Siri nzito ya Zombe na Bageni

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,955
22,135
Kesi ya Mauaji :Mshtakiwa atoboa siri awahusisha Zombe, Bageni

Na James Magai

MSHTAKIWA wa 12 katika kesi ya mauaji ya wafanyabiashara watatu kutoka Mahenge mkoani Morogoro na dereva teksi mmoja wa Manzese jijini Dar es Salaam, Koplo Rajabu Hamis Bakari, jana aliiambia mahakama jinsi watu hao wanne walivyouawa na jinsi baadhi ya viongozi wake walivyofanya njama za kuficha ukweli wa mauaji hayo.

Sambamba na maelezo hayo, Mahakama Kuu jana ilimfutia rasmi mashtaka aliyekuwa mshtakiwa wa 11 katika kesi hiyo, Koplo Rashid Lema aliyefariki dunia Aprili 3 akiwa amelazwa Taasisi ya Saratani ya Ocean Road.

Katika maelezo yake ya utetezi, Koplo Bakari ambaye pia ni shahidi wa nane upande wa utetezi (DW8) katika kesi hiyo, alisema tukio hilo lilikuwa ni kubwa na la ajabu sana kwake kiasi kwamba hajawahi kuliona.

Koplo Bakari, ambaye alikiri kushuhudia tukio hilo mwanzo hadi mwisho katika ushahidi wake uliochukua muda wa saa 5:32, aliieleza mahakama jinsi ambavyo baadhi ya viongozi wake walivyofanya njama za kuficha ukweli wa mauaji hayo kwa kutishwa wasieleze ukweli kuhusu mauaji hayo na kufundishwa jinsi ya kujieleza.

Mbele ya jopo la majaji lililoongozwa na Jaji Salum Masatti, koplo huyo aliieleza mahakama jinsi Christopher Bageni, ambaye alikuwa mkuu wa upelelezi wilayani Kinondoni, alivyoonekana kuratibu mauaji hayo na jinsi mkuu wa upelelezi mkoani Dar es Salaam, Abdallah Zombe alivyoshiriki kuficha ukweli wa mauaji hayo.

"Sikuweza kutoa taarifa popote kwa sababu kwanza tuliambiwa kuwa atakayeeleza kuhusu tukio hilo, atabebeshwa msalaba huo yeye mwenyewe," alisema Koplo Bakari baada ya kuulizwa na Mzee wa Baraza, Kimolo kuwa ni kwa nini baada ya tukio hilo hakutoa taarifa.

Hata hivyo aliieleza mahakama kuwa baada ya rais kuunda tume iliyokuwa chini ya Jaji Mussa Kipenka kuchunguza mauaji hayo, Zombe, mshtakiwa wa kwanza katika kesi hiyo, aliwaita wote waliohusika na kuwapa karatasi ambazo zilikuwa na maelekezo ya namna ya kujieleza mbele ya tume hiyo.

Akielezea tukio zima, Koplo Bakari alieleza kuwa siku hiyo (Januari 14, 2006) alikuwa kwenye doria na askari wenzake watatu, ambao aliwataja kuwa ni marehemu Lema, Koplo Saad (Alawi) na Koplo Frank ambaye alikuwa dereva wa gari lao la doria aina ya Pajero Mitsubishi. Koplo Saad na Koplo Frank bado wanatafutwa na polisi.

Alisema jioni waliporudi kituoni alikwenda kwa Christopher Bageni ili kumpa taarifa ya doria na kwamba alikutana naye njiani akishuka ngazi kutoka ofisini kwake na kumtaka amfuate na walipomfuata walikuta askari wenzake na baadaye Bageni akawaamuru waingie kwenye gari na kumwambia Koplo Frank aendeshe gari kuelekea barabara ya Sam Nujoma ambako aliwaeleza kuwa kuna tukio la ujambazi.

Kwenye eneo la Konoike lililo Barabara ya Sam Nujoma, walikuta gari moja aina ya lori likiwa limesimama katikati ya barabara huku watu wanne wakiwa nje ya gari hilo ambapo Bageni aliwahoji nao wakaeleza kuwa ni wafanyakazi wa kampuni ya Bidco na kwamba kuna watu walikuwa kwenye gari wakiwa na bastola wamewapora pesa kiasi cha Sh. 5milioni.

"Baada ya kuwahoji, Afande Bageni alisogea pembeni akaongea na simu ya mkononi lakini sikuweza kusikia alichokuwa akikiongea. Alipomaliza kuongea mara niliona gari la Polisi Chuo Kikuu aina ya Toyota Pick-up ya bluu likija likiwa na askari na watu wengine wanne wakiwa wamekalishwa chini," alieleza Koplo Bakari.

Alidai kuwa katika gari hilo aliwafahamu askari wawili tu Koplo James na dereva, PC Noel, mshtakiwa wa nne katika kesi hiyo aliyeachiwa huru, na akaongeza kuwa gari hilo la polisi la kituo cha Chuo Kikuu lilifuatiwa na gari jingine dogo lenye rangi ya bluu likiendeshwa na askari na kwamba baada ya muda mfupi lilifika gari jingine dogo jeupe ambalo lilikuwa na watu watatu.

Aliwataja watu hao kuwa ni mkuu wa upelelezi wa polisi kituo cha Urafiki, ASP Ahmed Makelle (mshtakiwa wa tatu), Koplo Abineth Saro (mshtakiwa wa 10) na WP Jane Andrew (mshtakiwa tano).

Alidai ASP, Makelle na Koplo James walitoa maelezo mbele ya Bageni kuwa watu wale waliokuwa nao waliwakuta Sinza wakiwa na bastola na pesa kiasi cha Sh.5milioni.

Alidai kuwa dereva wa lile gari la Bidco alidai kuwa mmoja kati ya watu wale alihisi kuwa ni miongoni mwa waliowapora, lakini wafanyakazi wenzake hawakusema lolote.

Alidai baada ya maelezo hayo Bageni alienda pembeni kidogo akaongea na simu na kwamba wakati huo yeye na Koplo Frank walisogea kando walikokuwa wameegesha gari lao hivyo hakuweza kusikia kile Bageni alichokuwa akikiongea.

Alidai baada ya muda mfupi ilikuja gari moja aina ya Landrover Defender TZR 9559 ambayo ni ya Polisi Oysterbay na kuwataja waliokuwamo kuwa ni dereva ambaye ni Koplo Benedict, DC John, na Dc Abubakar.

Koplo Bakari aliendelea kueleza kuwa baadaye waliondoka huku nyuma wakifuatwa na ile Defender aliyoiona hadi Bageni alipoamuru gari isimame na kugeuza, huku wakiwa hawajui ndani ya ile Landrover Defender kulikuwa na akina nani.

Alidai baada ya kugeuza Bageni, Koplo Lema Koplo Saad na Frank nao walishuka yeye na yule askari wa Mbezi Luis walibaki kwenye gari. Alidai akiwa kwenye gari alifungua Redio Call yake akasikia taarifa za tukio la ujambazi Kijitonyama.

Alidai wakati akisikiliza ile Radio Call mara alisikia mlio wa risasi na akashuka na kusogea na kwamba alipofika karibu aliona mtu akishushwa kwenye Defender akalazwa chini na baadaye Koplo Saad akampiga risasi.

Alidai alipoangalia chini aliona watu wengine watatu nao wakiwa wamelala chini wakiwa wamepigwa risasi. Hata hivyo alidai kuwa hakusikia amri hiyo ya kuuawa kwa watu hao kwa kuwa alikuwa mbali kidogo kabla ya kusikia milio ya risasi zile.

Alidai baada ya hapo miili ya watu wale ilipandishwa kwenye Defender na kuondoka na wao waliondoka kwenye lile gari walilokwenda nalo.

Alidai kutokana na tukio hilo, yule askari wa Mbezi Luis aliogopa sana na alionekana kama kuchanganyikiwa na kwamba alikataa asirudishwe kituoni na badala yake aliomba wamwache njiani na wao wakaondoka moja kwa moja hadi kituo cha Polisi cha Urafiki.

Alidai wakiwa Urafiki alimuona Makelle akiwa amesimama nje na mtu mwingine mara akaingia kwenye gari lake akachukua mkoba mweusi akaingia ofisini na Bageni naye akashuka na kuingia katika ofisi ile.

Wakiwa pale Urafiki ndani ya gari Koplo Bakari aliieleza mahakama kuwa alimuuliza Koplo Saad kuwa wale aliowaua walikuwa ni akina nani naye akamjibu kuwa ni wale watu walioletwa na askari wa Chuo Kikuu.

Aliongeza kuwa alipomuuliza kuwa ni kwa nini wamewaua, alimjibu kuwa Afande Bageni ndiye aliyetoa amri ya kuwaua.

Alidai baada ya kutoka hapo walienda kituoni Bageni akawaagiza waendelee na doria ambapo walifanya hadi asubuhi alipoondoka kwenda nyumbani na kumwacha Koplo Saada akifungua jalada la kutumia silaha.

Alidai siku chache baadaye Bageni aliwaamuru waende katika msitu wa Bunju kulipua risasi kwa kuwa alikuwa akihitaji maganda ya risasi. Alidai alishauri waende kwenye uwanja wa shabaha, lakini wenzake wakasema kuwa ni lazima waende Bunju jambo ambalo walilitekeleza.

Aliieleza mahakama kuwa kabla ya ushahidi wake mahakamani jana, aliwahi kutoa maelezo kwenye Timu ya Polisi ya Upelelezi wa tukio hilo na kwenye Tume ya Jaji Kipenka, lakini akasema maelezo aliyoyatoa sehemu hizo yanatofautiana kwa kuwa maelezo kwa Tume ya Kipenka yalikuwa ni ya maelekezo namna ya kuongea.

Alisisitiza kuwa walielekezwa na Zombe namna ya kujieleza na kupewa vikaratasi ambavyo vilikuwa na maelezo ya kusema kwenye Tume huku akidai kuwa kikaratasi hicho alimkabidhi wakili wake.

Alidai maelekezo hayo yalikuwa kwamba tukio hilo lilitokea katika ukuta wa Posta na kwamba waliambiwa na Zombe kuwa huo ndio msimamo wa Jeshi la Polisi.

Aliieleza mahakama kuwa Bageni ni muongo kutokana na maelezo yake wakati akijitetea kuwa yeye Bakari na wenzake ndio waliomtaarifu kuwa tukio hilo lilitokea katika ukuta wa Posta Sinza.

Alipoulizwa na wakili wake kuwa anasemaje kuhusu mauaji hayo, Koplo Bakari alisema: "Mtukufu Jaji, mimi binafsi kwa mashtaka haya sihusiki kwa lolote. Kwanza sikuua, pili sikukaa na kupanga na mtu yeyote kuwaua watu wale na tatu sijatumia nguvu yangu wala akili yangu wala mdomo wangu kufanikisha mauaji hayo."

Alidai katika mazingira yale na kwa nafasi aliyokuwa naye mtu yeyote angeweza kuingia katika matatizo hayo kwa sababu hata yeye hakuwa akijua lolote lilokuwa likiendelea.

Katika kesi hiyo, Zombe na wenzake wanatuhumiwa kuwa Januari 14, 2006 waliwaua kwa makusudi wafanyabiashara wa madini kutoka Mahenge, Morogoro, Sabinus Chigumbi, maarufu kama Jongo, na ndugu yake Ephrahim Chigumbi, Mathias Lunkombe na dereva teksi wa Manzese Dar e Salaam
 
we mrembo bageni kafanyaje leo?
Mahakama ya rufaa imemuhukumu ASP Christopher Bageni kunyongwa hadi kufa kwa kuua wafanyabiashara watatu wa madini wa mahenge na dereva teksi mmoja katika msitu wa Pande. Aliyekuwa mkuu wa upelelezi mkoa wa Dar Abdallah Zombe na wengine wawili wameachiwa huru Kwa kukosekana ushahidi

14369005_578043415716682_1056748747_n.jpg
 
Kumbe polisi nao huwa wanaogopa kifo?kwa yeyote aliyeona hofu aliyokuwanayo Bageni kwenye taarifa hawezi kuamini kuwa polisi wanaweza kuendelea kuhujumu maisha ya raia. Lakini ,kila Mara ama utasikia polisi wameua,au wamesababisha ulemavu.Ushauri kwao ni kuwa ,kama mtuhumiwa hajatishia uhai wako,huna sababu ya kumuua.Heshimuni uhai,si ninyi wenye jukumu la kuutoa,bali mwenyezi Mungu mwenyewe.
 
Kumbe polisi nao huwa wanaogopa kifo?kwa yeyote aliyeona hofu aliyokuwanayo Bageni kwenye taarifa hawezi kuamini kuwa polisi wanaweza kuendelea kuhujumu maisha ya raia. Lakini ,kila Mara ama utasikia polisi wameua,au wamesababisha ulemavu.Ushauri kwao ni kuwa ,kama mtuhumiwa hajatishia uhai wako,huna sababu ya kumuua.Heshimuni uhai,si ninyi wenye jukumu la kuutoa,bali mwenyezi Mungu mwenyewe.
Kwenye issue yao kwani walikuwa wafukuza majambazi? Walikuwa wanaiba PESA za RAIA na hiyo michezo wanaifanya sana tu
 
Back
Top Bottom