BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,789
- 288,011
Janja ya serikali yazuia mjadala wa Richmond
Sheria yawakuta wabunge wakiwa hawajajiandaa
na Charles Mullinda, Dodoma
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
Sheria yawakuta wabunge wakiwa hawajajiandaa
na Charles Mullinda, Dodoma
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
MKUTANO wa 14 wa Bunge, ulimalizika jana huku serikali ikifanikiwa kuzima mjadala wa maazimio 23 ya Bunge yanayohusu hatua ilizochukua baada ya kubainika kwa matatizo makubwa katika mkataba ulioipa ushindi wa zabuni ya kuzalisha umeme wa dharura Kampuni ya Richmond Development LLC.
Kuzimwa kwa mjadala huko kumewezeshwa na hatua ya serikali kuamua kumfungulia mashitaka, mkurugenzi wa kampuni hiyo akituhumiwa kuisababishia serikali hasara.
Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa maazimio hayo bungeni jana, Waziri Mkuu Mizengo Pinda, alisema anafanya hivyo akitambua kwamba, Kanuni ya Bunge namba 64 (1) (C) toleo la mwaka 2007, inalizuia Bunge kujadili au kuzungumzia jambo linalosubiri uamuzi wa mahakama.
Akinukuu kanuni hiyo, Pinda alisema: Bila ya kuathiri masharti ya Ibara ya 100 ya Katiba yanayolinda na kuhifadhi uhuru wa mawazo na majadiliano katika Bunge, mbunge hatazungumzia jambo lolote linalosubiri uamuzi wa mahakama.
Alisema kwa msingi huo na kwa uelewa wake, ameona ni vema kutoa maelezo ya jumla kuhusu mchakato wa mashauri yaliyopo katika mahakama yanayohusisna na mikataba baina ya TANESCO na Richmond.
Akizungumza kuhusu maazimio yaliyokwisha kutekelezwa na serikali alisema, Septemba 2008 alilifahamisha Bunge kuwa, mchakato wa utekelezaji wa maazimio 10 kati ya 23 ulikuwa umekamilika.
Alisema tangu wakati huo mpaka sasa, maazimio mengine mawili, namba 17 na 18, yamekamilika ambayo ni kufutwa kwa Kampuni ya Richmond Development kutoka kwenye orodha ya makampuni halali nchini na wamiliki wa kampuni ya Richmond kufikishwa mahakamani ili wafunguliwe kesi ya jinai kwa udanganyifu na ujanja wa kuiibia serikali.
Akizungumzia hatima za waliokuwa mawaziri wa Nishati na Madini kwa nyakati tofauti, Nazir Karamagi na wa kabla yake, Dk. Ibrahim Msabaha, ambao walitajwa katika maazimio hayo, Pinda alisema tayari taasisi za dola ziko katika hatua ya mwisho kukamilisha uchunguzi wa tuhuma zao kabla ya kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria au la.
Hata hivyo alisema katika azimio namba 14 lililotaka wanasiasa hao wawajibike, alisema tayari walikuwa wameshajiuzulu nyadhifa zao za uwaziri tangu Februari mwaka jana.
Alisema pamoja na hatua hizo, serikali iliona ni busara vyombo vya dola vifanye uchunguzi zaidi kwa lengo la kujiridhisha kama kulikuwa na utovu wa maadili katika kushughulikia mchakato wa zabuni hiyo au la.
Kuhusu azimio namba tano, saba, tisa na 14 pia alisema maudhui yake yanafanana kwa sababu yanaitaka serikali kuwawajibisha watumishi wote wa umma waliohusika katika mchakato wa mkataba huo wakiwemo wale wa TAKUKURU ambao walifanya uchunguzi kuhusu suala hilo.
Alisema mamlaka za nidhamu zinazohusika na watumishi hao wa umma, zimekamilisha uchambuzi wa maelezo ya utetezi yaliyotolewa na kila mtumishi aliyeshiriki kwenye mchakato wa zabuni hiyo.
Alisema uchunguzi kuhusu watumishi hao unaendelea na ushauri wa vyombo vya dola vya uchunguzi ndio utakaowezesha serikali kuona ni watumishi gani wanaostahili kuingia kwenye mchakato wa kuchukuliwa hatua za kinidhamu na wale watakaoonekana kutenda makosa ya jinai kuchukuliwa hatua zinazostahili.
Tanzania Daima ambayo tangu mwanzoni mwa wiki hii iliuona mwelekeo wa jambo hilo kutojadiliwa bungeni kutokana na uamuzi wa serikali kulipeleka mahakamani ilipowasiliana na wabunge kadhaa, wote walionyesha kuwapo kwa fursa ya kuendelea nalo.
Mbunge wa Kyela, Harrison Mwakyembe (CCM), aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati Teule ya Bunge iliyochunguza sakata la Richmond na kuwasilisha taarifa iliyosababisha kujiuzulu kwa aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa, Karamagi na Msabaha, alipoelezwa na mwandishi wetu Jumatatu wiki hii kuhusu utata wa kujadiliwa kwa suala hilo, alisema tayari serikali ilikuwa imeshawasilisha kwa kamati ya Bunge hoja zake kuhusu ilivyotekeleza maazimio ya Bunge.
Mwelekeo huo huo wa kuwapo kwa matumaini ya kuwapo kwa mjadala huo, ulionyeshwa pia na Mbunge wa Karatu, Dk. Wilbrod Slaa (CHADEMA), ambaye naye aliieleza Tanzania Daima kwamba hoja hiyo ya Richmond ilikuwa ni lazima ijadiliwe.