Simulizi: Mwanafunzi Mchawi (A Wizard Student)

Babu wa Kambo

JF-Expert Member
May 2, 2016
559
808
1467436675859.jpg


RIWAYA: Mwanafunzi Mchawi ( A Wizard Student )
MTUNZI: ENEA FAIDY

SEHEMU YA KWANZA
Ilikuwa ni majira ya saa moja jioni ambapo mkuu wa while ya Mabango alikuwa ofisini kwake akiwa amechanganyikiwa sana kwani hali ya shule hiyo ilizidi kutisha sana hasa baada ya kutokea kwa vifo vya wanafunzi kumi na tano mfululizo ndani ya wiki moja tu. Tena vifo vya ghafla tu.

Mkuu wa shule mama Dayana Mbeshi alikuwa kwenye wakati mgumu sana kubaini chanzo cha tatizo lakini bado hakupata majibu.Mara ghafla mlango wa ofisi ukagongwa, akaingia mwalimu wa malezi wa shule hiyo akiwa na USO wa huzuni sana hali iliyomshtua sana mkuu wa shule

"vipi kulikoni?"
"hali mbaya mkuu.. wanafunzi wawili wamefariki tena bwenini" mwalimu wa malezi alizungumza kwa huzuni iliyochanganyika na hofu.
"what? mmh! sio bure.. kuna kitu hapa..!" alisikika mwalimu Mbeshi huku akiinamisha kichwa chake chini na kukiegemeza kwenye kiganja chake.

******
Wanafunzi wengi walionekana kuwa na hofu sana baada ya vifo visivotarajiwa kuzidi kutokea katika shule yao. Kila MTU aliwaza sana juu ya vifo vile huku kila mmoja akihisi zamu yake IPO karibu. Nyuso za huzuni ndizo zilizotawala kwa wanafunzi wote si wa kike wala wa kiume. Hakuna aliyetamani kulala wala kukaa mbali na kundi la watu kwani hofu iliwajaa mioyoni mwao, hawakuweza hata kusoma.

Lakini hali ilikuwa tofauti sana kwa binti Doreen ambaye alikuwa na wiki tu toka ahamie shuleni hapo. Alionekana kutoogopa chochote wala kuguswa na misiba ya wanafunzi wenzake. Kila Mara alionekana akiwa na furaha, hali hii iliwatisha wanafunzi wenzake na kuwafanya wawe na maswali mengi juu yake.

Doreen alikuwa msichana mrembo, sura yake nyembamba iliyopambwa na macho makubwa legevu, kope ndefu nyeusi tii, pua nyembamba iliyochongoka vyema na midomo mizuri yenye mvuto wa aina yake vilimfanya awe tishio kila kona kwani alikuwa ni mzuri kupindukia lakini Tabia ilikuwa tofauti na uzuri wake.

Wakati wanafunzi wengine wakiwalilia wenzao Doreen alikuwa amejitenga peke take nyuma ya bweni alilokuwa anakaa na kulikuwa na Giza totoro. Alikuwa uchi wa mnyama huku mikono yake ikiwa imeshikilia vitu fulani huku akitamka maneno ambayo aliyaelewa mwenyewe....

Itaendelea.......
 
SEHEMU YA PILI

Ilipoishia sehemu ya kwanza ( kama hukuisoma bofya hapa)
.....Wakati wanafunzi wengine wakiwalilia wenzao Doreen alikuwa amejitenga peke yake nyuma ya bweni alilokuwa anakaa na kulikuwa na Giza totoro. Alikuwa uchi wa mnyama huku mikono yake ikiwa imeshikilia vitu fulani huku akitamka maneno ambayo aliyaelewa mwenyewe....

Sehemu ya pili
...DOREEN aliendelea kuongea maneno aliyoyajua mwenyewe akiwa bado yupo uchi wa mnyama nyuma ya bweni alilokuwa anaishi.

Ghafla kipande kidogo cha karatasi nyeupe kikashuka mikononi mwake bila kuonekana kilikotokea. Doreen alicheka kwa sauti Kali ya kutisha sana kisha akalikazia macho karatasi lile, matone ya damu yaliangukia kwenye karatasi lile kutoka kwenye macho yaliyotisha sana ya Doreen kwani yalikuwa na rangi nyeusi halafu yakawa na umbile kama macho ya paka.

"Nenda mpaka ofisi ya mkuu wa shule ukamalize kazi." alisema Doreen akiwa amelinyanyua karatasi like kwa mkono wake wa kushoto. Karatasi likatoweka mkononi mwake na kupepea kwa nguvu kama vile limerushwa na upepo mkali.

Doreen alipomaliza kazi hiyo akasimama vizuri kama mwanajeshi aliyejipanga kwaajili ya gwaride kisha akainamisha kichwa chake chini akapotea eneo lile.

**********
Wanafunzi wa shule ya sekondari Mabango walikuwa wanahofu kubwa sana kila wakikaa walifikiria kifo tu. Usingizi haukuwajia hata Mara moja hivyo usiku waliketi makundi makundi wakizungumza hili na lile.

Wakati huo Dorice rafiki kipenzi wa Doreen alikuwa amejitenga pembeni akizungumza na mpenzi wake aitwaye Eddy, kijana mtanashati, mzuri, mpole na akili nyingi sana darasani.Wasichana wengi shuleni pale walitamani kuwa nae lakini bahati ilimwangukia Dorice pekee.

"Eddy unajua naogopa sana.." ilikuwa sauti ya Dorice akiwa amemkumbatia Eddy kwani kigiza kile cha usiku kiliwaficha wasionekane hivyo wakajiachia.
"unaogopa nini Dorice mpenzi wangu?"
"Naogopa kufa!" binti Huyo wa kinyaturu, mrembo aliyeumbika aliongea kwa sauti ya madeko sana.
"siku zote nakwambia Dorice kama Mungu alipanga huwezi kupangua , mwanadamu asikutishe kwa lolote. Huyu anayeua wenzake naye IPO Siku yake tu!"
"Najua baby Ila hali inatisha"
"Tuzidi kuomba Mungu mpenzi wangu kila unalofanya muombe Mungu."
"Nakupenda "
"Nakupenda pia"

Wakati Eddy na Dorice wakiendelea kuzungumza maneno hayo, Doreen alikuwa nyuma ya mti waliosimama hivyo alisikia kila kitu.

Roho ilimuuma sana kwani tangu alipohamia shuleni hapo alitokea kumpenda sana Eddy na alitamani awe mpenzi wake kwani ndio chaguo la moyo wake lakini Dorice alikuwa kikwazo. .

Suala hilo lilimuumiza Doreen ndani kwa ndani. Akainuka pale kwenye mti na kupita katikati yao, akamwita Dorice pembeni.
"Dorice.. mimi nawahi kulala Ila kesho unione!"
"nikuone?"
"ndio kwani hujaelewa?" alijibu Doreen kwa ukali jambo lililomwachia maswali mengi Dorice. Lakini Doreen hakujali kitu akaondoka zake Ila moyoni alipanga jambo zito la kumfanyia Dorice siku ya kesho yake.

*********
Ilikuwa asubuhi tulivu sana majira ya saa kumi na mbili na nusu asubuhi ambapo mwalimu Dayana Mbeshi aliwahi ofisini kwake kama ilivyokuwa kawaida yake.

Majengo ya ofisi yalimkaribisha kwa shangwe naye akaitikia ukaribisho huo kwa kufungua ofisi yake kisha akasogeza mapazia ya dirishani ili kuruhusu mwangaza wa jua changa uweze kupenyeza vizuri.

Baada ya kukamilisha yote hayo Madam Mbeshi akasogeza kiti chake karibu na meza kisha akaketi halafu akaanza kusogeza vitu vilivyokuwepo mezani pale lakini ghafla akakutana na karatasi chafuchafu mezani kwake lakini ilikuwa na maandishi.

Akashtuka kidogo halafu akaichukua ili aisome vizuri. Mwalimu Mbeshi hakutaka kuamini kile alichokiona, akataharuki kwa hofu na mshangao...............

Itaendelea....
 
SEHEMU YA TATU

Ilipoishia sehemu ya pili ( kama hukuisoma bofya hapa)
...Baada ya kukamilisha yote hayo Madam Mbeshi akasogeza kiti chake karibu na meza kisha akaketi halafu akaanza kusogeza vitu vilivyokuwepo mezani pale lakini ghafla akakutana na karatasi chafuchafu mezani kwake lakini ilikuwa na maandishi.

Akashtuka kidogo halafu akaichukua ili aisome vizuri. Mwalimu Mbeshi hakutaka kuamini kile alichokiona, akataharuki kwa hofu na mshangao....

Sehemu ya tatu
...Mwalimu Mbeshi aliposoma ujumbe ule kutoka kwenye ile karatasi chafuchafu alizidi kuchanganyikiwa sana, mapigo ya moyo yalimwenda kasi kama gari iliyokata breki ikiwa mlimani. akarudia tena na tena ujumbe ule uliosomeka "POLE SANA MWALIMU KWA MASWAHIBU YALIYOKUKUTA SHULENI KWAKO.. MIMI DOREEN MBWANA NIMEFANYA YOTE HAYO! PIA MUDA WA KIFO CHAKO U KARIBU KWANI UMESOMA UJUMBE WA MWANAFUNZI MCHAWI"

Jasho jembamba lilimtiririka mwanamama yule bila kuelewa afanye nini. Akataka kulitupa chini karatasi lile lakini ghafla akaona karatasi lile limebadilika ghafla, sio karatasi tena bali kitu kama ngozi ya binadamu iliyooza sana huku ikitoa harufu mbaya ikiwa imeambatana na funza wengi wakitembea tembea.

Madam Mbeshi alihisi kinyaa sana huku woga ukiwa umemtawala kupita kiasi kwani katika maisha yake hakuwahi kushuhudia mauzauza ya namna ile hats Mara moja. Alitamani akimbie lakini miguu ilikuwa imeganda kama msumari kwenye sumaku.

Mbeshi alihangaika sana na wale funza mkononi mwake kwani walizidi kumpanda mwilini kwa kasi na kumtia ghasia. Machozi yalimtoka mwalimu mbeshi lakini kila tone lililodondoka lilikuwa damu.

Hofu ikamzidia sana, hakuwa na tumaini la kusalimika tena kwani kwa hatua aliyofikia ilitisha sana. Na yote hayo yalisababishwa na binti Doreen Mbwana.

Ghafla mlango wa ofisi ya mwalimu Mbeshi uligongwa lakini Mbeshi hakuwa hata na uwezo wa kuzungumza chochote. Mlango uligongwa sana lakini Mbeshi hakuweza kuufungua ingawa alitamani yule aliyegonga mlango aingie ili iwe ahueni kwake lakini ilishindikana.

Kila aliponyanyua kinywa ulimi ulikuwa mzito na hakuweza kuzungumza chochote ikambidi atulie kimya akiugulia mateso yake yalimzonga ndani ya muda mfupi tu.

"Masikini Mimi inamaana ndo nakufa? masikini familia yangu ambayo Mimi ndio tegemezi! ee Mungu nisaidie!" aliwaza Mbeshi huku machozi ya damu yakizidi kutiririka.

*******
Walimu hawakujua lolote linaloendelea ofisini kwa mkuu wa shule hivyo waliendelea na ratiba za shule kama kawaida.
Wanafunzi walienda mstarini, wakajipanga vizuri kwa mistari kuanzia kidato cha kwanza hadi cha NNE.

Mwalimu John ambaye alikuwa zamu kwa wiki ile alikuwa amesimama mbele kwaajili ya matangazo lakini ghafla akasikia wanafunzi wachache wakimzomea.

Moyo wake ukamlipuka akautazama msitu ule wa watu lakini macho yake yakatua moja kwa moja kwa wanafunzi wa kidato cha NNE, akamwona Dorice na nyuma yake alikuwa amesimama Doreen akiwa anacheka sana kwa sauti ya dharau na kiburi. Hasira za mwalimu John zikampanda akaumanisha meno yake kwa ghadhabu

"Doreen! hebu njoo mbele haraka sana!" alisema mwalimu John kwa sauti kali iliyojaa ghadhabu lakini bila aibu Doreen aliachia sonyo Kali iliyowafanya wanafunzi wote wamgeukie yeye na kumwangalia kwa mshangao.
"We mtoto! unanisonya Mimi? una adabu kweli?"
"Kwanini nisikudharau wakati we mwenyewe umejidharau?" alisema Doreen kwa kujiamini sana.
"Ati nini?"alishangaa mwalim John kwani hakutegemea kama Doreen angekuwa jeuri kiasi kile.
"We unavokuja kazini hivo unategemea nini?"
"Vipi" alishtuka Mwalimu John.
"Unakuja kazini bila kuvaa suruali ili iweje!?"
"Una wazimu wewe nani hajavaa suruali?"

"Jiangalie huko chini kama umevaa suruali;" alisema Doreen na kumfanya Mwalimu John ajiangalie vizuri akagundua kweli alikuwa hajavaa suruali.

Alishtuka kupita kiasi wanafunzi wote wakamtazama Mwalimu John kwa mshangao kwani kweli alikuwa hajavaa suruali. Baadhi ya wanafunzi walicheka, lakini baadhi walimhuzunikia wakiamini kuna mchezo kachezewa na si bure.

Mwalimu John akakimbia mstarini pale Kama mwendawazimu na kwenda ofisini lakini kila alipojaribu kuvuta kumbukumbu zake alikumbuka kuwa alipotoka nyumbani alikuwa amevaa suruali tena suruali yake mpya ya kadeti.

"Sasa imeenda wapi?? mnh hapana kuna MTU kanichezea lazima nimweendee Malawi hata Nigeria ntafika Ila siwezi kumwacha" aliwaza Mwalimu John na wakati huo waiimu wenzake waliamua kwenda nyumbani na kumletea suruali nyingine ili aweze kuondoka Nayo.

********
Baada ya wanafunzi kuingia darasani kwao. Doreen aliamua kumuita Dorice nje kwani alikuwa na mazungumzo nae mazito sana.Dorice alionekana kuogopa kwani wito ule haukuwa wa kawaida, akasimama kwa hofu akimtazama Doreen

"vipi mbona unaogopa, unaogopa nini?" alisema Doreen.
"siogopi kitu!"alijibu Dorice
"basi nisogelee"
Dorice akamsogelea Doreen kwa hatua chache.
"Jana ulikuwa na nani pale kwenye mti usiku?" aliuliza Doreen huku akiuchezesha mguu wake wa kulia chini na mkono mmoja akiwa kaushika kiunoni.
"hukuniona au?" aliuliza Dorice kwa mshangao.
"jibu swali!"
"OK! nilikuwa na Eddy"
"nani yako Eddy?"
"Doreen unanitisha ujue?"
"kha! nakutisha nina mapembe hapa? nijibu swali langu"
"Eddy mpenzi wangu!"
"nimekupata sasa... tangu lini Eddy mpenzi wako hujui kama ni mume wangu mtarajiwa?"
"Ati nini....... Eddy ni. .."

Itaendelea ......
 
SEHEMU YA NNE

Ilipoishia sehemu ya tatu ( kama hukuisoma bofya hapa)
Dorice akamsogelea Doreen kwa hatua chache.
"Jana ulikuwa na nani pale kwenye mti usiku?" aliuliza Doreen huku akiuchezesha mguu wake wa kulia chini na mkono mmoja akiwa kaushika kiunoni.
"hukuniona au?" aliuliza Dorice kwa mshangao.
"jibu swali!"
"OK! nilikuwa na Eddy"
"nani yako Eddy?"
"Doreen unanitisha ujue?"
"kha! nakutisha nina mapembe hapa? nijibu swali langu"
"Eddy mpenzi wangu!"
"nimekupata sasa... tangu lini Eddy mpenzi wako hujui kama ni mume wangu mtarajiwa?"
"Ati nini....... Eddy ni. .."
Sehemu ya nne
.... DORICE alishtuka sana kusikia Eddy ni mume mtarajiwa wa Doreen hakutaka kuyaamini maneno ya Doreen hata kidogo.
"hivi we Doreen umechanganyikiwa au upo timamu?" Dorice aliropoka kwa hasira.

" nikuulize wewe, hivi upo timamu au mwendawazimu unavomng'ang'ania mpenzi wangu Eddy? mpaka watu wanakushangaa! inaniuma sana Dorice usione nimekukaushia!" Alisema Doreen kwa msisitizo wa hali ya juu. Maneno ambayo yalizidi kumuumiza Dorice mpaka machozi yakaanza kumlengalenga machoni mwake. Alimtazama Doreen kwa hasira huku akiumanisha meno yake kwa ghadhabu, moyoni alitamani kumuadhibu vikali Doreen kwa kutaka kulitia DOA penzi lake na Eddy lakini hakuwa na uwezo huo.

"Ama kweli kikulacho ki nguoni mwako! sitaki kuamini kama rafiki yangu kipenzi Leo unageuka adui yangu!"alisema Dorice huku akipiga hatua na kutaka kuondoka mbele ya mbaya wake. Lakini ghafla Doreen akamvuta shati na kumrudisha pale alipokuwa amesimama.

"we vipi? hebu niache niondoke?"
"nitakuachaje sasa wakati unaniharibia penzi langu na Eddy?" alisema Doreen kwa kujiamini sana huku akibetua midomo yake kwa dharau utadhani Eddy ni mpenzi wake kweli kumbe hakuna lolote ni tamaa na wivu vinavyomsumbua.

"umefanikiwa kuniumiza moyo wangu Doreen mpaka najuta kukufahamu.... haya Fanya lolote utakalo tena ili kunyang'anya haki yangu ya mapenzi... do it!" alisema Dorice kwa kwikwi kwani alishindwa kuzuia kilio chake kutokana na maumivu makali aliyoyapata moyoni mwake kwani maneno ya Doreen yalikuwa kama mkuki wenye sumu katikati ya moyo wake.

"hata Mimi najuta kukutana na mwanaharamu wewe, Kwa usalama wako achana na Eddy... sijui unanielewa?"

Dorice hakusema chochote zaidi ya kumkazia macho ya hasira Doreen, bila kujua kuwa kutazamana na Doreen kwa wakati ule ilikuwa ni kujikaanga kwa mafuta yake mwenyewe kwani Doreen aliitumia nafasi ile vizuri sana.

Alijibadilisha macho yakawa ya kutisha sana kisha kila alipomtazama Dorice machoni alimhamishia vitu Fulani visivyoeleweka, kisha baada ya hapo Doreen alimsogelea Dorice na kumzodoa lakini haikuwa kumzodoa kwa kawaida Bali alimpaka vitu kama kamasi USO mzima na kumfanya Dorice atie kinyaa sana bila yeye mwenyewe kujitambua.

"hebu niondokee hapa mpuuzi wewe na ushukuru Mungu sijakufanya kitu kibaya" alisema Doreen baada ya kuhakikisha amekamilisha kazi yake aliyokusudia kwani sio siri Doreen alipania kumpata Eddy kwa vyovyote vile.

Dorice alitembea taratibu na kumfuata Eddy darasani huku akiendelea kulia.

**********
Walimu wote walikuwa hawaelewi mambo yanayoendelea shuleni pale, kwani kila siku liliibuka jipya. Suala la mwalimu John kuvuliwa suruali kwa mazingira ya kutatanisha lilizidi kuwapa maswali mengi walimu wa while ya sekondari mabango mpaka wakaogopa hata kuingia madarasani, kwani walihisi wanaweza kudhalilishwa kama ilivyomtokea mwalimu John.

Mbali na suala hilo pia suala la mkuu wa shule kujifungia ofisini liliwapa mtihani mkubwa kwani haikuwa kawaida yake.
"jamani nimeenda ofisi ya mkuu wa shule karibia Mara tatu nimegonga sana lakini hakutoa jibu hata nilipojaribu kusukuma mlango inaonekana amefunga kwa ndani!" alisema makamu mkuu wa shule baada ya kuingia staff.
"hata Mimi nimeenda pale ofisini lakini palikuwa kimya sana ingawa mlango unaonekana umefunguliwa kwa nje... nimepiga simu haipokelewi" alisema mtaaluma.
kiukweli iliibuka sintofahamu miongoni mwa walimu wote waliingiwa na hofu kubwa.
" mmh! hii sio kawaida ya mkuu kabisa inabidi tufanye jambo"
"Mimi naona tuvunje mlango tu" alipendekeza mwalimu wa nidhamu.

walimu wote walikubaliana kuvunja mlango wa ofisi ya mkuu wa shule. wakaebda moja kwa moja mpaka ofisini kwa mkuu na kuvunja mlango kisha wakaingia.. walichokutana nacho kila MTU hakuamini , walibaki midomo wazi huku machozi yakiwadondoka kama chemichemi katikati ya mlima.

Mwili wa mwalimu Mbeshi ulikuwa umeoza vibaya sana funza walitapakaa kila mahali wakisindikizwa na harufu mbaya iliyojaa ofisini mle. hakuwa mbeshi tena mwanamama aliyejipenda na kunukia marashi muda wote Bali jina lilibadilika na kuwa maiti.

Walimu walitulia kimya kwa muda wa dakika mbili nzima Vila kusema chochote lakini macho ya makamu mkuu wa shule yalitua mpaka mezani kwa mbeshi ambapo aliona karatasi ndogo nyeupe yenye ujumbe. Akaisogelea na kuichukua, kisha akaanza kuisoma. Ghafla alishtuka sana baada ya kusoma ujumbe ule "UNAFATA WEWE ULIYESOMA KARATASI HII."

Makamu yule kwa woga na hamaki akaropoka " Mimi sijasoma chochote... tusisingiziane hapa!" alisema huku akificha macho yake na kumkabidhi mtaaluma karatasi ile kwani walimu wote hawakujua kilichotokea hivyo wakatamani wasome ujumbe uliokuwemo mle.

********
Dorice alimtuma MTU amwitie Eddy darasani lakini mwanafunzi yule akakataa. hivyo Doreen aliamua kwenda mwenyewe darasani mle.

Darasa lilikuwa limetulia kimya sana, Dorice akafungua mlango na kuingia lakini ghafla alipoingia wanafunzi wote darasani mle wakacheka kicheko kikali sana kilichomtia hofu sana Dorice. lakini akajikaza kisabuni licha ya kwamba alijua wanamcheka yeye, akamsogelea Eddy na kumtaka watoke nje lakini Dorice aligundua mabadiliko makubwa sana kwa Eddy Ila hakuuliza chochote wakatoka nje. wanafunzi wakacheka tena kwa dharau kitendo kilichomuumiza sana Dorice.

"hivi we demu unajisoma??" alisema Eddy kwa ukali. maneno hayo yalimshtua sana Dorice.
"Eddy! sijakuelewa!"
" unajisoma kweli? hivi kwanza unajua majamaa wanakucheka kwa sababu gani?" maneno ya Eddy yalimfanya Dorice ataharuki.....

Itaendelea ......
 
SEHEMU YA TANO

Ilipoishia sehemu ya Nne ( kama hukuisoma bofya hapa)
"hivi we demu unajisoma??" alisema Eddy kwa ukali. maneno hayo yalimshtua sana Dorice.
"Eddy! sijakuelewa!"
" unajisoma kweli? hivi kwanza unajua majamaa wanakucheka kwa sababu gani?" maneno ya Eddy yalimfanya Dorice .....

SEHEMU YA 5
...DORICE alimtazama Eddy kwa mshangao wa hali ya juu kwani tangu walipoanza mahusiano hakuwahi kumuona akiwa na chuki dhidi yake kwa kiasi kile. Dorice alikosa ujasiri wa kuzungumza chochote kwa wakati ule kwani alihisi viungo vyake vyote vinakosa nguvu. Akabaki ameduwaa kama zuzu mbele ya Eddy.
"we Dorice nimekuuliza unajua wanakucheka nini darasani?" aliuliza Eddy kwa ukali.
"Sijui" alijibu Dorice kwa huzuni
" Sasa kama hujui wanakucheka jinsi ulivyomchafu, hebu jiangalie hizo kamasi ulizojipaka kama mtoto asiyejua hata kutembea, pili hiyo yako chafu, na tatu...." kabla Eddy hajamaliza Dorice alishtuka sana kusikia vile kwani alipofika darasani asubuhi alikuwa msafi kama ilivyokuwa kawaida yake.
"Eddy umesemaje?!" aliuliza Dorice kwa mshangao. Na wakati huo Doreen alikuwa alikuwa amejificha nyuma ya darasa karibu na waliposimama akina Dorice, na aliweza kusikia kila kitu kinachozungumzwa. Alisikiliza kwa umakini sana huku akiyafurahia majibu ya Eddy Kwa Dorice.
" Hujanisikia? tena ukome kunifuatilia, usahau kama nilishakuwa mpenzi wako , unifute akilini mwako, sikupendi?" alisema Eddy akiwa amenuna kama aliyekula ndimu.
"unasemaje Eddy! hebu rudia nisikie"
"Sikutaki , sikupendi na sikuhitaji!" alisema Eddy huku akiondoka
"Eddy! Eddy! nimekukosea nini mpenzi wangu?"
"Achana na Mimi Dorice! huna hadhi ya kuwa na mimi , demu mwenyewe huna hata mvuto!" alisema Eddy na kusonya. Kisha akaenda zake darasani.
Alimwacha Dorice kwenye bahari ya simanzi na machozi yasiyoweza kuzuilika. Alilia kwa uchungu kama MTU aliyefiwa na MTU muhimu, lakini kilio hicho cha Dorice kilikuwa shangwe na furaha kwa Doreen. Alijiona kama mshindi kwa kufanikiwa kulivuruga penzi la Eddy na Dorice bila hata huruma kwani wawili hao walipendana sana na walikuwa na malengo makubwa katika maisha ikiwa ni pamoja na kufunga ndoa pindi watakapotimiza malengo yao.

Doreen alicheka kwa dharau kisha akaondoka zake na kwenda darasani, ambapo alimfuata Eddy pale alipokuwa amekaa.
Eddy alimkaribisha Doreen kwa tabasamu mwanana na macho ya matamanio.
"Mambo Eddy handsome" alisema Doreen kwa sauti ya utulivu iliyomkuna vyema Eddy hadi akakosa ujasiri wa kuongea.
"Eddy mbona huitikii salam yangu?"
"Niko poa... vipi wewe mtoto mzuri"
"mh! nani mzuri Eddy?" Doreen alijifanya kuona aibu. Na kwakuwa darasa lilikuwa na kelele nyingi walipata mwanya wa kuzungumza zaidi.
"mzuri wewe hapo mtoto wa kitanga!"
"Acha hizo Eddy! mzuri no Dorice!"
"Eh! usinitajie huo uchafu"
"mh! uchafu tena? "
"ndio... Doreen bora umekuja hapa kukaa.. nina kitu muhimu sana nataka nikwambie"
"mh! kitu gani Eddy?" aliuliza Doreen huku akirembua jicho lake kubwa zuri kwa madaha.

***
Karatasi lile lenye ujumbe mzito lilitua mikononi mwa mtaaluma wa shule, kwa haraka macho yake yalitua kwenye maandishi yaliyoandikwa kwenye karatasi ile lakini maandishi yalikuwa tofauti na yale aliyoyasoma makamu mkuu wa shule, yalisomeka hivi "TOENI HUO MZOGA LA SIVYO MTAISHA"
Mwalimu yule wa taaluma aliogopa sana akashindwa kuongea akampasia karatasi mwalimu wa nidhamu lakini alipochukua tu ujumbe ulibadilika ukasomeka hivi "WEWE UTAMFUATA MAKAMU WA SHULE MAANA ULINITESA"

"ati nin? nilikutesa wapi Mimi? hata sio Mimi ujumbe haunihusu!" mwalimu wa nidhamu aliongea kwa kuchanganyikiwa na kwa hofu kubwa. Akampasia karatasi mwalimu mwingine lakini pindi anapompa mwalimu yule karatasi ujumbe ulibadilika tena "MNANISUMBUA! UKIMPA MWINGINE UJUMBE HUU UNAKUFA MUDA HUU.. NA UKINIWEKA CHINI UTAONA CHA MTEMA KUNI"
Mwalimu yule aliyefahamika kwa jina la mwalimu Jason alivuta pumzi ndefu sana huku mapigo ya moyo yakibadili mwendokasi na kwenda haraka sana. Akabaki ameshikilia karatasi lile mkononi mwake bila kuelewa cha kufanya .
WAlimu waliokuwa wanasubiri kusoma karatasi lile walimfokea mwalimu Jason kwa kuendelea kulishikilia karatasi lile kabla ya wao kulisoma.
"we vipi tupe na sisi tusome!"
"shukuru hamjasoma"
"Nini? usituzingue tupe hilo karatasi tusome bhana"
walimu walizidi kung'ang'ania karatasi lile lakini mwalimu Jason hakuwa tayari kuwapa ili kulinda uhai wake. Mwalimu Jasoni akaangalia upenyo ili aweze kutoka ofisini mle kisha akatoka mbio akiwa ameshikilia karatasi lake.

Mwalimu wa taaluma akaangalia pale chini ulipokuwepo mzoga wa Mbeshi akaona jinsi funza wallivyokuwa wakitapakaa kwa kasi.
"Jamani tumtoeni huyu tutakufa wote"alisema mtaaluma.
wakati huo makamu mkuu wa shule alikuwa akitokwa na haja ndogo kutokana na hofu ya kifo kama alivyoambiwa kwenye ujumbe.

***

Mwalimu John alionekana mwenye sana pindi aliporudi nyumbani kutokana na kitendo cha kudhalilika shuleni. Mkewe aliingia sebuleni na kumsogelea mwalimu John
"mume wangu vipi?"
"kwani vipi mke wangu?"
"nakuona hauna raha kulikoni?"
"nipo sawa... Ila... nina safari..!"
"kha! safari ya wapi tena mume wangu?"
"Naenda Malawi... Leo!"
"Malawi? kufanya nini mume wangu?"
"usijali kuna kazi muhimu naenda kufanya.."
"mbona ghafla sana? halafu mbona umevaa suruali ambayo si yako? au umefumaniwa?"
Aliuliza mke wa mwalimu john huku akimkagua mume wake kwa kupitisha macho kuanzia juu had I chin... ...

Itaendelea ......
 
SEHEMU YA SITA

IIlipoishia sehemu ya Tano ( kama hukuisoma bofya hapa).

Eddy alimwacha Dorice Solemba, akilia na moyo nje ya darasa. Na alipoingia darasani Eddy alifuatwa na Doreen kwenye kiti chake, na alitaka kumwambia kitu muhimu....

Endelea...
Doreen alizidi kujilegeza sana kwa Eddy ili amteke kimawazo na kiakili sawasawa. Alirembua macho kama aliyekula kungu huku akimtazama Eddy.. Hakika kwa urembo aliokuwa nao Doreen na vituko alivofanya alizidi kuziteka hisia za Eddy haswa.

Mtoto wa kiume alijikuta anaishiwa pozi, uvumilivu ukamshinda akajikuta anakohoa kidogo ili asafishe koo na kuweza kusema la moyoni.

"Eddy!" Doreen aliita kwa sauti ya mvuto sana.
"Naam"
"niambie basi.."
"ah!.. Doreen kama nilivosema awali wewe in mzuri sana hivyo basi .... nataka uwe mpenzi wangu.. please! naomba unielewe!" Eddy aliongea kwa sauti ya chini ili majirani wasiweze kusikia.
"Eddy! we ni shemeji yangu siwezi kumsaliti rafiki yangu Dorice!" Doreen alijifanya kukataa ingawa moyoni mwake alifurahia ushindi wa kumpata Eddy ilhali warembo wore shuleni pale waliikosa nafasi ile isipokuwa Dorice.
"Doreen! plz naomba nikubalie nakupenda sana "
"Na Dorice je?"
"habari za Dorice achana nazo me nimeachana nae, nakupenda wewe"
"mi sitaki Eddy!" sauti aliyoitoa Doreen ilionesha kabisa alikuwa anataka Ila alivunga tu.
"Nikubalie Dori.. nakupenda Doreen.. usinitese!" Eddy alisema huku machozi yakimlengalenga kwani hakutaka kumkosa Doreen. Ama kweli dawa za Doreen alizotafuna kabla ya kumfuata Eddy zilifanya kazi vizuri sana.
"Okey! nakubali kuwa na wewe!"
"Oh my God kweli Doreen unanipenda? asante sana!" Eddy aliachia tabasamu mwanana na alitamani hata kumkumbatia Ila aliogopa kufanya vile kwani walikuwa darasani.
"Nakupenda Eddy Ila kuna sharti moja muhimu inabidi ufate ili uwe na Mimi..."
"sharti gani tena?" Eddy alishtuka
"upo tayari?"
"ehm.. ah ndio coz I love u.. ntafanya"
"good.. nafurahi sana"
"Niambie basi mpenzi.." alisema Eddy akitabasamu.
"usijali nitakuambia baadae..."
Alisema Doreen huku akiinuka kitini na kuondoka zake. Eddy alikuwa na furaha sana hakuweza hata kusoma zaidi ya kumfikiria Doreen na kila Mara aliachia tabasamu.

Ilikuwa ni mchana majira ya SAA nane na nusu ambapo kengele iligongwa katika shule ya sekondari Mabango ambapo iliwaataarifu wanafunzi wote kuwa muda wa vipindi umekwisha na ni muda wa kupata chakula cha mchana.

Lakini haikuwa hivyo kwani wanafunzi walitakiwa waende mstarini ambapo Habari za kusikitisha sana zilipenya mioyoni mwa wanafunzi wote wa shule ile.

"Mkuu wa shule mama Dayana Mbeshi ameaga dunia Leo asubuhi kwa kifo cha ghafla kilichompata ofisini kwake..pia walimu wawili wana hali mbaya na wamefikishwa hospitalini kwa matibabu!" ilikuwa sauti ya masikitiko sana kutoka kwa Mwalimu Gallus iliyoonesha simanzi nzito sana aliyokuwa nayo.

Mwalimu huyo alishusha pumzi ndefu sana na kuendelea " Maombi yenu in muhimu sana kwa walimu wenu ambao wapo hospitali... na..." mwalimu Gallus alishindwa kuendelea kuzungumza kwani machozi yalikosa adabu yakashuka kwa kasi hivyo akaamua kuondoka eneo lile.

Wanafunzi wote waliondoka lakini mwishoni alibaki Eddy alitembea taratibu huku picha ya msichana katili anayejifanya mwema, Doreen ikizidi kumjia akilini mwake na kumfanya aisahau kabisa njaa aliokuwa nayo. Njia nzima alkuwa akizungumza peke yake kama mwehu mpaka alipofika bwenini.

"Ah Doreen! ni msichana mzuri sana! siamini kama amekuwa wangu..!" Aliwaza Eddy huku akiachia tabasamu kisha akabadili nguo na kujitupa kitandani.

Alionekana kutoguswa kabisa na msiba wa mwalimu mkuu kwani tayari alikuwa amechanganyikiwa na Doreen. Hakumkumbuka tena Dorice ambaye kila Mara alimuahidi kutomsaliti kwa namna yoyote.

*******
Dorice alikuwa amekaa kitandani kwake huku machozi yakitiririka mashavuni mwake. Weupe wa ngozi ya USO wake ulibadilika na kuwa mwekundu kutokana na kulia kwa muda mrefu, hakuamini kama Eddy angemtenda kiasi kiasi kwani siku zote aliamini Eddy ndiye MTU pekee wa kumuamini, aliamini kama Eddy ndio furaha pekee ya moyo wake iweje Leo amtupe kama taka ya msafiri ndani ya basi pale airushapo kupitia dirisha bila kujua itakapotua? Alimuona Eddy kama mnyama katili asiyekuwa na moyo wa utu.

Marafiki zake Dorice walizidi kumbembeleza atulie bila mafanikio yoyote.

"Kwa alichonifanyia Doreen, siwezi kumwacha kilahisi tu... lazima nimfanyie kitu..." Alijiapiza Dorice

" Ni lazima atajuta mpaka kifo chake... hatokaa anisahau kwa ntakachomfanyia.. lazima aelewe kuwa Mimi ni Dorice mtoto wa Kinyaturu sinyang'anywi tonge mdomoni kwa urahisi!" Alizidi kujiapiza Dorice akiwa amejifunika blanket mpaka usoni. Lakini baada ya muda mfupi Dorice aliinuka kitandani pale na kujifuta machozi kisha akapiga hatua za haraka kuelekea nje.

********
Mke wa Mwalimu John amuijia Juu Mumewe akitaka kujua suruali ile imetoka wapi. Lakini mwalimu John hakutaka kuweka wazi kile kilichomkumba shuleni.. alitaka iwe siri yake mpaka atakapofanikiwa kwenda Malawi kutafuta waganga wakumroga aliyemfanyia uchuro.

"John! umefumaniwa huko sio?" alifoka mke wa John
"usipaniki mke wangu tulia.. sijafumaniwa mim!" alijitetea mwalimu John bila mafanikio na wakati huo tayari mkewe alishaanza kumtandika makofi mumewe na alipoona haitoshi akanyanyua upawa na kumtandika nao Mwalimu John kichwani.

Ghafla John akanyong'onyea na kutulia kimya kitini bila kutikisika..
"John! John!" aliita mke wa mwlm John bila mafanikio John hakuweza kuitikia.
"Mime wangu... John wangu" alizidi kuita lakinu John alikuwa kimya, mkewe alichanganyikiwa sana.............

Itaendelea ......
 
SEHEMU YA SABA

Ilipoishia sehemu ya Sita ( kama hukuisoma bofya hapa).

.....DOREEN alimkubalia Eddy kuwa mpenzi wake lakini alimweleza kuwa kuna sharti ambalo Eddy lazima alifuate ndipo awe nae.Dorice hakutaka kukubali kirahisi kumwachia Doreen kuwa na Eddy hivyo alipanga kulipiza ili Doreen asije kumsahau.Mwalimu John alipigwa na mkewe mpaka akapoteza fahamu ambapo mkewe alichanganyikiwa sana baada ya kumwamsha bila mafanikio....

Endelea.....
...MWALIMU JOHN alikuwa kimya pale kitini akiwa hana fahamu yoyote, mkewe akazidi kuchanganyikiwa sana kwani alihisi tayari mumewe ameaga dunia.

"Jamani mume wangu amka bado nakupenda! Nisamehe Mimi John wangu!" Alizidi kulia mke wa mwalimu John kwa huzuni na majuto makali. Alijiona mjinga sana kwa kujichukulia maamuzi mkononi bila hata kumdadisi vizuri.

Simanzi ilimtanda mwanamke yule bila kujua la kufanya, machozi yalichuruzika kama mito miwili usoni kwake kwani ndio kwanza ndoa yao ilikuwa changa kabisa tangu waoane miezi mitano iliyopita sasa iweje John aage mapema kiasi hicho? Mkewe aliufikiria upweke ambao angekabiliana nao Siku za usoni. Huzuni ikamzidia.

Mwalimu John akiwa bado ameyafumba macho yake akahisi yumo kwenye usingizi mzito sana lakini alikisikia vyema kilio cha mkewe.

Alitamani aamke ili amtulize mkewe lakini mwili ulikuwa kama umegandishwa na sumaku. Hakuweza hata kutikisika, ghafla akahisi upepo mkali sana ndani ya nyumba yake alipotazama ukutani akakutana na sura ya kutisha sana.

Huku ikifuka moshi mdomoni, macho mekundu kama damu na kichwani yalichomoza mapembe mawili marefu. John aliogogopa sana kwani tangu azaliwe hakuwahi kukutana na kiumbe wa ajabu na wakutisha namna ile. Alitamani azinduke usingizini lakini hakuweza, hivyo alibaki akitetemeka.

Ghafla kiumbe yule akabadilika na kuwa sura ya msichana mrembo sana. Mwalimu John akabaki kinywa wazi akistaajabu ya Mussa. Alipotazama vizuri aligundua ni Doreen , akashtuka sana.Doreen alimtazama mwalimu John kwa dharau sana kisha akaachia kicheko kikali sana.

"Mimi ni Doreen Mbwana! Daima usinichezee maana sichezewi kirahisi.. Unataka kuniendea Malawi we? Hahahahah umechelewa sana John, nina nguvu kuliko unavofikiria"

Doreen akamsogelea John, na kutoa kucha zake ndefu nyembamba kama msumari kisha akamgusa mdomo John."Umeniita Nimekuja! Sasa utaipata fresh...! Hahahahahahahhh" alisema Doreen kisha akatoweka . John alihema kwa nguvu sana huku woga ukiwa umemtawala kupita kiasi kwani maneno ya Doreen yalimtisha.

Mke wa Mwalimu John alizidi kulia baada ya kuona mumewe haamki kwa muda mrefu. Kelele Za kilio chake ziliwafikia majirani ambao walikuja kwa wingi kushuhudia kilichotokea. Bila hodi majirani hao walitiririka kama utitiri nyumbani kwa mwalimu John.
"Kuna nini jirani?" Aliuliza Mzee mmoja aliyejulikana kama Makorokocho.
"Hata sielewi mume wangu kapatwa na nini jamani...sielewi mimi" mke wa John alizidisha kilio.
"Kwani imekuaje?"
"Msogelee umwangalie maana mimi sielewi.. Namwita haamki.."
"Mh!" Aliguna Mzee Makorokocho huku akimsogelea mwalimu John.
Akamtikisatikisa John akamwita lakini John hakuitika, Ingawa John alisikia kila kitu kinachoendelea ila hakuweza kuamka.
"Mh! Mama pole sana huyu tayari ametangulia mbele za haki..."
"Ati mini?"
"Ndo ivo mama chamsingi tuwapigie ndugu zake simu, taratibu za mazishi zifanywe!"
"Hapana! Mume wangu hajafa! Iweje John afe mbele yangu.. Aaah we Mungu we!!" Mke wa Mwalimu John alilia kwa uchungu sana.

Ndugu wa mwalimu John wakapigiwa simu kupewa taarifa za msiba, taratibu za mazishi zikaanza kufanywa.

*******
Dorice alipotoka bwenini kwao akaongoza moja kwa moja mpaka bweni la Mapambano ambalo ndilo alilokuwa akiishi Eddy, alitembea kama mwendawazimu mpaka alipotia timu katika bweni hill bila kujali ni bweni la wavulana pekee. Dorice aliongoza mpaka kitanda cha Eddy ambapo alimkuta Eddy akiwa na wenzake watatu. Na alikuwa akiwasimulia juu ya uhusiano wake mpya na Doreen.

"Habari zenu" alisalimia Dorice akiwa amevimba kama kiboko aliyekasirishwa. Eddy hakujibu isipokuwa wale rafiki sake.
"Umefuata nini hapa we mpuuzi?"
"Nimekufuata wewe nataka nijue kama unanipenda mimi au Doreen?"
"Hivi we mwanamke unawazimu we? Nikupende wewe kama nani? Doreen ndo mpenzi wangu, nampenda sana."
"Kweli!?"
"Ndio tena niondokee hapa, unanitia kinyaa!" Eddy alimsukuma Dorice kwanguvu Dorice akaanguka chini na kujigongesha kichwa kwenye kitanda.
"Eddy usifanye ivo bhana utamuumiza mwenzio" alisema rafiki mmoja wa Eddy kwani alimuonea huruma sana Dorice.
"Achana nae mpumbavu huyo"
"Lakini kumbuka mlikotoka"
"Achana na mimi kama unampenda si umchukue!"
Maneno Yale yaliziidi kumuumiza Dorice, aliinuka pale chini akajifuta vumbi maana bweni lilikuwa na vumbi kupita kiasi.
"Sawa Eddy! Daima kumbuka sio kila king'aacho ni dhahabu... Utanikumbuka!" Alisema Dorice kwa huzuni na kutoka.

"Akukumbuke nani wewe? We boya tu huna lolote" Eddy aliropoka maneno hayo huku akiwashangaza rafiki zake kwani daima hawakujua kama Eddy angemchukia Dorice kiasi kile kutokana na mapenzi yao yalivokuwa.

"Ama kweli watu wanabadilika..!" Alisema rafiki take Eddy na kuondoka zake.

Dorice aliondoka zake mpaka bwenini kwao, akachukua begi lake dogo na kuweka vitu vyake muhimu. Isipokuwa nguo za shule na madaftari, baada ya kupaki vizuri akachukua kanga akaivaa baada ya kutoa nguo kisha akaenda bafuni kuoga.

Alipooga na kujiandaa vizuri alikaa kitandani kwake huku kila Mara akitazama SAA yake ya mkononi ambayo alipewa na Eddy enzi za mapenzi yao. Ilikuwa SAA nzuri ya Dhahabu."Ikifika SAA kumi na mbili jioni lazima nitoroke ... Siwezi kubaki hapa!" Aliwaza Dorice akiwa kitandani kwake.

Muda huchelewa sana pale unapousubiri ndivyo ilivokuwa kwa Dorice. Muda ulichelewa lakini ukafika, kigiza kilipoanza tu akachukua begi lake na kutoka bwenini. Hakuvaa nguo za shule hivyo haikuwa rahisi kugundua kama ni mwanafunzi wa pale. Taratibu akazipiga hatua ili atoroke shuleni pale.

Licha ya kwamba alisumbuliwa na maswali ya wanafunzi wenzake ila hakujali ingawa aliwapa majibu ya uongo yanayoridhisha.

Shule ya mabango ilikuwa imezingirwa na miti mingi hivyo akapita katikati ya miti hiyo ili asioneakane kirahisi. Alipokuwa anaendelea kutembea ghafla akaona kitu mbele yake akashtuka.

********
Jioni ile tulivu Eddy na Doreen walikutana kwenye mti mmoja mzuri na tulivu. Walikuwa wamekumbatiana kimahaba huku wakipeana denda za kutosha.

"Baby nakupenda sana" alisema Eddy
"Nakupenda pia ila..."
"Ila nini mpenzi?"
"Sharti la kuwa na mimi ni kwamba hutuwezi kufanya mapenzi..." Alisema Doreen.
" eh! Kwanini?"
"Tukifanya hivyo kuna kitu kitatokea kwako?"
"Mh Doreen! Mbona sikuelewi, tutaishije kama wapenzi?"
"Nivumilie tu... Ila bado nina bikra"
"Nataka niitoe bikra yako Doreen please!"
" huwezi kufanya mapenzi na mimi, pia kuna sharti lingine mbali na hilo..."
"Bby hapa siwezi kuwa na wewe bila kufanya mapenzi, siwezi! Halafu pia siwezi kukuacha au huniamini?"
Alisema Eddy akiwa amezidiwa na hamu ya mapenzi na ilikuwa kazi ngumu sana kwake kujizuia....

Itaendelea ......
 
Back
Top Bottom