Shairi: Leo navunja kibubu

Dotto C. Rangimoto

JF-Expert Member
Nov 22, 2012
1,985
1,282
LEO NAVUNJA KIBUBU!
1
Leo navunja kibubu, pesa ninunue khanga,
Apendeze mahabubu, kama binti wa kitanga
Atokapo awe bubu, washindwe wano jigonga
Mniache nayajenga, mkome kunita zoba.
2
Sasa navunja kibubu, nipate nunua kanga,
Ale ashibe muhibu, kitoweo si mchunga,
Usiku tule kababu, uji pilipilimanga,
Mniache nayajenga, mkome kunita zoba.
3
Mimi navunja kibubu, nikagule kungumanga,
Nimpatie tabibu, mafusho toka Umanga,
Nimuenzi taratibu, niseme na zake nyonga
Mniache nayajenga, mkome kunita zoba.
3
Mie navunja kibubu, habibi apate shanga,
Mapambo yake dhahabu, vidoleni na kitanga,
Sawa nipate adhabu, apendeze wangu ninga,
Mniache nayajenga, mkome kunita zoba.
4
Njano navunja kibubu, lengo niweze kujenga,
Nyumba isiwe na tabu, mahaba yatie nanga,
Penzi lataka adabu, siwezi kulibananga,
Mniache nayajenga, mkome kunita zoba

Dotto Rangimoto Chamchua(Njano5)
0784845394/0762845394
mzalendo.njano5
Morogoro Tanzania

kwa mashairi mengine kama hayo waweza kujisomea katika blogu yangu, kwenye icon ya mashairi utabofya hapo kisha utayaona mashairi mengi nilitotunga

SASA HAMSINI RASI, HAMSINI MAJINUNI. | Kisima Cha Jangwani.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom