hadi atakaporejea jijini Dar es Salaam ili asome madai ya Mrema kabla ya kumjibu.

Kwa msisitizo, alisema anahutubia mikutano ya hadhara jimboni kwake, hivyo atakabiliana na kila jambo lililosemwa na mwenyekiti huyo aliyejinadi kuongoza chama cha nne kwa ukubwa nchini ambacho wanachama wake wanakadiriwa kufika 500,000.

“Nitayakabili mambo yote nitakaporejea Dar es Salaam… nina shughuli nyingi, kwa sasa nipo jimboni hivi ninavyokwambia nimemaliza mkutano wa pili, najiandaa kwenda kufanya mkutano wa tatu,” alisema.

Kuhusu hali ya kisiasa jimboni kwake, Sitta alisema: “Hali ya jimbo langu ni nzuri… watu wananielewa na ninavyoongea hapa nakaribia kuwahutubia wapiga kura.”

Jana, vyombo vya habari viliandika habari za Mrema kuwasilisha barua yenye kumbukumbu namba TLP/HQ/SIR/03/55, ambayo kusudio lake ni kumshitaki Sitta kwa kumwambia amefilisika kisiasa na kifedha, hivyo amechanganyikiwa.

Katika barua hiyo, Mrema alinukuu kauli za Sitta kwamba: “Mrema ni mhuni na amepitwa na wakati, pia amefilisika kisiasa na kipesa, sasa anatafuta jinsi ya kujinasua katika hali hiyo.

“Kuna uwezekano huyu bwana anapata pesa ili kuipigia debe CCM. Huyu Mrema ni mhuni katika siasa ndiyo maana anapotosha ukweli wa umma, nadhani amechanganyikiwa,” ilieleza sehemu ya barua hiyo ikinukuu malalamiko ya mwenyekiti wa TLP.

Aidha, Mrema anayejivunia kuutumikia umma kwa miaka 30 akishika nyadhifa mbalimbali, ikiwamo ya usalama wa taifa na naibu waziri mkuu, alisema kauli za spika huyo zinaweza kumharibia kwenye uchaguzi, kwa kuwa anatarajia kuwania ubunge wa Jimbo la Vunjo.

Awali, Mrema alimtaka spika huyo kuacha kukimbilia kwenye nyumba za ibada, akieleza kilichotokea bungeni na ndani ya kikao cha NEC ya CCM, pale alipobainisha kuwa alinusurika kuporwa kadi ya uanachama wake kwa kuwa anasema ukweli, ingawa kiongozi huyo wa Bunge hakuwa wazi ni ukweli upi huo.

“Kama Sitta na wenzake wanaona huko CCM wanaonewa, waje upinzani basi, asiwalaghai wananchi… anasema ukweli, ni ukweli upi huo?” alisisitiza Mrema na kumtaka Sitta kuacha kuvuruga amani iliyopo huku akidai kuwa amepoteza sifa za uongozi na utawala bora.

Alimtaka Sitta kuwaomba radhi Watanzania kwa kushindwa kuusimamia vema majadala wa Richmond akiwa bungeni, badala yake aliufunga ‘kibabe’ wakati wananchi hawajaelewa hatima yao, jambo aliloliita uchochezi.

Alisema wanaharakati wamekasirika kwa sababu ya mtu mmoja, hii si sawa, wakiandamana itakuwa doa kwa serikali, kutokana na spika kushindwa kusimamia vema mhimili huo.

Uamuzi wa Mrema kumshambulia Sitta ulitokana na kauli aliyoitoa spika huyo mjini Songea hivi karibuni, alipokaririwa akisema alikuwa amenusurika kufukuzwa uanachama wa CCM na vikao vya Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama hicho kutokana na kile alichokieleza kuwa ni msimamo wake wa kusimamia ukweli.

CHANZO: TANZANIA DAIMA
 
Back
Top Bottom