Siku ya mtoto wa Afrika (International Day of the African Child) - June 16

Kachocho T.K

Member
Feb 1, 2011
25
3
TAARIFA YA SIKU YA MTOTO WA AFRIKA

Kila mwaka tarehe 16/6 watoto wote Afrika huadhimisha siku ya mtoto wa afrika ikiwa ni Sehemu ya kumbukumbu ya kuwakumbuka watoto wenzetu waliouawa kikatiri huko Soweto Afrika kusini walipokuwa wakiandamana kwa amani kupinga utawala wa kibaguzi uliokuwa ukiendeshwa na makaburu. Katika siku hii watoto hutumia fursa hii kufikisha ujumbe kwa jamii juu ya masuala mbalimbali yanayohusu malezi, makuzi, matunzo ulinzi na usalama wa watoto. Katika maazimisho ya mwaka huu tatajaribu kuufishia umma wa watanzania hasa wananchi wa Milaya ya Missenyi masuala yahusuyo sheria mpya ya watoto iliyopishwa na bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzani November 2009 pamoja na ajenda ya watoto iliyopendekezwa na baraza la taifa la watoto.

Uamuzi wa kihistoria ulifikiwa tarehe 20 Novemba 1989 pale viongozi wa dunia waliporidhia Mkataba kuhusu Haki za Mtoto katika Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa. Tangu kuridhia kwake miaka 20 iliyopita , Mkataba huu umevunja rekodi kwa kuwa mkataba wa haki za binadamu iliowahi kuridhiwa na mataifa mengi kuliko yote katika historia. Tanzania ilikuwa miongoni mwa nchi za mwanzo kabisa zilizoridhia Mkataba huu katika mwaka 1990 na kwa kufanya hivyo ikawa imetambua rasmi kwamba watoto wote wanayo haki ya kuishi na kukua, kupatiwa ulinzi dhidi ya vurugu, matendo mabaya na unyanyasaji, kuheshimiwa kwa mawazo yao na kuzingatiwa kwa maslahi yao katika maamuzi yote yanayohusu ustawi wao.

Katika mwezi wa Novemba 2009, miaka kumi na tisa baadaye, Bunge la Tanzania lilipitisha Sheria ya Mtoto ya Mwaka 2009. Sheria mpya ya Mtoto inazingatia kikamilifu Mkataba wa Haki za mtoto kulingana na muktadha wa Tanzania pamoja na kuweka mazingira ya kufanikisha kupatikana kwa haki muhimu. Inaleta matumaini ya kubadili maisha ya watoto wa taifa hili walio katika mazingira ya hatarishi na kuongeza msukumo katika kuelekea kwenye ufanikishaji wa Malengo mengi ya Maendeleo ya Milenia.

Miaka ya hivi karibuni imeshuhudia mafanikio makubwa katika kusukuma mbele haki za watoto wa Tanzania. Haki yao ya kuishi imezingatiwa kikamilifu kwa uwekezaji mkubwa kinga na tiba dhidi ya malaria, chanjo na utoaji wa matone ya Vitamini A kwa watoto kama nyongezea ya virutubisho muhimu vya kuimarisha kinga zao na kuwasaidia kupambana na maradhi. Kutokana na juhudi hizo, vifo vya watoto wa umri wa chini ya miaka mitano vimepungua kwa takribani robo nzima tangu mwaka 2003/4. Changamoto kubwa imebakia katika kuokoa maisha ya watoto kiasi cha 400 wa umri wa chini ya miaka mitano ambao hufariki kila siku Tanzania, hata hivyo kiasi cha miaka michache tu iliyopita namba hiyo ya watoto waliofariki kila siku ilikuwa 500.


Hatua kubwa pia zimepigwa katika utekelezaji wa haki ya mtoto ya kupatiwa elimu. Utoaji wa elimu ya msingi bila malipo ulioanza mwaka 2001 umewezesha hata wale watoto wanaotoka kwenye familia duni kabisa kiuchumi kuandikishwa shuleni. Bado ipo haja kubwa ya kuinua ubora wa elimu na kupunguza tofauti za uwezo wa kimapato ili kuwawezesha watoto wote kujiunga na elimu. Watoto wenye ulemavu na wale wanaotoka katika makabila ya wafugaji wanaohamahama pamoja na wale wanaotoka katika familia ambazo zimeathiriwa sana na VVU na UKIMWI mara nyingi ndio ambao hushindwa kuhudhuria shuleni – na idadi kubwa ya watoto hawa hukatisha masomo kabla ya kuhitimu elimu ya msingi. Hata hivyo kuna badiliko linalokuja, wanafunzi wa kike ambao watapata ujauzito na kujifungua sasa hivi wana haki ya kurejea shuleni na kukamilisha elimu yao. Idadi ya wanafunzi wanaojiunga na elimu ya sekondari pia inaongezeka.

Sheria ya mtoto inashughulikia changamoto nyingi kubwa za ulinzi zinazowakabili watoto Tanzania.. Inashughulikia masuala ya kutokubaguliwa, haki ya jina na utaifa, haki na wajibu wa wazazi, haki ya kusikilizwa, haki ya kupewa ulinzi dhidi ya vitendo vya utesaji na udhalilishaji. Sheria hii pia inaweka mfumo wa kuhakikisha haki za watoto kisheria pale wanapofikishwa mbele ya sheria kama wahalifu, mashahidi au watuhumiwa. Inafafanua mchakato wa kuhakikisha ulinzi wa watoto wasio na familia ikiwa ni pamoja na uasilishaji wa mtoto kimataifa.

Pamoja na kwamba sheria hii mpya ina mapungufu yake – kwa mfano, haizungumzii chochote kuhusu ubaguzi unaohusiana na umri wa ndoa kisheria, ambao unabaki kuwa miaka 15 kwa wasichana na 18 kwa wavulana, na haifuti adhabu ya viboko - Sheria hii ni mfano mzuri wa upigaji hatua kuelekea kwenye mazingira yaliyosheheni haki kwa watoto. Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) pamoja na vyama vingi vya kiraia, timu ya wataalamu wa sheria, wanataaluma, na watoto wenyewe, wote wakiwa wameshirikishwa katika mchakato wa kibunge na katika mijadala ya umma kuhusu Sheria hii mpya, wanao wajibu wa kuhakikisha kwamba sheria hiyo inafanya kazi. Kwa pamoja tumedhamiria kufanya kazi na serikali pamoja na wadau mbalimbali – majaji, polisi, walinzi, waalimu, wahudumu wa afya, wafanyakazi wa sekta ya maendeleo ya jamii pamoja na wengine wengi – ambao jukumu lao litakuwa kutekeleza sheria hii, ili iweze kukidhi matarajio kwa vizazi vijavyo vya watoto wa Tanzania.

Mambo muhimu ya kuzingatia kwenye sheria mpya ya mtoto

Kama ilivyo Katika nchi nyingi za kiafrika kutokana na kuyumba kwa uongozi na vitendo vya Rushwa, kuna changamoto zilizo dhahili kuwa kusipokuwepo na mpango mkakati kabambe aw kuhakikisha sheria hii inatekerezwa kwa vitendo, pamoja na ubora wake haki, ulinzi, malezi na matunzo kwa watoto vitabaki kuwa kwenye maandishi tu huku watoto wakiendelea kunyanyaswa kuteswa na kufanyishwa kazi zisizo stahili hivyo kuathiri maendeleo na makuzi yetu kimwili na kiroho. Kwa mfano Sehemu ya 11 kifungu cha 13, kinasisitiza kuwa hairuhusiwi kwa mtu yeyote kumfanyia mtoto ukatili au vitendo vya kinyama, adhabu zinazokiuka utu na kumdhililisha ikiwa ni pamoja na mila na desturi zinazodhalilisha na kuumiza mwili na akili ya mtoto na maendeleo yake ya kiroho, lakini cha ajabu ni kwamba vitendo vya kinyama vinazidi kuongezeka kila kukicha ikiwa ni pamoja na watoto kuunguzwa kinyama, kubakwa na kupewa adhabu zisizolingana na kosa. Haya yote yanatendeka viongozi wa serikali wanashuhudia na pengine hupindisha sheria. Mtuhumiwa anapobainika kesi huishia Aidha mikononi mwa polisi au hata mahakama za chini bila kubainisha wazi adhabu zilizotolewa dhidi ya mtuhumiwa. Sisi watoto tunatamka kwa kiongozi atakayethubutu kumkingia kifua au kuhusika na njama za Rushwa ili mtuhumiwa asichukuliwe hatua za kisheria basin aye ahesabiwe kuhusika na kitendo hiki na hatua kalizichukuliwe ikiwa pamoja na kuachishwa kazi mara moja.

Pia kifungu cha 17(1) na (2), kinasema ni marufuku mfanyabiashara kuuza sigara, pombe, madawa, vileo au mvinyo kwa mtoto.na mtu atakaye bainika na kosa hili atahukumiwa kifungo kisichozidi mwaka mmoja au faini isiyipungua milioni moja za kitanzania au adhabu zote kwa pamoja. Hii ni pamoja na mtu yeyote atakayebainika kumuhusisha mtoto katika biashara hii, Jambo la kushangaza sana ni kuona siku hizi watoto wamegeuzwa kuwa wamachinga Katika maeneo tofauti ikiwemo kuuza bidhaa hizo haramu ambazo sheria inazizuia. Lakushangaza sana serikali imekaa kimya kukikemea hili na ni dhahili kuwa wanaliona kwani biashara hizi hufanyika maeneo yaliyowazi kabisa kama stendi za basi, magengeni na hata kwenye mahoteli na baa.

Vifungu vya 77 hadi 86 vinasema pamoja na mambo mengine mtoto mwenye umri kuanzia miaka 14, ana haki ya kufanya kazi nyepesi, lakini ieleweke kwamba kazi nyepesi ni zile ambazo haziathiri afya ya mtoto, hazikwamishi maendeleo yake kielimu au makuzi yake. Mtu haruhusiwi kumwajiri mtoto katika kazi yoyote ya kinyonyaji na mtu haruhusiwi kumwajiri mtoto katika kazi yoyote ambayo ni hatari katika afya yake, elimu, akili, maumbile na hata katika maendeleo yake ya kiroho. Baada ya saa za shule watoto tunanyimwa muda wa kupumzika na kusoma kwani tunatumikishwa na wazazi/walezi kwenye ajira tofauti ikiwa ni pamoja na kulazimishwa kufanya biashara ndogo ndoho ya kutembeza bidhaa kama samaki, dagaa, nyanya na karanga jambo ambalo ni kinyume cha sheria. Wakati mwingine yunalizamishwa kutembeze biashara hii maeneo hatarishi kama baa nyakati za usiku bila kujali jinsia au umri. Sio kwamba serikali hailiono hili kwani tunaamini watu wenye uwezo wa kwenda Sehemu za starehe kama baa asilimia kubwa ni viongozi wa saerikali.

Wajibu wa jamii

Kifungu cha 95 kinasema ni wajibu wa mwanajamii mwenye taarifa au ushahidi kuwa haki za mtoto zinavunjwa na mzazi, mleazi, ndugu au mtu yeyote ambaye kwa wakati huo anamlea mtoto au yuko chini ya uangalizi wake kutoa taarifa za unyanyasaji wa mtoto kwenye ofisi za serikali, taasisi au chombo chochote kinachoweza kumsaidia mtoto. Lakini wanajamii wamekaa kimya pindi waonapo matukio ya namna hii. Hii ni pamoja na kushindwa kuwakemea watoto pindi wanapokiuka wajibu wao kama kurandaranda hovyo wakati wa usiku. Watoto wanapoteza muda kwenye mambo yasiyo ya msingi kama kuangalia runinga hasa vipindi vya michezo na mieleka wakishindwa kutimiza wajibu wao wa msinga kama kusoma kwa bidii. Tuna uhakika wazazi,walezi, wanajamii na serikali wanayaona haya na kuyafumbia macho kwani huwa wanashirki na watoto kuangalia mambo haya yasiyo ya msingi na yanayotupotosha sisi watoto. Mapendekezo yetu ni kwamba serikali kwa kushirikiana na wanajamii wahakikishe vitendo hivi vina pigwa marufuku ikiwa ni pamoja kumuonya mtoto atakayebainika kwa mujibu wa sheria, lakini pia kiongozi mwanajamii yeyote atakayebainika kushindwa kudhibiti maeneo yanayopelea watoto kupotezea muda au kujifunza mambo ambayo ni kinyume na maadili awajibishwe na hafai tena kuendelea kuwa kiongozi.

Wajibu wa serikali kulinda haki za mtoto

Vifungu vya 94 hadi 96 vinasema, serikali ya mtaa atawajibika kulinda na kutetea maslahi ya mtoto katika eneo analoishi ili kuhakikisha kwamba Watoto wanalelewa katika mazingira stahiki na kwa mujibu wa maadili ya jamii na taifa letu. Serikali mishindwa kabisa kutengeneza mazingira yanayofaa kwa watoto kuisha na kukua, hii ni pamoja kushindwa kuweka masuala ya watoto kwenye mpango wa muda mrefu na utekerezaji wa shughuli za kila siku. Kwa mfano kwenye vikao vya maendeleo vya vijiji na kata mada zinazoongelewa sana ni masuala ya UKIMWI, afya, kilimo n.k lakini hakuna muakirishi hata mmoja wa kuwasilisha mambo yanayohusu watoto. Kamati za watoto wanaoishi Katika mazingira hatarishi ziliundwa karibu vijiji vyote Tanzania lakini kamati hizi zimeterekezwa hukohuko vijijni zikishindwa kujua wajibu na majukumu yake na kushindwa kuhusishwa kwenye masuala ya maendeleo kama ilvyo kwa kamati nyingine kama za afya na UKIMWI.

Serikali imeshindwa kuunda kamati hizi ngazi za kata na hata wilaya kama inavyoelekezwa kwenye muongozo wa uundaji wa kamati za kuhudumia watoto wanaoishi Katika mazingira hatarishi uliotilewa na idara ya ustawi wa jamii. Tunapendekeza serikali kuhakikisha masuala yanayohusu watoto yanawekwa kwenye vipaumbele ikiwa ni pamoja na kuwa na mwkirishi wa watoto kwenye vikao vya maendeleo vya kata, kuwa mjumbe wa kamati ya watoto wanoishi Katika mazingira hatarishi kwenye vikao vyote vya maendeleo kuanzia ngazi ya kata hadi wilayani na kuunda na kufufu kamati za watoto wanaoishi kwenye mazingira hatarishi ngazi zote kama inavyoelekezwa kwenye mwongozo wa uundaji wa kamati hizi.


Ajenda ya watoto

Kama mnavojua kuwa zaidi ya nusu ya watnzania ni watoto, hivyo kuwekeza kwa watoto ni kunufaisha familia zetu, jamii zetu na taifa letu. Dira ya Tanzania inayostawi kiuchumi na mpango wa maendeleo wa miaka mitano vinaweza kufikiwa tu ikiwa watoto watakua wakiwa na afya, wenye kupata lishe bora, elimu bora na kulindwa dhidi unyanyaswaji, vurugu na unyanyaji. Kila nchi iliyofikiwa kuwa na maendeleo ya kiuchumi ya kipato cha wastani imewekeza kwa watoto kwa kiwango kikubwa. Watoto kwa kuliona hili waliweza kutoa mapendekezo yao kupitia baraza la watoto la taifa na kumwomba mheshimiwa raisi na baadhi ya wagombea ngazi za ubunge na udiwani kuridhia kuwa watayaweka mapendekezo haya kwenye mipango yao ya maendeleo.

Ajenda hizo ni kuwekeza kuokoa maisha ya watoto na wanawake, kuwekeza kwenye lishe bora, kuwekeza kwenye usafi, miundombinu ya maji taka na ugavi wa maji mashuleni na kwenye huduma za afya, kuwekeza kumwendeleza mtoto akiwa mdogo, kuwekeza kwenye elimu bora kwa watoto wote, kuzifanya shule kuwa mahali pa usalama, kuwalinda watoto wachanga na wasichana dhidi ya VVU, kupunguza mimba za utotoni, kuwanusuru watoto dhidi ya vurugu, udhalilishaji na unyonyaji na kuwekeza kwa watoto wenye uremavu.


Ni takribani mwaka mmoja umepita tangu uchagui mkuu umepita lakini kuna dalili kuwa hata waliosaini kuzingatia ajenda hizi walisha sahau . Ni wajibu wetu sisi watoto kuwakumbusha lakini tunaomba serikali isaidie kufuatilia mipango ya waheshimiwa hawa kama inatekerezeka ikiwa in pamoja na masuala yahusuyo watoto
Mwisho tunatoa wito kwa serikali, jamii, wazazi na walezi mnatekereza kwa vitendo yote yaliyoainishwa kwenye shria ya mtoto na mapendekezo ya watoto kama yalivobainisha kwenye makaburasha na vipeperushi vya ajenda ya watoto, pia serikali ihakikishe maandiko haya muhimu yanasambazwa mpaka ngazi za chini na yanatafsiriwa kwa rugha rahisi.

Katika kupunguza athari za unyanyasaji wa watoto na ili kumlea na kumkuza mtoto tunapendekeza hatua zifuatazo zichukuliwe, Elimu juu ya ulinzi na malezi ya watoto, Sheria ndogondogo juu ya unyanyaswaji wa watoto zitungwe na kutekelezwa, Kuelimisha jamii juu ya haki za watoto na malezi kupitia vikundi vya mbalimbali vya kijamii, Uhamasishaji wa jamii juu ya makuzi na matuno ya watoto, Ushiriki wa serikali na asasi nyingine juu ya masuala ya watoto na kutunga sera za ulinzi wa watoto zitekelezwe
 
nawaachia wenyewe muweke mawazo yenu juu ya picha hiyo
 

Attachments

  • t f 000055.jpg
    t f 000055.jpg
    46.8 KB · Views: 211
Mungu mkubwa ... Ikiwa Siye tunanyanyasana "Wenyewe" !! mtoto atakuwa kwa kudra za mungu tu...
MwaAfrika anamkandamiza mwaAfrika tunategemea matokeo gani?
 
Back
Top Bottom