Siasa za ‘kifisadi’ zakwama kikaoni NEC-CCM Arusha, Wataka Mary Chatanda ang'olewe...

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
[h=1][/h]
Mwandishi Wetu - Raia Mwema




chatanda222.jpg



Katibu wa CCM Mkoa wa Arusha, Mary Chatanda


HALI ya kisiasa ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Arusha imendelea kuwa tete baada ya mkutano wa Halmashauri Kuu ya chama hicho kushindwa kufikia muafaka baada ya wajumbe wake kutofautiana kuhusu ajenda za mkutano huo.

Kikao hicho kilichofanyika Januari 15, mwaka huu, chini ya ulinzi mkali kutoka kikosi cha Green Guards cha chama hicho, katika ukumbi wa vijana uliopo eneo la Fire mjini Arusha, kilianza saa nne asubuhi na kuhudhuriwa na wajumbe karibu wote wanaounda Halmashauri Kuu wa CCM ya Mkoa wa Arusha, pamoja na baadhi ya viongozi wa Serikali.


Miongoni mwa waliohudhuria ni pamoja na Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi, Goodluck ole Medeye, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo na Mkurugenzi wa Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC) ambaye pia ni mjumbe wa NEC ya CCM ngazi ya taifa, Elishilia Kaaya.


Hata hivyo, baada ya malumbano makali yaliyoambatana na vijembe kati ya wajumbe wa pande zinazovutana kisiasa, hadi kufikia saa 11:45 jioni, kikao hicho kushindwa kufikia muafaka kuhusu ajenda moja.


Ajenda hiyo iliyozua tafrani na kisha kukosa muafaka ilijadiliwa kwa muda wa saa saba mfululizo na jina la Mbunge wa Monduli na Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa, likitajwa mara kwa mara.


Hadi muda huo unawadia, wajumbe hao walikuwa wamefanikiwa kujadili ajenda tatu kati tisa zilizowasilishwa mbele yao na sekretarieti ya mkoa na kwa hiyo, wakalazimika kuahirisha ajenda nyingine sita hadi kikao kijacho.


Taarifa zilizopatikana kutoka ndani ya kikao hicho zilieleza kuwa ajenda iliyoleta mtafaruku katika kikao hicho ni ile ya kuthibitisha muhtasari wa kikao kilichopita ikiwa pamoja na yatokanayo na kutathmini utekelezaji wa maazimio ya kikao hicho.


Maazimio hayo yanatajwa kuhusisha adhabu walizopewa viongozi wawili wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) mkoani Arusha.


Aidha kikao hicho pia kilikwama baada wajumbe waliokuwa wamepanga kupenyeza ajenda ya kumng’oa katika wadhifa wake, Katibu wa CCM Mkoa wa Arusha, Mary Chatanda, kushindwa kutimiza azma yao hiyo baada ya kubanwa kwa hoja na wajumbe wengine.


Taarifa zinadai kuwa wajumbe hao wanaotaka Chatanda ang’oke wanatajwa kuungwa mkono na Mwenyekiti wa CCM mkoani Arusha, Onesmo Nangole pamoja na Mwenyekiti wa UVCCM-Arusha, James ole Millya.


Kwa muda mrefu Millya na Nangole pia wamekuwa wakihusishwa na mtandao maalumu unaounga mkono harakati binafsi za kisiasa za Edward Lowassa, aliyepata kujiuzulu uwaziri mkuu pamoja na mawaziri wengine wawili kutokana na kashfa ya zabuni iliyotolewa kwa kampuni ya kufua umeme ya Richmond.


Nyuma ya mtandao huo ambao hata hivyo bado haujathibitishwa rasmi, kumekuwapo na madai kwamba Lowassa anayo malengo ya kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.


Katika kikao kilichopita, Millya na mjumbe wa Baraza Kuu la UVCCM ngazi ya taifa kutokea Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo, walipewa onyo kali linaloambatana na adhabu ya kuweka katika uangalizi kwa mwaka mmoja kuanzia Agosti 3, mwaka jana.


Vijana hao sasa wapo kwenye uangalizi huo hadi Agosti 3, mwaka huu, na kwa hali hiyo, inaelezwa kwamba hawawezi kuwania nafasi za uongozi ndani ya chama hicho, katika uchaguzi wa mwaka huu.


Habari zaidi kutoka ndani kikao hicho zinaeleza kuwa katika ajenda hiyo iliyozua mtafaruku, mchangiaji wa kwanza alikuwa ni Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Monduli, aliyetaka vijana hao wafutiwe adhabu hizo akirejea ziara ya mlezi wa chama hicho mkoani Arusha, Steven Wassira, ambaye anadaiwa kusuluhisha migogoro ndani ya chama Arusha.


Taarifa hizo kutoka kwa mmoja wa wajumbe wa kikao hicho (jina linahifadhiwa), zinaeleza kuwa lengo la mwenyekiti huyo wa Monduli ni kumfutia adhabu Millya ili aweze kugombea kwenye uchaguzi wa CCM utakaofanyika ngazi za uongozi zote mwaka huu.


“Lakini mkakati huo wa kumnasua Millya ulikwama pale mjumbe mmoja aliposimama kumjibu mwenyekiti huyo kuwa anapoteza muda wake kumpigania Millya ili afutiwe adhabu anayoitumikia,” anaeleza mtoa habari wetu.


Akimkariri mjumbe huyo aliongeza: “Mikakati yenu ya kijinga tunaijua na haitawasaidia nyinyi wala chama chetu…adhabu zipo kwa mujibu wa kanuni na taratibu hivyo hazitabatilishwa kamwe.”


Kutokana na kauli hiyo, inaelezwa kuwa Millya alisimama na kumjibu kuwa alikuwa anamheshimu sana, hata hivyo, kabla Millya hajamaliza kujibu mapigo, mjumbe huyo akasimama ghafla na kumjibu kuwa hana haja ya kuheshimiwa na mtu anayetumika “kijinga kama wewe”.


“Hapo hali ilikuwa mbaya wajumbe walirushiana vijembe na mipasho na hoja hiyo ilizimwa na wajumbe wengine wa Wilaya ya Arusha Mjini ambao hawamuungi mkono mmoja wa viongozi wa kisiasa anayedaiwa kuwa yuko katika mbio za kugombea urais mwaka 2015 kupitia chama chetu,” alisema.


Naye mjumbe mwingine kutoka Wilaya ya Arusha Mjini aliwaambia wajumbe kuwa wasipoteze muda kwenye jambo ambalo lilishafanyiwa kazi na uamuzi kufikiwa, badala yake wajikite katika kukijenga chama chao mkoani Arusha.


Mjumbe alisema; “Mbona vurugu hizi hamzifanyii kwenye wilaya zenu kama Monduli ila mnazileta Arusha mjini?...hata yale mambo yenu ya mashina ya Arusha mjini yalifanywa na watu wa Monduli, tuliona namna Hiace (Toyoya Hiace) zilivyojaza watu kutoka Monduli kwa ajili ya shughuli za Arusha mjini, mwenyekiti hizi ni fujo.”


Mjumbe huyo anaendelea kueleza; “Hata leo hii kabla ya kuja hapa wenzetu mlianzia vikao mahotelini, kulikoni? Nashauri nguvu hizo zitumike kuhakikisha tunashinda kata tano za udiwani hapa Arusha mjini badala kuendelea na tabia yenu ya ‘kuwawinda’ viongozi na wanachama wasiowaunga mkono katika harakati zenu binafsi.”


Baada ya hoja ya kumnasua Millya kukwama, wajumbe hao walimgeuzia ‘kibao’ Katibu wa Mkoa, Mary Chatanda, wakijenga hoja kuwa Katibu huyo ameshindwa kukidhi mahitaji ya chama kwa sasa hivyo aondolewe katika nafasi yake.


Katika kipindi cha hivi karibuni, Chatanda amekuwa katika mgogoro na Mwenyekiti wake, Nangole, katika kile kinachodaiwa kuwa ni hatua ya katibu huyo kubana matumizi holela ya mali za chama, kama matumizi ya magari na posho mbalimbali kwa kuweka utaratibu ambao inadaiwa kuwa mwenyekiti wake anapinga.


Mgogoro huo baina ya Chatanda na Mwenyekiti wake unaelezwa kukigawa chama hicho katika makundi na kusababisha mpasuko na kwa sasa, mgogoro umezidi kuongezeka na kuwahusisha wanachama wengine.


Hoja hiyo ya kumng’oa Chatanda ilianzishwa tena baadaye na Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Monduli, Mwenyekiti wa UVCCM, mjumbe wa Halimashauri Kuu ya CCM Arusha, kutoka wilaya ya Karatu. Hata hivyo, juhudi zao hizo za kurejesha hoja hiyo zinadaiwa kudhibitiwa na wajumbe wa Wilaya ya Arusha na wengine kutoka Wilaya ya Longido.


Mmoja wa wajumbe waliojibu hoja hizo ananukuliwa akisema kwamba; “....kwa mtu yeyote mwenye akili timamu akiangalia namna wajumbe hao walivyozungumza, atabaini kuwa wahusika wana ajenda maalumu au wametumwa kwa maslahi ya mtu na si chama.”


“Nyie mna lenu jambo kwa mtu mwenye busara akiwatathmini atagundua kuwa hapa mmekuja kwa maagizo ya mtu mwingine aliyeko nje ya kikao hiki kwa hiyo, mheshimiwa mwenyekiti naomba ajenda hiyo iondolewe kwa kuwa haina maslahi kwa chama chetu,”


“Wakati tunaingia tumejionea watu wanauza vitabu vyenye picha za Edward Lowassa, mwenyekiti huu si wakati wa kampeni naomba msitufanyie vurugu.


“Sisi wengine kwa nafasi zetu tuna masikio makubwa, tunajua mengi yaliyoko nje ya pazia, tunayajua mliyoyaandika kwenye mtandao wa Facebook leo kuhusu mkutano huu na tunataarifa na mikutano mliyoifanya huko Arumeru kuhusu mkutano wa leo,” alisema mjumbe huyo na kuongeza kuwa;


“Mheshimiwa Mwenyekiti elekeza wajumbe wajadili masuala yaliyoko kwenye ajenda, hayo mengine yafuate utaratibu na kama unaogopa kupeleka ajenda kamati ya siasa kwa sababu huamini kama utaungwa mkono ni bora ujiuzulu.”


Taarifa zaidi zilisema kuwa mmoja wa wajumbe alipendekeza iundwe tume maalumu ya wazee wa chama kumaliza tofauti kati ya Katibu (Chatanda) na Mwenyekiti wake (Nangole), lakini wajumbe wengine walikataa baada ya taarifa kuvuja kwamba, kati ya wajumbe waliopendekezwa kuongoza kamati hiyo atakuwa Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa.


Gazeti hili limedokezwa kuwa tayari mkakati ulikuwa umeandaliwa kumpendekeza Lowassa kama sehemu ya wazee hao ili kuendelea kumjenga kisiasa lakini mpango huo uligonga mwamba baada wajumbe kukubaliana kuwa, mgogoro kati ya katibu na mwenyekiti wake ushughulikiwe kwa kutumia vikao halali vya chama.


Akizungumzia yaliyojiri katika kikao hicho, Katibu wa CCM Mkoa wa Arusha, Mary Chatanda, alikanusha taarifa za kikao hicho kuvunjika.


“Si kweli kikao kilivunjika, tulimaliza salama na kuhusu malumbano yaliyotokea yalikuwa ya kawaida, katika masuala ya siasa wajumbe hushindana kwa hoja,” alisema Chatanda.


Katibu huyo alimalizia kwa kueleza kuwa katika kikao hicho pia walijadili masuala ya uhai wa chama, utekelezaji wa ilani ya uchaguzi na hali ya kisiasa mkoani Arusha.


Ameelza kwamba tofauti zilizopo miongoni mwa viongozi wa chama hicho ni za kimtazamo na haziwezi kuathiri uimara wa CCM.








 
Kwanini Mary Chatanda ana nguvu hivi? hakuna boss wake? Ana nguvu zaidi ya Mkuu wa Mkoa na Wabunge wote Mkoani Arusha
 
tatizo ni makundi ya EL ambayo yanatumia nguvu kubwa kuhakikisha Mary Chatanda anaodnoka AR
 
sasa nimeamini kweli Lowasa ni janga la kitaifa. jamani kama mna muda isomeni hiyo habari yote mtanielewa namaanisha nini.
 
sasa nimeamini kweli Lowasa ni janga la kitaifa. jamani kama mna muda isomeni hiyo habari yote mtanielewa namaanisha nini.

Pamoja na ushenzi wote anaoufanya na kubainishwa wazi wazi, lakini ajabu ni kwamba kuna watu huwaambii kitu juu ya EL.

Hata hapa JF kuna watu wamejibainisha wazi kwamba wao ni ProEL, subiri tu waione hii thread uone watakavyoivamia na kumtetea utadhani ni malaika.
 
Ni Kwanini watu wa EL hawamtaki Mary Chatanda? na kama aliletwa na CCM toka Tanga hadi Arusha?
 
Back
Top Bottom